Sunday, May 31, 2015

MANISPAA SONGEA NA MIKAKATI YA KUBORESHA MATIBABU KWA WAZEE

Na Muhidin Amri,
Songea.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, imekuwa ikitenga kiasi cha shilingi milioni 10 kila mwaka, ikiwa ni lengo la kuhakikisha kwamba wazee wanaoishi katika Manispaa hiyo wanapatiwa matibabu ipasavyo, wakiwemo na wategemezi wao.

Fedha hizo zinazotengwa hugharimia matibabu ya wazee 600 na wategemezi wao 2700, ambao hunufaika na mpango wa matibabu bima ya afya katika zahanati, vituo vya afya na hospitali mbalimbali zilizopo katika Manispaa hiyo.

Hayo yamebainishwa na Mratibu wa mfuko wa afya ya jamii mkoani Ruvuma (CHF) wa Manispaa ya Songea, Victor Nyenza alipokuwa akizungumza kwenye mdahalo wa wazi uliohusu usalama wa wazee hapa nchini, ambao ulifanyika mjini hapa.

Saturday, May 30, 2015

KANISA KUMFIKISHA MAHAKAMANI DIWANI

Askofu mkuu wa jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma, John Ndimbo.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

UONGOZI wa Kanisa katoliki Jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma, umesema upo katika hatua za kumfikisha Mahakamani Diwani wa kata ya Litembo kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Mbinga mkoani humo, Altho Hyera kwa kile walichodai kuwa diwani huyo amekuwa akitishia usalama wa wafanyakazi wa hospitali ya Litembo na kuharibu kwa makusudi, sifa ya hospitali na maendeleo yake.

Hospitali hiyo ambayo humilikiwa na jimbo hilo, umeeleza pia diwani huyo amekuwa akimdhalilisha Askofu mkuu wa jimbo la Mbinga, John Ndimbo kwa kuandikia barua kwa viongozi wa juu wa serikali ambazo gazeti hili nakala zake imezipata zikimtuhumu Askofu huyo kuwa ni mla rushwa, ameshindwa kusimamia maendeleo husika na ameitelekeza hospitali hiyo.

Taarifa ya uongozi wa kanisa katoliki wilayani humo, kutaka kumfikisha kizimbani kiongozi huyo wa CCM zilielezwa katika kikao kilichowakutanisha baadhi ya waumini wa vigango vya kanisa hilo kata ya Litembo, ambao ulifanyika kwenye ukumbi wa Parokia ya Litembo uliopo katika kata hiyo.

Friday, May 29, 2015

MARIO MILLINGA KUPAMBANA NA GAUDENCE KAYOMBO

Mario Millinga.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KADA wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, Mario Millinga ametangaza nia yake ya kutaka kugombea nafasi ya ubunge katika jimbo la Mbinga Mashariki mkoani Ruvuma ambalo hivi sasa linaongozwa na Mbunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Gaudence Kayombo.

Kada huyo wa CHADEMA alisema kuwa ameshawishika kugombea nafasi hiyo ili wananchi wa wilaya hiyo, waone jinsi uongozi wa chama chake unavyojali maslahi ya wananchi hasa kwa wale waishio vijijini ambao muda mwingi, wamekuwa wakisahulika katika mambo mbalimbali ya kimaendeleo.

“Ubunge ni uwakilishi wa wananchi katika eneo husika, tunapomchagua mbunge au diwani ambaye si mkazi wa eneo la uwakilishi tunajitwika mzigo wa shida sisi wenyewe, ndugu zangu mimi ni mzaliwa wa kijiji cha Tukuzi hapa Mbinga nimedhamiria kugombea katika nafasi hii, ili niweze kuwatumikia ipasavyo wananchi wa jimbo hili”, alisema Mario.

Mario alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, juu ya nia yake ya kutaka kuingia katika kinyang’anyiro hicho cha kuwania nafasi ya ubunge, jimbo la Mbinga Mashariki na kwamba ni kijana na kada wa siku nyingi wa chama hicho ambaye amebobea katika masomo ya biashara, uhasibu na uchumi kutoka chuo kikuu cha Dar es Salaam sehemu ya mlimani na kuhitimu elimu ya biashara ngazi ya Bachelor of Education in Commerce.

WALIOHUSIKA KUCHOMA MOTO BASI KUCHUKULIWA HATUA ZA KISHERIA


Baadhi ya wananchi wakishuhudia basi la kampuni ya Babu J Trans, likiteketea kwa moto baada ya kuchomwa na wananchi wenye hasira kali.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

SERIKALI wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma imeapa kwamba, haitawasamehe wananchi wa kijiji cha Mhuwesi na Msagula wilayani humo ambao wamehusika kuchoma moto basi la kampuni ya Babu J Trans, na kuliteketeza kabisa kutokana na basi hilo kugonga mtoto na kufariki dunia papo hapo.

Chande Nalicho ambaye ni Mkuu wa wilaya hiyo, alisema hayo alipokuwa katika eneo la tukio kwa lengo la kujionea uharibifu huo uliofanywa na wananchi wenye hasira kali kwa kujichukulia sheria mkononi, kinyume na taratibu za nchi zinavyotaka.

Mkuu huyo wa wilaya alilaani vikali kitendo hicho, baada ya basi hilo kumgonga mwanafunzi aliyefahamika kwa jina la Faidhi Ally (10) na kusababisha kifo papo hapo, katika ajali iliyotokea Mei 26 mwaka huu majira ya mchana.

WAHITIMU CHUO CHA SAYANSI WATAKIWA KUWAKOMBOA WATANZANIA

 
Upande wa kulia, Askofu Mkuu wa Jimbo kuu katoliki la Songea mkoani Ruvuma, Damian Dallu akimzawadia kompyuta mpakato (Laptop) mmoja wa wahitimu wa chuo cha sayansi na tekinolojia ya mawasiliuano cha Mtakatifu Joseph mjini Songea ambaye amevaa vazi jeusi, baada ya kufanya vizuri masomo yake na kushoto ni Mkuu wa chuo hicho Dokta Arulaj. 

Na Julius Konala,
Songea.

