Monday, February 24, 2014

MAFUNZO YA UTENGENEZAJI VITO VYA THAMANI MBINGA YAKAMILIKA, WASHIRIKI WAIOMBA SERIKALI KUUNGA MKONO

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
WASHIRIKI wa mafunzo ya kutengeneza vito vya thamani wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wameiomba serikali wilayani humo kuendelea kuunga mkono mafunzo waliyoyapata ili yaweze kuleta faida kwa kizazi cha sasa na kijacho.
 
Kauli hiyo ilitolewa kupitia risala yao iliyosomwa na mmoja kati ya washiriki hao, Editha Komba mbele ya mgeni rasmi Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga wakati wa kufunga mafunzo hayo ya wiki mbili yaliyofanyika katika chuo cha maendeleo ya wananchi (FDC) kilichopo mjini hapa.
 
Aidha katika risala hiyo washiriki hao walisema wameweza kujifunza kutengeneza ukataji wa vipande vya aluminiamu na shaba, kutengeneza mapambo mbalimbali kama vile heleni, cheni na bangili.
 
Walieleza kuwa wameweza kujifunza kutumia vitu vya asili kama vile mbegu za maembe, kahawa, maboga na manyoya ya kuku kutengeneza mapambo ya asili.

Friday, February 21, 2014

POLISI WAFANIKIWA KUKAMATA JAMBAZI LILILOKUWA LIKITESA WANANCHI WA MBINGA KWA MUDA MREFU

Jambazi linalodaiwa kuwa sugu Roster Ndunguru (katikati) akiwa chini ya ulinzi wa polisi katika hospitali ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, ambako amelazwa baada ya kuambulia kipigo kutoka kwa Polisi wakati akijaribu kutoroka.

Jambazi linalodaiwa kuwa sugu Roster Ndunguru (27) mkazi wa kijiji cha Mbangamao akiwa amefungwa pingu katika hospitali ya wilaya ya Mbinga ambako amelazwa baada ya kuambulia kipigo kikali kutoka kwa Polisi wakati akijaribu kutoroka mikononi mwao. (Picha zote na Kassian Nyandindi)



Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

JESHI la Polisi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, limefanikikwa kumkamata Roster Ndunguru mkazi wa kijiji cha Mbangamao wilayani humo ambaye anadaiwa kuwa ni jambazi sugu na amekuwa akifanya matukio mengi ya kiuhalifu ikiwemo kuwajeruhi watu na kunyang’anya mali zao.

Aidha Jambazi hilo lilikuwa likitafutwa kwa muda mrefu baada ya kumjeruhi Mratibu elimu kata ya Mbangamao, Florence Kowelo kwa kumjeruhi sehemu mbalimbali za mwili wake na kumpiga na kitu kizito kichwani.

Tukio hilo imeelezwa kuwa lilitokea majira ya usiku wakati Mratibu huyo akiwa nyumbani kwake amelala na familia yake, ambapo baada ya kupiga kelele majirani walijitokeza na jambazi hilo lilitokomea kusikojulikana.

Kwa mujibu wa chanzo cha uhakika kutoka Jeshi la Polisi wilayani Mbinga ambacho hakikutaka jina lake litajwe katika mtandao huu, kilisema kuwa Roster amekuwa na matukio mengi ya kiujambazi ambayo amekuwa akiyafanya katika maeneo mbalimbali wilayani humo.

Tuesday, February 18, 2014

HALMASHAURI YA MBINGA YAINGIA MKATABA WA MAFUNZO YA KUTENGENEZA VITO VYA THAMANI, WAKOREA KUJENGA KIWANDA

Mbunge wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo(aliyesimama) akisisitiza jambo wakati wa kumkaribisha mtaalamu wa madini kutoka Korea, Dokta Kim (katikati) ambaye ana lengo la kupanua soko la madini kwa wachimbaji wadogo wadogo wa madini na kutangaza fursa za kimaendeleo kwa mataifa mengine wilayani Mbinga. Kushoto ni mtaalamu mwenzake aitwaye Changlee.



