Monday, May 30, 2016

WAKULIMA WAIOMBA HALMASHAURI KUKAMILISHA UJENZI WA MRADI WA UMWAGILIAJI

Betramu Sanga ambaye ni afisa kilimo (katikati) akiwapa maelekezo juu ya kilimo bora cha zao la mpunga wakulima wa kijiji cha Mabuni kata ya Litumbandyosi wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma.



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WAKULIMA wanaozalisha zao la mpunga katika mradi wa umwagiliaji Sanga mabuni uliopo kijiji cha Mabuni kata ya Litumbandyosi wilaya ya Mbinga mkoa wa Ruvuma, wameiomba Halmashauri ya wilaya hiyo kufanya jitihada ya kukamilisha ujenzi wa mfereji wa kuleta maji shambani ili waweze kuzalisha zao hilo kwa wingi.

Aidha wameeleza kuwa mfereji huo unaoleta maji shambani ambao una urefu wa mita 5,850 kutoka kwenye banio kuu la umwagiliaji, ambapo zilizojengwa mpaka sasa ni mita 3,175 na kwamba zilizobakia ni mita 2,625 ambazo bado ujenzi wake haujakamilika na kuweza kuleta maji kwenye mashamba yaliyopandwa zao hilo.

Silvester Ngonyani ambaye ni Mwenyekiti wa mradi huo, alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ambao walitembelea kwa lengo la kujionea mafanikio wanayoyapata na changamoto mbalimbali ambazo hukabiliana nazo wakulima hao. 

WANANCHI MPITIMBI KUNUFAIKA NA UJENZI WA VISIMA VYA MAJI



Na Julius Konala,
Songea.

WANANCHI wanaoishi katika kata ya Mpitimbi wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, watanufaika na mradi wa visima vya maji ambavyo ujenzi wake unaendelea kufanyika katika kata hiyo na kwamba mpaka kukamilika kwake, vitaweza kuwafanya waweze kuondokana na adha ya upatikanaji wa maji ambayo imekuwa ikiwatesa kwa muda mrefu sasa.

Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na Diwani wa kata hiyo, Dionis Mang’omes wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu mjini hapa ambapo alisema ni visima 24 vya maji ya kupampu, ambavyo vinajengwa katika kata hiyo.

Mang’omes alisema kuwa mradi huo ambao unafadhiliwa na shirika la Times Life kupitia shirika la Watawa wa Benedictine wa Hanga, utawanufaisha wananchi wa vijiji vya Mpitimbi A na Mpitimbi B vilivyopo katani humo.

DED MBINGA APONGEZWA KWA KUCHUKUA HATUA YA KUDHIBITI MAPATO YATOKANAYO NA MKAA WA MAWE



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

BAADHI ya wananchi wanaoishi katika kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wamempongeza Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo Venance Mwamengo kwa kuchukua hatua ya kufunga mashine ya kukusanyia ushuru katika eneo la Amani Makolo, ambalo husafirishwa mkaa wa mawe kwenda nje ya wilaya hiyo kitendo ambacho kwa kiasi kikubwa kimesaidia kudhibiti mapato ya fedha yatokanayo na mkaa huo.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Walisema kuwa hapo awali kabla ya kufungwa kwa mashine hiyo ya Electronic (EFD’S) mapato mengi yalikuwa yakipotea kutokana na kukusanywa kwa njia ya vitabu vya risiti, ambapo watendaji waliokuwa wakipewa dhamana ya ukusanyaji wa fedha hizo za ushuru walikuwa hawawajibiki ipasavyo.

Theodosia Mahundi mkazi wa kijiji hicho aliwaeleza waandishi wa habari kuwa udhibiti huo wa mapato unapaswa kufanywa kwa kutumia mashine hiyo, katika kila eneo ambalo serikali inakusanya mapato ili kuweza kudhibiti mianya ya wajanja wachache, ambao wamekuwa wakitafuta njia za ufujaji wa fedha za serikali.

Mahundi alisema kuwa ni faraja kwao kuona mapato hayo jinsi yanavyodhibitiwa na kwamba wanaimani kuwa hata serikali, itaweza kuwahudumia wananchi wake kwa kuwapelekea huduma muhimu kama vile madawa kwenye zahanati na vituo vya afya kwa wakati.

Naye Renatus Mapunda mkazi wa kijiji cha Amani Makolo kata ya Amani Makolo alisema kuwa hapo awali madereva wengi wanaosafirisha mkaa wa mawe kwenda nje ya wilaya hiyo, ameshuhudia wakiwa wanakwepa kulipa ushuru huo ambapo alitoa ushauri kwa kuitaka serikali kuendelea kuongeza nguvu ya udhibiti wa mapato yatokanayo na mkaa huo, ili jamii iweze kunufaika nayo kwa njia ya kuwaletea maendeleo katika nyanja mbalimbali.

TFDA YATEKETEZA BIDHAA FEKI NJOMBE



Na Kassian Nyandindi,
Njombe.

MAMLAKA ya Chakula, Dawa na Vipodozi (TFDA) Kanda ya nyanda za juu Kusini imeteketeza kilo 1,000 za bidhaa aina mbalimbali, Halmashauri ya wilaya na mji wa Njombe mkoani hapa, ambazo zimekwisha muda wa matumizi yake kwa binadamu zenye thamani zaidi ya shilingi milioni 10.

Uteketezaji wa bidhaa hizo unafuatia msako mkali ulioendeshwa na mamlaka hiyo kwa muda wa siku mbili, baada ya kupata taarifa kutoka kwa wasamaria wema kwamba maduka mengi yaliyopo mkoani humo baadhi yake yamekuwa yakiuza bidhaa zilizopitwa muda wa matumizi yake.

Kaimu Mkuu wa mkoa wa Njombe, Anatory Choya amewatahadharisha wananchi wa mkoa huo kuwa makini na bidhaa hizo huku akikemea tabia ya wafanyabiashara kuacha mara moja, kuuza bidhaa zilizopitwa na wakati kwani wamekuwa wakihatarisha usalama wa afya za watumiaji.

Aidha Choya alisema kuwa msako huo utakuwa endelevu kwa kupita kukagua kila duka lililopo mkoani humo, ikiwa pia ni lengo la kutokomeza kabisa tabia kwa baadhi ya wafanyabiashara wanaoingiza bidhaa hizo zilizopigwa marufuku na serikali.