WAHITIMU wa chuo cha Sayansi na tekinolojia ya mawasiliano cha Mtakatifu Joseph, kilichopo katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wametakiwa huko waendako kutumia vyema elimu waliyoipata, kwa malengo ya kuwakomboa Watanzania na taifa kwa ujumla.

Aidha wameshauriwa kutumia kipawa walichonacho, kuongeza juhudi na maarifa waliyoyapata chuoni hapo ili waweze kuleta chachu ya mabadiliko katika jamii, kwa manufaa ya kizazi cha sasa na baadaye.

Rai hiyo ilitolewa na Askofu Mkuu wa jimbo kuu katoliki la Songea, Damian Dallu alipokuwa akizungumza na wanafunzi, wazazi na walimu kwenye mahafali ya sita ya chuo hicho yaliyofanyika mjini hapa.

MGAWANYO WA MAJIMBO YA UCHAGUZI MBINGA WAZUA MALALAMIKO

Kaimu Mkurugenzi wa uchaguzi Kailima R.K akizungumza hivi karibuni na vyombo vya habari hapa nchini, kuhusu uchunguzi wa mipaka na kugawa majimbo kwa ajili ya uchaguzi mkuu mwaka huu, katika ofisi za makao ya tume ya uchaguzi.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

PENDEKEZO la kuligawa Jimbo la Mbinga Mashariki, lililopo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma limeingia dosari kufuatia kuwepo kwa malalamiko yanayodaiwa kwamba mchakato huo wa kuligawa jimbo hilo, umefanywa na viongozi wachache bila kushirikisha wadau mbalimbali wa wilaya hiyo, kitendo ambacho kimeelezwa kuwa ni ukiukwaji wa maagizo na taratibu zilizotolewa na tume ya taifa ya uchaguzi hapa nchini.

Baadhi ya wananchi wa wilaya hiyo, walitoa malalamiko hayo walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti huku wakiitaka serikali kuwa makini na suala hilo ambalo kutokana na wadau husika kutoshirikishwa kama vile taratibu za tume katika kurekebisha mipaka, kugawa majimbo na kubadili majina zinavyotaka.

Mapendekezo hayo ya kuligawa jimbo hilo yamefanyika muda wa nusu saa katika kikao cha dharula cha baraza la madiwani, kilichoketi Mei 27 mwaka huu kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo mjini hapa.

Hata baadhi ya Madiwani ambao walikuwepo katika kikao hicho nao walionesha kushangazwa na hali hiyo, wakisema kuwa walitumiwa ujumbe kwa njia ya simu kwamba wanatakiwa katika kikao cha dharula kwa tarehe hiyo, bila kufafanuliwa kinahusu nini na walipowasili walikutana na ajenda hiyo ya pendekezo la kuligawa jimbo. 

NALICHO: WANANCHI TUSHIRIKIANE KUWAUA SIMBA

Mkuu wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Chande Nalicho akizungumza na wananchi wa wilaya hiyo katika moja ya ziara yake ya kikazi ambazo amezifanya hivi karibuni.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

CHANDE Nalicho ambaye ni Mkuu wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, amewataka wananchi wa vijiji vilivyopo katika tarafa ya Matemanga wilayani humo kutumia nguvu zao na kujituma kwa hali na mali, kuhakikisha kwamba simba ambao wamekuwa wakiwasumbua hasa nyakati za usiku wanauawa ili wananchi waondokane na adha wanayoipata sasa ya kushindwa kuishi kwa amani.

Nalicho alitoa kauli hiyo, alipokuwa akikabidhi askari wa nane idara ya wanyamapori wilayani humo, ambao walipelekwa katika tarafa hiyo kwa lengo la kupambana na simba hao kuhakikisha kwamba wanauawa.

Hatua hiyo imefuatia kutokana na simba hao wamekuwa wakishambulia mifugo ya wananchi hasa nyakati za usiku, jambo ambalo linahatarisha hata usalama wa binadamu kwa wakazi wanaoishi katika vijiji vilivyopo kwenye tarafa ya Matemanga.

WATENDAJI TUNDURU WATAKIWA KUTEKELEZA MAJUKUMU YAO

Na Mwandishi wetu,
Tunduru.

SERIKALI wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, imewaagiza watendaji wote wa vijiji wilayani humo kuhakikisha kwamba wanasimamia na kutekeleza ipasavyo sheria ndogo ndogo, ambazo zimetungwa na kupitishwa na baraza la Madiwani wa Halmashauri ya wilaya hiyo.

Aidha wameagizwa kuacha vitendo vya ulegevu, wakati wanapotekeleza majukumu yao ya kazi na kusababisha mwanya kwa wananchi kuvunja sheria husika, hatimaye maendeleo kushindwa kusonga mbele.

Katibu tawala wilayani Tunduru, Ghaibu Lingo alitoa agizo hilo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Matemanga wilayani humo.

Wednesday, May 27, 2015

WANACCM MBINGA KUMCHANGIA FOMU KELVIN MAPUNDA

Diwani wa kata ya Mbinga mjini mkoani Ruvuma, Kelvin Mapunda (Aliyevaa koti nyeusi) akizungumza na wanafunzi wa shule ya msingi Mbambi, Mbinga na Nyerere zilizopo katika kata hiyo wakati akiwa katika ziara yake hivi karibuni, akitembelea vituo vya masomo wakati wa likizo.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

BAADHI ya wazee na vijana wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kata ya Mbinga mjini mkoani Ruvuma, wamemtaka Diwani wa kata hiyo Kelvin Mapunda kwenda kuchukua fomu muda utakapofika kwa ajili ya kugombea tena, nafasi ya udiwani katika kata hiyo.

Aidha walieleza kuwa wapo tayari kutoa fedha zao mfukoni kwa ajili ya kumchangia fomu ya kuwania nafasi hiyo, kwa kile walichoeleza kuwa wamejenga imani naye kutokana na kazi zake alizozifanya katika kipindi cha miaka kumi ya uongozi wake aliowaongoza.

Wazee na vijana hao walisema hayo walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti mjini hapa, huku wakiongeza kuwa wao wanaona ndiye mwanachama ambaye yupo karibu nao katika kuendeleza maendeleo yao kwa faida ya sasa, na kizazi kijacho.

