Wednesday, January 29, 2014

DOKTA KAMANI AFUNGUKA AWATAKA WAFANYAKAZI WASIOENDANA NA KASI YAKE WAJIONDOE MAPEMA




Na Mwandishi wetu,


WAZIRI  wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi Dokta Titus Kamani, amesema ili kwenda na kasi ya maboresho ya wizara hiyo, inahitajika dhana ya uwajibikaji na uwazi sambamba na kujitolea kwa nguvu zote katika kufanya kazi.

Kamani, aliyasema hayo juzi katika mkutano wa kwanza uliowakutanisha wafanyakazi wote wa wizara hiyo, wakiwemo wastaafu wa mwaka jana katika ofisi ya wizara hiyo ilizopo Temeke jijini Dar es Salaam.

Alisema kama kuna mtu ambaye ni kikwazo katika kukwamisha shughuli za wizara, ni bora akawapisha mapema na kwamba kila mtumishi kwa nafasi yake, anatakiwa kuifanya kazi kwa uwazi na akaitaka wizara kufanya kazi na vyombo vya habari kwani ndio njia pekee ya kuwafanya watanzania wajue wizara inafanya nini.

“Wewe upo ofisini, halafu unaogopa ogopa vyombo vya habari, kwani unatatizo gani kuweni wazi mambo yenu yawe hadharani watanzania wa Mbeya wayajue, Rufiji mpaka Pemba, hakuna kuficha ficha jambo katika wizara yangu.” alisistiza Dokta Kamani.

Alisema wizara ya maendeleo ya mifugo na uvuvi ndio moyo wa taifa kwani huwajumuisha watanzania wengi wenye maisha ya kawaida, lakini amesikitishwa kwa jinsi ambavyo wizara hiyo imekuwa ikichukuliwa na baadhi ya watu kama ni wizara yenye migogoro na kuleta hasara maeneo mengine.

GUNINITA AMRUSHIA KOMBORA NAPE


Na Mwandishi wetu,
Dar es Salaam.

KITENDO cha Katibu mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Nape Nnauye cha kupinga uteuzi wa Mawaziri uliofanywa na Mwenyekiti wa chama hicho ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni mwendelezo wa tabia zake za ukosefu wa nidhamu kwa viongozi wake.

Hayo yamo katika taarifa yake kwa vyombo vya habari aliyoitoa hivi karibuni, ambapo aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Dar es salaam, John Guninita  amesema Nape ni mkiukwaji wa maadili, asiyeheshimu wakubwa ambao wamemteua kushika nafasi hiyo.

Alisema ni kiongozi ambaye anatakiwa kufanya kazi kwa  kuzingatia mipaka yake hivyo ni vema akafahamu kuwa madaraka ya kuteua Baraza la mawaziri ni kazi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano na sio vinginevyo.

Guninita alisema hata kama ingetokea Rais akashauriwa na washauri zaidi ya mia moja, bado uamuzi wake unapaswa kuheshimiwa na hakuna mtu anayeweza kuingilia au kubeza.

Wednesday, January 15, 2014

CHAMA CHA WALIMU MBINGA KWA CHAFUKA, NAIBU KATIBU MKUU TAIFA APOKELEWA KWA MABANGO

Baadhi ya Wanachama wa CWT wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakiwa wameshika mabango yenye ujumbe wa aina mbalimbali ambayo yanawashutumu Katibu wao wa mkoa huo Zebedayo Mwasandungila na wa wilaya hiyo Samwel Mhaiki, ambapo Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho kwa hasira alikataa kuyasoma na kuwaambia Wajumbe wa mkutano huo twendeni kwanza ndani kwenye ukumbi tukafanye mkutano.



Bado Wajumbe wa mkutano huo wakiwa ndani ya ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa ambako mkutano huo ulikuwa ukifanyika, wakiwa na hasira na kuendelea kushika mabango yenye ujumbe wa aina mbalimbali ambao ulikuwa ukiwashutumu baadhi ya viongozi wao wa mkoa na wilaya ya Mbinga .

Katibu Mkuu wa Chama Cha Walimu Tanzania, Ezekiah Oluoch, akihutubia katika ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa, mara baada ya Wanachama wa chama hicho kutuliza jazba zao. Upande wa kulia ni Mbunge wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo na kushoto ni Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo Hussein Ngaga. (Picha zote na Kassian Nyandindi) 



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) Ezekiah Oluoch amejikuta akiwa katika wakati mgumu, baada ya kupokelewa na wanachama wa chama hicho wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kwa malalamiko ya hapa na pale na mabango yaliyobeba ujumbe wa aina mbalimbali ambayo yalikuwa yakiwashutumu Katibu wa CWT wa mkoa huo na Wilaya hiyo.

Waliokuwa wakishutumiwa ni Zebedayo Mwasandungila ambaye ni Katibu wa CWT mkoa wa Ruvuma na Samwel Mhaiki, Katibu wa chama hicho wilayani Mbinga ambao wanalalamikiwa kutengeneza makundi ndani ya chama.

