Sunday, July 31, 2016

KAMPUNI YA TUTUNZE YAPONGEZWA KUCHANGIA SHUGHULI ZA MAENDELEO YA WANANCHI

Ofisi za makao makuu ya Kampuni ya Tutunze Kahawa Limited (TKL) zilizopo Mbinga mjini.


Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

WADAU wa maendeleo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma wameipongeza Kampuni ya Tutunze Kahawa Limited (TKL) iliyopo wilayani hapa, kwa jitihada zake za kuunga mkono na kuchangia shughuli mbalimbali za maendeleo ya wananchi wilayani humo.

Pongezi hizo zilitolewa juzi mjini hapa, wakati kampuni hiyo ilipokuwa ikikabidhi madawati 20 yenye thamani ya shilingi milioni 1.9 kwa uongozi wa halmashauri ya wilaya hiyo kwa ajili ya kukalia wanafunzi shuleni.

Walisema kuwa juhudi hizo zinazofanywa na TKL kuna kila sababu kwa makampuni mengine yaliyopo wilayani Mbinga, kuiga mfano huo katika kuchangia michango ya maendeleo ili wilaya hiyo iweze kusonga mbele na kukua kiuchumi.

Aidha naye Meneja masoko wa kampuni hiyo, Thomas Ngapomba kwa upande wake alisema kuwa katika juhudi za kuunga mkono kampeni iliyoanzishwa na Rais Dkt. John Magufuli ya kuondoa tatizo la madawati kwa shule za msingi na sekondari hapa nchini, Tutunze Kahawa Limited nayo iliona kuna umuhimu wa kuchukua jukumu la kuchangia madawati hayo kwa wilaya ya Nyasa na Mbinga.

Ngapomba alifafanua kuwa lengo la kufanya hivyo ni kuhakikisha kwamba wanafunzi wanakuwa na mazingira mazuri ya kusomea, pale wanapokuwa darasani ili waweze kuandika mwandiko mzuri.

HALMASHAURI WILAYA YA MBINGA YAJIWEKEA MIKAKATI UPIMAJI WA ARDHI MIJI MIDOGO




Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya  ya Mbinga mkoani Ruvuma, Ambrose Mtarazaki kushoto na baadhi ya Madiwani wa halmashauri hiyo wakimsikiliza kwa makini, Mthamini wa ardhi wa wilaya hiyo, Gabriel Kameka (hayupo pichani) wakati wa mafunzo ya siku moja ya kuwajengea uwezo madiwani hao juu ya umuhimu wa upangaji na upimaji ardhi katika miji midogo ya wilaya hiyo.

Na Kassian Nyandindi,        
Mbinga.

HALMASHAURI ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, imejiwekea mikakati ya kuhakikisha kwamba miji midogo iliyopo katika halmashauri hiyo ardhi yake inapimwa kisheria na kuwafanya wakazi waliopo katika maeneo husika, wasiweze kujenga kiholela.

Aidha katika vijiji kupitia kamati zake, watashirikishwa juu ya mamlaka ya taratibu husika za upangaji wa matumizi ya ardhi na kwamba upimaji huo utashirikisha pia wananchi kwa kuchangia gharama ndogo.

Hayo yalisemwa juzi na Mthamini wa ardhi wilaya ya Mbinga, Gabriel Kameka alipokuwa akitoa mafunzo elekezi ya siku moja kwa Madiwani wa halmashauri ya wilaya hiyo, yaliyofanyika kwenye ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa.

Kameka alifafanua kuwa kwa kutambua hilo serikali iliandaa sera ya ardhi mwaka 1995 pamoja na sheria zake, kwa madhumuni ya kuongoza ugawaji juu ya matumizi bora ya ardhi na kulinda haki zote zilizopo ndani yake.

BASI LA MAKEO LAPINDUKA NA KUUA WATU WATATU DEREVA ASHIKILIWA NA POLISI


Na Kassian Nyandindi,          
Songea.

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma, linamshikilia Frank Ndunguru (33) ambaye ni dereva wa Kampuni ya mabasi ya Makeo inayosafirisha abiria kutoka Manispaa ya Songea kwenda wilaya ya Mbinga mkoani humo, baada ya kusababisha ajali ya gari alilokuwa akiendesha kupinduka na kuua watu watatu.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Zubery Mwombeji alisema kuwa tukio hilo lilitokea Julai 30 mwaka huu majira ya saa 1:30 usiku katika kijiji cha Mkako kata ya Mkako wilayani Mbinga, ambapo dereva huyo alikuwa akiendesha gari lenye namba za usajili T. 534 CPV aina ya Mitsubish Rosa, ambalo linamilikiwa na Mohamed Makeo mkazi wa Songea mjini.
Zubery Mwombeji.

