Tuesday, January 29, 2013

UPINZANI WAPATA PIGO TUNDURU

  Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Ruvuma upande wa kulia Oddo Mwisho akipongezana na baadhi ya wazee wa Tunduru mara baada ya wanachama wa kambi ya upinzani kurudisha kadi zao na kuhamia CCM

 Na Steven Augustino,
Tunduru.

MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) katika Kata ya  Lingunga,  Mwenye Kwitanda akiwa na kundi la wanachama wake 300 wamehama chama hicho na kujiunga na  Chama  cha mapinduzi (CCM) ikiwa ni juhudi ya chama hicho kujiimarisha.

Hayo yalibainishwa katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika kata hiyo na
mjumbe wa halmashauri kuu ya Chama cha mapinduzi(CCM) taifa wa wilaya
hiyo Ajiri Kalolo na kuongeza kuwa kati ya wanachama hao wanachama 200 wametoka CHADEMA, wanachama 60 wametoka CUF na wanachama 40 wametoka TLP.

Kalolo aliendelea kueleza kuwa wengi wa wanachama hao ni kundi la vijana ambao katika uchaguzi mkuu  wa mwaka 2010, walirubuniwa na kujiunga na  vyama hivyo kwa ahadi za kuyafikia maendeleo kwa urahisi lakini mpaka sasa hakuna kinachoendelea.

"DC" ABURUTWA MAHAKAMANI MBINGA


Na Kassian Nyandindi,Mbinga.

ALIYEKUWA mkuu wa wilaya ya Makete, Osmund Kapinga amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, akituhumiwa kuiba shilingi milioni 26 mali ya kampuni ya Songea Network Solution iliyopo mjini hapa.

Mwendesha mashtaka wa polisi sajenti Seif alidai mbele ya Hakimu mkazi wa mahakama ya wilaya hiyo Joackimu Mwakyolo, kuwa mkuu wa wilaya mstaafu Osmund Kapinga aliiba fedha hizo.

Seif aliendelea kudai mahakamani hapo kwamba, Kapinga alitenda kosa hilo kwa kushirikiana na mdogo wake aliyetajwa kwa jina la John Kapinga ambapo waliiba fedha hizo ambazo ilitakiwa wazitumie kununulia kahawa vijijini kwa wakulima wilayani Mbinga.

Friday, January 18, 2013

WANANCHI WAHOFIA KUKOSA MAWASILIANO KUTOKANA NA BARABARA YA KUTOKA TUNDURU KWENDA SONGEA KUWA KATIKA HALI MBAYA





Hii ndiyo adha iliyopo barabara ya kutoka Tunduru kwenda Songea mjini. Serikali yaombwa kuingilia kati kwa kuchukua hatua za haraka katika kunusuru hali hii.(Picha na Steven Augustino)






 
Na Steven Augustino,
Tunduru.


WANANCHI wanaosafiri kupitia barabara ya Tunduru, kuelekea makao makuu ya mkoa wa Ruvuma, mjini Songea wamehofia kukosa mawasiliano na wenzao kufuatia barabara hiyo kuharibika vibaya, hasa kipindi hiki cha masika ambacho mvua nyingi zinaendelea kunyesha.

Baadhi ya abiria hao wakizungumza kwa nyakati tofauti ambao walifahamika kwa majina ya Mwanahawa Abdalah, Charles Haule na Asha Mohamed  walisema, barabara hiyo  ambayo kwa sasa inaelekea kuwa katika hali mbaya huenda ikajifunga kabisa na kusababisha magari ya abiria kushindwa kupita.  

Walisema hali hiyo imekuwa ni kero kubwa kwao na hivyo kusababisha nauli kupanda mara dufu  kutoka shilingi 15,000  hadi na wakati mwingine kufikia shilingi 35,000  jambo ambalo ni usumbufu kwa wananchi na jamii kwa ujumla.  

SOKO LA UHAKIKA ZAO LA KOROSHO TUNDURU LAZUA GUMZO, WAKULIMA WAIOMBA SERIKALI KURUHUSU KUUZA KWA WATU BINAFSI


Na Steven Augustino,
Tunduru.
 

WAKATI kukiwa na Sintofahamu juu ya upatikanaji wa soko la uhakika la kuuzia Korosho, wakulima wa zao hilo  wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wameiomba serikali itoe kibali cha kuruhusu korosho zao kuuzwa kwa wafanyabiashara binafsi ili kuwaepusha na hasara wanayoendelea kuipata wakati  huu, ambapo wanasubiri malipo yao ya mwaka uliopita.