Tuesday, May 26, 2015

NEC YATOA RATIBA YA UCHAGUZI MKUU MWAKA HUU

Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Jaji mstaafu, Damian Lubuva.

Na Mwandishi wetu,

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetoa ratiba ya uchaguzi Mkuu kwa mwaka huu 2015.
Katika taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa tume hiyo mbele ya waandishi wa habari, Jaji Damian Lubuva alisema kwamba;

v Agosti 21 – 2015: kutakuwa na uteuzi wa wagombea Urais, Ubunge na Udiwani.
v Agosti 22 – Oktoba 24, 2015: kutafanyika kampeni za uchaguzi.
v Oktoba 25 – 2015: itakuwa ni siku ya kupiga kura.

Sunday, May 24, 2015

DEREVA AFARIKI DUNIA FUVU LA KICHWA LAPASUKA BAADA YA KUPATA AJALI KONA YA MBWA

Na Steven Augustino,
Tunduru.

DEREVA mmoja ambaye amekuwa akiendesha magari makubwa ya mizigo na hufanya safari zake katika maeneo mbalimbali hapa nchini, amefariki dunia katika ajali iliyotokea kona ya mbwa eneo la Nakayaya, karibu na kiwanda cha kubangua korosho wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma.

Said Jiram (37) ndiye aliyefariki dunia ambapo ndani ya gari alilokuwa akiliendesha lenye namba za usajili T 481 ATZ aina ya Toyota Carina ambalo ndani yake alikuwa na wenzake wawili, ambao walinusurika kifo.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo, walieleza kuwa watu hao walipatwa na mkasa huo wakati walipokuwa wakielekea karibu na kiwanda hicho, kwa lengo la kwenda kupakia korosho kwenye lori hatimaye wasafirishe kwenda Jijini Dar es Salaam.

Akifafanua juu ya tukio hilo rafiki wa marehemu huyo, Mohamed Mponda ambaye ni mmoja aliyenusurika kwenye ajali hiyo alisema kuwa yeye na marehemu walikuwa pamoja kwenye gari hilo, ambapo wakiwa njiani kuelekea huko ghafla gari lilipinduka mara mbili na kusababisha kifo kutokana na Jiram kupatwa na majeraha mengi mwilini huku akitokwa na damu nyingi.

WANASIASA SONGEA WADAIWA KUKWAMISHA MPANGO WA TASAF

Na Muhidin Amri,
Songea.

MPANGO wa kunusuru kaya maskini ulioratibiwa na mfuko wa maendeleo ya jamii nchini (TASAF) awamu ya tatu, Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma umeweza kuibua kaya maskini 8492 sawa na asilimia 106 ikiwa ni ongezeko la kaya 464 ambazo zilikadiriwa hapo awali kufikiwa na mpango huo, katika Manispaa hiyo.

Aidha hadi sasa TASAF imeweza kutekeleza kazi zake katika mitaa 53 ya mjini hapa, ambayo nayo iliingizwa kwenye mpango kwa lengo la kukabiliana na changamoto zilizopo, hatimaye kuweza kufikia malengo iliyojiwekea.

Mratibu wa mpango wa kunusuru kaya maskini katika Manispaa ya Songea, Christopher Ngonyani alieleza hayo, alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu ofisini kwake.

Saturday, May 23, 2015

GOLD STAR YAWAJENGEA UWEZO MAFUNDI RANGI RUVUMA

Na Julius Konala,
Songea.

MAFUNDI rangi waliopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wamenufaika na mafunzo juu ya utumiaji wa tekinolojia ya upakaji rangi ikiwa ni lengo la kuwajengea uwezo, utendaji wa kazi zao za kila siku.

Zaidi ya mafundi 100 ndio waliopewa mafunzo hayo na kampuni ya Gold Star katika Manispaa hiyo, ambayo yalifanyika kwa muda wa siku moja kwenye ukumbi wa chuo cha Top one inn, mjini Songea ambayo yalishirikisha wanawake na wanaume.

Akizungumza katika mafunzo hayo Meneja mauzo wa kampuni hiyo, Ally Khalfan alisema kuwa lengo ni kuboresha taaluma ya upakaji rangi kwa mafundi hao, ili kuweza kuleta mabadiliko katika utendaji wa kazi zao.

Friday, May 22, 2015

FEDHA ZA KUNUNULIA BOTI ZILIZOTOLEWA NA WAZIRI MKUU PINDA WILAYANI NYASA ZAZUA MALALAMIKO

Wavuvi wakiwa katika ziwa Nyasa, wakitumia vifaa duni (mitumbwi) kuvulia samaki ambapo huhatarisha usalama wa maisha yao.
Na Kassian Nyandindi,
Nyasa.

VIKUNDI vinavyojishughulisha na uvuvi wa samaki Mbamba bay wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, vimeutaka uongozi wa Halmashauri ya wilaya hiyo kuchukua hatua za haraka kufanya manunuzi ya boti la kisasa la kuvulia samaki, ambalo Ofisi ya Waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda  alikwisha toa fedha kwa ajili ya kufanya manunuzi hayo.

Aidha wanakikundi hao ambao waliomba majina yao yasitajwe gazetini na hujishughulisha na shughuli za uvuvi katika ziwa Nyasa, walisema kuwa wanaushangaa uongozi wa wilaya hiyo tokea wapewe fedha shilingi milioni 14 na ofisi ya Waziri huyo, takribani miezi miwili imepita, hakuna majibu kamilifu waliyoyapata juu ya manunuzi ya boti hilo.

Walisema Waziri Pinda alitoa ahadi ya kununua chombo hicho cha kisasa kwa ajili ya kuwawezesha kuvua samaki kwa urahisi, alipokuwa hivi karibuni kwenye ziara yake ya kikazi wilayani humo baada ya kupokea kilio cha wavuvi hao kwamba wamekuwa wakipoteza maisha kwa kuzama na mitumbwi majini, kutokana na kukosa kifaa cha kisasa cha kuvulia samaki.

MADIWANI WATAKIWA KUTOWAOGOPA WATUMISHI

Na Kassian Nyandindi,
Namtumbo.