Sunday, May 29, 2016

WAKULIMA TUNDURU WATAKIWA KUFUATA MAELEKEZO YA WATALAAMU WA UGANI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

WAKULIMA wanaozalisha mazao ya aina mbalimbali wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wametakiwa kufuata maelekezo wanayopewa na wataalamu wa ugani wa wilaya hiyo ili waweze kujiletea maendeleo katika sekta ya kilimo na kuondokana na umaskini uliokithiri miongoni mwao, ambao umekuwa ukiwasumbua kwa miaka mingi katika maeneo ya vijiji vyao wanavyoishi.

Mwito huo ulitolewa na mwakilishi wa Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Tunduru, Afisa kilimo wa Halmashauri hiyo Chiza Marando wakati akizungumza na vikundi vya wakulima kutoka vijiji vya Legezamwendo, Kidodoma, Machemba na Mkwajuni.

Aidha Marando alisema kuwa mtindo wakati wote kuwalaumu wataalamu hao ambao umekuwa ukifanywa na wananchi wengi katika vijiji wilayani humo, hauwezi kuwasaidia na kwamba kinachotakiwa waitikie wito na kusikiliza maelekezo wanayopewa ili waweze kuzalisha mazao bora.

WARATIBU ELIMU KATA WATAKIWA KUKUSANYA TAKWIMU SAHIHI

MKuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu.


Na Joyce Joliga,
Songea.

WARATIBU elimu kata katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wameshauriwa kuhakikisha kwamba wanasimamia kikamilifu zoezi la ukusanyaji  takwimu kwa umakini mkubwa ili kuweza kupata usahihi wa takwimu za idadi ya wanafunzi kwa kila shule za msingi, ziweze kusaidia kuhakikisha vyandarua vinavyogawiwa kwa wanafunzi hao vinatumika kwa walengwa husika, kwani ikibainika kutoa takwimu za uongo watachukuliwa hatua kali za kisheria.

Agizo hilo limetolewa juzi na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa hiyo, Jenifer Christian wakati alipokuwa akifungua mafunzo ya siku moja ya  mpango wa ugawaji vyandarua mashuleni, yaliyofanyika mjini hapa.

Hii ni awamu ya nne kwa Waratibu kata, zaidi ya 30 toka Halmashauri tatu za Manispaa ya Songea, Madaba, pamoja na wilaya ya Songea kupata vyandarua hivyo ambapo mafunzo hayo yaliandaliwa na shirika lisilo la kiserikali la PSI.

NYASA WALALAMIKIA KUNYANYASWA WANAPOHITAJI HUDUMA ZA MATIBABU



Na Muhidin Amri,
Nyasa.

BAADHI ya wajasirimali wadogo wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, wamesema wanashindwa kujiunga  na mfuko wa Taifa wa bima ya afya (NHIF) na mfuko wa afya ya jamii (CHF) kutokana na  manyanyaso wanayopata wanachama wa mfuko huo, pale wanapokwenda katika  zahanati na vituo vya kutolea huduma za matibabu wilayani humo.

Walisema kuwa wanapenda kujiunga na mpango huo wa huduma za afya, NHIF na CHF lakini tatizo kubwa linalowafanya wasite kujiunga na mifuko hiyo ni pale wanaposhuhudia wenzao ambao tayari wamejiunga, kutopata matibabu ya haraka kutokana na watoa huduma kwenye vituo hivyo kuwanyanyapaa kwa madai kwamba wanakosa fedha kutoka kwa watu ambao wanakuja na fedha taslimu kulipia matibabu.

Walitoa kauli hiyo hivi karibuni, wakati wa zoezi la uhamasishaji wajasiriamali wadogo ambao ni wateja wa Benki ya Wananchi Mbinga (MCB) wilayani humo ili waweze kujiunga na mpango huo, ambapo jumla ya wajasirimali 112 waliweza kujitokeza na kujiunga.

WAVUVI WAMTAKA RAIS MAGUFULI KUMCHUKULIA HATUA MKURUGENZI MTENDAJI WILAYA YA NYASA

Rais John Magufuli.


Na Muhidin Amri,
Nyasa.

MAISHA ya wavuvi katika  mji wa Mbambabay wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma yako hatarini, kufuatia wavuvi hao kutumia maji ya ziwa Nyasa ambayo sio safi na salama kwa ajili ya kunywa na matumizi mengine ya kawaida, katika maisha yao ya kila siku.

Imeelezwa kuwa hali hiyo inatokana na kukosekana kwa huduma hiyo ya maji katika eneo wanalofanyia shughuli zao za biashara ya kuuza samaki.

Wavuvi hao pia wameilalamikia Ofisi ya maliasili na uvuvi wilayani humo kwa kushindwa kupeleka huduma hiyo na miaka mingi sasa imepita, kwa ajili ya matumizi  ya wavuvi na wananchi wengine wanaofika kwa ajili ya kujipatia kitoweo cha samaki na kufanya shughuli  zao za kujiongezea kipato.

Kutokana na hali hiyo, kuna uwezekano mkubwa wa eneo hilo kukumbwa na magonjwa hatari ya mlipuko au kuambukiza kama vile kuhara, kipindupindu na magonjwa ya matumbo ambayo ni hatari kwa maisha ya binadamu.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti wavuvi hao  walisema kuwa, Ofisi husika katika Halmashauri hiyo haina msaada wowote kwa wavuvi kwani hata pale inapotokea dharura ziwani  ya watu kuzama maji, wao wenyewe ndiyo wanaofanya jitihada ya kujiokoa wenyewe.

Tuesday, May 24, 2016

SERIKALI YAPELEKA BOTI TATU NYASA KUFANYA KAZI YA KUTAFUTA MIILI YA WATU AMBAO WAHOFIWA KUFA MAJI ZIWA NYASA



Na Kassian Nyandindi,

Songea.

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma, limesema miili ya watu 11 ambao wahofiwa kufa maji katika ziwa Nyasa wilayani Nyasa mkoani humo, kufuatia boti walilokuwa wakisafiria kupoteza muelekeo bado haijapatikana hivyo serikali imeongeza maboti matatu, ambayo yatafanya kazi ya kuendelea kutafuta miili hiyo katika ziwa hilo.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma, Zubery Mwombeji.
Akizungumza na mwandishi wetu Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Zubery Mwombeji alisema kuwa ni siku ya nne sasa imepita tokea tukio hilo lilipotokea Mei 20 mwaka huu majira ya jioni, wakati watu hao wakitokea mji wa Mbamba bay kwenda nchi jirani ya Malawi wakiwa kwenye boti ndogo la mizigo.