Kilio hicho kimepazwa kwa nyakati tofauti na wakulima hao, na kuungwa mkono na viongozi walioshiriki katika mkutano mkuu maalum wa chama kikuu cha ushirika wilaya ya Tunduru(TAMCU) kilichoketi kwenye ukumbi wa chama hicho, uliopo mjini hapa.


Wakifafanua taarifa hiyo wakulima hao walisema kuwa hali hiyo inatokana na  muda wa uvumilivu kupita na hata kuvuka kikomo, hivyo wameamua kuchukua maamuzi hayo ya kuitaka serikali, ichukue hatua haraka ili wasiendelee kupata hasara kama ilivyotokea katika msimu wa mwaka 2010/2011.

Thursday, January 17, 2013

WAKULIMA WA KAHAWA WAKIFUATILIA KWA KARIBU UTENGENEZAJI WA MBOLEA AINA YA BIWI

Wanakikundi cha Bagamoyo kijiji cha Bagamoyo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakifuatilia mafunzo ya utengenezaji wa Mbolea ya asili aina ya  biwi kijijini humo.


WAKULIMA WA KAHAWA MBINGA WAPEWA MAFUNZO YA UTENGENEZAJI WA MBOLEA ZA ASILI

Wakulima wa kahawa kikundi cha Unango wilayani Mbinga, Ruvuma wakiwa pamoja na mtaalamu wa mimea na udongo Kaminyoge Mhamerd, wakifuatilia kwa karibu namna ya kuandaa wadudu waozeshaji watumikao kutengeneza mbolea aina ya Biwi. Mbolea hiyo ambayo ni ya asili utengenezaji wake  huchukua siku 45 na baada ya hapo tayari inaweza kutumika kwa kuwekwa mashambani.

WANUFAIKA NA MAFUNZO YA KUDHIBITI UBORA WA KAHAWA

     Mtaalamu wa mimea na udongo Kaminyoge Mhamerd upande wa kushoto, akiwa na wanakikundi cha Lumeme asili wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakifuatilia mafunzo ya kudhibiti ubora wa kahawa yaliyokuwa yakiendeshwa na mtaalamu huyo kijijini humo.


MATUMIZI YA DAWA ZA ASILI KATIKA SHAMBA LA KAHAWA NI JAMBO AMBALO HALINA MJADALA

Mkulima Manfred  Komba wa kikundi cha Unango akipulizia dawa ya asili shambani kwake kwa lengo la kuua wadudu waharibifu wa zao la kahawa. Kwa mujibu wa maelezo ya wataalamu wanasema kuwa hata mkojo wa Ng'ombe umekuwa ukitumika katika kazi ya kuua wadudu ambapo unavundikwa kwa siku 14 katika chombo maalum, baada ya hapo unachanganywa na majivu na kisha kupulizwa kwa siku saba katika mmea wa kahawa. Ni dawa nzuri ambayo inaua wadudu aina ya Vidung'ata na Vidugamba wakulima wanashauriwa sana kutumia njia hiyo na kuepukana na madawa ya viwandani ambayo yana kemikali kali ambazo hupoteza ladha ya tunda kahawa.

WAKULIMA WAKIPEWA MAFUNZO NAMNA YA UTUNZAJI BORA WA KAHAWA

Mtaalamu wa mimea na udongo kutoka kampuni ya Sustainable Harvest wilayani Moshi mkoa wa Kilimanjaro, Kaminyoge Mhamerd akiwafundisha baadhi ya wakulima wilayani Mbinga, Ruvuma mbinu bora za kupogolea miti ya kahawa.

WAKULIMA WA KIJIJI CHA UNANGO WANUFAIKA NA MAFUNZO YA KUTENGENEZA MBOLEA ZA ASILI

Wakulima wa kijiji cha Unango wilayani Mbinga, Ruvuma wakiwa mbele ya mbolea aina ya Biwi ambayo ni ya asili waliyoitengeneza kwa ajili shamba darasa kwa lengo la kuboresha mashamba yao ya kahawa. Utengenezaji wa mbolea hizo wamefanikiwa baada ya kupewa mafunzo na kampuni ya Sustainable Harvest ya kutoka makao makuu yake wilayani Moshi, mkoa wa Kilimanjaro.

WAKULIMA WA KAHAWA MBINGA WATAKIWA KUJENGA MAZOEA YA KUTUMIA DAWA NA MBOLEA ZA ASILI


Hao ni wanakikundi cha Bagamoyo ambao hujishughulisha na kilimo cha zao la kahawa wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakifuatilia kwa umakini mafunzo juu ya matumizi ya viuatilifu asilia, kutoka kwa mtaalamu wa mimea na udongo Kaminyoge Mhamerd wa pili kutoka kushoto.





Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.


