Monday, December 23, 2013

UJENZI WA BARABARA KIWANGO CHA LAMI SONGEA HADI MBINGA UTATA MTUPU

Na Kassian Nyandindi,
Songea.
 
UJENZI wa barabara kiwango cha lami kuanzia eneo la Likuyufusi pacha ya Peramiho wilaya ya Songea hadi Mbinga, umeanza kuzua malalamiko kutokana na barabara hiyo kuanza kuwekwa viraka kabla ya kukabidhiwa rasmi mikononi mwa serikali.
 
Barabara hiyo ambayo ni ya kilometa 78 inagharimu kiasi cha shilingi bilioni 79.8 na kutekelezwa chini ya mradi mkuu wa changamoto za milenia Tanzania (MCAT).
 
Fedha za ujenzi wa barabara hiyo ni miongoni mwa dola 698 za Kimarekani zilizotolewa nyakati za mwisho katika utawala wa Rais mstaafu George Bush, ikiwa ni sehemu ya msaada kwa ajili ya kujenga miradi mbalimbali ya kimaendeleo hapa nchini.
 
Malalamiko hayo yalitolewa kwa nyakati tofauti wakati mwandishi wa habari hizi alipokuwa akizungumza na wananchi wa Songea na Mbinga, ambapo walisema kuwa ni jambo la kushangaza kuona ujenzi wa barabara hiyo kabla haijakabidhiwa rasmi imeanza kuwekwa viraka baadhi ya maeneo.

Sunday, December 22, 2013

TAMCU TUNDURU WALIA NA TAKWIMU ZA KOROSHO



Na Steven Augustino,

Tunduru.

CHAMA kikuu cha ushirika Wakulima wa korosho wilaya ya Tunduru (TAMCU) mkoani Ruvuma, kimefanikiwa kukusanya tani  554 ambazo ni kidogo, kati ya tani 9115 zilizokadiriwa kuzalishwa katika msimu wa mwaka huu.

Hayo yalisemwa na Katibu mkuu wa chama hicho wilayani humo, Imani Kalembo akiwemo na Mwenyekiti wake Mahamudu Katomondo mbele ya waandishi wa habari, waliokuwa wakifanya mahojiano nao mjini hapa juu ya maendeleo ya uzalishaji wa zao hilo.

Viongozi hao walifafanua kwamba wamepata wakati mgumu kukusanya takwimu hizo za uzalishaji, kwa kile walichoeleza kuwa kutokana na wilaya hiyo kuwa na utaratibu mbovu uliotumika kununulia zao hilo katika msimu wa mwaka huu.

"Takwimu tulizowapeni ni zile ambazo tu zimetokana na manunuzi yaliyofanywa na TAMCU kupitia vyama 18 vya ushirika vya wakulima ambavyo vipo katika tarafa za Lukumbule, Namasakata, Nalasi, Matemanga, Mlingoti Nakapanya na Namtumbo ambako chama kilipeleka fedha kwa ajili ya ununuzi wa Korosho", alisema Kalembo.

MAHAKAMA KUTOA MAAMUZI JUU YA MAUZO MBAO ZILIZOKAMATWA KATIKA OPARESHENI TOKOMEZA UJANGILI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

MAHAKAMA ya wilaya Tunduru mkoani Ruvuma, imepanga kutoa maamuzi ya kuuza au kutouzwa kwa mbao 8,328 zenye thamani ya shilingi milioni 291.4 ambazo zilikamatwa kupitia “Oparesheni tokomeza ujangili”, iliyofanyika hivi karibuni kuanzia Oktoba hadi Desemba mwaka huu.

Hakimu mfawidhi wa Mahakama hiyo Ernest Mgongolo alisema hayo wakati alipokuwa akijibu, maombi yaliyotolewa na Mawakili waliokuwa wakiwakilisha upande wa serikali katika kesi tano zinazowakabili watuhumiwa saba ambao walinaswa wakati wa oparesheni hiyo wakiwa na na mbao hizo kinyume cha sheria.