Mtaalamu wa madini ambaye ni wa kwanza kutengeneza vito vya thamani Korea kusini Dokta Kim, (kushoto) akiweka sahihi katika mkataba aliotiliana nao na Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma katika hafla fupi iliyofanyika ukumbi wa chuo cha maendeleo uliopo mjini hapa, Upande wa kushoto kwa Dokta Kim ni mkuu wa chuo cha maendeleo ya jamii (FDC) wilayani Mbinga Aidan Mchawa naye akiweka sahihi katika mkataba huo wa kutoa mafunzo ya kutengeneza vito hivyo na kujenga kiwanda cha kutengeneza vito vya thamani wilayani humo, kiwanda hicho kinatarajiwa kujengwa na wakorea hao miaka mitano ijayo. Wanaoshuhudia kutoka kushoto ni Askofu wa jimbo la Mbinga John Ndimbo na anayefuatia ni Mbunge wa jimbo la Mbinga Gaudence kayombo. (Picha na Kassian Nyandindi)

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
HALMASHAURI ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma kupitia chuo chake cha maendeleo ya jamii (FDC) kilichopo mjini hapa, kimeingia mkataba na mtaalamu wa madini ambaye anafahamika kwa jina la Dokta Kim kutoka nchi ya Korea kusini, kwa ajili ya kutoa mafunzo ya wiki mbili ya utengenezaji wa vito vya thamani.
 
Pia mkataba huo unalenga miaka mitano ijayo mtaalamu huyo ataweza kujenga kiwanda cha kutengeneza vito vya thamani wilayani humo, jambo ambalo litaweza kupanua soko la ajira kwa wananchi wa wilaya hiyo.
 
Akizungumza katika hafla fupi ya kutiliana sahihi katika ukumbi wa chuo cha maendeleo uliopo Mbinga mjini, Dokta Kim alisema yeye ni mtu wa kwanza katika nchi hiyo ya Korea kusini ambaye anaongoza kwa utengenezaji wa vito vya thamani, hivyo anawaomba washiriki walioteuliwa kujiunga na mafunzo hayo kuwa makini wakati watakapo kuwa darasani.
 
Dokta Kim alisema kuwa wazo hili la kuja Mbinga na kutaka kufanya hayo ni jitihada zilizofanywa na Mbunge wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo, ambapo mafunzo hayo yataweza kuwafungua vijana wa wilaya hiyo waweze kufanya shughuli za utengenezaji wa vito hivyo na kuweza kuondokana na umasikini.

Monday, February 17, 2014

WAZAZI WILAYANI MBINGA WASHAURIWA KUPELEKA WATOTO WAO KATIKA CHUO CHA UFUNDI PILIKANO

Kibao kikionyesha mwelekeo wa chuo cha ufundi Pilikano, ambacho kipo umbali wa kilometa 18 kutoka Mbinga mjini mkoani Ruvuma.

Wanafunzi wakijifunza ufundi wa umeme wa majumbani.

Baadhi ya wanafunzi wakiwa darasani wakijifunza fani ya ushonaji.

Mkurugenzi wa chuo cha ufundi Pilikano, Bruno Kapinga, akizungumza na mwandishi wa habari hizi (Hayupo pichani) wakati wa mahojiano yaliyofanywa juu ya maendeleo ya chuo hicho. (Picha zote na Gwiji la matukio Ruvuma)



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WADAU wa elimu wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wametakiwa kuwa na mwamko wa kupeleka watoto wao katika vyuo vya ufundi hususani kwa vile ambavyo vipo karibu na maeneo yao, ili waweze kupata ujuzi wa aina mbalimbali.

Aidha imeleezwa kuwa watoto wanaomaliza darasa la saba wilayani humo, wamekuwa wengi wakizurula mitaani hivyo ni vyema sasa wakapelekwa katika vyuo hivyo ili waweze kuwa na maendeleo katika fani za ufundi kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.

Wito huo ulitolewa na Mkurugenzi wa chuo cha ufundi Pilikano Bruno Kapinga, kilichopo katika kata ya Mkumbi wilayani Mbinga wakati alipokuwa akihojiwa na mwandishi wa habari hizi juu  ya maendeleo ya chuo hicho.

Kapinga alisema kuwa chuo hicho kimesajiliwa na VETA na kilianza rasmi kutoa mafunzo ya ufundi mwaka 2012 katika fani ya ushonaji, magari na umeme.

Mkurugenzi huyo alisema kwamba wazo la kujenga chuo alilipata baada ya kupata ufadhili kutoka Uholanzi, ambapo wafadhili kutoka katika nchi hiyo waliweza kumsaidia vifaa vya ufundi katika fani hizo.

Tuesday, February 11, 2014

MBINGA NAKO KWA CHAFUKA WAFANYABIASHARA WAGOMA

Jakaya Kikwete, Rais wa Tanzania.