MATUMIZI sahihi ya mbolea za asili katika uzalishaji wa zao la kahawa, imekuwa ikisaidia kwa kiasi kikubwa kuboresha na kuongeza uzalishaji wa zao hilo, hivyo wakulima wametakiwa kujenga mazoea ya kutumia mbolea hizo mashambani mwao.

Pia uzalishaji wa zao hilo, inashauriwa kutumia dawa za asili ambazo humfanya mkulima kuvuna kahawa yenye kiwango cha juu na yenye ubora unaokubalika katika soko la dunia.

Rai hiyo imetolewa na mtaalamu wa mimea na udongo Kaminyoge Mhamerd wa kampuni ya Sustainable Harvest, ya kutoka wilaya ya Moshi mkoani kilimanjaro, ambayo hujishughulisha na uboreshaji wa zao hilo.

Wednesday, January 16, 2013

IFAHAMU TAARIFA YA MAENDELEO MIAKA SABA MKOANI RUVUMA KUANZIA MWAKA 2005 HADI 2012


OFISI YA MKUU WA MKOA
RUVUMA

TAARIFA YA MKOA WA RUVUMA YA UTEKELEZAJI WA ILANI KATIKA KIPINDI CHA 2005 HADI 2012 KUPITIA VYOMBO VYA HABARI ILIYOTOLEWA NA MKUU WA MKOA SAID THABIT MWAMBUNGU MJINI SONGEA JUMAMOSI 05 JANUARI, 2013
 UTANGULIZI:

Ndugu Wananchi na Viongozi wenzangu wote wa Mkoa  wa RUVUMA.  Napenda kuwashukuru na kuwapongeza sana wana Habari kwa kukubali mwaliko wangu ambao unaniwezesha kupitia kwenu kuiwasilisha Taarifa ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi ya  Awamu ya Nne ya Utekelezaji wa ILANI na kwa jumla mafanikio ya Serikali katika kipindi cha Miaka SABA toka ilipoingia madarakani 2005 hadi 31 Desemba, 2012 kwa wananchi  wa Mkoa wetu.

Sote tunajua kuwa ni vigumu sana kuwa na fursa ama jukwaa lolote linaloweza kuwafikia Wana-RUVUMA wote kwa pamoja.  Lakini kwa kweli kupitia vyombo vyetu vya habari vya hapa  Mkoani  na vile vya Kitaifa  tunaweza kwa wigo mpana zaidi kuwafikia wananchi wengi zaidi kwa wakati mmoja. Baada ya taarifa hii ya Mkoa, kila Wilaya kupitia Mkuu wa Wilaya atatoa taarifa ya maendeleo ya wilaya yake ya kipindi hiki cha miaka saba ya Serikali ya Awamu ya Nne.

Naomba kwanza niseme kwa ujumla tu kuwa Mkoa wetu umefanikiwa sana kupiga hatua kubwa ya maendeleo kwa kila Sekta. Kwa kuutazama na kuupima Mkoa kwa vigezo vyote vya msingi vinavyotumika kupima kiwango cha maendeleo mtakubaliana na mimi kuwa tumepiga hatua ya kujivunia.  Hatujafika mbali lakini RUVUMA hii ya leo siyo ile ya mwaka 2005 au nyuma yake.  Kwa mfano pato la Mwana-Ruvuma limeongezeka toka shilingi 656,869 (2005) hadi shilingi 866,191 (2010) ambalo ni ongezeko la asilimia 31.9.  Ongezeko hili limetokana na jitihada kubwa za  pamoja za wananchi na Serikali yao kujiletea maendeleo.  Kwa mujibu wa Takwimu za  Ofisi ya Takwimu ya Taifa za mwaka 2010, Mkoa wetu ni wa sita Kitaifa kwa pato la mtu mmoja mmoja (GDP) tukitanguliwa na Mkoa wa Dar es Salaam, Iringa, Arusha, Mbeya na Kilimanjaro.

SEKTA YA KILIMO:
UZALISHAJI

Uzalishaji wa mazao mbalimbali ya chakula/nafaka umeongezeka toka tani 652,291 mwaka 2005 hadi tani 1,322,128 (2012) wakati ambapo uzalishaji wa mazao mbalimbali ya biashara umeongezeka toka tani 41,306 mwaka 2005 hadi tani 67,148 mwaka 2012.
Uhakika wa Usalama wa Chakula kuanzia ngazi ya kaya na Afya za wananchi zimeboreka zaidi.

