Thursday, June 4, 2015

ASKARI JKT ATAFUTWA NA JESHI LA POLISI KWA UNYANYASAJI

Na Steven Augustino,
Songea.

ROBERT Mkika (26) ambaye ni askari wa kikosi cha Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Mlale mkoani Ruvuma, anatafutwa na Jeshi la Polisi mkoani humo ili aweze kujibu tuhuma ya kumtesa mtoto wa ndugu yake, ambaye alikuwa akiishi naye.

Mtoto huyo ambaye anafahamika kwa jina la Frank Kiria (9) anasoma darasa la tatu katika shule ya msingi mkombozi, Manispaa ya Songea mkoani hapa.

Kamanda wa polisi mkoa wa Ruvuma, Mihayo Msikhela amethibitisha juu ya tukio hilo na kueleza kuwa katika kuhakikisha mtoto huyo anapata uangalizi salama hivi sasa wapo katika mchakato wa kufanya mawasiliano na vituo vya kulea watoto yatima, ili waweze kumkabidhi huko hadi taratibu za kumrejesha kwao Bukoba kwa wazazi wake zitakapokamilika.

Msikhela alifafanua kuwa Frank alikimbia nyumbani kwa askari huyo wa JKT Mei 27 mwaka huu, na kwenda kwa rafiki yake Jackson Malekela kutokana na manyanyaso aliyokuwa akiyapata.

Tuesday, June 2, 2015

MADAKTARI BINGWA WAPONGEZWA KWA KUTIBU WAGONJWA WENYE MAGONJWA SUGU TUNDURU

Na Steven Augustino,
Tunduru.

WAGONJWA 63 kutoka wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, wameripotiwa kufanyiwa upasuaji mkubwa na Madaktari bingwa, kutoka Hospitali mbalimbali Jijini Dar es Salaam na KCMC iliyopo mkoani Kilimanjaro.

Mganga mkuu wa hospitali ya wilaya hiyo, Dokta Alex Kazula alisema hayo alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake na kuongeza kuwa katika matibabu hayo madaktari hao, pia waliwafanyia uchunguzi wagonjwa 171 ambapo kati yao wengine walipewa ushauri na wengine kufanyiwa matibabu.

Alieleza kuwa zaidi ya wagonjwa 200 walishindwa kuonana na wataalamu hao kutokana na muda wao kwisha, pamoja na wodi za hospitali ya wilaya hiyo kujaa na kukosekana na nafasi ya kuwahifadhi.

WANAFUNZI VYUO VYA ELIMU WATAKIWA KUREJESHA MIKOPO KWA WAKATI

Wahitimu wa chuo cha sayansi na tekinolojia cha Mtakatifu Joseph mjini Songea mkoani Ruvuma, wakiwa wamekaa katika picha ya pamoja.
Na Julius Konala,
Songea.

WANAFUNZI wanaosoma katika vyuo vya elimu ya juu hapa nchini, wamekumbushwa kurejesha mikopo yao kwa wakati ambayo ilitolewa na serikali kupitia Bodi ya mikopo ya wanafunzi hapa nchini, kadiri ya makubaliano yaliyofanywa kwenye mikataba yao ili iweze kusaidia wengine.

Mkurugenzi anayeshughulikia urejeshaji mikopo katika bodi hiyo, Juma Chagonja alisema hayo alipokuwa akizungumza na wahitimu wa chuo cha sayansi na tekinolojia ya mawasiliano, cha Mtakatifu Joseph mjini Songea mkoani Ruvuma.

Alisema kwamba bodi imefikia maamuzi hayo, baada ya kuona baadhi ya wanafunzi ambao wamenufaika na mkopo husika kuwa wagumu katika kurejesha ingawa wapo kwenye ajira, huku akiongeza kuwa wanapaswa kutambua kuwa haikutolewa kama zawadi.

Monday, June 1, 2015

MWENYEKITI UWT AWATAKA WAANDISHI KUZINGATIA MAADILI YA KAZI ZAO

Na Mwandishi wetu,
Mbinga.

WANAHABARI mkoani Ruvuma, wametakiwa kuzingatia maadili ya taaluma yao, kwa kujenga ukweli katika kazi zao za kila siku ambazo huripoti katika vyombo vya habari, ikiwemo kufichua watu wanaojihusisha na vitendo vya kuomba, kupokea na kutoa rushwa hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba, 25 mwaka huu.

