Friday, January 22, 2016

ULIPUAJI MIAMBA MGODI WA MAKAA YA MAWE NGAKA WAATHIRI WANAFUNZI



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WANAFUNZI wanaosoma shule ya msingi Ntunduaro iliyopo katika kata Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, majengo wanayotumia kusomea yapo katika hali mbaya na huenda yakabomoka wakati wowote kutokana na kujenga nyufa zinazosababishwa na mtetemeko mkubwa wa ulipuaji wa miamba, kwenye mgodi wa makaa ya mawe Ngaka uliopo katika kijiji hicho.

Hali ya mazingira ya shule hiyo hivi sasa ni mbaya na kwamba husababishwa na kuendelea kwa shughuli hizo za ulipuaji wa baruti katika miamba, jambo ambalo huenda likaleta madhara makubwa katika jamii.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Ngaga alisema hayo alipokuwa kwenye kikao maalumu, katika kata ya Ruanda na uongozi wa kampuni ya Tancoal Energy ambao ndio wamiliki wa mgodi huo, wakiwemo na baadhi ya wananchi wa kata hiyo wakijadili juu ya athari mbalimbali zitokanazo na mgodi huo.

UJENZI KIWANDA CHA KUSAGA NAFAKA PERAMIHO KUPUNGUZA UKOSEFU WA SOKO LA MAHINDI



Na Julius Konala,
Songea.

IMEELEZWA kuwa ujenzi wa Kiwanda cha kusaga nafaka katika mtaa wa Namiholo kata ya Peramiho wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, utagharimu zaidi ya shilingi milioni 300 hadi kukamilika kwake na kusaidia kupunguza tatizo la ukosefu wa soko la kuuzia mahindi, kwa wakulima wa vijiji vinavyozunguka eneo la mradi huo.

Hayo yalisemwa na msimamizi wa mradi huo, Fredrick Lunje alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu mara baada ya kutembelea eneo la mradi kwa ajili ya kujionea shughuli mbalimbali za ujenzi, ambazo zinaendelea katika mji huo mdogo wa Peramiho.

Lunje alisema kuwa ujenzi wa kiwanda hicho upo katika hatua za mwisho, kwa madai kwamba vifaa vyote vya ujenzi vimekamilika  na kwamba kinachosubiriwa ni  mafundi wa kufunga mashine hiyo kutoka Afrika ya kusini, ili ifikapo mwezi Mei mwaka huu kianze kufanya kazi.

Wednesday, January 20, 2016

MKUU WA WILAYA YA MBINGA AITAKA NEMC KUINGILIA KATI JUU YA UCHAFUZI WA MAZINGIRA MGODI WA MAKAA YA MAWE NGAKA



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga amelitaka Baraza la Usimamizi wa Mazingira ya Taifa (NEMC) kuchukua hatua za haraka dhidi ya tatizo la uchafuzi wa mazingira, ambalo linaendelea kufanyika katika mgodi wa makaa ya mawe Ngaka uliopo kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda mkoani humo.

Aidha alifafanua kuwa kampuni ya Tancoal Energy, ambayo ndiyo imepewa dhamana ya uchimbaji wa makaa hayo, licha ya kupewa maelekezo na NEMC mara kwa mara namna ya utunzaji wa mazingira ikiwemo kudhibiti maji taka yasiweze kuingia kwenye mto ambao hutumika kwa shughuli za kibinadamu na wananchi wa kata hiyo, bado wamekuwa wakipuuza na hawazingatii maelekezo husika waliyopewa.

“Jambo hili limekuwa likijirudia mara kwa mara, nitawasiliana na watu wa baraza la mazingira kuona ni namna gani hatua zichukuliwe juu ya tatizo hili, ambalo uharibifu wa mazingira bado unaendelea”, alisema Ngaga.

SERIKALI YAWATAKA WATUMISHI AMBAO HAWAENDANI NA KASI YA HAPA KAZI TU WAJIONDOE WENYEWE



Na Steven Augustino,
Tunduru.