Mwombeji alifafanua kwamba wameweza kuyapata majina ya watu hao wanaohofiwa kupoteza maisha katika ziwa hilo baada ya ndugu zao kujitokeza na kuweza kuyataja kuwa ni, Benjamin Seme (41) na Florian Mwamlenga (31) wote wakazi wa wilaya ya Kyela mkoani Mbeya.

WANANCHI WAISHIO PEMBEZONI MWA TUNDURU WATESEKA NA MAMBA MTO RUVUMA



Na Steven Augustino,
Tunduru.

WATU watatu wamelazwa katika hospitali ya Misheni ya Mbesa wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, baada ya kujeruhiwa na mamba katika matukio tofauti yaliyojitokeza wilayani humo.

Hayo yamebainishwa na Mganga mkuu wa hospitali hiyo, Dokta Ires Sekreman wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu katika mahojiano yaliyofanyika kwa njia ya simu, ambapo pamoja na mambo mengine hospitali hiyo ambayo ipo pembezoni mwa Tanzania imekuwa msaada mkubwa kwa wananchi hao, ambao hukumbwa na matatizo ya aina mbalimbali ya kiafya.

Dokta Sekreman alisema kwamba amekuwa akipokea majeruhi na wagonjwa wengi kutoka katika vijiji vilivyopo nchi jirani ya Msumbiji hasa ambao hujeruhiwa na mamba, ambayo huwapata wakati wakivua samaki na kufanya shughuli hizo katika mto Ruvuma.

Monday, May 23, 2016

WAPOTEZA MAISHA WAKATI WAKISAFIRI KUTOKA MBAMBA BAY KWENDA MALAWI KATIKA ZIWA NYASA

Ziwa Nyasa.


Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WATU 11 wahofiwa kufa maji wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, kufuatia boti walilokuwa wakisafiria katika ziwa Nyasa wilayani humo kupoteza muelekeo na kuzama kwenye maji ya ziwa hilo, wakati wakielekea nchi jirani ya Malawi.

Aidha imeelezwa kuwa  tukio hilo lilitokea Mei 20 mwaka huu majira ya jioni, wakati watu hao wakitokea katika mji wa Mbamba bay kwenda Malawi wakiwa kwenye boti ndogo la mizigo.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma, Zubery Mwombeji amethibitisha hayo na kueleza kuwa miili na majina ya watu hao bado haijapatikana na kwamba jitihada zinaendelea za kuitafuta, kwa kushirikiana na askari wa idara ya uhamiaji wilayani hapa.

UKWELI JUU YA UBADHIRIFU FEDHA ZA UCHAGUZI MKUU MBINGA UPO WAPI?


Na Kassian Nyandindi,

SERIKALI siku zote imekuwa ikiwataka watumishi au watendaji wake wa serikali, kufanya kazi kwa uadilifu mkubwa na kuachana na vitendo vya ubadhirifu wa fedha au mali za umma.

Kassian Nyandindi, Mwandishi wa makala haya.
Tuhuma za wizi wa fedha tumekuwa tukizisikia kupitia vyombo vya habari kila kukicha, kufuatia viongozi waliopo madarakani kuibua hoja hizo na kuunda tume za kuchunguza mambo haya ili kuweza kubaini wabadhirifu waliohusika kufanya hivyo.

Katika makala haya ya uchambuzi, napenda kuelezea kwa ufupi juu ya mwenendo wa hoja iliyotolewa hivi karibuni wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kuhusiana na fedha za Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwaka jana zinazodaiwa kufanyiwa ubadhirifu kutokana na ukiukwaji wa matumizi mabaya au kutofuata miongozo husika ya matumizi yake.

Tuhuma za ubadhirifu wa fedha hizo shilingi bilioni 1.4 ambazo zilitolewa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwenda kwa Halmashauri ya wilaya hiyo kufanya kazi iliyolengwa, ilitolewa na Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga katika baraza la Madiwani wa halmashauri hiyo ambalo liliketi Mei 11 mwaka huu mjini hapa.

Sunday, May 22, 2016

WAKULIMA TUNDURU WATAKIWA KUACHANA NA IMANI ZA USHIRIKINA



Na Steven Augustino,
Tunduru.

WAKULIMA wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wametakiwa kuondokana na tabia za imani ya mambo ya ushirikina kwa madai kwamba wamekuwa wakikosa mavuno katika mashamba yao kutokana na kuchukuliwa kimazingara maarufu kwa jina la Chitola, jambo ambalo limekuwa likiwafanya washindwe kupiga hatua mbele za kimaendeleo.

Aidha kufuatia hali hiyo wameshauriwa kutumia mbinu za kilimo bora, ili waweze kupata mazao mengi shambani badala ya wakati wote kuendekeza imani hizo ambazo hazina faida katika maisha yao ya kila siku.

Katibu tawala wa wilaya hiyo, Ghaibu Lingo ambaye alikuwa akimwakilisha Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Agnes Hokororo alisema hayo alipokuwa akizungumza kwenye maadhimisho ya sherehe za siku ya wakulima shambani iliyofanyika katika mashamba darasa ya kilimo cha mahindi na mpunga, yaliyopo kijiji cha Legezamwendo wilayani humo .

Aidha Lingo aliwataka wakulima hao, kuondokana na mila hizo potofu badala yake wawatumie pia wataalamu wa kilimo yaani maafisa ugani, ili waweze kuzalisha mazao yao kwa ubora na viwango vinavyokubalika.

MADIWANI NAMTUMBO WAILALAMIKIA KAMPUNI YA MANTRA KWA KUTOTOA USHIRIKIANO KWA HALMASHAURI

Baadhi ya Waandishi wa habari mkoa wa Ruvuma, ambao walitembelea Kampuni ya Mantra inayotarajia kuanza kuchimba madini aina ya Urani wilayani Namtumbo mkoani humo, wakipata ufafanuzi juu ya madini hayo kutoka kwa Wataalamu wa kampuni hiyo.


Na Steven Augustino,
Namtumbo.

KAMPUNI ya Mantra inayotarajia kuchimba madini ya Urani,  katika  eneo  la  mto Mkuju wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma imetuhumiwa kwamba imekuwa haitoi ushirikiano kwa Halmashauri ya wilaya hiyo, pale wanapoalikwa kuhudhuria mikutano ya baraza  la Madiwani wilayani humo.