UMWAGILIAJI:

Eneo la umwagiliaji limeongezeka toka hekta 4,500 zilizomwagiliwa kwa miundombinu ya asili mwaka 2005 hadi hekta 17,655 sasa (2012) ambao zinamwagiliwa kwa miundombinu ya kisasa na hivyo kuendesha uzalishaji wa kisasa.  Uzalishaji wa mazao ya chakula kupitia umwagiliaji wa kisasa umeongezeka toka tani 84,096 mwaka 2005 hadi tani 294,018 mwaka 2012.

PEMBEJEO:

Matumizi ya mbolea yameongezeka toka tani 12,500 mwaka 2005 hadi tani 26,557 mwaka 2012.

Vocha za pembejeo za kilimo zimeongezeka toka vocha 269,000 zenye thamani ya shilingi 8,791,400 mwaka 2005 hadi vocha  577,407 mwaka 2012 zenye thamani ya shilingi 13,087,892,000/=.

 USHIRIKA:
Vyama vya kuweka/kukopa (SACCOS) wanachama wake wameongezeka toka wanachama 22,762 mwaka 2005 hadi wanachama 56,047 mwaka 2012.
Mitaji yake imeongezeka toka shilingi 1,781,656,736 mwaka 2005 hadi kufikia shilingi 7,607,213,318 mwaka 2012.
Mikopo inayotolewa imeongezeka toka shilingi 1,831,150,835 mwaka 2005 hadi 12,244,968,443/=.

UVUVI:

Idadi ya wafugaji wa samaki imeongezeka toka wafugaji 2,134 mwaka 2005 hadi wafugaji 3,547 mwaka 2012.

Mavuno ya samaki toka ziwa Nyasa yameongezeka toka tani 1108.78 zenye thamani ya shilingi 704,590,213 mwaka 2005 hadi tani 6,709.12 zenye thamani ya shilingi 5,439,239,792 mwaka 2012.

Idadi ya mabwawa ya kuzalisha vifaranga vya samaki  yameongezeka toka moja tu mwaka 2005 hadi vituo  vitatu vya uzalishaji wa vifaranga mwaka 2012.

URINAJI ASALI:
Tumeanzisha karibu kila wilaya ufugaji wa nyuki  kwa ajili ya upatikanaji wa asali ili kukuza kipato cha wananchi na kuboresha afya. Idadi ya mizinga imeongezeka kutoka 1,200 (2005) hadi 3,000 (2012).  Tumeamua kujiimarisha zaidi kwenye biashara hii yenye tija tena kwa gharama nafuu.
ZANA ZA KILIMO BORA:

Matrekta makubwa ya kilimo yameongezeka toka matrekta 48 mwaka 2005 hadi 151 mwaka 2012 baada ya ongezeko la matrekta mapya 103 mwaka ( jana) 2012

CHANGAMOTO:

Changamoto zinazoikabili Sekta hii ya kilimo ni nyingi hasa zinazohusu masoko ya mazao ya wakulima na hususani zao la Tumbaku, Korosho na Kahawa, ambalo Serikali inaendelea na jitihada za kukabili kikamilifu ili mazao haya yatoe tija kwa mkulima.

UCHAMBUZI WA UZALISHAJI WA ZAO MOJA MOJA:

Uzalishaji wa mazao ya biashara 2005/2006 – 2001/2012
Mazao ya biashara
2005/2006
2011/2012


Hekta
Tani
Hekta
Tani

Tumbaku
10,890
5,383
9,210
5,898

Kahawa
36,356
8,135
36,922
7,546

Korosho
29,073
10,406
23,783
6,939

Alizeti
3,406
2,178
3,644
3,207

Ufuta
8,366
4,142
16,691
14,271

Karanga
17,324
10,493
21,732
20,871

Soya
809
569
5,197
4,196 
Mengine
-
-
1,605
4,220

Jumla
106,224
41,306
118,784
67,148

           Mwenendo wa uzalishaji wa mazao ya chakula 2005/206    – 2011/2012:

Mazao ya biashara
2005/2006
2011/2012


Hekta
Tani
Hekta
Tani

Mahindi
140,764
281,594
193,253
535,653

Mpunga
55,373
101,503
93,854
254,726 
Maharage
26,015
21,172
35,174
34,260

Muhogo
95,298
170,269
119,852
338,654

Viazi Vitamu
16,983
54,887
27,065
108,649

Ulezi
12,113
8,632
13588
10,841

Kunde
16,732
13,232
10,448
9,877

Mtama
961
1,002
2,319
2,432

Mengine
-
-
5,198
27,036

Jumla
364,239
652,291
500,751
1,322,128 

SEKTA YA ELIMU:
ELIMU YA AWALI

Madarasa ya Elimu ya Awali yameongezeka toka madarasa 554 mwaka 2005 hadi madarasa 730 mwaka 2012 sawa na ongezeko la asilimia 24.