Watuhumiwa hao ni wakazi wa Jijini Dar es Salaam na Mtwara  ambapo awali wakitoa maombi, Wanasheri  wa serikali  Mwahija Sembeni na Francis Aloyce waliiomba Mahakama kwa mamlaka iliyonayo kutumia kifungu cha sheria namba 352 kifungu kidogo (2) kinacho ambacho huruhusu kutoa kibali cha kuuzwa kwa kidhibiti chochote au mali ambayo ipo mbele ya mahakama na yenye kuweza kuharibika.

Wednesday, December 18, 2013

MKUU WA MKOA WA RUVUMA ALIA NA WAKUGURUGENZI WA HALMASHAURI KUWAPA KAZI WAKANDARASI WAZEMBE

Na Muhidin Amri,

Ruvuma.

SERIKALI mkoani Ruvuma imewaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri  za wilaya katika mkoa huo, kutowapa tena zabuni Wakandarasi ambao ni wababaishaji, wazembe na wenye rekodi mbaya katika utendaji wa kazi zao, ili wasiweze kuisababishia serikali hasara ya kuingia gharama nyingine upya ya ujenzi wa miradi ya Wananchi.

Mkuu wa mkoa huo Said Mwambungu aliyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati akifungua kikao cha siku moja cha Wajumbe wa jumuiya ya serikali za mitaa(ALAT) kilichofanyika mjini Namtumbo mkoani humo, ambapo alitumia nafasi hiyo kupiga marufuku wakandarasi wasiokuwa na sifa kuomba na kufanya kazi katika mkoa wa Ruvuma kwani wamekuwa wakiurudisha nyuma maendeleo ya taifa letu kwa ujumla.

Mwambungu amesikitishwa na usimamizi mbovu wa fedha zinazotolewa na serikali wakati wa utekelezaji wa miradi mbalimbali, ambapo imebainika kuwa wakandarasi wengi wamekuwa na tabia ya wizi kwa kuingia mikataba hewa na halmashauri husika na wakishapata fedha hukimbia bila kukamilisha kazi walizoomba kufanya, tatizo ambalo alidai kuwa linachangiwa kwa kiasi fulani na baadhi ya watumishi hasa wakuu wa idara wasiokuwa waaminifu.

Alisema ni kosa kumpa kazi Mkandarasi mwenye rekodi mbaya huku akiwaonya Wakurugenzi na Wenyeviti wa Halmashauri  juu ya tabia ya kuwa na urafiki wa jirani na wakandarasi hao kwa kile alichoeleza kuwa kinatokana na tamaa ya fedha huku akisisitiza ni vema  kutoa kipaumbele kwa wakandarasi waaminifu  na wenye sifa ambao wanatimiza majukumu yao ya kazi kwa viwango vinavyotakiwa.

AURIC AIR YAJIVUNIA MAFANIKIO YAKE MKOANI RUVUMA

















Na Mwandishi wetu,
Songea.

WAKAZI wa mkoa wa Ruvuma wameombwa  kuunga mkono juhudi mbalimbali za wawekezaji wanaokwenda kuwekeza katika mkoa huo, badala ya kubeza kwani hali hiyo inaweza kuwakatisha tamaa wawekezaji hao na hatari ya kubaki watazamaji  na  mabingwa  wa kusifia maendeleo yaliyopo kwenye mikoa mingine.

Wito huo umetolewa mjini Songea na mfanyabiashara   Abbas Hemani wakati akizungumza na Mwandishi wetu, kuhusu fursa nyingi za uwekezaji zilizopo katika mkoa wa Ruvuma na kuongeza kuwa iwapo wakazi wa mkoa huo hawataunga mkono juhudi hizo basi mkoa huo,   utabaki na umasikini licha ya kuwepo kwa fursa na rasilimali nyingi.