Tuhuma hizo zilitolewa na Mwenyekiti wa baraza hilo, Daniel Nyambo mbele ya Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Ally Mpenye wakati akizungumza na Madiwani hao katika kikao cha baraza  hilo kilichoketi hivi  karibuni wilayani humo.

Wakifafanua taarifa hiyo kwa nyakati tofauti, Nyambo na Mkurugenzi wa  Halmashauri  hiyo, Ally Mpenye waliwaeleza Madiwani hao kwamba kila wanapowalika viongozi wa kampuni hiyo kwa ajili ya kuhudhuria  vikao  vya  baraza hilo, hawafiki jambo linalowaletea mashaka juu ya mambo wanayotaka kuficha wakati wa utekelezaji wa mradi huo na madhara yanayoweza kujitokeza kwa jamii.

AFISA ARDHI TUNDURU AHUKUMIWA KWENDA JELA MIAKA MIWILI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

MAHAKAMA ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, imemhukumu Ofisa mthamini ardhi mstaafu wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Bernad Nyasi (60) kutumikia kifungo cha miaka miwili jela baada ya kupatikana na hatia katika kosa la kughushi nyaraka na kutoa hati za uongo, kwa wateja waliotakiwa kupewa vipande vya ardhi wilayani humo.

Adhabu hiyo ambayo pia ilimpatia nafasi kwa kumtaka mtuhumiwa huyo kulipa faini ya shilingi 500,000 ilitolewa na Hakimu mfawidhi wa Mahakama ya wilaya hiyo, Gladys Barthy baada ya kuridhika na ushahidi uliotolewa katika shauri hilo la jinai namba 6/2016.

Katika hukumu hiyo Mahakama hiyo, pia imewaachilia huru washtakiwa wengine wawili waliokuwa wanakabiliwa na shtaka hilo ambapo  mpima ardhi wa Halmashauri hiyo, Mohamed Hamis (35) na mhudumu wa ofisi ya ardhi ya wilaya ya Tunduru Masud Kanduru (40).

Kwa mujibu wa hati ya mashtaka hayo, Mahakama hiyo ilimkuta na hatia Ofisa ardhi huyo katika shtaka la nane kati ya makosa 10 yaliyokuwa yanawakabili watuhumiwa hao ambalo ni la kughushi hati namba TUR/77 ya Mei 20 mwaka 2015 iliyokuwa ikimtambulisha Mariam Nyenje kuwa ni mmiliki halali wa kiwanja namba 104 Ploti namba 0 katika eneo la Nakayaya wilayani hapa.

Friday, May 20, 2016

MAAMBUKIZI VIRUSI VYA UKIMWI BADO NI TATIZO MKOA WA RUVUMA




Na Kassian Nyandindi,
Songea.

TANGU ilipoanzishwa Huduma ya Tiba na Matunzo (CTC) katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma mwaka 2004, kwa watu wanaoishi na Virusi Vya Ukimwi (VVU) hadi sasa watu 21,347 wamegundulika kuwa na ugonjwa huo, ambapo tayari watu 20,576 wamesajiliwa na kupewa huduma husika.

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Thabit Mwambungu.
Aidha kufuatia hali hiyo, Wadau wa afya katika Manispaa hiyo wamesikitishwa na hali mbaya ya maambukizi ya ugonjwa huo ambao hivi sasa unakua kwa kasi, huku watu waliopima VVU 213,212 kati yao 21,347 waligundulika kuwa na maambukizi ya ugonjwa huo.

Hayo yalisemwa juzi na Mratibu wa ukimwi na kinga katika Manispaa ya Songea, Felista Kibena kwenye hafla fupi iliyoshirikisha wadau, wasambazaji na wauzaji wa bidhaa ya kondomu ambayo ilifanyika mjini hapa na kuandaliwa na shirika lisilo la kiserikali la PSI Tanzania ikilenga pia kujadili juu ya usambazaji wa bidhaa hizo za afya.

Felista alifafanua kuwa Manispaa hiyo, imefanikiwa Kupunguza kiwango cha maambukizi toka asilimia 4.8 mwaka 2014 hadi kufikia asilimia 4 mwaka 2015 ambapo zaidi ya asilimia 60 wanatambua hali zao za maambukizi na kwamba kati ya hao waliosajiliwa ni wagonjwa 9,130 ambao wanatumia dawa za kupunguza makali ya VVU ikiwa ni sawa na asilimia 44.

DED MBINGA AWATAKA VIONGOZI KUWA WAADILIFU


Mkurugenzi mtendaji Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Venance Mwamengo upande wa kushoto, akizungumza na wakulima wa zao la Mhogo kijiji cha Kigonsera kata ya  Kigonsera wilaya humo ambapo aliahidi kuwasaidia fedha, kwa ajili ya kununulia mashine ya kisasa kusindika zao hilo na mazao mengine.
Na Mwandishi wetu,
Mbinga.

MKURUGENZI Mtendaji Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Venance Mwamengo, amewataka viongozi waliopo katika vikundi  vya  wakulima wilayani humo kuwa waaminifu na waadilifu ili kuvifanya vikundi hivyo viweze kufikia malengo yake yaliyokusudiwa na kuweza kupunguza kero na matatizo mbalimbali, yanayowakabili wakulima waweze kuondokana na umaskini au ukosefu wa ajira.

Mwamengo alitoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki, alipokuwa akizungumza na wakulima wa kikundi cha Jitegemee ambacho hujishughulisha na kilimo cha mbaazi, mhogo, mahindi na alizeti katika kijiji cha Kigonsera wilayani humo huku akisisitiza kwamba  uaminifu wa viongozi hao utasaidia kwa kiasi kikubwa vikundi hivyo kuwa endelevu.

Alisema serikali imekuwa  ikivisaidia fedha na hata ushauri kwa kuwapeleka huko watalaamu wake, lakini tatizo kubwa lililopo viongozi wasiotambua wajibu wao katika vikundi wamekuwa kikwazo kikubwa kutokana na kutaka kujinufaisha kupitia mgongo wa wenzao kwa manufaa yao binafsi,  jambo ambalo huchangia kwa kiasi kikubwa visiweze kusonga mbele.