Licha ya kufanya hivyo, wamehimizwa kujiendeleza kielimu jambo ambalo litawafanya waweze kuwa na uwezo mkubwa wa kuandika habari hasa zile za uchunguzi, ambazo husaidia jamii kuleta chachu ya kimaendeleo.

Pendo Ndumbaro ambaye ni Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake (UWT) wilayani Mbinga, alisema hayo alipokuwa akifungua semina ya siku mbili kwa akina mama wa umoja huo waliotoka katika kata zote za wilaya hiyo, yenye kulenga kuwahamasisha na kuwajengea uwezo wanawake hao kugombea nafasi mbalimbali za uongozi.

Sunday, May 31, 2015

MANISPAA SONGEA NA MIKAKATI YA KUBORESHA MATIBABU KWA WAZEE

Na Muhidin Amri,
Songea.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, imekuwa ikitenga kiasi cha shilingi milioni 10 kila mwaka, ikiwa ni lengo la kuhakikisha kwamba wazee wanaoishi katika Manispaa hiyo wanapatiwa matibabu ipasavyo, wakiwemo na wategemezi wao.

Fedha hizo zinazotengwa hugharimia matibabu ya wazee 600 na wategemezi wao 2700, ambao hunufaika na mpango wa matibabu bima ya afya katika zahanati, vituo vya afya na hospitali mbalimbali zilizopo katika Manispaa hiyo.

Hayo yamebainishwa na Mratibu wa mfuko wa afya ya jamii mkoani Ruvuma (CHF) wa Manispaa ya Songea, Victor Nyenza alipokuwa akizungumza kwenye mdahalo wa wazi uliohusu usalama wa wazee hapa nchini, ambao ulifanyika mjini hapa.

Saturday, May 30, 2015

KANISA KUMFIKISHA MAHAKAMANI DIWANI

Askofu mkuu wa jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma, John Ndimbo.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

UONGOZI wa Kanisa katoliki Jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma, umesema upo katika hatua za kumfikisha Mahakamani Diwani wa kata ya Litembo kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Mbinga mkoani humo, Altho Hyera kwa kile walichodai kuwa diwani huyo amekuwa akitishia usalama wa wafanyakazi wa hospitali ya Litembo na kuharibu kwa makusudi, sifa ya hospitali na maendeleo yake.

Hospitali hiyo ambayo humilikiwa na jimbo hilo, umeeleza pia diwani huyo amekuwa akimdhalilisha Askofu mkuu wa jimbo la Mbinga, John Ndimbo kwa kuandikia barua kwa viongozi wa juu wa serikali ambazo gazeti hili nakala zake imezipata zikimtuhumu Askofu huyo kuwa ni mla rushwa, ameshindwa kusimamia maendeleo husika na ameitelekeza hospitali hiyo.

Taarifa ya uongozi wa kanisa katoliki wilayani humo, kutaka kumfikisha kizimbani kiongozi huyo wa CCM zilielezwa katika kikao kilichowakutanisha baadhi ya waumini wa vigango vya kanisa hilo kata ya Litembo, ambao ulifanyika kwenye ukumbi wa Parokia ya Litembo uliopo katika kata hiyo.

Friday, May 29, 2015

MARIO MILLINGA KUPAMBANA NA GAUDENCE KAYOMBO

Mario Millinga.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KADA wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, Mario Millinga ametangaza nia yake ya kutaka kugombea nafasi ya ubunge katika jimbo la Mbinga Mashariki mkoani Ruvuma ambalo hivi sasa linaongozwa na Mbunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Gaudence Kayombo.

Kada huyo wa CHADEMA alisema kuwa ameshawishika kugombea nafasi hiyo ili wananchi wa wilaya hiyo, waone jinsi uongozi wa chama chake unavyojali maslahi ya wananchi hasa kwa wale waishio vijijini ambao muda mwingi, wamekuwa wakisahulika katika mambo mbalimbali ya kimaendeleo.

“Ubunge ni uwakilishi wa wananchi katika eneo husika, tunapomchagua mbunge au diwani ambaye si mkazi wa eneo la uwakilishi tunajitwika mzigo wa shida sisi wenyewe, ndugu zangu mimi ni mzaliwa wa kijiji cha Tukuzi hapa Mbinga nimedhamiria kugombea katika nafasi hii, ili niweze kuwatumikia ipasavyo wananchi wa jimbo hili”, alisema Mario.

