Tuesday, June 24, 2014

MGOGORO WA MIPAKA NA ARDHI: MKUU WA WILAYA YA NYASA MKOANI RUVUMA ALALAMIKIWA NA WANANCHI WAKE


 
Mkuu wa wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma Ernest Kahindi, akiwa ofisini kwake wilayani humo. (Picha na Kassian Nyandindi)
Na Kassian Nyandindi,
Nyasa.

SAKATA la mgogoro wa kugombea ardhi na mipaka katika kitongoji cha Mshangano kijiji cha Liparamba tarafa ya Mpepo wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, limechukua sura mpya kufuatia Wakazi wa maeneo hayo kumlalamikia Mkuu wa wilaya hiyo Ernest Kahindi huku wakimnyoshea kidole kwamba ameshindwa kumaliza mgogoro huo kwa kufuata taratibu husika  ikiwemo ridhaa ya wananchi, badala yake  anatumia nguvu kubwa  kunyanyasa viongozi wa kijiji hicho.  

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati  tofauti kijijini hapo, wakazi hao walisema Kahindi amefikia hata hatua ya kumweka mahabusu kwa siku tatu katika kituo kikuu cha polisi wilaya ya Nyasa, Mwenyekiti wa kijiji Joseph Komba bila kosa lolote huku akizuia dhamana.

Uchunguzi umebaini kuwa Mwenyekiti huyo aliwekwa mahabusu kuanzia siku ya Ijumaa Juni 20 na kudhaminiwa Juni 23 mwaka huu majira ya jioni, ambapo kufikia saa 11 jioni siku hiyo ndipo alichukuliwa maelezo na kuambiwa atafute mtu wa kumdhamini huku akipewa usumbufu wa kuendelea kuripoti kila siku katika kituo hicho cha polisi.

Wednesday, June 11, 2014

KASI YA UPIMAJI VVU MBINGA NI NDOGO BULEMBO AUTAKA UONGOZI WA WILAYA KUHAMASISHA WANANCHI


Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa Alhaj Abdallah Bulembo, akipokea vazi na kadi ya chama cha upinzani kutoka kwa mama Maria Ndimbo ambaye alikuwa mfuasi wa Chama Cha Wananchi (CUF) na kuhamia CCM. Tukio hilo lilifanyika katika uwanja wa soko kuu mjini hapa.

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi Taifa Alhaj Abdallah Bulembo, amemwagiza Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga kuhakikisha kwamba wilaya hiyo inaweka mikakati madhubuti ya kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi kupima afya zao.

Agizo hilo lilifuatia baada ya kusomewa taarifa ya maendeleo ya wilaya hiyo katika ukumbi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani humo, ambayo ilionesha kwamba watu 300,000 tu ndio waliopima afya zao katika kipindi cha mwaka 2013 hadi mwaka huu, ili waweze kujitambua kama wana maambukizi ya virusi vya ukimwi kiasi ambacho ni kidogo kutokana na wilaya hiyo kuwa na watu wengi.

“Nimegundua hapa hamasa ya upimaji VVU ni ndogo ukizingatia kwamba Mbinga kuna watu wengi sana, kuanzia sasa tengenezeni hili liwe kama agenda katika vikao vyenu sio tuna kaa kimya tuweke mazingira ambayo yenye programu ya muda mrefu na endelevu”, alisema Bulembo.

Tuesday, June 10, 2014

CHADEMA YAPATA PIGO MBINGA WASEMA NI CHAMA AMBACHO HAKINA MWELEKEO

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi Taifa, Alhaj Abdallah Bullembo akihutubia leo mamia ya wakazi wa Mbinga mjini katika uwanja wa soko kuu mjini hapa.

Alhaj Abdallah Bulembo akimkabidhi kadi ya CCM aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, Desderius Haulle katika mkutano wa hadhara uliofanyika mjini hapa, baada ya kurejesha kadi ya CHADEMA.