Mwombeji alifafanua kuwa chanzo cha ajali hiyo kinatokana na uzembe wa dereva huyo, baada ya kuendesha gari katika mwendo kasi na hatimaye kushindwa kukata kona kali kisha kupinduka mara tatu, baada ya gari hilo kupoteza mwelekeo.

“Dereva wa gari hili yupo mikononi mwa Polisi, tunaendelea kumuhoji na kukamilisha hatua za upelelezi ili aweze kuchukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kufikishwa Mahakamani”, alisema Mwombeji.

Kamanda huyo wa Polisi alitoa wito kwa madereva wa magari hapa mkoani Ruvuma, kuzingatia sheria za usalama barabarani, ili isiweze kutokea uzembe kama huo ambao unasababisha watu kupoteza maisha na wengine kuwa na ulemavu wa kudumu.

Saturday, July 30, 2016

URAIA WA NCHI MBILI WAMSHITUA MKUU WA WILAYA NAMTUMBO



Na Yeremias Ngerangera,
Namtumbo.

MKUU wa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Luckness Amlima ameshitushwa na taarifa ya uraia wa nchi mbili Msumbiji  na Tanzania ambao unafanywa na wananchi wa kijiji cha Likuyumandela, kata ya Likuyu wilayani humo bila kufuata taratibu husika.

Amlima alishitushwa na taarifa hiyo wakati wa ziara yake ya kikazi wilayani humo, ambayo ilienda sambamba na kuzungumza na wajumbe wa baraza la maendeleo la kata katika kata zote za wilaya ya Namtumbo.

Luckness Amlima katikati, akiwa na kamati yake ya maendeleo.
Akisoma taarifa ya maendeleo kata ya Likuyu kwa Mkuu wa wilaya huyo, Mratibu elimu kata, Ireneus Fusi alisema kuwa pamoja na changamoto zingine kuwepo lakini kata hiyo inachangamoto kubwa kwa wananchi wake, kuwa na makazi ya kuhamahama ambapo wakati mwingine wanaishi Tanzania au Msumbiji.

Fusi alifafanua kuwa hali hiyo ya kuhamahama imekuwa ikiwayumbisha watoto wao hasa kwa wale ambao ni wanafunzi, wanaosoma shule za msingi na sekondari.

Wednesday, July 27, 2016

WAFANYABIASHARA WASIOTOA RISITI KUSHTAKIWA MAHAKAMANI



Na Kassian Nyandindi,     

Songea.

MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) mkoani Ruvuma, imewataka wananchi wake kudai risiti wanaponunua bidhaa dukani huku ikiwasisitiza wafanyabiashara wenye maduka hayo, kuhakikisha kwamba wanatoa risiti za Kieletroniki (EFD’S) kwa wateja wao bila kuwepo usumbufu wa aina yoyote ile.
 
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi juzi ofisini kwake, Meneja wa TRA mkoani humo Rosalia Mwenda alisema kuwa Mamlaka hiyo imetoa matangazo yake yenye kusisitiza kuwa mwananchi atakayeshindwa kudai risiti kwa mfanyabiashara husika wakati wa kununua bidhaa na mfanyabiashara huyo, akabainika kushindwa kutoa risiti ni makosa kufanya hivyo na kwamba wote kwa pamoja wakikamatwa watashtakiwa na serikali.

ASKARI WA MAUAJI YA MWANDISHI WA HABARI DAUD MWANGOSI AHUKUMIWA JELA MIAKA 15


Rais wa Umoja wa Klabu za Waandishi wa habari Tanzania (UTPC) Deo Nsokolo akizungumza na waandishi wa habari, mara baada ya hukumu ya kesi hiyo.
Jinsi mauaji yalivyofanyika.

IRINGA:
MAHAKAMA  kuu ya Tanzania  kanda  ya  Iringa, leo  imemuhukumu kwenda  jela miaka 15 askari wa Kikosi cha  Kutuliza Ghasia (FFU) mwenye  namba G. 2573 Pacificius Cleophace Simon (27)  aliyemuua mwandishi  wa  habari  wa  kituo  cha Chanel Ten, Daudi  Mwangosi.

Akisoma hukumu hiyo, Jaji wa Mahakama hiyo Dkt. Paul Kihwelo alisema kuwa mshtakiwa huyo amekutwa na hatia ya kuua bila kukusudia katika shitaka la pili lililosomwa Mahakamani hapo leo, baada ya la kwanza kusomwa na kukutwa hana hatia.