Mario alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, juu ya nia yake ya kutaka kuingia katika kinyang’anyiro hicho cha kuwania nafasi ya ubunge, jimbo la Mbinga Mashariki na kwamba ni kijana na kada wa siku nyingi wa chama hicho ambaye amebobea katika masomo ya biashara, uhasibu na uchumi kutoka chuo kikuu cha Dar es Salaam sehemu ya mlimani na kuhitimu elimu ya biashara ngazi ya Bachelor of Education in Commerce.

WALIOHUSIKA KUCHOMA MOTO BASI KUCHUKULIWA HATUA ZA KISHERIA


Baadhi ya wananchi wakishuhudia basi la kampuni ya Babu J Trans, likiteketea kwa moto baada ya kuchomwa na wananchi wenye hasira kali.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

SERIKALI wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma imeapa kwamba, haitawasamehe wananchi wa kijiji cha Mhuwesi na Msagula wilayani humo ambao wamehusika kuchoma moto basi la kampuni ya Babu J Trans, na kuliteketeza kabisa kutokana na basi hilo kugonga mtoto na kufariki dunia papo hapo.

Chande Nalicho ambaye ni Mkuu wa wilaya hiyo, alisema hayo alipokuwa katika eneo la tukio kwa lengo la kujionea uharibifu huo uliofanywa na wananchi wenye hasira kali kwa kujichukulia sheria mkononi, kinyume na taratibu za nchi zinavyotaka.

Mkuu huyo wa wilaya alilaani vikali kitendo hicho, baada ya basi hilo kumgonga mwanafunzi aliyefahamika kwa jina la Faidhi Ally (10) na kusababisha kifo papo hapo, katika ajali iliyotokea Mei 26 mwaka huu majira ya mchana.

WAHITIMU CHUO CHA SAYANSI WATAKIWA KUWAKOMBOA WATANZANIA

 
Upande wa kulia, Askofu Mkuu wa Jimbo kuu katoliki la Songea mkoani Ruvuma, Damian Dallu akimzawadia kompyuta mpakato (Laptop) mmoja wa wahitimu wa chuo cha sayansi na tekinolojia ya mawasiliuano cha Mtakatifu Joseph mjini Songea ambaye amevaa vazi jeusi, baada ya kufanya vizuri masomo yake na kushoto ni Mkuu wa chuo hicho Dokta Arulaj. 

Na Julius Konala,
Songea.

WAHITIMU wa chuo cha Sayansi na tekinolojia ya mawasiliano cha Mtakatifu Joseph, kilichopo katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wametakiwa huko waendako kutumia vyema elimu waliyoipata, kwa malengo ya kuwakomboa Watanzania na taifa kwa ujumla.

Aidha wameshauriwa kutumia kipawa walichonacho, kuongeza juhudi na maarifa waliyoyapata chuoni hapo ili waweze kuleta chachu ya mabadiliko katika jamii, kwa manufaa ya kizazi cha sasa na baadaye.

Rai hiyo ilitolewa na Askofu Mkuu wa jimbo kuu katoliki la Songea, Damian Dallu alipokuwa akizungumza na wanafunzi, wazazi na walimu kwenye mahafali ya sita ya chuo hicho yaliyofanyika mjini hapa.

MGAWANYO WA MAJIMBO YA UCHAGUZI MBINGA WAZUA MALALAMIKO

Kaimu Mkurugenzi wa uchaguzi Kailima R.K akizungumza hivi karibuni na vyombo vya habari hapa nchini, kuhusu uchunguzi wa mipaka na kugawa majimbo kwa ajili ya uchaguzi mkuu mwaka huu, katika ofisi za makao ya tume ya uchaguzi.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

PENDEKEZO la kuligawa Jimbo la Mbinga Mashariki, lililopo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma limeingia dosari kufuatia kuwepo kwa malalamiko yanayodaiwa kwamba mchakato huo wa kuligawa jimbo hilo, umefanywa na viongozi wachache bila kushirikisha wadau mbalimbali wa wilaya hiyo, kitendo ambacho kimeelezwa kuwa ni ukiukwaji wa maagizo na taratibu zilizotolewa na tume ya taifa ya uchaguzi hapa nchini.