Vilevile Mhaiki alikuwa akinyoshewa kidole kwamba yeye na kamati yake ya chama wilayani humo, wameshindwa kukiongoza chama na badala yake makato wanayokatawa wanachama ya asilimia 15 katika mishahara yao hawarejeshewi katika matawi yao, hivyo hawaoni sababu ya kuendelea kubaki na viongozi hao na kuwataka wajiuzuru mara moja.

Walisema wamekwisha mpatia Bw. Mhaiki notisi ya siku 30 kwa lengo la kusudio la kumfikisha Mahakamani ili haki zao ziweze kupatikana.

“Tumekwisha mwona mwanasheria kwa lengo la kusudio la kumfikisha Mahakamani ndugu Samwel Mhaiki, na sasa tumempatia notisi ya siku 30 atuambie fedha zetu za makato ya kila mwezi zipo wapi”, walisikika wakisema kwa sauti.

Wednesday, January 8, 2014

WATUHUMIWA MAUAJI YA MLINZI WA GAPCO WAPANDISHWA KIZIMBANI

Watuhumiwa wanaodaiwa kumuua mlinzi wa kampuni ya GAPCO inayouza mafuta wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakipandishwa katika Karandika la Polisi baada ya kusomewa mashtaka yao katika Mahakama ya wilaya hiyo leo. (Picha na Kassian Nyandindi)










Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WATU watano wakazi wa Mbinga mjini mkoani Ruvuma, wameburutwa katika Mahakama ya wilaya ya Mbinga mkoani humo kwa tuhuma ya mauaji ya mlinzi wa kituo cha kuuza mafuta GAPCO, kilichopo mjini hapa.

Mwendesha mashtaka wa Polisi Inspekta Nassib Kassim alidai mbele ya Hakimu wa Mahakama ya wilaya hiyo, Joackimu Mwakyolo kuwa tukio hilo lilitokea Desemba 31 mwaka huu majira ya usiku.

Kassim aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Thito Turuka (30), Boniface Nombo (40), Ally Aman Chinga (29), Egno Nchimbi (24) na Felix Turuka (38).

Monday, January 6, 2014

TUNDURU WATAKIWA KUJENGA MSHIKAMANO NA UPENDO



Aliyesimama Diwani wa kata ya Majengo Athuman Nkinde akisisitiza jambo kabla ya kugawa vifaa vya kutengeneza batiki na sabuni za maji na vipande, kwa vikundi vya Majengo A na B wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma. Ambao wameketi ni viongozi wengine wa kata hiyo.  


Na Steven Augustino,
Tunduru.

WANACHAMA na wakereketwa wa chama cha Mapinduzi (CCM) katika kata ya Majengo wilayani Tunduru Ruvuma, wamehimizwa kudumisha muungano na upendo miongoni mwao na kuhakikisha wanapata ushindi wa  chama chao katika chaguzi zijazo za serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika mwaka huu.

Mariwani Athumani Nkinde wa Kata hiyo na  Diwani waviti maalumu wa tarafa ya Mlingoti Bi. Atingala Mohamed walisema hayo kwa nyakati tofauti  wakati wa  uzinduzi wa mradi wa maji safi ya bomba ugawaji wa vifaa vya kutengenezea Batiki, mafuta ya kupaka, sabuni za maji, na vipande katika kata hiyo.

Madiwani hao walisema kuwa endapo wanaCCM hawatashikamana katika ujenzi na uimarishaji wa chama chao ipo hatari ya mamluki kuingia miongoni mwao, na kuwavuruga kwa lengo la kuvipatia ushindi vyama pinzani.
 
Akifafanua taarifa ya ujenzi wa mtandao wa bomba la maji hayo na vifaa hivyo Diwani Athuman Nkinde, alisema kuwa hadi kukamilika kwake miradi hiyo imegharimu shilingi 400,000 na akatumia nafasi hiyo kuwaomba waitumie na kuitunza.

WAKAZI WA MBINGA MJINI WASHAURIWA KUTOA MSAADA KWA WAGONJWA

Mganga wa zamu wodi ya watoto (kulia) katika hospitali ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma,  Revina Kayombo akipokea msaada wa sabuni za kufulia wagonjwa, kutoka kwa Philiberth Hyera (aliyevaa suti nyeusi ambaye amekaa) mkazi wa Mbinga mjini. Hyera alitoa wito kwa wakazi wengine waliopo mjini hapa kupenda kuwasaidia wagonjwa.

Aliyevaa suti nyeusi ni Philiberth Hyera mkazi wa Mbinga mjini akitoa msaada wa sabuni za kufulia, kwa wagonjwa ambao wamelazwa katika wodi ya akina mama hospitali ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, hivi karibuni. (Picha zote na Kassian Nyandindi)

Thursday, January 2, 2014

UWT MBINGA YAWATAKA AKINA MAMA KUEPUKANA NA MAKUNDI YA ANASA

Wanachama wa UWT wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kukabidhi zawadi zao walipokwenda kuwataka hali akina mama wenzao ambao wamelazwa katika hospitali ya wilaya hiyo iliyopo mjini hapa.


