Saturday, August 30, 2014

OFISA USHIRIKA MBINGA AONJA JOTO YA JIWE, WANACHAMA WAMKATAA WASEMA HAWANA IMANI NAYE


Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Hussein Ngaga.


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

OFISA ushirika wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Raphael Luvanda amejikuta akiwa katika wakati mgumu kufuatia Wanachama wa chama cha kuweka na kukopa, Mbinga Lutheran SACCOS kilichopo wilayani humo kumjia juu na kumweleza kwamba hawana imani naye katika utendaji wa kazi zake, hivyo hawamtaki kumuona akifanya kazi za ukaguzi katika umoja huo.

Sambamba na hilo wanachama hao ambao walionekana kukerwa na tabia za Ofisa ushirika huyo walisema, sababu zao za msingi za kumkataa wamekuwa wakimtuhumu kwa muda mrefu kwamba anafanya kazi zake kwa mrengo wa kushoto kwa kutofuata taratibu husika.

Walieleza kuwa bodi husika itazifikisha tuhuma husika kwa mwajiri wake ambaye ni Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya Mbinga, ili ziweze kufanyiwa kazi huku wakitaka kuanzia sasa shughuli za ukaguzi zifanywe na ofisa ushirika mwingine kutoka katika halmashauri hiyo na sio vinginevyo.

BODI YA LESENI YA GHALA YATAKIWA KUTEKELEZA MAJUKUMU YAKE IPASAVYO



Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

WADAU wanaozalisha mazao ya chakula na biashara wilayani Mbinga na Nyasa mkoa wa Ruvuma, wameitaka bodi ya leseni ya ghala Tanzania kuhakikisha kwamba wanatekeleza mapema mfumo wa stakabadhi ghalani hususani kwa zao la kahawa, ili kuweza kuzuia uharibifu na upotevu wa mazao wilayani humo.

Walisema lengo la kufanya hivyo itasaidia walengwa wa mfumo huo ambao ni wakulima, wafanyabiashara na vikundi husika kuweza kujijengea uwezo na hatimaye waweze kuinua uchumi wao.

Ilielezwa kuwa mfumo wa stakabadhi ghalani endapo utatekelezwa kwa haraka katika wilaya hizo, utaleta fursa ya kufanyika kwa mnada wa zao la kahawa na kuuzwa katika kipindi hiki cha msimu wa mavuno ya zao hilo.

Friday, August 22, 2014

VIONGOZI WAPYA CHADEMA MBINGA WAPEWA SOMO


Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kimepata viongozi wapya ambao watakiongoza chama hicho wilayani humo baada ya kufanya uchaguzi wake, huku wakitakiwa kufanya kazi bila ubaguzi au upendeleo wa aina yoyote ile.

Aidha viongozi hao waliochaguliwa wameshauriwa kutojenga makundi katika kipindi cha uongozi wao ikiwa ni lengo la kuondoa mipasuko ndani ya chama ambayo inasababisha malalamiko yasiyokuwa ya lazima.

Hayo yalibainishwa na Wajumbe wa mkutano Mkuu wa uchaguzi wa viongozi wa CHADEMA ngazi ya wilaya ya Mbinga, uliofanyika kwenye ukumbi wa Tulivu uliopo mjini hapa.

Uchaguzi huo ulisimamiwa na Mwakilishi wa chama hicho Kanda ya kusini Menlufu Mapunda, ambapo wajumbe hao kwa nyakati tofauti walisema itakuwa ni jambo la kusikitisha endapo watawaona viongozi wao wakiwatenga katika mambo mbalimbali, huku wakisisitiza ni vyema kuanzia sasa pawepo na mabadiliko chanya ambayo yataleta maendeleo kwa wanachama na chama kwa ujumla.

Saturday, August 16, 2014

WALEMAVU NAMTUMBO WAPATIWA MAFUNZO YA KUTAMBUA HAKI ZAO

Na Kassian Nyandindi,


Namtumbo.

SHIRIKA lisilo la kiserikali la kuendeleza watu wenye ulemavu na watoto yatima Tanzania (SHIKUWATA) lenye makao yake makuu mkoani Ruvuma, limeendesha mafunzo ya siku tano kwa watu wenye ulemavu na Watendaji wa kata ya Namabengo Wilayani Namtumbo mkoani humo, kwa lengo la kuwafundisha juu ya kujua sera ya maendeleo na huduma kwa watu wenye ulemavu.