Baadhi ya wananchi wa wilaya hiyo, walitoa malalamiko hayo walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti huku wakiitaka serikali kuwa makini na suala hilo ambalo kutokana na wadau husika kutoshirikishwa kama vile taratibu za tume katika kurekebisha mipaka, kugawa majimbo na kubadili majina zinavyotaka.

Mapendekezo hayo ya kuligawa jimbo hilo yamefanyika muda wa nusu saa katika kikao cha dharula cha baraza la madiwani, kilichoketi Mei 27 mwaka huu kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo mjini hapa.

Hata baadhi ya Madiwani ambao walikuwepo katika kikao hicho nao walionesha kushangazwa na hali hiyo, wakisema kuwa walitumiwa ujumbe kwa njia ya simu kwamba wanatakiwa katika kikao cha dharula kwa tarehe hiyo, bila kufafanuliwa kinahusu nini na walipowasili walikutana na ajenda hiyo ya pendekezo la kuligawa jimbo. 

NALICHO: WANANCHI TUSHIRIKIANE KUWAUA SIMBA

Mkuu wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Chande Nalicho akizungumza na wananchi wa wilaya hiyo katika moja ya ziara yake ya kikazi ambazo amezifanya hivi karibuni.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

CHANDE Nalicho ambaye ni Mkuu wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, amewataka wananchi wa vijiji vilivyopo katika tarafa ya Matemanga wilayani humo kutumia nguvu zao na kujituma kwa hali na mali, kuhakikisha kwamba simba ambao wamekuwa wakiwasumbua hasa nyakati za usiku wanauawa ili wananchi waondokane na adha wanayoipata sasa ya kushindwa kuishi kwa amani.

Nalicho alitoa kauli hiyo, alipokuwa akikabidhi askari wa nane idara ya wanyamapori wilayani humo, ambao walipelekwa katika tarafa hiyo kwa lengo la kupambana na simba hao kuhakikisha kwamba wanauawa.

Hatua hiyo imefuatia kutokana na simba hao wamekuwa wakishambulia mifugo ya wananchi hasa nyakati za usiku, jambo ambalo linahatarisha hata usalama wa binadamu kwa wakazi wanaoishi katika vijiji vilivyopo kwenye tarafa ya Matemanga.

WATENDAJI TUNDURU WATAKIWA KUTEKELEZA MAJUKUMU YAO

Na Mwandishi wetu,
Tunduru.

SERIKALI wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, imewaagiza watendaji wote wa vijiji wilayani humo kuhakikisha kwamba wanasimamia na kutekeleza ipasavyo sheria ndogo ndogo, ambazo zimetungwa na kupitishwa na baraza la Madiwani wa Halmashauri ya wilaya hiyo.

Aidha wameagizwa kuacha vitendo vya ulegevu, wakati wanapotekeleza majukumu yao ya kazi na kusababisha mwanya kwa wananchi kuvunja sheria husika, hatimaye maendeleo kushindwa kusonga mbele.

Katibu tawala wilayani Tunduru, Ghaibu Lingo alitoa agizo hilo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Matemanga wilayani humo.

Wednesday, May 27, 2015

WANACCM MBINGA KUMCHANGIA FOMU KELVIN MAPUNDA

Diwani wa kata ya Mbinga mjini mkoani Ruvuma, Kelvin Mapunda (Aliyevaa koti nyeusi) akizungumza na wanafunzi wa shule ya msingi Mbambi, Mbinga na Nyerere zilizopo katika kata hiyo wakati akiwa katika ziara yake hivi karibuni, akitembelea vituo vya masomo wakati wa likizo.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

BAADHI ya wazee na vijana wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kata ya Mbinga mjini mkoani Ruvuma, wamemtaka Diwani wa kata hiyo Kelvin Mapunda kwenda kuchukua fomu muda utakapofika kwa ajili ya kugombea tena, nafasi ya udiwani katika kata hiyo.

Aidha walieleza kuwa wapo tayari kutoa fedha zao mfukoni kwa ajili ya kumchangia fomu ya kuwania nafasi hiyo, kwa kile walichoeleza kuwa wamejenga imani naye kutokana na kazi zake alizozifanya katika kipindi cha miaka kumi ya uongozi wake aliowaongoza.