MADIWANI wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, wametakiwa kutowaogopa watumishi na watendaji wa serikali waliopo katika wilaya hiyo, badala yake wawabane na kuwahoji ikiwemo hata kufanya ufuatiliaji wa fedha za miradi ya maendeleo ya wananchi, ambazo hupelekwa katika maeneo yao.

Mbali na hatua hiyo, pia wamehimizwa kuwashirikisha wananchi ili  nao waweze kushiriki vyema katika shughuli za miradi hiyo jambo ambalo litawezesha wilaya, kufikia malengo yake iliyojiwekea ikiwemo kupiga hatua katika nyanja ya kiuchumi.

Rai hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Stephen Nana alipokuwa akizungumza na watumishi pamoja na madiwani katika kikao cha baraza la madiwani, ambacho kiliketi mjini hapa.

Tuesday, May 19, 2015

MAOFISA UGANI RUVUMA WAJENGEWA UWEZO

Na Julius Konala,
Songea.

MAOFISA ugani katika Halmashauri nne zilizopo mkoani Ruvuma, wameweza kujengewa uwezo juu ya matumizi sahihi, katika tekinolojia mpya ya uhifadhi wa mazao.

Lengo la maofisa hao kupewa elimu hiyo, ni kuwataka katika maeneo ambayo wanafanyia kazi mkoani humo, waende kwa wakulima vijijini wakawaelimisha juu ya tekinolojia hiyo na baadaye waweze kuhifadhi mazao yao katika hali nzuri.

Mafunzo juu ya matumizi sahihi ya uhifadhi wa mazao, yalifanyika jana kwenye ukumbi wa mikutano Walimu SACCOS mjini Songea, ambayo yalikuwa yakiendeshwa na shirika la CARITAS na CRS.

Jumla ya maofisa ugani 32 kutoka wilaya ya Songea, Namtumbo, Mbinga na Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wameweza kupata elimu hiyo.

Mwakilishi mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Georgina Mbawala alisema washiriki hao mara baada ya kumaliza kupewa mafunzo hayo watakuwa walimu wazuri, katika suala la uhifadhi huo ambao unalenga kuhifadhi mazao katika kipindi cha miaka mitatu bila ya kushambuliwa na wadudu waharibifu.

Monday, May 18, 2015

NAIBU KATIBU MKUU WIZARA YA FEDHA AWASHUKIA WATUMISHI WA UMMA


Waandishi na wadau mbalimbali wa habari kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini, leo wakiwa kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee Jijini Dar es Salaam, katika semina na maadhimisho ya miaka kumi ya Mamlaka ya udhibiti na manunuzi (PPRA)
Na Kassian Nyandindi,
Dar es Salaam.

IMEELEZWA kuwa watumishi wa umma kwa kushirikiana na watu binafsi hapa nchini, baadhi yao wamekuwa hawafuati  taratibu ambazo zinaongoza manunuzi katika sekta ya umma, kitendo ambacho kimekuwa kikisababisha kuathiri ustawi wa maendeleo ya wananchi.

Aidha imeshauriwa kuwa uadilifu na uwazi katika kusimamia mfumo wa manunuzi ya umma ni jambo ambalo linapaswa kuzingatiwa wakati wote, ili kuwezesha upatikanaji wa thamani halisi ya fedha na matokeo yenye tija kijamii na kiuchumi.

Hayo yalisemwa na Naibu katibu Mkuu Wizara ya fedha, Dorothy Mwanyika ambaye alikuwa akimwakilisha Naibu Waziri wa fedha, Mwigulu Nchemba katika semina ya siku moja iliyowakutanisha Waandishi na wadau wa habari.  

Semina hiyo ilikuwa ikiendeshwa na Mamlaka ya udhibiti wa manunuzi Tanzania (PPRA) ambayo pia inaadhimisha miaka kumi tokea ianzishwe hapa nchini, kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee Jijini Dar es Salaam.

WAKULIMA WA KOROSHO WATAKIWA KUSAFISHA MASHAMBA YAO

Na Steven Augustino,
Tunduru.

HALMASHAURI ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, imeagiza na kuwataka wakulima wa korosho wilayani humo kuanza palizi mapema katika mashamba yao ya mikorosho, ili kuweza kuboresha zao hilo na kuzalishwa kwa wingi.

Faridu Khamis, ambaye ni Mwenyekiti wa halmshauri hiyo alitoa agizo hilo kwenye kikao cha baraza la madiwani kilichoketi hivi karibuni, ukumbi wa Klasta ya walimu mlingoti mjini hapa.

Khamis alisisitiza kuwa wakati wakulima hao, watakapokuwa wanafanya palizi katika mashamba yao waache vitendo vya uchomaji moto ambapo wakifanya hivyo, wanaweza wakasababisha mikorosho kuungua.

Saturday, May 16, 2015

FAMILIA WILAYANI TUNDURU YAOMBA MSAADA KUTOKA KWA WASAMARIA WEMA

Na Steven Augustino,
Tunduru.

FAMILIA ya Athuman Mbwana, wa kijiji cha Nambalapi kata ya Masonya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma inawaomba wasamaria wema kutoa msaada wa kuwawezesha kulea watoto wao watatu, ambao walizaliwa kwa wakati mmoja ndani ya familia yao.

Mbwana alitoa ombi hilo, alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu baada ya wauguzi na wakunga wa Hospitali ya wilaya hiyo, kumtaarifu kuwa mkewe kipenzi Rehema Rashid ambaye alipelekwa hospitalini hapo akiwa mjamzito, kajifungua watoto hao kwa mpigo.

Aidha anaiomba serikali na taasisi binafsi kuwa na jicho la huruma, ili waweze kumsaidia kutunza watoto hao kutokana na yeye binafsi kuwa na kipato kidogo cha kumwezesha kuishi.

Alisema kupata watoto hao ni neema ya mwenyezi Mungu, na matokeo hayo hayakuwa matarajio yake hivyo anaomba msaada wa hali na mali ili aweze kuwatunza na kuwapatia mahitaji muhimu, ambayo yatawafanya waishi na kukua vizuri.

MADIWANI TUNDURU HAMASISHENI KUJIANDIKISHA KATIKA BVR

Na Steven Augustino,
Tunduru.