Uandikishaji wa wanafunzi wa awali umeongezeka toka watoto 33,014 mwaka 2005 hadi watoto 40,183 mwaka 2012 sawa na asilimia 18.

Walimu wa Elimu ya Awali wameongezeka toka 222 mwaka 2005 hadi 571 mwaka 2012 sawa na asilimia 61.

ELIMU YA MSINGI
Shule za msingi zimeongezeka toka 663 mwaka 2005 hadi 745 mwaka 2012 sawa na asilimia 11.

Nyumba za walimu zimeongezeka toka  1,914 mwaka 2005 hadi nyumba 2,570 mwaka 2012 sawa na asilimia 26.
Tumeongeza ujenzi wa madarasa toka 3,995 mwaka 2005 hadi 5,194 mwaka 2012 kati ya mahitaji yetu halisi ya madarasa 7,763.  Ongezeko hilo la madarasa ni asilimia 26.

Uandikishaji wa wanafunzi umeongezeka toka 41,519 mwaka 2005 hadi 55,928 mwaka 2012 sawa  na asilimia 26.

Walimu wameongezeka toka 5,561 mwaka 2005 hadi walimu 6,830 mwaka 2012 sawa na ongezeko la asilimia 19.  Mahitaji yetu ya walimu wote Kimkoa ni 7,766.

Idadi ya wanafunzi wanaofaulu imeongezeka toka wanafunzi 13,256 mwaka 2005 hadi wanafunzi 16,578 mwaka 2012 sawa na ongezeko la asilimia 20.

Hali ya utoro wa wanafunzi imepungua toka watoto 382 mwaka 2005 hadi watoro 200 mwaka 2012, upungufu huu ni asilimia 48.

Mimba za shuleni Elimu ya Msingi zimepungua toka 274 mwaka 2005 hadi mimba 47 mwaka 2012.

ELIMU YA SEKONDARI

Idadi ya Shule za Sekondari zimeongezeka toka 68 mwaka 2005 hadi shule 179 mwaka 2012 sawa na ongezeko la asilimia 62.

Idadi ya Shule za Sekondari za “A-Level” (Kidato cha V na VI) zimeongezeka toka shule 8 mwaka 2005 hadi 20 mwaka 2012 sawa na ongezeko la asilimia 60.

Idadi ya wanafunzi waliojiunga kidato cha kwanza 2005 walikuwa 6,739 na kuongezeka hadi 12,823 mwaka 2012 sawa na ongezeko la asilimia 47.

Idadi ya walimu imeongezeka toka 581 mwaka 2005 hadi walimu 1,845 mwaka 2012.

Walimu wa masomo ya Sayansi wameongezeka toka walimu 175 mwaka 2005 hadi 366 mwaka 2012.

Nyumba za walimu zimeongezeka toka 225 mwaka 2005 hadi 482 mwaka 2012 sawa na ongezeko la asilimia 53.

Vyumba vya madarasa vimeongezeka toka 333 mwaka 2005 hadi 1,131 mwaka 2012.

Shule zilizokuwa na Maabara ya Sayansi zimeongezeka toka 24 mwaka 2005 hadi  43 mwaka 2012.

Utoro usio wa mimba umepungua toka 97 mwaka 2005 hadi 32 mwaka 2012.

Mimba zimeongezeka toka 37 mwaka 2005 hadi 167 mwaka 2012.

SEKTA YA MAJI:

MAJI VIJIJINI
Kiwango cha upatikanaji wa huduma ya Maji Vijijini imeongezeka toka asilimia 52.5 mwaka 2005 hadi asilimia 61 mwaka 2012.

Miradi inayotumia Bomba Vijijini imeongezeka toka mabomba 515 mwaka 2005  hadi 613 mwaka 2012.

Visima vya pampu ya mkono vimeongezeka toka 1,372 mwaka 2015 hadi 1,680 mwaka 2012.

Kamati za maji vijijini vimeongezeka toka 529 mwaka 2005 hadi 637 mwaka 2012.

Mifuko ya Maji imeongezeka toka 219 mwaka 2005 hadi 309 mwaka 2012

MAJI MIJINI (Songea, Mbinga Tunduru na Namtumbo)

Wakazi wa Mijini wanaopata huduma ya maji safi na salama wameongezeka toka 108,167 mwaka 2005 hadi 149,422 mwaka 2012 sawa na asilimia 68.8.

Mtambo wa mabomba ya maji mjini umeongezeka toka kilometa 109.6 mwaka 2005 hadi kilometa 368.1 mwaka 2012.

Mtandao wa bomba la kuondoa maji taka mjini Songea imeongezeka toka 0 mwaka 2005 hadi kilomita 37 mwaka 2012.