Mafunzo hayo ambayo yalifunguliwa na Diwani wa kata ya Namabengo wilayani humo Vitus Ngonyani, ambayo yalifanyika katika ukumbi wa Namabengo Saccos uliopo mjini hapa na kushirikisha wananchi mbalimbali wanaoishi kuzunguka eneo la kata hiyo.

Mratibu wa shirika hilo Laura Martin akizungumza katika mafunzo hayo, alisema kuwa lengo la kutoa elimu kwa walemavu hao ni kuwafanya wajue haki zao na wajibu wa kujihudumia pamoja na kuangalia nafasi waliyonayo katika jamii na serikali kwa ujumla.

Laura alisema kuwa washiriki hao katika kipindi chote cha siku tano watakachokuwa darasani wataweza kujifunza mambo mbalimbali ikiwemo kujua hali ya watu wenye ulemavu, huduma za watu wenye ulemavu, haki na ulinzi wa kisheria, dira na mwelekeo wa sera, matamko ya sera kwa watu wenye ulemavu na mgawanyo wa majukumu katika ulinzi na usalama kwa watu wenye ulemavu.

Friday, August 15, 2014

ASKOFU MKUU DAMIAN DALLU AWAASA WAUMINI WAKE

Watoto wa shirika la kipapa (mtoto Yesu) parokia ya Mbangamao Jimbo la Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakisherehekea siku ya maadhimisho ya miaka 50 ya uinjilishaji wa parokia hiyo. Sherehe hizo zilifanyika nje ya viwanja vya kanisa hilo.

Askofu mkuu Damian Dallu wakati akitoa mahubiri katika maadhimisho hayo kwa waumini wa kanisa Katoliki (hawapo pichani) Parokia ya Mbangamao Jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma. (Picha zote na Julius Konala)

Na Julius Konala,
Mbinga.

ASKOFU mkuu Damian Dallu, wa Jimbo kuu Katoliki la Songea mkoani Ruvuma ameipongeza Parokia ya Mbangamao iliyopo katika Jimbo la Mbinga mkoani humo, kwa mchango wake mkubwa wa kusukuma maendeleo hususani katika sekta ya elimu kwa kipindi cha miaka 50 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1964 chini ya Paroko wake wa kwanza mzalendo Hayati Askofu Maurus Komba.

Askofu Dallu ametoa pongezi hizo wakati akiwahubiria mamia ya Waumini wa kanisa hilo kwenye maadhimisho ya Ibada ya misa takatifu ya shukrani, Jubilei ya miaka 50 ya parokia hiyo iliyofanyika nje ya viwanja vya kanisa hilo na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwemo maaskofu, mapadre, watawa, waumini pamoja na viongozi wa serikali.

Alisema Parokia hiyo kupitia Shirika la Wavisenti imefanikiwa kupanua wigo mkubwa wa kutoa huduma kwa jamii, ikiwemo kuongeza idadi ya shule za msingi hadi kufikia 15, shule za sekondari tatu na ujenzi wa shule za chekechea kwa kila kigango.

Vilevile ameeleza kuwa wameweza kutoa huduma ya maji safi na salama kwa wakazi wa eneo hilo ikiwemo pamoja na parokia hiyo kuzaa parokia mpya ya Mpepai iliyopo wilayani humo na kufanya ukarabati wa zahanati, shule za msingi na ujenzi wa sekondari. 

WAFANYABIASHARA WA MAHINDI RUVUMA WALIA NA SERIKALI



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

BAADHI ya Wasafirishaji wa mazao ya nafaka mkoani Ruvuma, wameiomba Serikali kuangalia uwezekano wa kuharakisha kulipa madeni yao ya usafirishaji wa mahindi kutoka kwenye vituo vya ununuzi na kuyafikisha kwenye kitengo cha hifadhi ya chakula (NFRA) Songea mkoani humo, katika msimu wa kilimo wa mwaka 2013/2014 kwa lengo la kunusuru kuuziwa mali zao na taasisi za kifedha ambako walikopa kwa ajili ya kuendeshea shughuli hiyo.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wasafirishaji hao ambao ni wazawa hawakutaka majina yao yatajwe, walidai kwamba hali hiyo imewaathiri zaidi  waajiriwa waliopitia mgongo wa nyuma kufanya kazi ya usafirishaji wa zao hilo baada ya matajiri wao kuingia mkataba na NFRA.