WAKULIMA WA KAHAWA WASHAURIWA KUTUMIA MICHE YA VIKONYO



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WAKULIMA wanaozalisha zao la kahawa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wameshauriwa kuendelea kutumia miche bora ya kahawa aina ya vikonyo ambayo haishambuliwi na wadudu waharibifu kwa urahisi na wakati wa mavuno, huwafanya waweze kupata mazao mengi shambani.

Aidha Taasisi ya utafiti wa zao la kahawa (TaCRI) wilayani humo, imepongezwa kwa jitihda zake inazoendelea kuzifanya, kwa kutoa elimu kwa wakulima wa zao hilo hususan katika uzalishaji wa miche hiyo bora ya kahawa ambayo huwaletea tija kubwa wakulima na kuwafanya waondokane na umaskini.

Hayo yalisemwa na mkulima mmoja maarufu wa zao hilo kutoka kijiji cha Sepukila kata ya Kilimani wilayani hapa, Festo Mapunda alipokuwa akihojiwa na waandishi wa habari juu ya uendelezaji wa kilimo bora cha zao hilo katika wilaya ya Mbinga.

“Mimi binafsi naishukuru taasisi hii ya TaCRI, kwa kutupatia elimu ya kilimo bora cha kahawa, hivi sasa wakulima tunaweza kuzalisha miche ya vikonyo na kutoa ushauri juu ya kilimo bora cha zao hili kwa wengine ambao wanapenda kulima kahawa”, alisema Mapunda.

Sunday, May 15, 2016

WAKULIMA MBINGA WAIOMBA SERIKALI KUWAPATIA MASHINE YA KUSINDIKA ZAO LA MHOGO

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WAKULIMA wa zao la Mhogo katika kijiji cha Kigonsera kata ya Kigonsera wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wameiomba serikali kuangalia uwezekano wa kuwapatia mashine ya kusindika  zao hilo na mazao mengine wanayolima, ili waweze kuongeza thamani ya uzalishaji na kuwafanya waweze kupata soko la uhakika la kuuzia mazao yao.

Hayo yalibainishwa hivi karibuni na wakulima hao, walipokuwa wakizungumza na mwandishi wetu  wakiwa kwenye shamba darasa  la mhogo  linalotumika kwa ajili ya kufundishia wakulima kutoka maeneo mbalimbali ya wilaya ya Mbinga na wakulima wa wilaya nyingine za mkoa huo, juu ya kilimo bora cha mhogo.

Katibu wa kikundi cha Jitegemee, Oscar Ndunguru alisema kuwa wamekuwa wakulima wazuri  wa zao la mhogo na mazao mengine ya chakula na biashara  kutokana na elimu wanayoipata kutoka kwa maofisa ugani, ambapo changamoto kubwa wanayokabiliana nayo sasa ni ya ukosefu wa mashine hiyo ya kusindika mazao wanayozalisha, jambo ambalo linasababisha wakose soko la uhakika la kuuzia mazao yao.

“Tumekuwa wakulima wazuri ambao tunafuata kanuni bora za kilimo hiki cha mhogo, bado tatizo kubwa linalotukabili hapa kwetu ni ukosefu wa soko la uhakika ambalo linachangiwa kwa kiasi kikubwa kutokana na ukosefu wa mashine ya kisasa ya kusindika zao hili, ili tuweze kuongeza thamani”, alisema Ndunguru.

TUNDURU WAMUOMBA MAGUFULI KUTATUA KERO YA MGOGORO WA ARDHI

Rais John Pombe Magufuli.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

SERIKALI imeombwa kuingilia kati na kutafuta ufumbuzi juu ya mgogoro wa mashamba ambao unaendelea kufukuta katika kitongoji cha Ndiyomana kilichopo kijiji cha Msinji kata ya Ligoma wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, kati ya wakulima na wageni wa kutoka shirika la WWF ambao hufanya uwekezaji wa utunzaji wa misitu na ufugaji wa wanyama wilayani humo.

Mgogoro huo ambao umedumu kwa muda mrefu sasa na kufikia hatua ya kuwa kero kwa wananchi wa kitongoji hicho, wamemwomba Rais John Magufuli kuingilia kati na kuweka msimamo ambao utaweza kumaliza kero hiyo.

Wakulima zaidi ya 690 ndio wanaolalamikia juu ya hali hiyo baada ya wageni wa hao kupora ardhi yao huku uongozi wa wilaya ya Tunduru licha ya kupelekewa kero hiyo mezani, bado haijaona umuhimu wa kusikiliza kilio chao na kuchukua hatua za haraka dhidi ya malalamiko ya wakulima hao.

Saturday, May 14, 2016

FEDHA ZA UCHAGUZI SHILINGI MILIONI 513 ZADAIWA KUTAFUNWA MKUU WA WILAYA MBINGA AWAJIA JUU WATENDAJI WAKE WA HALMASHAURI


Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga amewajia juu watendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo ambao wanadaiwa kuhusika kwa namna moja au nyingine kufanya ubadhirifu wa fedha shilingi bilioni 1.4 ambazo zilitolewa na serikali kwenda wilayani humo, kupitia Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwa ajili ya kufanya kazi iliyolengwa katika uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25 mwaka jana.

Ngaga alisema kuwa ubadhirifu huo umebainika, baada ya ofisi yake kuunda tume ndogo ambayo ilifanya kazi kwa ushirikiano wa baraza la kamati ya ulinzi na usalama la wilaya hiyo na kuweza kubaini wizi huo, uliofanyika katika fedha hizo za serikali.

Senyi Ngaga, Mkuu wa wilaya ya Mbinga.
Aidha alisema kuwa tume hiyo iliyoundwa ambayo inaendelea na uchunguzi wake na majina ya waliohusika kuwekwa bayana hapo itakapomaliza kazi yake, ambapo taarifa za awali katika fedha hizo zinathibitisha kwamba maofisa waliopewa dhamana ya kuendesha uchaguzi huo wilayani hapa kwa kushirikiana na idara ya fedha na manunuzi ya wilaya hiyo, ndio wanaodaiwa kuhusika kutengeneza mianya ya kutafuna fedha hizo.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa wilaya hiyo, Ngaga kwenye kikao cha baraza la Madiwani wilayani humo kilichoketi juzi kwenye ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa na kwamba alieleza kuwa ubadhirifu huo umefanyika kupitia watu kulipana posho, ununuaji wa mafuta na vipuri vya magari, chakula na vifaa vingine vya ofisi (Stationary) kinyume na taratibu za miongozo iliyotolewa na serikali.