SERIKALI imewataka wataalamu na watumishi wa idara mbalimbali katika Halmashauri zote nchini, kuondokana na utendaji wa kufanya kazi kwa mazoea katika utekelezaji wa majukumu ya utumishi wa umma, ili kuweza kufikia mabadiliko ya kweli yatakayolifanya taifa lisonge mbele.

Aidha watendaji hao wametakiwa kujipima kama wanao uwezo wa kwenda sambamba na kauli mbiu ya serikali ya awamu ya tano ya ‘Hapa kazi tu’ na kwamba, kama wapo watakaojiona kuwa  hawawezi kuendana na kasi hiyo ya mabadiliko hayo wajitoe mapema wenyewe.

Hayo yalisemwa na Naibu Waziri wa nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Utawara Bora, Suleiman Saidi Jafo wakati alipokuwa akizungumza na watumishi wa idara za halmashauri ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, katika kikao kilichofanyika ukumbi wa Klasta ya walimu wa tarafa ya Mlingoti mjini hapa.

Waziri Jafo alisema katika kuleta mabadiliko ya kweli, inatakiwa kila mtumishi ajipange kufanya kazi kwa juhudi na maarifa kwa kujitoa kwa moyo wa dhati kwa manufaa ya Watanzania wote.

"Katika kuhakikisha kwamba dhana ya hapa kazi tu inafanikiwa, kila mfanyakazi katika idara yake afanye kazi kwa  uadilifu na weledi wa hali ya juu vinginevyo mtumishi ambaye hataki kufuata nyayo hizi, hafai kuendana na kasi ya serikali ya awamu ya tano", alisema Naibu Waziri Jafo.

Tuesday, January 19, 2016

TUNDURU YAPOKEA MILIONI 129.1 KWA AJILI YA KUBORESHA ELIMU



Na Steven Augustino,
Tunduru.

JUMLA ya shilingi milioni 129,125,000 zimepokelewa wilayani Tunduru, mkoa wa Ruvuma ili zeweze kutumika katika shughuli za utoaji wa elimu bure kulingana na ahadi iliyotolewa na Rais wa awamu ya tano, Dkt. John Pombe Magufuli. 

Hayo yalisemwa na Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Agnes Hokororo wakati alipokuwa akizungumza hivi karibuni na wataalamu wake katika kikao cha kazi kilichofanyika ukumbi wa Klasta ya walimu wa tarafa ya Mlingoti mjini hapa.

Aidha Hokororo  aliwatahadharisha watendaji hao kwamba fedha hizo ni za moto, unaowaka na kiongozi atakayejidai kuchakachua ajiandae kuunguzwa na moto huo.

Katika kikao hicho Mkuu huyo wa wilaya alikuwa akizungumza na wakuu wa idara za halmashauri ya wilaya hiyo, wakuu wa shule za sekondari 21 na msingi, waratibu elimu kata ambao pia alikuwa anawapa maelekezo hayo juu ya matumizi ya fedha hizo.

UNAJUA NINI KUHUSU BARAZA LA ARDHI LA KATA ?



Na Bashir Yakub,

TUNAPOZUNGUMZIA mgogoro  wa ardhi  tunazungumzia mgogoro  katika  viwanja, mashamba, nyumba  na  majengo. Wengi  wetu  tunapokutwa  na  migogoro  ya  ardhi  hukimbilia  Mahakama  za  wilaya  au  Mahakama  kuu  ya  ardhi, lakini  tunasahau  kuwa  lipo  baraza  la  ardhi  la kata  ambalo  baadhi  ya  migogoro  haifai  kwenda huko  wilayani  au  mahakama  kuu kabla  ya  kupitia  hatua  hiyo.  Sasa makala  haya yataelezea  kuhusu  baraza  la  ardhi  la  kata  na  mashauri  yanayotakiwa  kuanzia  hapo.

1. NGUVU  YAKE  NI  KATIKA  KATA  TU.

Baraza la  ardhi  la  kata  ni  mahakama  ya  ardhi  katika  kata husika. Hii  ni  kwa  mujibu  wa kifungu  cha  10 ( 1 )  cha  sheria  ya  mahakama  za  usuluhishi  wa  migogoro  ya ardhi.   