Aliyekuwa Mwenyekiti wa CHADEMA Desderius Haulle akiwa amebebwa na Wafuasi wa CCM baada ya kurejesha kadi ya chama hicho pinzani na kuhamia chama tawala. (Picha zote na Kassian Nyandindi)
Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimepata pigo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kufuatia aliyekuwa Mwenyekiti wake wa chama hicho wilayani humo Desderius Haulle kujitoa uanachama na kuhamia Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Tukio hilo limejitokeza leo katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa soko kuu uliopo mjini hapa, ambao ulikuwa ukihutubiwa na Mwenyekiti wa taifa wa Jumuiya ya Wazazi ya Chama Cha Mapinduzi Alhaj Abdallah Bulembo.

Sambamba na hilo katika mkutano huo pia alijitokeza mwanachama mmoja wa Chama Cha wananchi CUF, Maria Ndimbo naye alirejesha kadi yake ya chama hicho na kuhamia CCM.

Haulle alirudisha kadi ya CHADEMA na kukabidhiwa ya CCM, ambapo alipopewa nafasi ya kuzungumza alisema amechoshwa na sera za chama hicho pinzani ambazo hazina utekelezaji.

“Leo nimeamua kurejesha kadi hii na kuhamia katika chama hiki tawala kwa sababu nafahamu mambo mengi yanayofanywa na CHADEMA, hivyo nilivumilia kwa muda mrefu lakini leo imefikia mwisho wake naomba tuungane pamoja tujenge taifa letu”, alisema Haulle.

UNYAMA WA KUTISHA: WATOTO WATEKETEA KWA MOTO BAADA YA KUFUNGIWA NDANI


Na Kassian Nyandindi,
Nyasa.

SIMANZI na majonzi vilitawala katika mji mdogo wa Mbamba bay wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, kufuatia wanafunzi wawili wakazi wa mji huo wanaosoma shule ya msingi Mbamba bay wilayani humo kufariki dunia, baada ya kuteketea kwa moto katika chumba walichokuwa wamelala ambacho inadaiwa kuwa walifungiwa nje kwa kufuli na kuwafanya washindwe kujiokoa.

Kwa mujibu wa vyanzo vya uhakika vya habari vimeeleza kuwa tukio hilo lilitokea Mei 23 mwaka huu majira ya usiku, ambapo chanzo cha moto huo hadi sasa hakijulikana na kwamba watoto hao walifungiwa kwenye chumba ambacho ni duka la bidhaa mbalimbali ambalo vitu vilivyokuwa ndani yake navyo viliteketea kabisa.

Watoto waliokumbwa na mkasa huo ni Sharifa Nurudin (13) ambaye anasoma darasa la saba na Ismail Nurudin (11) wa darasa la tano katika shule hiyo, imedaiwa kuwa walikuwa wakifungiwa mara kwa mara kwenye duka hilo lenye jina maarufu ‘Kwa mjomba Nuru’ nyakati za usiku, kwa lengo la kulinda  mali zilizomo ndani yake.

“Watoto hawa walikuwa siku zote wanafungiwa nje na kufuli na baba yao mzazi Nurudin Mohamed, licha ya watu kumweleza acha kuwatumikisha watoto hawa kwa mtindo huu alikuwa hataki kusikia na leo watoto wamepoteza maisha kwa sababu ya ujinga wa huyu baba”, alisema mama mmoja mkazi wa mji mdogo wa Mbamba bay ambaye hakutaka jina lake litajwe gazetini.

Sunday, June 8, 2014

ASASI ZISIZO ZA SERIKALI WILAYANI MBINGA LAWAMANI

Ofisa maendeleo ya jamii Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Paschal Ndunguru akisisitiza jambo alipokuwa akifungua mkutano wa Wadau mapambano dhidi ya UKIMWI uliofanyika kwenye ukumbi wa shule ya sekondari Kigonsera uliopo wilayani humo. Katikati ni Mwenyekiti wa Mamlaka ya mji mdogo wa Mbinga Steven Matesso na upande wa kulia ni Ofisa maendeleo ya jamii Henry Digongwa, anayeshughulikia kitengo cha UKIMWI na tiba. (Picha na gwiji la matukio mkoani Ruvuma)



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

IDARA ya Maendeleo ya Jamii katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, imezinyoshea kidole baadhi ya asasi zisizo za kiserikali wilayani humo kwamba, hazitekelezi majukumu yake ya kazi ipasavyo.