BARAZA la Madiwani Halmashauri ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, limewataka viongozi wa serikali katika vijiji vya wilaya hiyo kutoa hamasa kuhakikisha wananchi wanajitokeza kwa wingi, kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura kupitia mfumo wa kieletroniki (BVR).

Mwenyekiti wa baraza hilo la Madiwani la wilaya hiyo, Faridu Khamis alitoa rai hiyo alipokuwa akizungumza nao katika kikao walichoketi ukumbi wa Klasta ya walimu, tarafa ya Mlingoti mjini humo.

“Uhamasishaji wa wananchi waweze kujitokeza na kujiandikisha ni jambo la lazima ndugu zangu, jitahidini kuwahamasisha ili tuweze kufikia lengo husika”, alisisitiza.

DIWANI MBINGA ADAIWA KUNYANYASA WAPIGA KURA WAKE, ATUHUMIWA KUTUMIA MADARAKA YAKE VIBAYA

Vibanda vya nyasi ambavyo wanaishi baadhi ya wananchi wa kijiji cha Ilela, ambao waliyakimbia makazi yao baada ya kuogopa kukamatwa na askari polisi wa kituo kidogo cha Maguu wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kwa shinikizo la kuwataka wakaishi katika kijiji cha Ugogo wilayani humo. 

Baadhi ya akina mama wa kijiji cha Ilela wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, ambao wamelazimika kuyakimbia makazi yao na kuishi porini wakiwa katika makazi yao mapya kama wanavyoonekana pichani. 
Na Muhidin Amri,
Mbinga.

ZAIDI ya watu 200 waishio katika kijiji cha Ilela kata ya Mikalanga wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wamehama makazi yao na kulazimika kuishi porini kwa kile walichoeleza kuwa wanaepuka kukamatwa, kuwekwa mahabusu na kuteswa na askari Polisi wa kituo kidogo cha Maguu wilayani humo ambao wanalazimisha kutoa michango ya fedha, kwa ajili ya ujenzi wa kituo kidogo cha polisi katika kata hiyo.

Mbali na hilo watoto chini ya miaka mitano wanashindwa kupata huduma ya matibabu ya kliniki, baada ya uongozi wa kijiji hicho kudaiwa kuandika barua kwenda uongozi wa zahanati ya Ilela ikizuia watoto wenye wazazi ambao wamekimbilia porini, wasipatiwe huduma ya matibabu.

Akina mama nao imefikia hatua sasa, hulazimika kutembea umbali wa kilometa tisa kwenda katika kijiji cha Burma, kufuata huduma hiyo ya matibabu kwa watoto wao.

Kufuatia hali hiyo, pia wanamtuhumu Diwani wao wa kata hiyo Joachimu Kowelo kwa kitendo chake cha kuwagawa wananchi wa kata hiyo kwa kuuagiza uongozi wa kijiji na kata kuwahamisha kwa nguvu baadhi ya wananchi wake, wakaishi kijiji kipya cha Ugogo kwa maslahi yake binafsi kitendo ambacho kimefafanuliwa kuwa ni cha kinyama.

Tuesday, May 12, 2015

STENDI FC TUNDURU YATAWAZWA KUWA BINGWA WA PEACE AND LOVE

Na Mwandishi wetu,
Tunduru.

TIMU ya Stendi FC Tunduru mjini mkoani Ruvuma, imetawazwa kuwa bingwa ligi ya kuitangaza Hoteli mpya ya Peace and Love iliyopo mjini hapa, baada ya kuwachapa magoli mawili kwa moja, mahasimu wao wa timu ya Usalama FC ya mjini humo.

Mchezaji Shaban Chitepete, ndiye aliyefungua milango ya wapinzani hao baada ya kuifungua timu yake kwa goli la kwanza ambalo lilitikisa nyavu za wapinzani wao katika dakika, ya 21 huku la pili likigonga tena nyavu hizo kwa dakika ya 23 ambalo lilifungwa na Exavia Chimgege, mchezo ambao ulikuwa ukisakatwa katika uwanja wa Chama Cha Mapinduzi mjini Tunduru.

Upande wa usalama FC goli la kufuta machozi lilifungwa na Fakihi Maliyatembo, katika dakika ya 39na kuwahadaa walinzi wa Stendi FC baada ya kufyatua mkwaju mkali, ambao ulimwacha golikipa wa timu hiyo njia panda.

Akizungumzia juu ya mashindano hayo, Mwenyekiti wa Chama cha mpira wa miguu (TDFA) wilaya ya Tunduru, Kitwana Mzee alisema ligi hiyo ambayo ilianza Aprili 9 mwaka huu kwa kushirikisha timu 12 kutoka ndani ya wilaya hiyo.

Monday, May 11, 2015

TUNDURU MCHIMBAJI WA VITO AFARIKI DUNIA KWA KUANGUKIWA NA KIFUSI

Na Steven Augustino,
Tunduru.

Ramadhan Ayubu (48) ambaye ni mchimbaji wa madini ya vito vya thamani, katika kijiji cha Mitwana kata ya Lukumbule wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, amefariki dunia baada ya kuangukiwa na kifusi.

Shuhuda wa tukio hilo, Mbangu Eliasi alieleza kuwa lilitokea Mei 9 mwaka huu majira ya asubuhi wakati walipokuwa, wakiendelea na kazi ya uchimbaji.

Eliasi alifafanua kuwa wakati tukio linatokea kila mmoja alikuwa akichimba katika shimo lake yeye na marehemu, ambapo ghafla alisikia kishindo kikubwa na kufuatiwa na ukimya uliotawala kwa muda mrefu kati yake na mwenzake, hali ambayo ilimfanya atoke haraka nje katika shimo lake na kwenda kumuangalia mhanga huyo kama yupo salama.

“Mimi na marehemu tulikuwa tunachimba katika mashimo ambayo yalikuwa yamekaribiana, tulikuwa tunazungumza lakini ghafla niliona kimya na kila nilipokuwa nikijaribu kuzungumza naye sikupata majibu”, alisema.

NJOWOKA ASAMBAZA VIFAA VYA MICHEZO NYASA

Na Kassian Nyandindi,
Nyasa.