Baraza  hili mipaka  yake  ni  katika  kata  husika  kwa maana  kwamba  mipaka  ya  kata ndio  mamlaka  yake  kijiografia, kila  kata   hutakiwa  kuwa na  baraza  lake  la  usuluhishi  wa  migogoro  ya  ardhi na baraza la  ardhi  la  kata  fulani  haliwezi  kuvuka  mipaka  na  kwenda  kuamua  mgogoro  wa  ardhi  wa  kata  nyingine. 


2.  JE  INATAKIWA  WAAMUZI  WANGAPI  KATIKA  BARAZA.

Unapokuwa  na mgogoro  katika  baraza  hili  ni  muhimu  kujua  ni  watu  wangapi  wanatakiwa  kuamua  mgogoro  wako. Mara    kadhaa  hasa  huko  vijijini  waamuzi  katika  mabaraza  haya  wamekuwa  wakijikalia  tu  na kutoa  maamuzi  pasipo kuzingatia akidi. 

TANESCO WATAKIWA KUBADILI MWENENDO WA KAZI ZAO



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WAZIRI wa Nishati na Madini  Profesa Sospeter Muhongo, amelitaka shirika la umeme Tanzania (TANESCO) hapa nchini, kubadili mwenendo wake wa utendaji kazi, kwa kujenga mahusiano mazuri na wadau, mashirika ya watu binafsi yenye mitambo ya kufua umeme kwa kutumia  maporomoko ya maji, ili kuweza kupunguza tatizo la upatikanaji wa nishati hiyo muhimu.

Profesa Muhongo alitoa  rai hiyo hivi karibuni, alipokuwa kwenye ziara yake ya kikazi mkoani Ruvuma, akikagua na kutembelea mitambo mbalimbali ya kuzalisha umeme pamoja na mgodi wa Ngaka unaozalisha makaa ya mawe uliopo katika kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoani humo.

Uchimbaji wa makaa hayo ya mawe hufanywa na kampuni ya Tancoal Energy ambapo Waziri huyo alipokuwa kwenye mgodi huo, alijionea kazi inayofanywa na kampuni hiyo, huku akisisitiza kwamba hakuna sababu ya Watanzania kukosa  umeme kwa sababu makaa hayo yana uwezo wa kuzalisha umeme wa megawati 400 wenye gharama nafuu, ambao utaunganishwa katika gridi ya taifa na kusambazwa katika maeneo mbalimbali.

Saturday, January 16, 2016

WAZIRI WA NISHATI NA MADINI AITAKA TANESCO KUSHIRIKIANA NA ANDOYA HYDRO ELECTRIC POWER


Menas Mbunda Andoya enzi ya uhai wake, akiwa na mkewe na Waziri Mkuu Mizengo Pinda wakati wa uzinduzi wa mradi wa kuzalisha umeme vijijini, ambao ulibuniwa miaka 13 iliyopita.

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

SHIRIKA la ugavi nishati ya umeme Tanzania (TANESCO) limeagizwa kujenga ushirikiano na kampuni binafsi ya Andoya Hydro Electric Power (AHEPO) ambayo inazalisha umeme utokanao na nguvu ya maji wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, ili mradi huo uweze kuwa endelevu.

Aidha umeme huo wa maporomoko ya maji umeunganishwa katika njia kuu ya gridi ya TANESCO ambao husambazwa kwa wateja waliopo wilayani humo.

Waziri wa nishati na madini, Profesa Sospeter Muhongo alitoa agizo hilo juzi alipokuwa katika ziara yake ya kikazi wilayani humo.

Awali akisoma taarifa ya maendeleo ya mradi huo, Mkurugenzi wa kampuni ya AHEPO, Alex Andoya alimweleza Waziri Muhongo kuwa madhumuni ya kuzalisha umeme katika mradi huo ni Megawati 1 na umeunganishwa kwa wateja wa awali 922 kati ya 3,835 katika vijiji vya Lifakara, Kilimani na Mbangamao wilayani Mbinga na ziada huuzwa katika shirika hilo la ugavi wa umeme ukilenga kupata umeme kwa njia endelevu na bei nafuu.