AFARIKI DUNIA KWA KUVILIGWA NA WAYA WA UMEME



Na Steven Augustino,
Tunduru.

WATU wawili wamefariki dunia katika matukio tofauti, yaliyotokea wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, likiwemo la mtu mmoja kuviligwa na waya wa umeme wakati akipita barabarani.

Zubery Mwombeji.
Taarifa za matukio hayo zinasema kuwa tukio la kwanza lilitokea katika msitu wa hifadhi ya Muhuwesi, baada ya mkazi wa kitongoji cha Ngoloanga kijiji cha Chalinze Kata ya Muhuwesi, Fakii Rashid Mabula (43) alikutwa akiwa amefariki dunia baada ya kung'atwa na nyoka.

Mwenyekiti wa kitongoji hicho, Said Omari Likomanje alisema kuwa mwili wa marehemu huyo uligundulika Mei 5 mwaka huu baada ya kuripotiwa kupotea tangu Mei 1 mwaka huu, kwa madai kuwa alikwenda katika msitu huo kwa ajili ya kutafuta mabanzi ya kujengea zizi lake la mifugo.

WAZAZI NAMTUMBO WATAKIWA KUPELEKA WATOTO WAO SHULE



Na Steven Augustino,
Namtumbo.

WAZAZI wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma, wameshauriwa kupeleka watoto wao katika Chuo cha ualimu cha ushirika kilichopo wilayani humo, ili waweze kupata elimu ambayo itawakomboa katika maisha yao, hatimaye wataweza kuondokana na umaskini.

Mkuu wa chuo hicho, Wallfram  Mpulo  alisema hayo katika mahafali ya kwanza ya wahitimu wa ualimu ngazi ya cheti daraja la tatu A, tangu kilipoanzishwa mwezi Julai mwaka 2014 wilayani humo.

“Wazazi msiogope kuleta wazazi wenu katika chuo hiki, leteni vijana wenu wasome hapa shuleni na waweze kujipatia elimu itakayowasaidia katika maisha yao, chuo hiki kimesajiliwa na wizara husika na kinatambulika kisheria”, alisema.

Friday, May 13, 2016

WATUMISHI HEWA MBINGA WAJISALIMISHA POLISI WALIPA FEDHA ZA SERIKALI WALIZOJIPATIA ISIVYO HALALI


Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

ZOEZI la uhakiki Watumishi hewa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, linaendelea kupamba moto ambapo watumishi 46 ambao walikwisha staafu wamebainika kuendelea kuchukua mishahara hewa, huku wakijua kwamba kufanya hivyo ni kinyume cha sheria na taratibu za nchi.

Rais John Pombe Magufuli.
Aidha kufuatia msako mkali unaoendelea kufanyika na timu ya uongozi wa halmashauri hiyo, kati ya hao watumishi 14 wamejisalimisha kituo kikuu cha Polisi wilayani humo na kwamba wamewekwa mahabusu, kutokana na kujipatia fedha hizo isivyo halali.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Venance Mwamengo alisema hayo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake na kuongeza kuwa asilimia kubwa ya waliokamatwa ni wa kutoka idara ya kilimo na elimu.

TAKUKURU YAWATAKA WAANDISHI WA HABARI KUFANYA KAZI ZAO KWA WELEDI



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WAANDISHI wa habari mkoani Ruvuma, wametakiwa kusaidia juhudi zinazofanywa na Rais Dkt. John Magufuli katika kuwafichua watumishi wa umma ambao wanajihusisha na vitendo vya rushwa na ufisadi, ambavyo vinachangia kurudisha nyuma kasi ya  kuleta maendeleo kwa wananchi.
Yustina Chagaka.

Aidha imeelezwa kuwa, vitendo hivyo vinavyofanywa na watumishi hao hasa katika miradi  ya maendeleo inakwamisha malengo ya serikali katika kupunguza tatizo la umaskini kwa baadhi ya maeneo hapa nchini, kwani miradi inayosimamiwa au kutekelezwa na wala rushwa inajengwa chini ya kiwango na hivyo kushindwa kuleta tija iliyokusudiwa.

Hayo yalisemwa hivi karibuni na Mkuu wa Taaisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoani Ruvuma, Yustina Chagaka wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini Songea.

Wednesday, May 11, 2016

WANAFUNZI SHULE YA MSINGI NGAPA TUNDURU WAKOSA MAHALI PA KUSOMEA TANGU MWAKA 2014

Jengo la shule ya msingi Ngapa wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, ambalo limeezuliwa kwa mvua iliyoambatana na upepo mkali mwaka 2014.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

WANAFUNZI 589 wanaosoma shule ya msingi Ngapa, wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma wapo katika hatari ya kufanya vibaya katika masomo yao, kutokana na shule hiyo kubomoka na kukosa mahali pa kusomea masomo yao.

Hali hiyo inawafanya wanafunzi hao, kusoma kwa kupeana zamu katika madarasa matatu kati ya saba yanayohitajika wakati wanapokuwa katika vipindi vyao vya masomo darasani.
Jengo ambalo limeezekwa kwa nyasi wanalotumia sasa kusomea.

Tatizo hilo limedumu kwa muda mrefu na kusababisha madarasa manne yaliyopo katika shule hiyo kubomolewa na mvua ya mawe, ambayo iliambatana na upepo mkali Februari 5 mwaka 2014.

Aidha taarifa za awali zinaeleza kuwa, sambamba na kubomolewa kwa madarasa hayo shule hiyo haina hata vyoo vya kujisaidia wanafunzi hao jambo ambalo linawafanya wajisaidie porini kipindi chote tangu mwaka huo, shule hiyo ilipokumbwa na mkasa huo.

MSUFI WAZUA MAAJABU NAMTUMBO

Na Yeremias Ngerangera,
Namtumbo.

MTI aina ya Msufi ambao uliangushwa na Kampuni ya Sogea Satom kupisha ujenzi wa barabara ya lami kutoka Songea kuelekea wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, umezua maajabu na kuwaacha wananchi wa eneo hilo kuishi kwa wasi wasi.

Ujenzi huo wa barabara hiyo ambao ulifanyika mwaka 2014, wananchi wa kijiji cha Nahoro wilayani humo hivi karibuni walifurika katika kijiji hicho kujionea tukio hilo, huku wakiishia kutahamaki na kubaki na mshangao baada ya kujionea mti huo ukiwa umesimama jirani na shimo ulipotolewa.