Walisema kuwa tangu kufunguliwa kwa msimu huo Julai 15 mwaka jana wamekuwa wakiendesha shughuli hizo kwa kutegemea mikopo kutoka benki, na wengine kudaiwa na baadhi ya wamiliki wa vituo vya mafuta ambako walikopa.

Tuesday, August 12, 2014

WANASIASA WANYOSHEWA KIDOLE KWA KUWATUMIA VIJANA KATIKA USHABIKI WA MAMBO YA KISIASA

Katibu wa Chama cha Mapinduzi wilaya ya Songea mjini mkoani Ruvuma, Josephat Ndulango. (Picha na Kassian Nyandindi)
Na Kassian Nyandindi,

Songea.

CHAMA cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Songea mjini mkoani Ruvuma kimewanyoshea kidole wanasiasa ambao wamekuwa wakiwatumia vijana kwa maslahi yao binafsi, kupitia mchakato huu wa kutengeneza katiba mpya unaoendelea huko Bungeni badala yake kimewataka waachane na ushabiki wa mambo ya kisiasa, na wawatumie vijana kwa maslahi ya taifa kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho.

Aidha imeelezwa kuwa utengenezaji wa katiba mpya ni jukumu la Wabunge wa bunge maalum la katiba, hivyo kwa wale waliokimbia mapambano bungeni ni kutowatendea haki wananchi na ni dhambi ambayo itaendelea kuwatafuna kila siku maishani mwao, badala yake warudi bungeni ili kuweza kumaliza misuguano inayoendelea kufukuta na kuhatarisha ustawi wa maendeleo ya nchi yetu.

Katibu wa CCM wilaya ya Songea mjini, Josephat Ndulango alisema hayo wakati alipokuwa akizungumza na Majira mjini hapa, huku akieleza kuwa vyama vya upinzani ndio vimekuwa chagizo kwa kukataa kujenga maridhiano ya pamoja juu ya mchakato huo wa kuipata katiba mpya.

Saturday, August 9, 2014

ASILMIA 90 YA FAMILIA WILAYANI MBINGA HUTEGEMEA KILIMO NA UFUGAJI

Upande wa kulia Diwani wa kata ya mkako Ambrose Nchimbi akiangalia nyara mbalimbali za serikali katika banda la Maliasili na mazingira wilayani Mbinga, siku ya maonesho ya wakulima yaliyofanyika katika kilele chake kijiji cha Lusonga wilayani humo.

Mke wa Mbunge wa Jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma, Leah Kayombo akitoa maelezo juu ya shughuli zinazofanywa na umoja wa kikundi cha Mbalawala katika maonesho ya wakulima yaliyofanyika wilayani Mbinga katika kijiji cha Lusonga mkoani humo.


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa asilimia 90 ya familia wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, hutegemea kilimo na ufugaji katika kuendesha shughuli za kimaendeleo katika maisha yao ya kila siku.

Aidha kati ya hizo asilimia 50 zinazalisha zao la kahawa wilayani humo, na ndio zao kuu ambalo hutegemewa kwa kukuza uchumi wa wilaya hiyo.

Hayo yalisemwa na Kaimu mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Mbinga, Oscar Yaspesa alipokuwa akisoma taarifa ya maendeleo ya kilimo na mifugo kwa mgeni rasmi Diwani wa kata ya Mkako Ambrose Nchimbi alipokuwa kwenye maonesho ya wakulima (Nane nane) yaliyofanyika katika kijiji cha Lusonga wilayani humo.

Sunday, August 3, 2014

DEREVA ALIYETOKOMEA KUSIKOJULIKANA BAADA YA KUSABABISHA AJALI AJISALIMISHA MIKONONI MWA POLISI

Gari hili lenye namba za usajili T 759 BVR aina ya Nissan Civillian ndilo lililopata ajali na kuua watu sita, 18 kujeruhiwa vibaya likiwa limetumbukia kwenye korongo katika kijiji cha Burma kata ya Nyoni wilayani Mbinga, wakati linaelekea wilaya ya Nyasa. (Picha na Gwiji la matukio Ruvuma)
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
DEREVA aliyetokomea kusikojulikana ambaye alisababisha ajali ya gari kutumbukia katika korongo, watu sita kufariki dunia na 18 kujeruhiwa vibaya, waliokuwa wakisafiri kwa basi kutoka Mbinga mjini kwenda wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma, amejitokeza na kujisalimisha mikononi mwa Jeshi la Polisi akiwa katika hali mbaya.
 