SEKTA YA ARDHI/MIUNDOMBINU:
ARDHI
Mkoa umepima viwanja 50,109 mwaka 2012 ikilinganishwa na viwanja 32,750 mwaka 2005.

Mashamba yaliyopimwa yameongezeka toka hekta 8,136.6 mwaka 2005 hadi 16,972.753 mwaka 2012.
Vijiji vilivyopimwa vimeongezeka toka vijiji 387 mwaka 2005 hadi vijiji 401 mwaka 2012.

Vijiji vyenye vyeti vya ardhí ya kijiji vimeongezeka toka 5 mwaka 2005 hadi 164 mwaka 2012.

Vijiji vilivyoandaliwa kwa matumizi bora ya Ardhi vimeongezeka toka 36 mwaka 2005 hadi 101 mwaka 2012.

Hati miliki za kimila zilizoandaliwa zimefikia 6,548 (2012).

BARABARA
Juhudi za wazi za Serikali zinaonekana za kuufungua Mkoa wetu kwa barabara za lami kupitia barabara zote kuu zinazoingia Mkoa wetu.  Uwezo wa sasa wa kuingia Mkoa wa RUVUMA ni mkubwa na wa uhakika ikilinganishwa na ilivyokuwa mwaka 2005.

Mtandao wa barabara za lami kwa Mkoa wa RUVUMA utafikia asilimia 8.6 toka asilimia 4 (2005) baada ya miradi mikubwa yote ya barabara itakapokamilika kuanzia mwezi Juni 2013 mwaka huu.

Barabara pekee ya lami mwaka 2005 iliyokuwepo ni ile ya Njombe Songea na sehemu ndogo ya Songea Likuyufusi Peramiho.

Barabara za lami za sasa  kimkoa zina urefu wa Km.223.4 ambapo Km.207.84 zinahudumiwa na TANROADS wakati kilometa 15.2 ni Manispaa ya Songea  na za Mji wa Mbinga.

Barabara kuu zinazoendelea kujengwa kwa lami hadi sasa ni:
Barabara ya Songea – Namtumbo    - Km.  67
Barabara ya Namtumbo – Tunduru -Km.193
Barabara ya Tunduru – Mangaka - Km.139
Barabara ya Peramiho – Mbinga -     Km.  78
Barabara ya Mbinga – Mbamba-bay- Km.   64

Barabara ambazo zipo kwenye mchakato wa hatua mbalimbali ya  kuandaliwa kujengwa kwa kiwango  cha lami ni pamoja na
Likuyufusi – Mkenda - (Km.124)
Lumecha, Kitanda, Londo – Kilosa kwa Mpepo (Morogoro)
Mbamba-bay – Liuli – Lituhi – Luanda -  Kitai.

USAFIRI WA ANGA
Mkoa unafikika kwa uhakika kwa usafiri wa ndege kwa kutumia  uwanja wa ndege wa Songea.

Huduma  za ndege  kupitia Shirika la Ndege la AURICK  AIR unapatikana kila siku isipokuwa Jumapili.

Mawasiliano ya simu za kiganjani
Huduma za simu ya viganjani zimepanuka sana hata kufikia vijiji vingi ikilinganishwa na mwaka 2005.

SEKTA YA AFYA:
Mkoa umefanikiwa katika kutoa huduma za afya kwani kwa mwaka 2005 ulikuwa na jumla ya vituo vya kutolea huduma za Afya 210 ambapo kwa mwaka 2012 vimeongezeka hadi kufikia vituo 272.
Hospitali za Serikali zipo tatu (3) hadi mwaka 2012.
Vituo vya afya vimeongezeka kutoka 16 mwaka 2005 hadi 19 mwaka 2012.
Zahanati zimeongezeka kutoka 132 mwaka 2005 hadi 197 mwaka 2012.

Hali ya Vifo vya Wajawazito:
Mkoa umefanikiwa kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi kutoka 65 mwaka 2005 hadi 41 mwaka 2012 kwa kila watoto 100,000.

Vifo vya watoto chini ya miaka 5 vimepungua kutoka 57 mwaka 2005 hadi 9 mwaka 2012 kwa kila watoto 1,000 waliozaliwa hai.

Vifo vya watoto wa umri wa mwaka 1 – 5 vimepungua kutoka 128 mwaka 2005 hadi 17 mwaka 2012 kwa kila watoto 1,000 waliozaliwa hai.