Abbas ambaye  ni wakala wa shirika la ndege la AURIC AIR ambalo ndege zake hufanya safari kati ya Dar es slaam na Songea mkoani humo, amewaomba wakazi wa mkoa huo hususani wafanyabiahara kutumia usafiri wa ndege za kampu8ni hiyo, ili kumuunga mkono katika jitihada zake  za kutaka mkoa wa Ruvuma unakuwa miongoni mwa mikoa  yenye usafiri wa uhakika  na kusaidia kuleta maendeleo.

Alisema lengo la kuanzisha usafiri huo wa ndege ni  kuisaidia serikali katika kuboresha baadhi ya huduma ambazo yenyewe ilishajitoa, hivyo kutoa nafasi kwa wananchi wenye uwezo  waweze kuwekeza katika maeneo mbalimbali kwa lengo la kuwahudumia  wananchi.

Tuesday, December 17, 2013

KADA WA CHAMA CHA MAPINDUZI AFARIKI DUNIA KWA KUJINYONGA


















Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KADA mmoja wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambaye ni mkazi wa kitongoji cha Lulambo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, amekutwa akiwa amefariki dunia baada ya kujinyonga katika msitu uliopo jirani na kitongoji hicho.

Tukio hilo ambalo limetokea hivi karibuni, imethibitishwa kuwa Kada huyo ambaye ni Gisberth Haulle (45) alikuwa Mwenyekiti wa tawi la Ngamanga kupitia tiketi ya CCM ambalo lipo katika kitongoji hicho.  

Kwa mujibu wa maelezo ya Mwenyekiti wa kitongoji cha Lulambo, Gisberth Ndimbo alisema chanzo cha tukio hilo inadaiwa kuwa marehemu huyo alifikia uamuzi wa kujinyonga kutokana na ugomvi ambao ulidumu kwa muda mrefu katika familia yao.

TUNDURU WAWEKA MIKAKATI YA KUKABILIANA NA NJAA, SHERIA KUUNDWA KUWABANA WAZEMBE



Steven Augustino,
Tunduru.

SERIKALI wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, imeweka mkakati wa kuhakikisha kuwa kila kaya inakuwa na chakula cha kutosha wilayani humo ili kuweza kuepukana na baa la njaa ambalo linaweza kutokea hapo baadaye.

Mikakati hiyo inaenda sambamba kwa kuanza kuwapeleka Mahakamani  watu wote, ambao hawatakuwa na mashamba ya kuzalisha mazao ya chakula katika msimu wa mvua wa mwaka huu na kuendelea.

Chande Nalicho ambaye ni Mkuu wa wilaya hiyo, ndiye aliyetangaza msimamo huo wa serikali na kuitaka jamii ya wanatunduru kuhakikisha suala hilo linatekelezwa mara moja.

Kadhalika serikali itafanya mzunguko kwa kupita kutoa elimu kwa wananchi wote wilayani Tunduru, na kwamba kesi za wavivu zichukuliwe hatua kwa walengwa wanaoshinda vijiweni ikiwemo kufungwa.

Msimamo huo ulitangazwa na mkuu huyo wa wilaya, wakati alipokuwa akizungumza katika mdahalo wa uzinduzi wa kampeni ya kutokomeza njaa duniani uliofanyika katika ukumbi wa Sky way, uliopo mjini hapa.

ABIRIA TUNDURU WALALAMIKIA KUNYANYASWA, SUMTRA YAOMBWA KUINGILIA KATI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

WADAU na Abiria ambao hufanya safari zao kutoka wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, kwenda jijini Dar es Salaam wamelalamikia kutozwa nauli za mabegi jambo ambalo linasababisha usumbufu mkubwa kwao.

Sambamba na tukio hilo pia wasafiri hao walidai kuwa wamekuwa wakitukanwa na kutolewa lugha chafu na wafanyakazi wa mabasi ambayo hufanya safari katika ukanda huo wa kusini.