Friday, January 15, 2016

SERIKALI KUZICHUKULIA HATUA HOSPITALI ZINAZOKIUKA TARATIBU

Waziri wa afya, maendeleo ya jamii, wazee na watoto Ummy Mwalimu akisalimiana na Abate msaidizi wa Abasia ya Peramiho wilaya ya Songea mkoani Ruvuma Padri Lucius O.S.B  juzi alipotembelea hospitali ya rufaa ya Mtakatifu Joseph Peramiho mkoani Ruvuma, ambapo Waziri huyo alizungumza pia na watumishi wa hospitali hiyo.


Na Mwandishi wetu,
Songea.

SERIKALI imesema kuwa, itazichukulia hatua kali baadhi ya hospitali na vituo vya afya vya serikali ambavyo huwatoza fedha akina mama wajawazito, watoto wadogo walio chini ya umri wa miaka mitano na wazee ambao wanapaswa kupatiwa matibabu bure.

Kauli hiyo imetolewa jana wilayani Songea na Waziri wa afya, maendeleo ya jamii, wazee na watoto Ummy Mwalimu wakati alipokuwa akizungumza na watumishi wa hospitali ya rufaa ya Mtakatifu Joseph Peramiho wilayani  humo.

Alisema sera ya afya, huduma za kujifungua, matibabu kwa wazee na watoto zinatolewa bure hivyo hospitali hazipaswi kuwatoza fedha makundi hayo badala yake zifuate maelekezo ya serikali,  kwani ni utekelezaji wa ahadi yake wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu uliopita.

WAZIRI WA AFYA ASIKITISHWA NA WANAWAKE KUTUPA WATOTO

Waziri wa afya, maendeleo ya jamii, wazee na watoto Ummy Mwalimu kushoto, akimjulia hali  mkazi wa mtaa wa Mshangano Manispaa ya Songea Cosma Mvulla (65) aliyekuwa katika zamu ya kusubiri kuonana na madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo katika hospitali ya mkoa wa Ruvuma.


Na Muhidin Amri,
Songea.

WAZIRI wa afya, maendeleo ya jamii, wazee na watoto Ummy Mwalimu amewataka wanawake  kujiepusha na matumizi ya dawa za asili pindi wanapokuwa wajawazito, ili waweze kujiepusha na uwezekano wa kupata matatizo mbalimbali wakati wa kujifungua.

Mwalimu ametoa rai hiyo jana mjini Songea, alipokuwa akizungumza na  madakatari na wauguzi   wakati alipotembelea hospitali ya mkoa Songea, ambapo alijionea uhaba wa vitanda katika wodi namba ya tatu  inayotumiwa na akinamama waliojifungua pamoja na mlundikano wa wagonjwa.

Alisema kuwa sera ya afya serikali awamu ya tano, inalenga kuboresha huduma za matibabu kwa wananchi wake kwa kuongeza vifaa tiba, wauguzi na madakatari na kwamba alieleza kuwa ni jambo la kushangaza kuona baadhi ya watu hadi tunaingia karne hii ya 22 bado wanaendelea kutumia  madawa ya asili   kutibu maradhi waliyonayo.

Alibainisha kuwa serikali itaendelea kuboresha huduma zake za matibabu katika vituo vya afya, zahanati na hospitali zote bhapa nchini, hivyo ni vyema wananchi wajitokeze kupata huduma za matibabu pale wanapohisi  dalili za homa badala ya kutumia dawa za asili ambazo wakati mwingine zina madhara makubwa kwa mtumiaji.

Thursday, January 14, 2016

WAZIRI MUHONGO AYATAKA MAKAMPUNI KUTUMIA MAKAA YA MAWE YANAYOZALISHWA HAPA NCHINI



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MAKAMPUNI yanayotumia makaa ya mawe kufua umeme ambao huendesha viwanda vyao kwa ajili ya kuzalisha bidhaa mbalimbali hapa Tanzania, yametakiwa kutumia makaa yanayozalishwa hapa nchini na sio kuagiza nchi za nje.