SEKTA YA UTAWALA BORA:
Katika kipindi cha Serikali ya Awamu Nne (2005 – 2012), Utawala Bora umeimarika Mkoani Ruvuma kwani nguzo na misingi mikuu inayojenga mfumo huu umezingatiwa kwa ukamilifu.  Misingi hiyo ni Demokrasia, Ushirikishwaji wa wananchi, Utawala wa Sheria, Utoaji wa Haki kwa watu wote, Uwazi, Uwajibikaji, Uadilifu, Uzingatiaji wa Masuala ya Jinsia.

Kanuni hizi za Utawala Bora zimezingatiwa katika ngazi zote za uongozi na utawala katika Mkoa, yaani Serikali Kuu, Mamlaka za Serikali za Mitaa (Halmashauri), Taasisi za Sekta Binafsi na Asasi za Kiraia.  Kwa muhtasari hali halisi ya utekelezaji wa vigezo hivyo ni kama ifuatavyo:

Demokrasia:
Kuongezeka kwa majimbo ya uchaguzi:
Mkoa ulikuwa na majimbo 6 ya uchaguzi kama ifuatavyo: (Mbinga 2, Tunduru 1, Namtumbo 1, Songea (2) mwaka 2005  hadi majimbo 7 mwaka 2012.

Kuongezeka kwa maeneo ya Utawala
Mkoa ulikuwa na wilaya 4 ambazo ni Tunduru, Namtumbo, Songea na Mbinga mwaka 2005 hadi 5 baada ya wilaya mpya ya Nyasa kuanzishwa mwaka 2012.

Halmashauri:
Mkoa ulikuwa na Halmashauri 4 za wilaya na Halmashauri 1 ya Manispaa mwaka 2005. Mkoa unatarajiwa kuwa na Halmashauri 6 muda wowote kuanzia sasa.

Tarafa
Mkoa ulikuwa na Tarafa 21 mwaka 2005 hadi 24 mwaka 2012 (Tarafa mpya za Kigonsera, Mkumbi na Hagati) kuanzishwa
Kata
Kulikuwa na Kata 100 mwaka 2005 hadi Kata 140 mwaka 2012.
Vijiji
Kulikuwa na Vijiji 476 mwaka 2005 hadi Vijiji 508 mwaka 2012.

Ushirikishwaji wa Wananchi
Ongezeko la ufanisi wa ufanyikaji wa mikutano ya kisheria katika ngazi ya Halmashauri, Kata, Mitaa, Vijiji na Vitongoji umeongezeka kutoka asilimia 65 mwaka 2005 hadi asilimia 98 mwaka 2012.

Ongezeko la wastani wa mahudhurio ya wananchi katika mikutano ya kisheria asilimia 50 mwaka 2005 hadi asilimia 80 mwaka 2012.

Ongezeko la idadi ya asasi zisizo za kiserikali.  Kulikuwa na asasi 126 mwaka 2005 hadi asasi 961 mwaka 2012.
NISHATI YA UMEME:
Mkoa wa RUVUMA kwa sasa una huduma ya Nishati ya Umeme kwa Makao Makuu ya Wilaya za Songea, Mbinga na Tunduru wakati Makao Makuu ya Wilaya ya Namtumbo umeme utaanza kuwake mapema mwezi ujao (Februari) kufuatia kukamilika kwa kazi ya ujenzi wa kituo cha uzalishaji wa meme na utandazaji wa nguzo na nyaya.

Wilaya mpya ya Nyasa, hatua za awali za kitaalamu zimekamilika na kwamba kwa sasa kinachoendelea ni upatikanaji wa fedha ili kukamilisha uzalishaji wa umeme huo wa kilowati mia tatu (300) kwa ajili ya Makao Makuu ya wilaya hiyo mpya mjini Mbamba-bay.

Mwaka 2005 mji pekee uliokuwa na umeme ulikuwa ni Songea tu, Makao Makuu ya Mkoa.

UWEKEZAJI:
Mkoa una miradi mikubwa miwili ya uwekezaji katika madini.  Mradi wa Makaa ya Mawe wilayani Mbinga kata ya Luanda kijiji cha Mtunduwalo, makaa ambayo pamoja na mengine yanatarajiwa kuzalisha umeme wa megawati 400 ambazo ni muhimu sana kwa Taifa kwani utaongeza  vya kutosha uwezo wa gridi ya Taifa na kukuza sana uchumi wa Mkoa wetu.  Kazi ya uzalishaji wa Makaa hayo imekwishaanza ambapo miongoni mwa wateja wakubwa kwa sasa wa makaa hayo ni pamoja na jirani zetu Malawi, kiwanda cha saruji cha Mbeya na kile cha Tanga.