Omary Kumbakumba mkazi wa kijiji hicho, alisema kuwa hajawahi kuona tukio la aina hiyo ambapo aliwataka wenzake washirikiane naye kuusukuma, ili waweze kuona kama hauanguki.

WAKULIMA WA TUMBAKU WATAKIWA KUTOKATISHWA TAMAA

Na Mwandishi wetu,
Namtumbo.

WAKULIMA wa zao la tumbaku wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma, wametakiwa kutokatishwa tamaa kutokana na changamoto mbalimbali zinazolikabili zao hilo, badala yake waongeze juhudi katika uzalishaji wake hatua ambayo itawawezesha kuinua  hali zao za maisha.

Wito huo ulitolewa na  Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Alli Mpenye alipokuwa akifafanua juu ya mikakati mbalimbali ya kufufua zao hilo kwa waandishi wa habari, ofisini kwake.

Aidha Mpenye alibainisha kuwa, tatizo la kushuka kwa uzalishaji wa zao la tumbaku  wilayani humo katika miaka ya hivi karibuni kumechangiwa na wakulima kukatishwa tamaa na viongozi wa vyama vya ushirika wilayani humo,  ambao walishirikiana na makampuni yanayonunua tumbaku kuwaibia wakulima na hata wakati mwingine kuwabambikia madeni makubwa ya pembejeo.

Kadhalika ameishukuru serikali kuanza kuwachukulia hatua za kisheria viongozi wote waliohusika kutafuna fedha za wakulima hao, na wale walioua vyama vya ushirika ambao kwa kiasi kikubwa ndiyo walishiriki kwa namna moja au nyingine kuua zao la tumbaku kwa kufanya vitendo visivyofaa dhidi ya wakulima.

Saturday, May 7, 2016

MADIWANI MBINGA WALALAMIKIA HUDUMA YA MAJI

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa, Mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira katika mji wa Mbinga mkoani Ruvuma (MBIUWASA) endapo haitajidhatiti kuboresha utoaji wa huduma hiyo kwa viwango vinavyotakiwa, kuna uwezekano mkubwa kwa wananchi waishio katika mji huo kuugua homa za matumbo kutokana na maji wanayotumia sasa kuwa machafu.

Aidha mji huo hivi sasa unakabiliwa na tatizo kubwa la uhaba wa maji, ambapo wakazi wake wakati mwingine hulazimika kuyafuata kwenye vijito vinavyowazunguka ndani ya mji, ambapo hali hiyo imedumu kwa muda mrefu na kuwa kero miongoni mwa jamii.

Hayo yalisemwa na Madiwani wa Halmashauri ya mji wa Mbinga, kwenye kikao chao cha baraza la madiwani kilichoketi juzi katika ukumbi wa Chuo cha maendeleo ya wananchi, kilichopo mjini hapa.

Walisema kuwa huduma ya maji itolewayo sasa na Mamlaka hiyo ni hafifu haikidhi mahitaji husika, na kwamba maji yanayosambazwa ni machafu huku yakiwa yana rangi ya vumbi jambo ambalo ni hatari kwa afya ya binadamu.

KAMPUNI YA OVANS YAWEKA MIKAKATI YA VIJANA KUEPUKANA NA UHARIBIFU WA MAZINGIRA

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

VIJANA wanaojishughulisha na kazi ya ufyatuaji tofari za udongo katika mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, wameshauriwa kujiunga na Kampuni ya Ovans Construction Limited ili waweze kufanya kazi hiyo kwa kutumia mashine ya kisasa ya kufyatua tofari za kuchanganya mchanga na simenti, ikiwa ni lengo la kuepukana na uharibifu wa mazingira katika mji huo.

Uhamasishaji huo wa vijana kuachana na kazi ya ufyatuaji wa tofari za udongo ambao hufanywa mabondeni, ni njia ya kuepukana pia na uharibifu wa vyanzo vya maji ambao unaendelea kushika kasi kila siku katika mji huo.

Valence Urio.
Mkurugenzi wa Kampuni hiyo, Valence Urio alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake ambapo alifafanua kuwa kazi hiyo ya uundaji wa tofari za udongo pia huchangia kwa kiasi kikubwa uharibifu wa misitu, ambapo wafyatuaji hulazimika kukata miti msituni kwa ajili ya kuweza kupata kuni za kuchomea tofari.

Valence alisema kuwa baada ya kuona uharibifu huo wa mazingira ukiwa unaendelea katika mji huo aliona ni vyema anunue mashine ya kisasa ambayo itaweza kufanya kazi ya kufyatua tofari za kuchanganya mchanga na simenti, na kuwataka vijana wanaojishughulisha na kazi hiyo wajikusanye kwa pamoja na yeye atawasaidia kuunda kikundi ambacho kitasajiliwa kisheria na kuweza kufanya kazi hiyo ya kuwaletea kipato.

Thursday, May 5, 2016

GAMA SONGEA ATOA MSAADA WA MAGARI YAKUWAHUDUMIA WANANCHI WAKE

Na Julius Konala,
Songea.

MBUNGE wa Jimbo la Songea mjini mkoani Ruvuma, Leonidas Gama ametoa msaada wa magari mawili ikiwemo la kubebea wagonjwa kwa ajili ya kusaidia wananchi wa jimbo hilo kwenda hospitali, pale wanapougua au kuzidiwa na magonjwa mbalimbali.

Msaada huo ulitolewa na Mbunge huyo kwenye hafla fupi iliyofanyika uwanja wa michezo wa Majimaji uliopo mjini hapa, ikishuhudiwa na wananchi ambao walihudhuria hafla hiyo.

Gama alisema kuwa ameamua kununua magari hayo, kupitia mkopo ambao atakuwa anakatwa kwenye mshahara wake kutokana na kuguswa na changamoto zinazowakabili baadhi ya wananchi wake, ikiwemo baadhi yao kutokuwa na uwezo wa kukodi magari ya kuwapeleka hospitali kupata matibabu pale wanapougua ghafla.

MADIWANI HALMASHAURI MJI WA MBINGA WALIA NA WALIMU KUKIMBILIA MJINI

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

BARAZA la Madiwani wa Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, limemtaka Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Oscar Yapesa kuchukua hatua ya kuhamisha walimu wa shule za msingi na sekondari ambao wengi wao wapo katika shule za mjini huku zilizopo pembezoni mwa mji huo, zikiwa hazina walimu wa kutosha jambo ambalo linakwamisha maendeleo ya taaluma katika shule hizo.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Ngaga.
Madiwani hao walisema kuwa mwalimu mmoja hulazimika kufundisha vipindi vingi vya masomo darasani, huku wakitolea mfano shule ya msingi Changarawe iliyopo katika kata ya Mpepai ambayo ina walimu wawili tu, kutoka darasa la kwanza hadi la saba.