Kesi hiyo ilianza kusikilizwa mwezi Februari 12, mwaka 2012 na kufikia hukumu hiyo ya kumtia hatiani na kwamba tukio hilo lilitokea Septemba 2 mwaka 2012 katika kijiji cha Nyololo, wilaya ya Mufindi mkoani Iringa.

POLISI WAVURUGA UTULIVU MAHAKAMA KESI YA MWANGOSI


IRINGA:

BAADHI ya askari Polisi waliokuwepo ndani ya chumba cha Mahakama Kuu Kanda ya Iringa, wakati askari mwenzao Pacificius Cleophace Simoni akitiwa hatiani kwa kosa la mauaji ya bila kukusudia ya mwanahabari Daudi Mwangosi, walivuruga utulivu wa mahakama hiyo baada ya simu zao kupigwa wakati Jaji Paulo Kiwehlo akiendelea kusoma maelezo ya kesi hiyo.

Hatua hiyo iliyowashangaza wanahabari na raia wengine waliojitokeza kusikiliza hukumu hiyo, ilitokea muda mfupi baada ya mmoja askari Polisi aliyekuwepo ndani ya mahakama hiyo kutoa tangazo liliwatisha watu wengine kabla shughuli ya mahakama hiyo haijaanza.

Huku akionekana ana hasira, kwa sauti ya ukali askari huyo alimtaka kila mtu aliyepo ndani ya mahakama hiyo azime simu yake na shughuli ya mahakama itakapokwisha anyanyuke kimyakimya na kutoka nje kwa utulivu kama hataki kukutana na nguvu ya jeshi hilo, ambalo waliokuwepo mahakamani hapo jana walishuhudia jinsi lilivyokuwa limejipanga kukabiliana na raia wasio na hatia waliokwenda kushuhudia kilichokuwa kikiendelea mahakamani hapo.

NYASA WATAKA UJENZI WA VITUO VYA MAFUTA



Na Kassian Nyandindi,         
Nyasa.

BAADHI ya wananchi wa wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma, wamesema kwamba wanapata adha kubwa na hufikia hatua ya kushindwa kufanya shughuli zao mbalimbali za kimaendeleo, kutokana na ukosefu wa huduma ya vituo vya kuuza mafuta katika wilaya hiyo.

Aidha wameomba watu wenye uwezo mkubwa wa kifedha, kujitokeza kwenda wilayani humo kuwekeza katika sekta hiyo muhimu hatua ambayo itarahisisha upatikanaji wa huduma hiyo na kuharakisha kukua kwa shughuli zao za kiuchumi.

Akizungumza kwa niaba ya wananchi wenzake, mkazi mmoja wa mji wa Mbamba bay wilayani Nyasa Petro Ndembele alisema kuwa wilaya hiyo tangu ianzishwe mwaka 2013 hakuna huduma ya vituo vya kuuza mafuta, jambo ambalo linachangia kwa kiasi kikubwa maisha ya wakazi wengi wilayani hapa kuwa magumu sambamba na kuongezeka kwa nauli kutoka sehemu moja kwenda nyingine katika magari ya kusafiria abiria na kuwafanya waendelee kuwa maskini.

MADIWANI CUF TUNDURU WAHAMASISHA UJENZI WA MADARASA

MKUU wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Juma Homera upande wa kushoto akishiriki kwa vitendo katika zoezi la kufyatua tofari za shule ya Msingi Umoja iliyopo kata ya Nanjoka wilayani humo, Kushoto kwake ni Mratibu Elimu Kata Issa Selemani na wa mwisho kushoto ni diwani wa kata hiyo, Rajab Mkwawa ‘Mtimbalugono’.


Na Steven Augustino,
Tunduru.

MADIWANI wa Chama Cha Wananchi (CUF) wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wameahidi kuunga mkono kwa vitendo juhudi zinazofanywa na serikali ya awamu ya tano, katika kuondoa kero mbalimbali zinazowakabili wananchi wa wilaya hiyo ili waweze kusonga mbele kimaendeleo.

Ahadi hiyo ilitolewa na Madiwani wa kata ya Nanjoka, inayoongozwa na Rajab Mtimbalugono, kata ya Majengo, Abdallah Rajabu na diwani wa kata ya Mlingoti Mashariki, Mohamed Aloyce. 

Madiwani hao walisema hayo walipokuwa wakizungumza na Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Juma Homera alipowatembelea katika eneo la kufyatulia matofari kwa ajili ya ujenzi wa madarasa ya shule ya msingi Umoja iliyopo mjini hapa.