Mradi mwingine mkubwa wa madini ni wa uchimbaji wa madini ya URANIUM ambao upo wilayani Namtumbo na ambao hatua zote muhimu zinazohitajika kisheria katika kuuwezesha kuanza zipo katika hatua ya mwisho tayari kuanza kwa mradi huu mkubwa na muhimu kwa uchumi wa nchi yetu na Mkoa wetu.
Ipo pia miradi mingine mikubwa ya kilimo kikubwa cha zao la kahawa katika shamba kubwa la Lipokela wilaya ya Songea Vijijini, licha ya kukuza kilimo cha kahawa Mkoani kwetu lakini pia linasaidia sana ajira kwa wananchi wetu.

CHANGAMOTO:
Kama nilivyoeleza hapo awali katika utangulizi wa taarifa hii kuwa mafanikio yetu haya mbalimbali katika kusukuma maendeleo ya Mkoa inaambatana na changamoto mbalimbali karibu katika kila sekta ambazo hata hivyo Serikali ya Mkoa kwa kushirikiana na wananchi na wadau wetu wa maendeleo tunazikabili hatua kwa hatua.

Changamoto zitokanazo na ufinyu wa bajeti yetu kimkoa na zile za Halmashauri zetu.  Wigo mdogo wa makusanyo yake ya ndani ya Halmashauri zetu yaani “OWN SOURCE”.  Changamoto ya mwamko mdogo juu ya umuhimu wa Elimu kwa watoto wetu walionao wananchi wengi hasa vijijini.  Changamoto ya kuongezeka kwa kukatisha masomo kwa wanafunzi wa kike kutokana na mimba na hususan wanafunzi wa sekondari na nyingine za aina hii.

Hatua mbalimbali tunazichukua kukabili changamoto hizo.  Kwa mfano katika kukabili mimba mashuleni tumeanzisha kampeni maalum yenye kauli mbiu “ZUIA MIMBA KABLA YA KUINGIA”  yenye nia ya kumnusuru mtoto wa kike kwa kuwabana wanaume waliokubuhu kwa uhalifu huu wa kukatiza masomo ya binti zetu kwa kuwapa mimba.

Chini ya kampeni yetu hii ya “ZUIA MIMBA KABLA YA KUIINGIA”, tunampa zawadi ya shilingi 20,000/= mtu yeyote atakayetuwezesha kumkamata mwanaume mwenye nyendo za waziwazi za kutaka kufanya mapenzi/ngono na binti mwanafunzi na kumfikisha Polisi na Mahakamani kwa kosa la kutaka kukatiza maisha ya elimu ya binti huyo.

MWISHO:
Mafanikio yetu ni mengi mno ambayo siyo rahisi kuyaorodhesha yote katika kila Sekta lakini haya tuliyoyaorodhesha yatosha kuonyesha ari yetu kubwa kama Mkoa kuendelea kujiletea maendeleo kila mwaka kwenda mbele zaidi kuliko mwaka uliopita.


SAID THABIT MWAMBUNGU
MKUU WA MKOA
RUVUMA.


Monday, January 14, 2013

WALEMAVU MBINGA WAPATIWA MAFUNZO YA KUANZISHA NA KUENDESHA BIASHARA KWA MAFANIKIO PAMOJA NA MPANGO MKAKATI

Baadhi ya washiriki wa mafunzo ya siku tano yanayohusu Kuanzisha na kuendesha biashara kwa mafanikio pamoja na mpango mkakati, wakifuatilia leo kwa umakini mada ambazo zilikuwa zikitolewa na mkufunzi wa kutoka Chemba ya wafanyabiashara na wenye viwanda(TCCIA) tawi la wilaya ya Mbinga mkoa wa Ruvuma, Philomen Msigwa, (hayupo pichani). Walioshiriki mafunzo hayo ni walemavu wa makundi mbalimbali wanaoishi wilayani humo.(Picha na Kassian Nyandindi)

Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

 

JAMII imetakiwa kuondokana na dhana potofu ambayo imejengeka miongoni mwao kwamba, watu walio katika kundi lenye ulemavu ni mzigo na hawezi kufanya shughuli za kimaendeleo katika jamii.


Kauli hiyo ilitolewa leo na ofisa mtendaji wa Chemba ya wafanyabiashara na wenye viwanda(TCCIA) tawi la wilaya ya Mbinga, Philomen Msigwa kwenye ukumbi wa UVIKITWE uliopo Mbinga mjini mkoani Ruvuma, katika mafunzo ya siku tano ya kuwawezesha baadhi ya walemavu wa wilaya hiyo kuanzisha na kuendesha biashara kwa mafanikio kwa kuzingatia mpango mkakati.


Msigwa alisema jamii inafanya makosa kuwadharau watu wenye hali hiyo, huku wengine wakifikia hatua ya hata kuwaficha ndani ya majumba yao.