Hayo yalisemwa na Madiwani hao walipokuwa kwenye baraza la mji huo ambalo liliketi mjini hapa, ambapo pamoja na mambo mengine walisisitiza kuwa walimu waliopo mashuleni wanapaswa kujitolea kufundisha kwa moyo katika maeneo yao ya kazi, ili kuweza kuleta matokeo mazuri kwa watoto wanaosoma katika shule hizo.

“Mheshimiwa Mwenyekiti sijafurahishwa kabisa na mwenendo huu wa watumishi hawa wa idara elimu, kuwa na tabia ya kuhama na kukimbilia hapa mjini huku shule zetu zilizopo pembezoni wanafunzi wakiwa wanateseka kutokana na kukosa vipindi vya masomo darasani, hali hii inapaswa kudhibitiwa kuanzia sasa na walimu waliorundikana hapa mjini waondolewe na kwenda kuziba pengo la shule za pembezoni mwa mji wetu”, alisema Benedict Ngwenya Diwani wa kata ya Mpepai.

Wednesday, May 4, 2016

TUJIKUMBUSHE YALIYOJIRI SIKU YA BONANZA LA VIJANA UWANJA WA TAIFA MBINGA MJINI


Wachezaji wa timu ya soka ya NMB tawi la Mbinga, wakiwa na nyuso za furaha katika picha ya pamoja siku ya maadhimisho Bonanza la vijana wa Mbinga baada ya kuibuka kidedea na kuicharaza mabao 2 kwa 1 Timu Bonanza ya mjini hapa, mchezo ambao ulifanyika Aprili 24 mwaka huu kwenye uwanja wa Taifa Mbinga mjini. (Picha na gwiji la matukio Ruvuma)


GAMA AFANYA UZINDUZI WA JIMBO CUP

Leonidas Gama, Mbunge wa Songea mjini.
Na Julius Konala,
Songea.

MBUNGE wa jimbo la Songea mjini mkoani Ruvuma, Leonidas Gama amefanya uzinduzi wa tamasha la michezo lijulikanalo kwa jina la Jimbo Cup, ambalo litashirikisha kata 21 za Manispaa ya Songea mkoani humo.

Uzinduzi huo ulifanyika hivi karibuni kwenye uwanja wa michezo Majimaji uliopo mjini hapa, ambapo mamia ya wananchi wa Manispaa hiyo waliweza kushiriki ikiwemo na vikundi mbalimbali vya sanaa.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Gama alisema lengo la kuandaa tamasha hilo ni kwa ajili ya kuimarisha tamaduni za mkoa wa Ruvuma, ikiwemo hata kuibua na kukuza vipaji vya vijana.

DIWANI KILIMANI AWATAKA WANANCHI WAKE KUJITOKEZA KATIKA UJENZI WA KITUO CHA AFYA

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

DIWANI wa kata ya Kilimani katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Simon Ponela amewataka wananchi wake kujitokeza kwa wingi katika ujenzi wa kituo cha afya cha kata hiyo, ikiwemo kuchangia nguvu zao ili ujenzi huo uweze kukamilika kwa wakati.

Oscar Yapesa Mkurugenzi Halmashauri mji wa Mbinga. 
Aidha ujenzi wa kituo hicho ambao hivi sasa umefikia kwenye hatua ya kuweka kenchi kwa ajili ya kuezeka bati, amewataka wananchi hao wajitokeze kuchangia mchanga, tofari na uchanaji wa mbao katika msitu wa kijiji hicho ili ziweze kusaidia katika ukamilishaji wa kazi hiyo ya ujenzi wa kituo cha afya.

Hayo yalisemwa na diwani huyo alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi, ambaye alitembelea katika kata hiyo kwa ajili ya kujionea shughuli mbalimbali za kimaendeleo zinazofanywa na wananchi wa kata hiyo.

Ponela alisema kuwa ujenzi wa kituo hicho cha afya ulikuwa ukisuasua kutokana na uhaba wa vitendea kazi lakini baada ya yeye kuingilia kati na kuhamasisha wananchi wake na kuushirikisha uongozi wa Halmashauri hiyo kikamilifu, hivi sasa utekelezaji wake unakwenda vizuri ikiwa ni lengo la kuwafanya wananchi waweze kuondokana na kero ya upatikanaji wa matibabu.

Tuesday, May 3, 2016

MAHAKAMA YADAIWA KUMWACHIA HURU MBAKAJI

Na Steven Augustino,
Tunduru.

MAHAKAMA ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, imemwachilia huru Mmanga Abdalah Hamdani (47) ambaye ni mtuhumiwa wa kosa la ubakaji, mtoto wa miaka 13 wa darasa la sita shule ya msingi Nanjoka wilayani humo.

Akitoa hukumu hiyo Hakimu mkazi mfawidhi Mahakama hiyo, Gladys Barthy alisema kuwa mahakama hiyo imechukua hatua hiyo baada ya kujiridhisha na ushahidi uliotolewa na wataalamu wa utabibu, mganga wa hospitali ya serikali ya wilaya ya Tunduru Dkt. Gaofrid Mvile kuwa mtoto huyo hakubakwa.

Akifafanua hukumu hiyo, Hakimu huyo alisema kuwa kufuatia hali hiyo mahakama imeamua kutenda haki kwa kutoa uamuzi huo wa kumwachilia huru kwa madai kwamba, huenda binti huyo alimsingizia mbakaji huyo ambaye ni mjomba wake kwa lengo la kutaka kumkomoa.

Akinukuu taarifa ya ushahidi uliotolewa na Dkt. Mvile, Hakimu huyo alisema kuwa taarifa zinaeleza kuwa hadi siku wanamfanyia vipimo vya ukaguzi wa kuthibitisha tukio hilo la ubakaji, malalamikaji hakuonesha kuwa na dalili za kuingiliwa na badala yake alionekana kuwa na bikra yake na kwamba kilichobainika katika uchunguzi huo ni uwepo wa mrundikano wa damu, ambazo zilitolewa kwa kumfanyia upasuaji wa tumbo lake.