Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MADIWANI wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wameulalamikia uongozi wa idara ya afya wilayani humo, kwa kushindwa kudhibiti vitendo vya wizi wa madawa ya kutibu wagonjwa, ambao umekuwa ukifanyika katika hospitali ya wilaya hiyo.

Sambamba na hilo imeelezwa katika kikao hicho kwamba licha ya tatizo hilo kuwepo, pia kumekuwa na upungufu mkubwa wa madawa hayo katika zahanati na vituo vya afya.

Malalamiko hayo yalitolewa hivi karibuni katika kikao cha baraza la madiwani kilichoketi kwenye ukumbi wa jumba la maendeleo uliopo mjini hapa.

Walisema dawa zinazosafirishwa na kupelekwa katika vituo vya afya au zahanati huko vijijini, wakati mwingine zimekuwa hazifikishwi kwenye maeneo husika, jambo ambalo limekuwa likisababisha wagonjwa kukosa matibabu.