Waziri wa Wizara ya nishati na madini, Profesa Sospeter Muhongo alitoa agizo hilo jana alipokuwa ametembelea mgodi wa makaa ya mawe Ngaka uliopo katika kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda, katika ziara yake ya siku moja wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma.

Profesa Muhongo alifafanua kuwa makampuni hayo yanafanya hivyo kwa lengo la kukwepa kulipa ushuru wa ndani, kwa sababu mkaa unaotoka nje ya nchi wamekuwa hawalipi ushuru au kodi ya aina yoyote ile.

“Tunataka makampuni yanayotumia makaa ya mawe hapa kwetu yatumie mkaa unaozalishwa hapa nyumbani, malighafi hii tunazalisha kwa wingi na yana ubora unaokubalika, kwa nini wasitumie mkaa wa kwetu”?, alihoji Profesa Muhongo.

MHAGAMA ASEMA SERIKALI AWAMU YA TANO IMERUDISHA HESHIMA



Na Muhidin Amri,
Songea.

WAZIRI wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, sera, uratibu, bunge na walemavu Jenister Mhagama amesema serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Dokta John Magufuli imefanikiwa kurudisha heshima ya nchi, ambayo awali ilipoteza matumaini kwa wananchi wake.

Jenister ambaye pia ni mbunge wa Jimbo la Peramiho mkoani Ruvuma, alitoa kauli hiyo hivi karibuni katika kijiji cha Lundusi wilaya ya Songea mkoani humo wakati alipokuwa akizungumza na wananchi wa kijiji hicho katika eneo la ujenzi wa ofisi ya makao makuu ya halmashauri ya wilaya hiyo.

Alisema kuwa wananchi wa jimbo hilo wanahitaji mabadiliko makubwa ya kimaendeleo hivyo viongozi waliopewa dhamana wanapaswa kuongeza jitihada na uwajibikaji katika maeneo yao ya kazi ili kuweza kuleta ufanisi kwa faida ya sasa na baadaye.

UCHANGIAJI WA CHAKULA SONGEA WAZAZI WAZUA MZOZO



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

KITENDO cha kusitisha zoezi la Wazazi kuchangia chakula, kwa shule za sekondari za kutwa za serikali zilizopo katika Manispaa ya Songea mkoani humo baadhi ya Wakuu wa shule hizo wamesema kwamba, ni ukiukwaji wa maagizo yaliyotolewa na serikali kupitia mwongozo wake uliosambazwa katika mikoa yote hapa nchini.

Aidha kufuatia hali hiyo shule hizo ambazo sasa zimefunguliwa na kuanza muhula wa masomo Januari 11 mwaka huu, nimeshuhudia watoto wakikosa chakula shuleni huku wakilazimika kuhudhuria vipindi vya masomo darasani bila kula chakula, kuanzia majira ya asubuhi hadi saa 10:00 jioni wanaporejea majumbani kwao.

Ukiukwaji huo wa agizo la serikali, wanasema kuwa unathibitisha kufuatia mwongozo uliotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Novemba 23 mwaka jana (nakala tunayo) wenye kumbu kumbu namba DC. 297/507/01/146 katika kipengele cha 4 ukielekeza kwamba majukumu ya mzazi ni pamoja na kuhakikisha kwamba huduma ya chakula kwa wanafunzi wa kutwa anachangia, yakiwemo na mahitaji mengine ya kibinadamu kama vile sare za shule na michezo, matibabu, vifaa vya kujifunzia ikiwemo daftari na kalamu.