WANANCHI wa wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma, ambao baadhi yao hujishughulisha na michezo ya mpira wa miguu na pete wameanza kunufaika kwa kupewa mipira, jezi na vifaa maalum vya michezo hiyo ili viweze kuwarahisishia wakati wanaposakata kandanda wilayani humo.

Vifaa hivyo vimetolewa na Kamanda wa Jumuiya ya Umoja wa Vijana ya Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) wilaya ya Nyasa, Cassian Njowoka alipokuwa katika ziara yake ya kikazi wakati akitembelea kata mbalimbali za wilaya hiyo.

Njowoka ambaye hivi sasa ni ziara yake ya pili tangu aliposimikwa kuwa kiongozi wa UVCCM wa Nyasa na kwamba lengo kuu la ziara hiyo, pia ni kufungua ligi za michezo hiyo na kujionea changamoto mbalimbali ndani ya wilaya, hatimaye zipatiwe ufumbuzi.

Sunday, May 10, 2015

NAMTUMBO WAJIVUNIA UANDIKISHAJI WAPIGA KURA KUENDELEA VIZURI

Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Alli Mpenye akizungumza katika kikao cha robo tatu ya mwaka baraza la Madiwani wa wilaya hiyo, kilichofanyika hivi karibuni mjini hapa. Kushoto kwake ni Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo Stephen Nana. (Picha na Muhidin Amri)
Na Muhidin Amri,
Namtumbo.

KATA tano zilizopo katika Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, zimefanikiwa kuandikisha watu 30,832 katika daftari la kudumu la wapiga kura idadi ambayo imeelezwa kuwa ni moja kati ya mafanikio makubwa wakati zoezi hilo likiendelea kutekelezwa wilayani humo.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Alli Mpenye alisema katika awamu ya kwanza zoezi hilo lilihusishwa katika kata tano za Mgombasi ambapo watu waliojiandikisha walikuwa 5,186, Namtumbo 9,041, Likuyu 4,952, Rwinga 7,586 na kata ya Luegu watu waliojiandikisha walikuwa 4,064.

Mpenye alifafanua kuwa hivi sasa wanaendelea na kata nyingine, na kwamba wamelazimika kufanya kwa wamu kutokana na ufinyu wa vifaa ikiwemo mashine ya kuandikishia wapiga kura (BVR) ambapo baadhi yake zilizoletwa na tume ya taifa ya uchaguzi ni mbovu na hushindwa kufanya kazi ipasavyo na kulazimika kutumia mashine chache zilizopo ambazo hufanya kazi.

WANANCHI TUNDURU WAISHI KWA HOFU SIMBA WALETA BALAA

Na Steven Augustino,
Tunduru.

WANANCHI waishio katika vijiji ambavyo vipo kata ya Matemanga, Ndenyende, Milonde, Fundimbanga na Namwinyu katika tarafa ya Matemanga wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wanaishi katika hofu ya kuvamiwa na kutafunwa na mnyama mkali aitwaye Simba.

Hofu hiyo imetokana na kundi la wanyama hao, kuvamia katika maeneo hayo na kuanza kuleta madhara ya kuua mifugo ya wananchi.

Taarifa kutoka katika maeneo hayo zinafafanua kwamba, tayari wameua na kula mbuzi 18 na mbwa wa nne mali ya baadhi ya wakazi wa maeneo hayo.

Wananchi hao walisema, simba hao ambao wamekuwa wakionekana kuzunguka mara kwa mara walianza kuwasumbua mwishoni mwa mwezi Machi, mwaka huu hali ambayo inaendelea kuwaweka kwenye wakati mgumu na kuwafanya waishi kwa wasiwasi.

Saturday, May 9, 2015

NANA: MADIWANI NAMTUMBO ACHENI KUWA VIGEU GEU

Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Stephen Nana, akifungua kikao cha baraza la Madiwani wa halmashauri hiyo ambapo aliwataka madiwani wake kuchapa kazi kwa bidii, sambamba na kusimamia maendeleo ya wilaya hiyo. Kushoto ni Makamu wake Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Khalifa Majumba.
Na Muhidin Amri,
Namtumbo.

MWENYEKITI wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Stephen Nana amewataka Madiwani wa halmashauri hiyo kujifunga kibwebwe katika kusimamia mapato sambamba na ukusanyaji wa ushuru ipasavyo, ili kuifanya wilaya hiyo iweze kusonga mbele kimaendeleo.

Nana alitoa rai hiyo juzi, alipokuwa akifungua kikao cha robo mwaka cha baraza la madiwani hao huku akisisitiza muda wa kufanya kazi kwa mazoea umepita kilichobaki sasa ni kuhakikisha wananchi, wanapatiwa huduma za kijamii kwa wakati.

Alifafanua kuwa muda uliobaki kabla ya kufanyika uchaguzi mkuu ujao, ni vizuri kila diwani ajitathimini mwenyewe, namna alivyoleta mchango wa maendeleo kwa wananchi wake na wilaya kwa ujumla.

Thursday, May 7, 2015

CUF WAIRUSHIA KOMBORA CCM

Cresencia Kapinga,
Songea.

NAIBU katibu Mkuu bara, Chama Cha Wananchi (CUF) Magdalena Sakaya amewataka wananchi wa Jimbo la Songea mjini mkoani Ruvuma, wafanye mabadiliko kwa kutokipatia kura ya ndiyo Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika uchaguzi mkuu ujao, kwa kile alichodai kuwa chama hicho kimekuwa kikiwacharaza bakora za ugumu wa maisha na kuwafanya vijana wazeeke kabla ya wakati wao.

Akihutubia kwenye mkutano wa chama hicho ambao ulifanyika katika viwanja vya Majengo mjini hapa, Magdalena alikirushia kombora CCM akisema kuwa ndio kilichowafikishia wananchi wake ugumu wa maisha waliyonayo sasa watanzania, na kusababisha migogoro na migomo ambayo imekuwa ikijitokeza mara kwa mara.

Naibu katibu huyo alieleza kuwa hata gharama za maisha hivi sasa zimepanda tofauti na miaka ya nyuma, jambo ambalo mwananchi mwenye kipato cha chini huendelea kuwa masikini na kuteseka na maisha.