Kilio cha wasafiri hao kiliwasilishwa na Leonsi Kimario wakati akizungumza na maafisa wa Mamlaka ya udhibiti wa usafiri wa nchi kavu na majini (SUMATRA) katika kikao kilichofanyika ukumbi wa New Generation bar uliopo mjini hapa.
   
Kimario ambaye alionekana kuungwa mkono na wajumbe wengi waliohudhuria mkutano huo, alisema abiria hao wamekuwa wakitozwa fedha  kati ya shilingi 10,000 na 5,000 kama malipo ya nauli ya mabegi yao hali ambayo imekuwa ikiwakwaza abiria wengi ambao hufanya safari zao kutoka katika maeneo hayo.

Wednesday, December 11, 2013

VYAMA VYA KUWEKA NA KUKOPA VYATAKIWA KUTOA TAARIFA SAHIHI KWA WANACHAMA WAKE



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

VIONGOZI wa Chama cha kuweka na kukopa (SACCOS) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wametakiwa kujenga ukweli na uwazi katika utendaji wa kazi zao za chama, na sio kutoa taarifa zisizo sahihi kwa wanachama ambazo baadaye zinaweza kusababisha migogoro isiyokuwa ya lazima.

Aidha wametakiwa kutuoa ushirikiano wa kutosha kwa Mamlaka husika ambayo inasimamia vyama vya ushirika, kufanya ukaguzi na kutoa hali halisi ya mwenendo wa chama kwa wanachama, ili waweze kuwa na uhakika wa usalama wa mali zao.

Rai hiyo ilitolewa na Ofisa elimu Msingi wilaya ya Mbinga, Mathias Mkali alipokuwa mgeni rasmi kwenye mkutano mkuu wa chama cha kuweka na kukopa cha Mbinga Kurugenzi SACCOS, uliofanyika kwenye ukumbi wa Jimbo la Mbinga uliopo mjini hapa.

Vilevile aliwashauri wanachama wa umoja huo, wahakikishe kuwa wanarejesha mikopo waliyokopa kwa wakati ili chama kiweze kusonga mbele.

“Napenda niwashauri, tujenge tabia ya kurejesha mikopo tunayokopa kwa wakati uliopangwa na tukifanya hivyo chama hiki kitakuwa na mzunguko mzuri kifedha, pia ili tuweze kufanikiwa jambo hili elimu ya ushirika itolewe kwa wanachama”, alisema Mkali.

Tuesday, December 10, 2013

NGAGA ALIA NA KATIBU WA CWT, AMSHUKIA ASEMA NI KIKWAZO CHA MAENDELEO YA ELIMU WILAYANI MBINGA

Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga akitoa msisitizo wake mbele ya Wadau wa elimu wa wilaya hiyo(Hawapo pichani) katika ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa, juu ya Katibu wa CWT wilaya humo kuwa ni kikwazo cha maendeleo ya elimu. 


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga amemshukia Katibu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) tawi la Mbinga Samwel Mhaiki, akidai kwamba ni kikwazo cha maendeleo ya elimu wilayani humo, kutokana na katibu huyo kupenda kuendesha migogoro na kuchonganisha walimu mashuleni.

Ngaga alisema hayo alipokuwa akizungumza na Wadau wa elimu, Kata ya Mbinga mjini juu ya kukuza maendeleo ya sekta ya elimu wilayani humo, katika hafla fupi iliyofanyika ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa.

Alisema kuwa katibu huyo amekuwa kinara namba moja wa kupita mashuleni na kushinikiza walimu waache kufundisha (Wagome) hadi watakapolipwa madai yao, jambo ambalo alilieleza kuwa limekuwa likileta mgogoro usio na tija katika jamii.

Alieleza kwamba licha ya Mhaiki kuitwa mara nyingi ofisini kwake na kumtaka aache kuendeleza migogoro hiyo, anashangaa kumuona bado akiifanya.