Monday, January 11, 2016

TASWIRA KATIKA PICHA: HEKA HEKA ZA UTAFUTAJI VIFAA VYA SHULE

Baadhi ya wazazi,walezi na wanafunzi wa shule za msingi na sekondari wakiwa wamesongamana katika duka la Abbas Bookshop and Stationary lililopo katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, kwa ajili ya kununua vifaa vya shule ikiwa sehemu ya maandalizi ya kufunguliwa kwa shule baada ya kumaliza likizo ndefu kama kamera yetu ilivyowanasa. (Picha na Julius Konala)

Friday, January 8, 2016

MAJALIWA AMSIMAMISHA KAZI KIGOGO KIWANDA CHA KUSINDIKA TUMBAKU SONGEA


Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa, amemsimamisha kazi Meneja Shughuli wa Kiwanda cha kusindika tumbaku mkoani Ruvuma (SONTOP) Paul Balegwa, na kuvunja bodi ya kiwanda hicho, akidaiwa kushiriki kwa namna moja au nyingine kufanya ubadhirifu wa fedha za wakulima wanaozalisha zao hilo na kusababisha kiwanda hicho, kusitisha uzalishaji kwa zaidi ya miaka 18 iliyopita.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye ukumbi wa mikutano wa Ikulu ndogo ya Songea, Waziri Mkuu Majaliwa alisema kuwa amefikia uamuzi wa kumsimamisha kazi Meneja huyo kutokana na ubabaishaji mkubwa wa uendeshaji wa kiwanda hicho ambao ulikuwa ukifanywa kwa kushirikiana na mhasibu wake Nurdin Ponela, ambaye sasa inadaiwa amekimbia na kutokomea kusikojulikana.

Vilevile Waziri Mkuu huyo alifafanua kuwa wakulima wa zao la tumbaku kwa muda mrefu wamekuwa wakiulalamikia uongozi wa kiwanda hicho kwamba, viongozi wao kuwa ni wababaishaji huwakata fedha zao za mauzo ya tumbaku bila kufuata utaratibu.

BENKI YA POSTA YAJIVUNIA MAFANIKIO YAKE

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akifungua tawi la benki ya Posta Songea mkoani Ruvuma.

Na Kassian Nyandindi,
Songea.

TATIZO la kutokuwa na wafanyakazi wabunifu katika Benki ya Posta Tanzania, imeelezwa kuwa ni moja kati ya changamoto ambayo ilichangia kudorola kiuchumi na kuifanya benki hiyo, ishindwe kusonga mbele kimaendeleo katika kuwahudumia wateja wake.

Aidha imefafanuliwa kuwa baada ya kubaini tatizo hilo, benki hiyo imeunda utaratibu mwingine mpya ambao hivi sasa kasi yake ni kubwa ya uendeshaji wa huduma za kibenki, na kufanikiwa kutengeneza faida ya shilingi bilioni 10.3 katika miaka mitatu iliyopita.

Sabasaba Mushinge ambaye ni Mkurugenzi mtendaji wa benki ya Posta hapa nchini, alisema hayo juzi katika hafla fupi ya uzinduzi wa tawi jipya la benki ya Posta Songea mkoani Ruvuma, ambayo ilizinduliwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa.

Mushinge aalisema kuwa wameweza kufikia asilimia 70 ya ukarabati wa matawi yote yaliyopo hapa nchini, na kwamba mafanikio hayo yametokana na mabadiliko ya kiuongozi baada ya benki kwa muda mrefu kudorola kiuchumi.

SERIKALI KUWEKA MPANGO WA MATUMIZI YA TREKTA KWA WAKULIMA



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

SERIKALI hapa nchini imesema kuwa, itaweka mpango mzuri wa kuhakikisha kwamba kila mwananchi katika maeneo anayozalisha kilimo cha mazao ya chakula na biashara, anahamasishwa alime mazao yake shambani kwa kutumia matrekta na kuachana na jembe la mkono ili mazao hayo waweze kuzalisha kwa wingi.

Aidha imeelezwa kuwa mpango huo unaweza kuwafikia wakulima hao kwa urahisi, endapo viongozi waliopo madarakani katika ngazi za halmashauri ya wilaya hadi mkoa, wataweza kuweka mikakati madhubuti katika bajeti zao kwa kuhakikisha kwamba wakulima wanapewa matrekta hayo ya kulimia kwa gharama nafuu.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Majaliwa Kassim Majaliwa alisema hayo hivi karibuni mjini Songea akiwa katika ziara yake ya siku tatu mkoani humo, akiwajibika kupita katika maeneo mbalimbali kuona hali halisi ya maendeleo na kuweka msisitizo wa namna ya utendaji kazi.