“Nikiangalia hapa vijana wengi wa Songea nyuso zenu ni za hazuni tupu, hii inatokana na ugumu wa maisha ambayo yameletwa na chama hiki tawala vijana wengi wamekuwa wazurulaji, wazee hawapati matibabu bure hali kadhalika akina mama wanapokwenda kujifungua hospitali wanapata taabu tu”, alisema Sakaya.

MHOMA: WAANDISHI WA HABARI FUATENI MISINGI YA TAALUMA YA HABARI

Na Mwandishi wetu,
Mbinga.

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, imewataka waandishi wa habari kufuata misingi ya taaluma yao kwa kuandika habari zenye ukweli ili kuifanya nchi isiweze kuingia katika machafuko, hasa kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu, Oktoba mwaka huu.

Aidha imewataka kuwa watu wa kwanza katika kufichua vitendo vya rushwa, hatua ambayo itawawezesha wananchi wa kawaida kupata haki zao za msingi na kupenda kushiriki katika shughuli mbalimbali za maendeleo.

“Mapambano dhidi ya rushwa sio ya mtu mmoja, kila mtu anapaswa kushiriki kikamilifu ili kuifanya serikali ipate muda wa kusimamia shughuli za maendeleo ya wananchi wake ipasavyo”, alisema Ditram Mhoma.

WASHAURIWA KUJIUNGA NA HUDUMA YA MATIBABU NIHF

Na Muhidin Amri,
Songea.

VIONGOZI wa vyama vya akiba na mikopo mkoani Ruvuma, wameombwa kusaidia wanachama wao kujiunga na mfuko wa taifa wa bima ya afya (NIHF) ili waweze kupata huduma bora ya matibabu pale wanapougua, badala ya kutembea na kiasi kikubwa cha fedha mifukoni kwa lengo la kwenda kupata matibabu katika hospitali mbalimbali. 

Aidha wameaswa kuwa waaminifu na waadilifu kwa wanachama wao, katika kuwaongoza na kuacha ubadhirifu wa fedha na mali zao katika chama ambapo kutokana na hali hiyo, baadhi ya wanachama wanashindwa kuendelea kujiunga katika vyama hivyo na kubaki wakikata tamaa.

WAKULIMA NAMTUMBO WANUFAIKA NA TEKINOLOJIA YA KILIMO CHA KISASA

Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Ally Mpenye wa pili kutoka kushoto akipata maelezo kutoka kwa mmoja wa wakulima wa zao la mpunga wilayani humo, Gerold Haulle ambaye amevaa kofia kushoto kwake katika moja ya shamba darasa la majaribio kilimo cha zao hilo. Wa kwanza kushoto ni Mratibu wa taasisi ya Briten nyanda za juu Kusini, Ainea Mgulambwa. 
Na Julius Konala,
Namtumbo.

WAKULIMA wanaozalisha zao la mpunga wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma, wamenufaika na elimu ya matumizi sahihi ya pembejeo za kilimo na upandaji wa zao hilo katika mashamba darasa, yanayoendeshwa na taasisi isiyo ya kiserikali ya Briten kupitia ufadhili wa shirika la kuleta mapinduzi ya kijani barani Afrika, AGRA.

Zaidi ya wakulima 2,660 ndio walionufaika na mpango huo, ambapo Mratibu wa kitengo cha shamba darasa na mtaalamu wa kilimo cha zao la mpunga wilayani humo, Saamy Mwakyusa alisema hayo kwenye uzinduzi wa siku ya mkulima kiwilaya iliyofanyika kijiji cha Namtumbo mbele ya Mkurugenzi wa wilaya hiyo, Ally Mpenye.

Mwakyusa alisema kuwa, elimu hiyo ambayo wameipata wakulima wake imeleta tija kwa madai kwamba jumla ya mashamba darasa 76 katika vijiji vya wilaya hiyo, vimeonyesha kufanya vizuri na wakulima wengi wamepata mafunzo ya kilimo hifadhi ya udongo.

Monday, May 4, 2015

TUNDURU ATAKAYELETA VURUGU KATIKA ZOEZI LA UANDIKISHAJI KUKIONA CHA MOTO

Na Mwandishi wetu,
Tunduru.

SERIKALI wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, imeapa kutofumbia macho kitendo chochote kitakachojitokeza juu ya uvunjifu wa amani katika zoezi la uandikishaji wa daftari la kudumu la wapiga kura, ambalo hivi sasa linaendelea wilayani humo.

Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama wilayani hapa, Chande Nalicho ambaye pia ni Mkuu wa wilaya ya Tunduru alitoa rai hiyo alipokuwa akizungumza hivi karibuni, katika maadhimisho ya sherehe za wafanyakazi zilizofanyika kwenye uwanja wa michezo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) uliopo mjini hapa.

Kwa mujibu wa Mkuu huyo wa wilaya alisema kwamba, amechukua hatua ya kutoa tamko hilo kufuatia taarifa za kiintelejensia ambazo zimemfikia ofisini kwake kuwa, kuna mbinu chafu zinasukwa chini kwa chini na watu wenye nia mbaya kwa lengo la kutaka kuleta vurugu ili zoezi hilo lisiweze kufanikiwa kama ilivyopangwa.

WAIOMBA SERIKALI WASAIDIWE MADAKTARI BINGWA

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

WANANCHI wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wameiomba serikali kuangalia uwezekano wa kupeleka Madaktari bingwa katika Hospitali za mikoa ili kuwasogezea huduma ya afya kwa karibu, kutokana na wengi wao kusumbuliwa na magonjwa sugu na kushindwa kumudu kusafiri umbali mrefu kufuata huduma hiyo katika hospitali za rufaa.

Kauli hiyo ilitolewa na wananchi hao, walipokuwa wakipatiwa huduma ya matibabu na madaktari bingwa waliowasili katika hospitali ya serikali ya wilaya hiyo, kwa ajili ya kutibu magonjwa mbalimbali ikiwa ni lengo la kuongeza nguvu ya utoaji wa huduma ya matibabu katika hospitali hiyo.