Wazee na vijana hao walisema hayo walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti mjini hapa, huku wakiongeza kuwa wao wanaona ndiye mwanachama ambaye yupo karibu nao katika kuendeleza maendeleo yao kwa faida ya sasa, na kizazi kijacho.

Tuesday, May 26, 2015

NEC YATOA RATIBA YA UCHAGUZI MKUU MWAKA HUU

Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) Jaji mstaafu, Damian Lubuva.

Na Mwandishi wetu,

TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetoa ratiba ya uchaguzi Mkuu kwa mwaka huu 2015.
Katika taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa tume hiyo mbele ya waandishi wa habari, Jaji Damian Lubuva alisema kwamba;

v Agosti 21 – 2015: kutakuwa na uteuzi wa wagombea Urais, Ubunge na Udiwani.
v Agosti 22 – Oktoba 24, 2015: kutafanyika kampeni za uchaguzi.
v Oktoba 25 – 2015: itakuwa ni siku ya kupiga kura.

Sunday, May 24, 2015

DEREVA AFARIKI DUNIA FUVU LA KICHWA LAPASUKA BAADA YA KUPATA AJALI KONA YA MBWA

Na Steven Augustino,
Tunduru.

DEREVA mmoja ambaye amekuwa akiendesha magari makubwa ya mizigo na hufanya safari zake katika maeneo mbalimbali hapa nchini, amefariki dunia katika ajali iliyotokea kona ya mbwa eneo la Nakayaya, karibu na kiwanda cha kubangua korosho wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma.

Said Jiram (37) ndiye aliyefariki dunia ambapo ndani ya gari alilokuwa akiliendesha lenye namba za usajili T 481 ATZ aina ya Toyota Carina ambalo ndani yake alikuwa na wenzake wawili, ambao walinusurika kifo.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo, walieleza kuwa watu hao walipatwa na mkasa huo wakati walipokuwa wakielekea karibu na kiwanda hicho, kwa lengo la kwenda kupakia korosho kwenye lori hatimaye wasafirishe kwenda Jijini Dar es Salaam.

Akifafanua juu ya tukio hilo rafiki wa marehemu huyo, Mohamed Mponda ambaye ni mmoja aliyenusurika kwenye ajali hiyo alisema kuwa yeye na marehemu walikuwa pamoja kwenye gari hilo, ambapo wakiwa njiani kuelekea huko ghafla gari lilipinduka mara mbili na kusababisha kifo kutokana na Jiram kupatwa na majeraha mengi mwilini huku akitokwa na damu nyingi.

WANASIASA SONGEA WADAIWA KUKWAMISHA MPANGO WA TASAF

Na Muhidin Amri,
Songea.

MPANGO wa kunusuru kaya maskini ulioratibiwa na mfuko wa maendeleo ya jamii nchini (TASAF) awamu ya tatu, Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma umeweza kuibua kaya maskini 8492 sawa na asilimia 106 ikiwa ni ongezeko la kaya 464 ambazo zilikadiriwa hapo awali kufikiwa na mpango huo, katika Manispaa hiyo.

Aidha hadi sasa TASAF imeweza kutekeleza kazi zake katika mitaa 53 ya mjini hapa, ambayo nayo iliingizwa kwenye mpango kwa lengo la kukabiliana na changamoto zilizopo, hatimaye kuweza kufikia malengo iliyojiwekea.

Mratibu wa mpango wa kunusuru kaya maskini katika Manispaa ya Songea, Christopher Ngonyani alieleza hayo, alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu ofisini kwake.

Saturday, May 23, 2015

GOLD STAR YAWAJENGEA UWEZO MAFUNDI RANGI RUVUMA

Na Julius Konala,
Songea.

MAFUNDI rangi waliopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wamenufaika na mafunzo juu ya utumiaji wa tekinolojia ya upakaji rangi ikiwa ni lengo la kuwajengea uwezo, utendaji wa kazi zao za kila siku.

Zaidi ya mafundi 100 ndio waliopewa mafunzo hayo na kampuni ya Gold Star katika Manispaa hiyo, ambayo yalifanyika kwa muda wa siku moja kwenye ukumbi wa chuo cha Top one inn, mjini Songea ambayo yalishirikisha wanawake na wanaume.