Sunday, July 24, 2016

HALMASHAURI YA MBINGA YATOA SHUKRANI KWA WADAU WA MAENDELEO



Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

HALMASHAURI ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, imetoa shukrani kwa Wadau wa maendeleo wilayani humo, kwa kutoa msaada wa magari ambayo yametumika kubebea madawati kutoka mjini Songea mkoani humo kwenda wilayani hapa, kwa ajili ya kukalia wanafunzi darasani.

Wilaya hiyo imepata mgawo wa madawati 537 ambayo yametengenezwa na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Mlale mkoani hapa, kupitia fedha za mfuko wa jimbo ambazo hutolewa na serikali kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo ya wananchi.

Emmanuel Kapinga ambaye ni Ofisa utumishi wa wilaya ya Mbinga, alitoa shukrani hizo kwa niaba ya Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo Gumbo Samanditu, wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake juu ya mkakati wa kumaliza tatizo la madawati kama ilivyoagizwa na Rais Dkt. John Magufuli.

WATOTO WENYE ULEMAVU WA NGOZI MBINGA WAPATIWA MSAADA WA MAFUTA MAALUM YA KUPAKA

Katibu tawala wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Gilbert Simya na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya mji wa Mbinga, Robert Mageni waliosimama nyuma wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wanachama wa chama cha albino wilaya ya Mbinga, baada ya kukabidhi msaada wa mafuta yenye thamani ya shilingi laki 870,000 yaliyotolewa na chama cha walemavu wilayani humo kwa ufadhili wa hospitali ya KCMC ya mjini Moshi mkoani Kilimanjaro.
Katibu tawala wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Mhandisi Gilbert Simya akikabidhi mafuta maalum ya kuzuia magonjwa ya ngozi kwa watu wenye ulemavu wa ngozi jana, wakati wa kukabidhi msaada wa mafuta hayo yenye thamani ya shilingi 870,000 yaliyotolewa na Chama cha walemavu wilayani humo.


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

JAMII imetakiwa kuwalea, kuwatunza na kuwajali watu wenye ulemavu wa ngozi albino kwa kuhakikisha kwamba wanaishi katika mazingira mazuri, yenye usalama na sio kuwanyanyapaa pale wanapohitaji mahitaji yao ya msingi.

Aidha Chama Cha Walemavu Tanzania (CHAWATA) tawi la Mbinga mkoa wa Ruvuma kimeshauriwa kuendelea kushirikiana na serikali, ili walemavu hao pia waweze kupata elimu juu ya afya ya usalama wa ngozi pamoja na kutatua matatizo mbalimbali yanayowakabili katika maisha yao.

Hayo yalisemwa na Katibu tawala wa wilaya ya Mbinga, Mhandisi Gilbert Simya wakati alipokuwa akipokea msaada wa mafuta maalum ya kupaka watu wenye ulemavu wa ngozi albino katika hafla fupi iliyohudhuriwa na walemavu hao ambayo ilifanyika kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa.

Mafuta hayo yalitolewa na Chama hicho cha walemavu kwa watu 87 wenye ulemavu wa ngozi Halmashauri ya mji wa Mbinga, baada ya kuyapokea kutoka kitengo cha magonjwa ya ngozi Hospitali ya KCMC Moshi mkoani Kilimanjaro ambayo yanathamani ya shilingi 870,000.

Saturday, July 23, 2016

MATUKIO MBALIMBALI KATIKA PICHA MJINI DODOMA

  Kundi la Tot Plus likiongozwa na Khadija Kopa akiimba mbele ya Wajumbe wapatao zaidi ya 2000 wa mkutano Mkuu Maalum wa CCM mjini Dodoma leo.
 
Baadhi ya wageni waalikwa kutoka vyama mbalimbali vya upinzani pia walihudhuria mkutano huo wa CCM. Ambapo vyama vya siasa vipatavyo 12 vilialikwa na vyote vimefika katika mkutano huo isipokuwa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Wajumbe wapatao zaidi ya 2000 wa mkutano Mkuu maalum wa CCM wakitumbuizwa ndani ya ukumbi wa Dodoma Convetion Center (DCC) ulioko nje kidogo ya mji wa Dodoma, hivi sasa kundi la TOT Plus likiongozwa na Mwana mama mkongwe Khadija Kopa.
 
Baadhi ya Wageni waalikwa wakiwemo mabalozi wa nchi mbalimbali wakiwa ndani ya ukumbi huo leo kwenye mkutano Mkuu maalum wa CCM  mjini Dodoma.
 