Upande wa kushoto aliyevaa shati la kijani ni Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, Pendo Ndumbaro akifurahia jambo baada ya kushika mtoto mchanga ambaye alizaliwa usiku wa kuamkia mwaka mpya (2014) alipokuwa ametembelea jana wodi ya akina mama katika hospitali ya wilaya hiyo iliyopo mjini hapa kwa lengo la kuwataka hali, na wanaoshuhudia ni baadhi ya akina mama ambao wamelazwa katika hospitali hiyo. (Picha zote na Kassian Nyandindi).



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
WANAWAKE wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma wametakiwa kuwa makini katika kuendesha maisha yao kwa kujishughulisha na kilimo, biashara na kujiunga na vyama vya akiba na mikopo ili waweze kuepukana na kujiingiza kwenye anasa ambazo zinachangia maambukizi ya virusi vya ukimwi.
 
Sambamba na hilo wameshauriwa kushirikiana na kuchukua hatua katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili katika maisha yao ya kila siku kwa kufanya kazi kwa bidii.

Rai hiyo ilitolewa  jana na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) wilayani Mbinga Pendo Ndumbaro, alipokuwa akizungumza na akina mama waliolazwa katika hospitali ya wilaya hiyo iliyopo mjini hapa ambao aliwatembelea kwa lengo la kuwataka hali na kuwapa zawadi mbalimbali.

Pia Mwenyekiti huyo alikuwa ameambatana na wanachama wenzake wa umoja huo ambao walishiriki kwa pamoja kwenda kuwaona wagonjwa hao waliokuwa wamelazwa katika hospitali hiyo.

GAUDENCE KAYOMBO ASIKITISHWA NA UJENZI WA BARABARA KIWANGO CHA LAMI KUTOKA SONGEA KWENDA MBINGA

Gaudence Kayombo.



















Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MBUNGE wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo amesema, ujenzi wa  barabara kiwango cha lami kuanzia eneo la Likuyufusi pacha ya Peramiho wilaya ya Songea hadi Mbinga, katika baadhi ya maeneo umejengwa kwa kiwango kisichoridhisha kutokana na barabara hiyo kuanza kuwekwa viraka kabla ya kukabidhiwa rasmi mikononi mwa serikali.

Kayombo alisema hayo alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini hapa, huku akisisitiza kuwa hali hiyo huenda ikatokana na wataalamu husika kutozingatia ipasavyo vipimo vya kimaabara na ndio maana barabara hiyo hubomoka na kulazimika kuweka viraka.

Alisema uzembe huo uliofanywa wa kutozingatia viwango husika ni hasara kubwa kwa serikali kutokana na fedha nyingi iliyotumika kujengea barabara hiyo kutofanya kazi yake kama ilivyokusudiwa.

MLINZI AUAWA NA MAJAMBAZI KWA KUKATWA KOROMEO


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MLINZI wa kituo cha kuuza mafuta GAPCO kilichopo Mbinga mjini mkoani Ruvuma, amekutwa akiwa ameuawa kikatili na watu wasiojulikana kwa kukatwa koromeo na kujeruhiwa vibaya sehemu mbalimbali za mwili wake.

Kwa mujibu wa taarifa zilizolifikia gazeti hili imeelezwa kuwa aliyeuawa ni Kelvin Mapunda(52) mkazi wa mjini hapa, ambapo mwili wake ulikutwa ukiwa umetelekezwa karibu na eneo la kituo hicho cha mafuta.

Mwandishi wa habari hizi alipofika katika eneo la tukio hilo, alikuta umati mkubwa wa watu ukiwa umezunguka mwili wa marehemu huyo huku wakionekana kuchukizwa na kitendo hicho cha kinyama.

WAKIMBIA FAMILIA ZAO WAKIHOFIA KUKAMATWA NA POLISI


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

BAADHI ya Wanaume wa kijiji cha Mbangamao kati, kata ya Mbangamao wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma wamezikimbia familia zao wakihofia kukamatwa na polisi baada ya kuvamia nyumba ya Mratibu elimu wa kata hiyo Florence Kowelo, na kumjeruhi kwa kumpiga nondo kichwani.

Watu hao wanadaiwa kufanya kitendo hicho na kutishia usalama wa Watumishi wengine wa serikali, katika kata hiyo baada ya kuwatuhumu wamekuwa na tabia ya kufanya mapenzi na wake zao.

Tukio hilo lilitokea usiku wa Desemba 27 mwaka huu na kwamba vibaka hao ambao wanatamba kijijini hapo kwa jina la M 23, kuwa wameapa kupambana na Watumishi wote waliopo katika kata ya Mbangamao.