 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
HALI  si shwari  katika  mji  wa Mbinga mkoani Ruvuma, kufuatia  kuanza kwa mgomo  usio na kikomo wa wafanyabiashara kama njia ya  kufikisha ujumbe  kwa Waziri wa viwanda na biashara   na  serikali ya  Rais Jakaya  Kikwete,  juu ya gharama za mashine za kutolea risiti (EFD) wakidai kwamba gharama hizo ni kubwa na ni sawa na kumtishwa mzigo mfanyabiashara ambao hauna tija kwake.  


Mgomo huo umeanza leo  asubuhi  hii  huku  makundi ya wafanyabiashara wakiwa wamekusanyika katika maeneo mbalimbali ya mji huo, huku wakipanga kufanya maandamano  kuwaadhibu wenzao wanaokiuka mgomo huo ambao wataonekana wamefungua maduka.


Hali kwa upande wa wakazi wa Mbinga mjini  na wale wa maeneo ya vijijini ambao  wanakuja kwa ajili ya kupata huduma mbalimbali imewafanya wawe katika wakati mgumu kutokana na mgomo huo, hivyo kujikuta wakiambulia makufuri katika maduka hayo.


Wafanyabiashara  hao  wametoa onyo kwa  wenzao iwapo  watafungua  maduka yao  watakiona cha moto  na  kuanzia  wakati  wowote sasa,  wataanza msako wa duka moja hadi jingine kwani wamesema mgomo  huo ni wa nchi nzima na wao  wametii uamuzi wa  wafanyabiashara wenzao katika mikoa yote iliyopo hapa nchini.

Saturday, February 8, 2014

OFISA ELIMU SHULE ZA SEKONDARI MBINGA AVULIWA MADARAKA, WAZIRI ASEMA NIMEMSHUSHA MADARAKA AKAFUNDISHE AKIWA MWALIMU WA KAWAIDA

Naibu Waziri Elimu na Mafunzo ya Ufundi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Kassim Majaliwa, akiwasili wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma baada ya kupokelewa na Mkuu wa wilaya hiyo (Kulia kwake) Senyi Ngaga katika eneo la Kanisa Katoliki (Jimboni) lililopo mjini hapa.

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Kassim Majaliwa akiweka sahihi katika vitabu vya wageni baada ya kuwasili kwenye ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Ngaga ambaye yupo mbele yake akishuhudia.

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Kassim Majaliwa akizungumza na Walimu hawapo pichani wa wilaya hiyo katika ukumbi wa UVIKAMBI uliopo Mbinga mjini, upande wa kulia mwanzo kwake Waziri ni Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga na wa mwisho kutoka kwa Mkuu wa wilaya hiyo ni Katibu tawala wa wilaya hiyo Stephano Ndaki. (Picha zote na Gwiji la Matukio Ruvuma)


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

NAIBU Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ofisi ya Waziri mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Kassim Majaliwa amemvua madaraka kwa kumshusha cheo Ofisa elimu shule za sekondari wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Hanji Yusuph Godigodi kwenda kuwa mwalimu wa kawaida wa sekondari kutokana na Ofisa huyo kushindwa kutekeleza majukumu yake ya kazi na kufanya ubadhirifu wa shilingi milioni 268 za maendeleo ya elimu ya sekondari wilayani humo.

Aidha amewashusha vyeo Wakuu wa shule za sekondari sita za wilaya hiyo kwenda kuwa walimu wa kawaida, kutokana na walimu hao wakidaiwa
kushirikiana na Ofisa huyo wa sekondari kufanya ubadhirifu wa fedha hizo.

Hatua ya Naibu Waziri huyo kuwashusha vyeo viongozi hao ilifikiwa katika kikao ambacho alikuwa akizungumza na Walimu wa shule za msingi na sekondari wilayani humo, ambacho kiliketi kwenye ukumbi wa Uvikambi uliopo mjini hapa na kwamba Waziri huyo yupo katika ziara yake ya kikazi wilayani Mbinga kwa muda wa siku mbili.

Waziri Majaliwa aliwataja wakuu wa shule za sekondari wilayani Mbinga ambao wameshushwa madaraka kuwa ni William Hyera ambaye ni wa shule ya
sekondari Maguu, Clemence Sangana anatoka shule ya sekondari Mkuwani, Method Komba Langilo sekondari, John Tillia Ukilo sekondari, Leonard Juma Luli Sekondari huku akimtaja kwa jina moja mwalimu Konga ambaye yupo sekondari ya Kihangimahuka.