Thursday, December 5, 2013

KUKOSEKANA KWA SHULE MAALUM YA WALEMAVU WILAYANI MBINGA KUNASABABISHA WALEMAVU KUKOSA HAKI ZAO ZA MSINGI

Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga (upande wa kulia) akizungumza na wananchi na watu wenye ulemavu katika kijiji cha Luhagara kata ya Litumbandyosi wilayani humo, katika maadhimisho ya sherehe za siku ya walemavu.

Kutoka kushoto Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Allanus Ngahy, katikati ni Diwani wa kata ya Litumbandyosi James Yaparama na upande wa kulia ni Mkuu wa wilaya hiyo Ngaga, akiweka sahihi katika kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika uwanja wa maadhimisho ya sherehe hizo kijiji cha Luhagara. (Picha zote na Kassian Nyandindi)

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa kukosekana kwa shule maalum kwa watu wenye ulemavu wa aina mbalimbali wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kunasababisha watu hao kukosa haki zao za msingi za kupata elimu, ambayo ingelifanya kundi hilo, kuweza kuondokana na maadui wawili ujinga na umasikini.

Kutokana na ukosefu huo baadhi yao kutoka katika familia zenye uwezo mkubwa hulazimika kwenda kusoma mikoa mingine ambayo ipo mbali kwa kutumia gharama kubwa, hivyo serikali imeombwa kunusuru hali hiyo kwa kujenga shule ya watu wenye ulemavu wilayani humo.

Hayo yalisemwa na Katibu mkuu wa Chama Cha Walemavu (CHAWATA) wilayani Mbinga Kassian Nyandindi, wakati alipokuwa akisoma risala ya watu wenye ulemavu hivi karibuni mbele ya mgeni rasmi Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga, katika siku ya maadhimisho ya sherehe za watu hao zilizofanyika kijiji cha Luhagara kata ya Litumbandyosi wilayani humo.

Wakati akisoma taarifa hiyo alisema bado kundi hilo linakabiliwa na tatizo la miundo mbinu ya majengo mbalimbali kutokuwa rafiki kwao na gharama kubwa ya viungo bandia kuwa bei ghali na kufikia hatua wengi wao hushindwa kuvinunua.

Vilevile watu wenye ulemavu wilayani humo wamelalamikia kukosa uwakilishi kuanzia ngazi ya mtaa, vitongoji mpaka kwenye vikao vya Madiwani (Full Council) ili uwakilishi huo uweze kutetea haki zao za msingi.

Sunday, December 1, 2013

MBINGA WATAKIWA KUKABILIANA NA ATHARI ZA MABADILIKO YA TABIA NCHI

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
VIONGOZI kwa kushirikiana na Wananchi wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wametakiwa kuhakikisha kwamba wanakabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi, na sio kusubiri nguvu au misaada kutoka nje jambo ambalo ni hatari kwa kizazi cha sasa na kijacho.
 
Rai hiyo ilitolewa na Wananchi wa wilaya hiyo walipokuwa wakitoa maoni yao kwenye mdahalo uliohusu athari za mabadiliko ya tabia nchi, ambao ulikuwa ukiendeshwa na shirika lisilo la kiserikali (MBINGONET) lililopo wilayani humo, uliofanyika kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa.
 
Walisema kuwa katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi, viongozi kwa kushirikiana na jamii lazima wabuni ufumbuzi wao wenyewe na sio kungojea misaada kutoka nje, wakati wilaya hiyo na taifa kwa ujumla linazidi kuangamia siku hadi siku.
 
Mkazi mmoja wa Mbinga mjini Godfrey Ngonyani alieleza kuwa imefika wakati sasa, elimu itolewe katika jamii juu ya kunusuru hali hiyo isiweze kuendelea na Viongozi hapa nchini wanapaswa kushikilia msimamo wa kuhakikisha kuwa athari hizo tunakabiliana nalo, na kama haitafanyika hivyo ni wazi kuwa tunatengeneza mazingira mabaya ambayo ni hatari hapo baadaye.