Kamanda wa Polisi wa mkoa huo Mihayo Msikhela amemtaja dereva huyo kuwa ni Paul Nchimbi (31) mkazi wa kijiji cha Liparamba wilayani Nyasa, ambapo wakati anajisalimisha mwili wake umejaa majeraha.
 
Mihayo alifafanua kuwa baada ya dereva huyo kupatikana kwa hiari yake na kuripoti katika kituo kikuu cha polisi wilaya ya Mbinga amepelekwa kwa ajili ya kupewa matibabu, hospitali ya wilaya hiyo huku akiwa chini ya ulinzi mkali.
 
Alisema atakapomaliza kupatiwa matibabu na kupona, jeshi hilo litafanya mahojiano naye ili kuweza kujua chanzo cha tukio hilo ambalo limesababisha baadhi ya Watanzania, waliokuwa wakisafiri katika basi alilokuwa akiendesha lenye namba za usajili T 759 BVR aina ya Nissan Civillian mali ya Dismas Ndomba mkazi wa kijiji cha Kingirikiti wilayani wilayani humo, kupata ajali katika kijiji cha Burma majira ya saa 10:30 jioni Agosti Mosi mwaka huu.  

Saturday, August 2, 2014

WATU SITA WAFARIKI DUNIA NA 18 WAJERUHIWA VIBAYA KATIKA AJALI YA BASI MBINGA


Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma Mihayo Msikhela akimtaka hali mmoja kati ya majeruhi Joseph Matembo aliyelazwa katika hospitali ya wilaya ya Mbinga mkoani humo, ambaye amevunjika mikono na miguu katika ajali ya gari aina ya basi lenye namba za usajili T 759 BVR aina ya Nissan Civillian wakati akisafiri kutoka Mbinga mjini kwenda wilaya mpya ya Nyasa mkoani humo. Majeruhi 18 wamelazwa katika hospitali hiyo na hali zao ni mbaya.



Gari hilo lililopata ajali likionekana katika picha tofauti likiwa limetumbukia katika korongo kijiji cha Burma kata ya Nyoni wilayani Mbinga, baada ya dereva kuikosa kona kali wakati alipokuwa kwenye mwendo kasi. (Picha zote na Kassian Nyandindi)


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.   
  
WATU sita ambao ni abiria waliokuwa wakisafiri kwa basi kutoka Mbinga mjini kwenda makao makuu ya wilaya mpya ya Nyasa, mkoani Ruvuma wamefariki dunia na wengine 18 kujeruhiwa vibaya baada ya gari hilo walilokuwa wamepanda, kuacha njia na kutumbukia kwenye korongo.

Akizungumza na Mwandishi wa habari hizi, Kamanda wa Polisi wa mkoa huo Mihayo Msikhela, alisema gari hilo lenye  namba za usajili T 759 BVR aina ya Nissan Civillian mali ya mfanyabiashara mmoja maarufu mjini hapa (jina halijapatikana) lilipata ajali Agosti Mosi mwaka huu, majira ya saa 10:30 jioni katika kijiji cha Burma kata ya Nyoni wilayani Mbinga.

Mihayo alifafanua kuwa ajali hiyo ilisababishwa na gari kuwa katika mwendo kasi, ambapo dereva aliyekuwa akiliendesha alishindwa kulimudu kwenye kona kali na hatimaye lilitumbukia katika shimo kubwa (korongo) na kusababisha mauaji na majeruhi hao.

“Mpaka sasa dereva aliyekuwa akiliendesha gari hili bado jina lake halifahamiki kutokana na kukimbia kusikojulikana, Jeshi la polisi tunafanya jitihada ya kumtafuta ili aweze kupatikana na baadaye tupate maelezo yakinifu juu ya tukio hili”, alisema Mihayo.