Sambamba na hilo imeelezwa kuwa taarifa za kazi inazofanya hazitolewi kabisa juu ya nini asasi husika inafanya, jambo ambalo ni kinyume na taratibu zilizowekwa wakati zinasajiliwa na kupewa majukumu ya kwenda kuyafanya.

Kauli hiyo ilitolewa na Ofisa maendeleo ya jamii Henry Digongwa anayeshughulikia kitengo cha UKIMWI na tiba, katika halmashauri hiyo alipokuwa kwenye mkutano wa siku mbili na Wadau wa mapambano dhidi ya ugonjwa huo, uliofanyika ukumbi wa shule ya sekondari Kigonsera iliyopo wilayani humo.

Saturday, June 7, 2014

MALUMBANO YA VIGOGO MBINGA YAENDELEA KUIBUA MAPYA

Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete.

























Na Mwandishi wetu,

Mbinga.

IMEBAINIKA kwamba kumekuwa na mgogoro mzito unaoendelea kufukuta wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kufuatia kuwepo kwa malumbano yasiyokuwa na ulazima, kati ya baadhi ya vigogo ngazi ya wilaya hiyo, askari polisi na madereva wa pikipiki.  

Hali hiyo imefikia hatua kwa baadhi yao kudaiwa kunyanyasa madereva wa pikipiki wa wilaya hiyo huku uongozi wa umoja wa madereva hao (UWAMBI) uliopo wilayani hapa, ukijipanga kwenda kwa mkuu wa mkoa huo Said Mwambungu ili waweze kufikisha kilio chao.

Ukweli juu ya mgogoro huo ulijitokeza hivi karibuni katika kikao kilichoketi Mei 22 mwaka huu mjini hapa, endelea kufuatilia mkasa huu kama ifuatavyo;

UWAMBI wanena kwenye kikao hicho:

Kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa na Katibu wa umoja huo Bern Mangeni mbele ya mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga, kwa niaba ya wanachama wenzake alisema wamekuwa wakinyanyaswa na Ofisa mmoja wa usalama wa taifa wilayani hapa (jina tunalo) na Mkuu wa polisi wa wilaya hiyo Justine Joseph.

“Mheshimiwa mkuu wa wilaya sisi tutaendelea kusonga mbele ngazi ya juu kwa sababu inaonesha umeshindwa kutusaidia, tumebaki kwenye hali ya sintofahamu juu ya tatizo hili”, alisema Bern Mangeni.

Wednesday, June 4, 2014

MBINGA WACHUKIZWA NA MALUMBANO YA VIGOGO WAIOMBA SERIKALI KUINGILIA KATI

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu.



















Na Mwandishi wetu,

Mbinga.

BAADHI ya wakazi wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma wameshauri na kulitaka Jeshi la polisi mkoani humo, lijiepushe  kufanya kazi zake kwa kusikiliza majungu na maneno ya fitina katika utendaji wake wa kazi za kila siku na endapo wasipozingatia hilo, mwisho wa siku huenda jeshi hilo linaweza kujikuta likabaki na askari wachache wasiokuwa na sifa au weledi.

Ushauri huo ulitolewa kwa nyakati tofauti walipokuwa wakizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, kufuatia kuwepo kwa malumbano yasiyokuwa na ulazima ambayo yanaendelea kati ya baadhi ya vigogo ngazi ya wilaya na askari polisi.

Walieleza kuwa hali hiyo imesababisha hata baadhi yao kutoelewana ambapo kigogo mmoja ambaye ni Ofisa usalama wa taifa (jina tunalo) na Mkuu wa polisi wa wilaya ya Mbinga (OCD) Justine Joseph wanadaiwa kutoelewana na Mkuu wa kituo cha polisi wilayani humo Geofrey Ng’humbi.

Walisema malumbano ya vigogo hao hayana faida katika jamii na yanatokana na Ng’humbi kufanya kazi zake kwa kuzingatia utawala bora, hivyo kuonekana kuwa mwiba kwa wenzake.