Madaktari hao waliwasili hapo wakitokea hospitali mbalimbali Jijini Dar es salaam, KCMC Moshi na kwamba wananchi wa wilaya ya Tunduru walishukuru kwa ujio wao hasa kwa wale ambao walikuwa wakisumbuliwa na magonjwa kwa muda mrefu, bila kupatiwa matibabu ya kudumu.

WAANDISHI WA HABARI WATAKIWA KUACHA KUNUNULIWA NA WANASIASA

Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WAANDISHI wa habari nchini, wametakiwa kuacha tabia ya kununuliwa na wanasiasa kwa lengo la kuandika habari zao ambazo zimekuwa zikiegemea upande mmoja na kusahau matatizo ya wananchi, jambo ambalo limekuwa likisababisha jamii kukosa imani nao.

Aidha imeelezwa kuwa jamii inatambua wajibu na mchango wa wanahabari, hivyo  ni chombo muhimu kinachopaswa kupongezwa wakati wote kutokana na kuibua mambo kadha wa kadha ambayo yakikaliwa kimya, nchi yetu inaelekea kubaya.

Hayo yalisemwa na Wakili wa serikali mwandamizi mkoani Ruvuma kanda ya Songea, Renatus Mkude alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari wa mkoa huo kwenye maadhimisho ya siku ya uhuru wa habari duniani, yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Masista mjini hapa.

Sunday, May 3, 2015

MKUU WA WILAYA TUNDURU AWAJIA JUU WANANCHI WAKE, AWATAKA KUZINGATIA USAFI

Na Steven Augustino,
Tunduru.

MKUU wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Chande Nalicho amewajia juu na kuwataka wananchi wa wilaya hiyo kujenga tabia ya kufanya usafi katika nyumba zao wanazoishi, ikiwa ni pamoja na kufua vyandarua vyao wanavyojifunika wakati wanapolala ili kuweza kuepukana na wadudu aina ya kunguni, ambao muda mwingi wamekuwa wakilalamika huwauma nyakati za usiku.

Aidha akatumia nafasi hiyo, kuwataka wananchi hao kupeleka watoto wao shule ili wakapate elimu ambayo itawawezesha kujitambua na kupambanua mambo, katika maisha yao ya kila siku na sio muda mwingi kuutumia kulalamika.

Hali hiyo imejitokeza kutokana na kuwepo kwa baadhi ya watu wilayani Tunduru, kujenga dhana ya kuendelea kulaumu serikali kwamba, imewasambazia vyandarua vyenye mayai ya kunguni na kusababisha kuwatesa hasa nyakati za usiku wanapokuwa wamelala.

WANAOTAFUTA MADARAKA KWA MTINDO WA RUSHWA, TUWABEZE

Na Mwandishi wetu,

TUMEONA na tutazidi kuona wanaotangaza nia ya kuwania nyadhifa mbalimbali, katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwezi Oktoba 2015 kuna mengi yamejitokeza na bado yataendelea kujitokeza hivyo ni vyema tukayajadili kwa mapana kuanzia ngazi ya udiwani, ubunge na hata nafasi ya urais.

Napenda kuhoji, je hao wanaotangaza nia wanatangaza nia kweli au ni dhidi ya rushwa? kwa hali ya kawaida katika jamii yetu ya kitanzania imegubikwa na wimbi la rushwa, hivyo msamiati huu umekuwa ni wa kawaida hivyo hata mtu ukimtuhumu ni mlarushwa inaonekana ni jambo la kawaida.

Hivyo wengi wametegwa na rushwa, sitakosea nikisema mifumo yetu imekuwa lege lege dhidi ya kupambana na vita ya rushwa tena hata ufisadi.

Wakati tukiyasemea haya hivi sasa tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu, huko ndiko tunakotarajia kuwapata viongozi watakao tuongoza kwa kipindi cha miaka mitano ijayo, endapo tutacheza karata nzuri nina hakika tutaweza kuwapata viongozi waadilifu na pia endapo tutacheza vibaya tutaishia kupata viongozi ambao sio waadilifu hivyo karata zetu, zitakuwa ni shida na mateso makubwa katika kipindi hicho cha miaka mitano.

Friday, May 1, 2015

WANANCHI TUNDURU WATESEKA NA MALARIA

Mkuu wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Chande Nalicho akiwahutubia wananchi wa kijiji cha Njenga katika maadhimisho ya siku ya Malaria Africa.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

IMEELEZWA kuwa asilimia 38.3 ya vifo vilivyotokea mwaka 2014 wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, vilitokana na ugonjwa hatari wa Malaria.

Hayo na mengine mengi, yalibainishwa katika taarifa iliyosomwa na mratibu msaidizi wa ugonjwa huo wilayani humo, Ayub Joseph katika maadhimisho ya siku ya Malaria Africa yaliyofanyika kijiji cha Njenga wilayani humo.

Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa siku hiyo, jumla ya watu 487 waliripotiwa kupoteza maisha katika vituo vya kutolea huduma za afya wilayani Tunduru.

Akizungumzia mkakati wa kupambana na ugonjwa huo, Joseph alisema pamoja na uwepo wa juhudi hizo za kupambana na Malaria idara yake imekuwa ikikabiliana na changamoto ya upatikanaji wa madawa na vifaa tiba, ambavyo mgawo wake umekuwa ukitolewa bila kuzingatia uwiano na bohari ya dawa hapa nchini (MSD).

WATAKIWA KUPELEKA WATOTO WAO KWENYE CHANJO

Na Mwandishi wetu,
Tunduru.

WANANCHI wilaya ya Tunduru mkoani hapa, wamehimizwa kupeleka watoto wao katika vituo vya kutolea huduma za afya ili waweze kupatiwa chanjo za magonjwa pingamizi, katika ukuaji wa watoto hao.

Chande Nalicho alitoa rai hiyo wilayani humo, wakati wa zoezi la uzinduzi wa wiki ya utoaji wa chanjo duniani, ambalo Tunduru lilifanyika katika viwanja vya hospitali ya serikali ya wilaya hiyo.

Aidha Mkuu huyo wa wilaya, aliwataka akina mama ambao walijitokeza katika zoezi hilo kuwa wajumbe wa kusambaza taarifa kwa wenzao, ili kuweza kuhamasisha jamii iweze kujitokeza kwa wingi na kupatiwa huduma hiyo.