“Tutatumia mkoa wenu wa Ruvuma kama mfano ndani ya nchi, kupitia kilimo mmeweza kuwa watano kitaifa katika kukuza pato la mwananchi mmoja mmoja, hivyo basi nasisitiza maeneo yote ya mabondeni, tuwahamasishe pia wananchi waendeshe kilimo cha umwagiliaji, kuna kila sababu kwenye eneo hili tuhakikishe tunajikita zaidi”, alisisitiza Waziri Mkuu Majaliwa.

Pia alieleza kuwa kutokana na wananchi wa mkoa huo kuonekana wengi wao wana kipato kizuri, hivyo wanapaswa kuwa na matumizi mazuri ya fedha ili waweze kujiletea maendeleo kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.

Wednesday, January 6, 2016

WAZIRI MKUU AKEMEA NA KUPIGA MARUFUKU VITENDO VYA UTOAJI MIMBA HOSPITALI YA RUFAA SONGEA



Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

MADAKTARI na Wahudumu wa afya wanaofanya kazi katika Hospitali ya Rufaa mkoani Ruvuma, wamejikuta wakiwa katika wakati mgumu baada ya Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaliwa, kuwajia juu na kukemea vitendo vya utoaji mimba ambavyo vimeshamiri katika hospitali hiyo.

Hali hiyo ilijitokeza katika ukumbi wa mikutano wa hospitali hiyo, ambapo Waziri Mkuu Majaliwa alimweleza Mganga mkuu, Daniel Malekela kwamba watumishi wake hasa madaktari wamekuwa na mazoea ya kufanya vitendo hivyo hasa kwa wanafunzi wanaosoma shule ya msingi na sekondari.

“Mganga Mkuu, hospitali yako inayosifa ya kutoa mimba, madaktari wamekuwa wakitumia wodi namba tano kufanyia kazi hii sasa natoa onyo kali ni marufuku kuanzia leo, sitaki kusikia tena jambo hili nitawafukuza kazi na kuwafunga”, alisisitiza Waziri Mkuu Majaliwa.

Waziri Mkuu huyo alifafanua kuwa utoaji mimba, umekuwa ukifanyika hata katika jengo la upasuaji lililopo hospitalini hapo na kuongeza kuwa jambo hilo hataki kuliona linarudia tena na kwamba, hatakuwa na msamaha wowote kwa atakayehusika na kitendo hicho.

WAZIRI MKUU MAJALIWA AITAKA NFRA KUPELEKA MAGUNIA KWA WAKULIMA VIJIJINI



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WAZIRI Mkuu Majaliwa Kassim Majaliwa, ameutaka uongozi wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA) hapa nchini, kuhakikisha kwamba wanajipanga kikamilifu katika kuhakikisha kwamba wakulima wa zao la mahindi wanapatiwa magunia ya kuhifadhia zao hilo, katika maeneo ambayo yametengwa huko vijijini msimu ujao wa mavuno ya mazao ya chakula.

Agizo hilo amelitoa leo katika ziara yake ya siku tatu ya kutembelea na kuona maendeleo ya sekta mbalimbali mkoani Ruvuma, na kuhakikisha kwamba anatekeleza agizo la Rais John Magufuli linalosema hakuna Mtanzania atakayekufa njaa.

Alieleza kwamba, wafanyabiashara ambao wamekuwa wakipatiwa magunia na NFRA kwa ajili ya kununulia mahindi na wakulima wanapojaribu kutafuta namna ya kuyapata magunia hayo, imekuwa ni tatizo kwao kuyapata kwa urahisi.

Monday, January 4, 2016

WAZIRI MKUU MAJALIWA ASHANGAZWA NA VIONGOZI WA USHIRIKA SONGEA KUTAKA KUJENGA VIBANDA VYA BIASHARA KATIKA JENGO LA KIWANDA CHA KUSINDIKA TUMBAKU

Waziri Mkuu, Majaliwa Kassim Majaliwa kulia, akisalimiana jana na Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu mara baada ya kuwasili uwanja wa ndege wa songea, kwa ajili ya kuanza ziara yake ya siku tatu mkoani humo.


Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Majaliwa Kassim Majaliwa amemuagiza Mkuu wa mkoa huo, Said Mwambungu ahakikishe kwamba kabla hajamaliza ziara yake ya siku tatu anahitaji kuonana na viongozi wa Chama Kikuu cha Ushirika cha Tumbaku wilaya ya Songea na Namtumbo (SONAMCU) mkoani humo.

Agizo la Waziri mkuu huyo, amelitoa leo wakati alipokuwa Ikulu ndogo ya Songea kufuatia kusuasua kwa uzalishaji wa zao la tumbaku na kutofanya kazi kwa muda wa miaka 18 kiwanda cha kusindika zao hilo kilichopo Manispaa ya Songea mkoani hapa.

“Kabla sijamaliza ziara yangu, nahitaji kuonana na viongozi wote wa chama hiki kikuu cha uzalishaji wa tumbaku na mwakilishi mmoja mmoja kwa kila mkulima, ili niweze kupata mpango wao mkakati wa uendelezaji wa zao hili sambamba na ufufuaji wa kiwanda”, alisisitiza Majaliwa.

Saturday, January 2, 2016

WAZIRI MKUU MAJALIWA KUFANYA ZIARA YA KIKAZI MKOANI RUVUMA



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WAZIRI Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa atawasili mkoani Ruvuma kesho Jumapili kwa ajili ya kufanya ziara yake ya kikazi, ikiwemo kukagua shughuli mbalimbali za kimaendeleo na kuzungumza na wananchi.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Mkuu wa mkoa huo Said Mwambungu alisema kuwa Majaliwa atawasili majira ya saa 6:00 mchana, katika uwanja wa ndege mjini Songea.

Kassim Majaliwa.
Mwambungu alifafanua kuwa Waziri huyo atakuwa na ziara ya siku tatu ambapo baada ya kupokelewa katika uwanja huo wa ndege, atakwenda Ikulu ndogo Songea na kusomewa taarifa ya maendeleo ya mkoa huo.

Alisema kuwa siku itakayofuatia Januari 3 mwaka huu, atafanya ufunguzi wa ofisi za jengo jipya la shirika la Posta lililopo mjini hapa, ukaguzi wa ghala la chakula (NFRA) na maendeleo ya ujenzi wa ofisi za Halmashauri ya wilaya ya Songea vijijini iliyopo Peramiho wilayani humo.

ELIAS MWALEWELA AKAMATWA AKISAFIRISHA KAHAWA KWA NJIA YA MAGENDO



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MFANYABIASHARA mmoja ambaye anajulikana kwa jina la Elias Mwalewela (46) anayeishi mtaa wa Manzese Mbinga mjini mkoani Ruvuma, amekamatwa akitorosha kahawa ya maganda isiyokobolewa kiwandani, kwenda Jijini Mbeya kwa njia ya magendo bila kufuata taratibu na sheria husika.  

Aidha imeelezwa kuwa wakati zao hilo analitorosha, alikuwa akitokea wilayani Mbinga mkoani humo kwa lengo la kuipeleka huko, huku akijua fika kahawa ya maganda hairuhusiwi kusafirishwa kutoka wilaya moja kwenda nyingine.

Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Venance Mwamengo alisema kuwa baada ya kupata taarifa kutoka kwa wasamaria wema juu ya utoroshaji huo, alichukua jukumu la kufuatilia suala hilo ndipo baadaye alifanikiwa kumkamata katika kijiji cha Liganga wilaya ya Songea vijijini mkoani hapa kwa kushirikiana na askari aliokuwa nao.

Alifafanua kuwa alimkamata Disemba 30 mwaka jana, majira ya saa tano usiku akiwa na gari aina ya Fuso lenye namba za usajili T 818 ADH ambalo lilikuwa likiendeshwa na Geati Mwajungwa mkazi wa Lujewa wilaya ya Mbarali mkoani Mbeya.