Akizungumza katika mafunzo hayo Meneja mauzo wa kampuni hiyo, Ally Khalfan alisema kuwa lengo ni kuboresha taaluma ya upakaji rangi kwa mafundi hao, ili kuweza kuleta mabadiliko katika utendaji wa kazi zao.

Friday, May 22, 2015

FEDHA ZA KUNUNULIA BOTI ZILIZOTOLEWA NA WAZIRI MKUU PINDA WILAYANI NYASA ZAZUA MALALAMIKO

Wavuvi wakiwa katika ziwa Nyasa, wakitumia vifaa duni (mitumbwi) kuvulia samaki ambapo huhatarisha usalama wa maisha yao.
Na Kassian Nyandindi,
Nyasa.

VIKUNDI vinavyojishughulisha na uvuvi wa samaki Mbamba bay wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, vimeutaka uongozi wa Halmashauri ya wilaya hiyo kuchukua hatua za haraka kufanya manunuzi ya boti la kisasa la kuvulia samaki, ambalo Ofisi ya Waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mizengo Pinda  alikwisha toa fedha kwa ajili ya kufanya manunuzi hayo.

Aidha wanakikundi hao ambao waliomba majina yao yasitajwe gazetini na hujishughulisha na shughuli za uvuvi katika ziwa Nyasa, walisema kuwa wanaushangaa uongozi wa wilaya hiyo tokea wapewe fedha shilingi milioni 14 na ofisi ya Waziri huyo, takribani miezi miwili imepita, hakuna majibu kamilifu waliyoyapata juu ya manunuzi ya boti hilo.

Walisema Waziri Pinda alitoa ahadi ya kununua chombo hicho cha kisasa kwa ajili ya kuwawezesha kuvua samaki kwa urahisi, alipokuwa hivi karibuni kwenye ziara yake ya kikazi wilayani humo baada ya kupokea kilio cha wavuvi hao kwamba wamekuwa wakipoteza maisha kwa kuzama na mitumbwi majini, kutokana na kukosa kifaa cha kisasa cha kuvulia samaki.

MADIWANI WATAKIWA KUTOWAOGOPA WATUMISHI

Na Kassian Nyandindi,
Namtumbo.

MADIWANI wa Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, wametakiwa kutowaogopa watumishi na watendaji wa serikali waliopo katika wilaya hiyo, badala yake wawabane na kuwahoji ikiwemo hata kufanya ufuatiliaji wa fedha za miradi ya maendeleo ya wananchi, ambazo hupelekwa katika maeneo yao.

Mbali na hatua hiyo, pia wamehimizwa kuwashirikisha wananchi ili  nao waweze kushiriki vyema katika shughuli za miradi hiyo jambo ambalo litawezesha wilaya, kufikia malengo yake iliyojiwekea ikiwemo kupiga hatua katika nyanja ya kiuchumi.

Rai hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Stephen Nana alipokuwa akizungumza na watumishi pamoja na madiwani katika kikao cha baraza la madiwani, ambacho kiliketi mjini hapa.

Tuesday, May 19, 2015

MAOFISA UGANI RUVUMA WAJENGEWA UWEZO

Na Julius Konala,
Songea.

MAOFISA ugani katika Halmashauri nne zilizopo mkoani Ruvuma, wameweza kujengewa uwezo juu ya matumizi sahihi, katika tekinolojia mpya ya uhifadhi wa mazao.

Lengo la maofisa hao kupewa elimu hiyo, ni kuwataka katika maeneo ambayo wanafanyia kazi mkoani humo, waende kwa wakulima vijijini wakawaelimisha juu ya tekinolojia hiyo na baadaye waweze kuhifadhi mazao yao katika hali nzuri.

Mafunzo juu ya matumizi sahihi ya uhifadhi wa mazao, yalifanyika jana kwenye ukumbi wa mikutano Walimu SACCOS mjini Songea, ambayo yalikuwa yakiendeshwa na shirika la CARITAS na CRS.

Jumla ya maofisa ugani 32 kutoka wilaya ya Songea, Namtumbo, Mbinga na Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wameweza kupata elimu hiyo.

Mwakilishi mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Georgina Mbawala alisema washiriki hao mara baada ya kumaliza kupewa mafunzo hayo watakuwa walimu wazuri, katika suala la uhifadhi huo ambao unalenga kuhifadhi mazao katika kipindi cha miaka mitatu bila ya kushambuliwa na wadudu waharibifu.