Wajumbe wapatao zaidi ya 2000 wa mkutano Mkuu maalum wa CCM wakiwa tayari ndani ya ukumbi wa Dodoma Convetion Center (DCC) kukamilisha mchakato wao wa kumchagua Mwenyekiti mpya wa chama hicho.
 
Baadhi ya Wageni waalikwa kutoka sehemu mbalimbali wakiwa ndani ya ukumbi ambapo leo mkutano Mkuu maalum wa CCM umefanyika kwa ajili ya kumchagua Mwenyekiti mpya wa chama cha Mapinduzi (CCM) kwa miaka kumi, Rais John Pombe Magufuli na kukabidhiwa kijiti hicho kutoka kwa Mwenyekiti ambaye amemaliza muda wake leo, Rais mstaafu wa awamu ya nne, Dkt. Jakaya Kikwete mkutano huo umefanyika ndani ya ukumbi wa Dodoma Convetion Center (DCC) ulioko nje kidogo ya mji wa Dodoma. (Picha zote kwa hisani ya Michuzi blog)

KIKWETE AKABIDHI RASMI UENYEKITI WA CCM KWA DOKTA JOHN MAGUFULI LEO JIONI MKOANI DODOMA

 Mwenyekiti aliyemaliza Muda wake Dkt. Jakaya Kikwete pamoja na Mwenyekiti mpya wa chama cha Mapinduzi (CCM) Rais Dkt. John Pombe Magufuli wakiwapungia mkono Wajumbe wa mkutano Mkuu maalum mara baada ya matokeo kutangazwa rasmi na kwamba Dkt. Magufuli aliibuka mshindi kwa kura zote za ndio 2,398 na hakuna kura iliyoharika.
 
 Mwenyekiti aliyemaliza muda wake leo, Rais wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Kikwete akimkabidhi vitendea kazi mbalimbali vya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mwenyekiti mpya, Rais Dkt. John Pombe Magufuli mara baada ya kumaliza kupigiwa kura za ndiyo.
 
 Makamu Mwenyekiti wa Zanzibar Dkt. Shein akimpongeza Mwenyekiti Mpya, Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa CCM. Pichani katikati anayeshuhudia ni Mwenyekiti aliyemaliza muda wake Dkt. Jakaya Kikwete.
 
  Katibu Mkuu wa CCM, Ndugu Abdulrhaman Kinana akimpongeza Mwenyekiti mpya, Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa chama hicho kwa miaka 10.
 
 Mwenyekiti mpya wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Dkt. John Pombe Magufuli akihutubia mbele ya Wajumbe wa mkutano Mkuu maalum wa chama hicho, mara baada ya kutangazwa rasmi kuwa Mwenyekiti wa CCM.
 
Rais Mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin William Mkapa akimpongeza Mwenyekiti mpya, Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa chama hicho kwa miaka 10.
 
Mwenyekiti mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akimkumbatia Mwenyekiti mpya, Rais Dkt. John Pombe Magufuli mara baada ya kutangazwa rasmi kuwa Mwenyekiti wa chama hicho.
 
 Baadhi ya Wajumbe wa Mkutano mkuu maalum wa CCM wakipiga kura kumchagua Mwenyekiti mpya wa chama hicho leo mjini Dodoma.
 
 Wajumbe kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini wakipiga kura.
 
 Wajumbe wamekwisha piga kura na maboksi ya kupigia kura yakiwa tayari kuhesabiwa na baadae kutolewa majibu.
 
 Rais mstaafu wa awamu ya pili, Ally Hassan Mwinyi akipiga kura ya kumchagua Mwenyekiti mpya wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) jioni ya leo.
 
 Baadhi ya Wajumbe wa Mkutano mkuu maalum wa CCM wakifuatilia yaliyokuwa yakijiri kwenye mkutano huo uliofanyika katika ukumbi wa Dodoma Convetion Center,uliopo nje kidogo ya mji wa Dodoma.
 
 Mwenyekiti wa CCM ambaye amemaliza muda wake leo, Rais wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Kikwete akisalimiana na baadhi ya Wajumbe wa mkutano mkuu, Makamu wa Rais Mama Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa kabla ya matokeo ya kumpata Mwenyekiti wa chama hicho hayajatangazwa rasmi jioni ya leo.
 
 Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana akijadiliana jambo na Mwenyekiti mstaafu aliyemaliza muda wake leo, Dkt. Jakaya Kikwete pamoja na Mwenyekiti wa chama hicho, Rais Dkt. John Pombe Magufuli.
 
 Kada Mkongwe wa CCM Mzee Makamba akimpongeza Mpendazoe kwa kurejea CCM.
 







Picha zote kwa hisani ya Michuzi blog mkoani Dodoma.