Monday, March 24, 2014

KIGONSERA AFYA ZAO ZIPO HATARINI, WANANCHI WATISHIA KULALA BARABARANI KUZUIA MSAFARA WA RAIS


Hivi ndivyo ilivyo katika chanzo cha maji Kigonsera ambako maji yametegwa kwa ajili ya matumizi ya binadamu, hali ni mbaya hatua husika zinapaswa kuchukuliwa mapema.(Picha na Gwiji la matukio Ruvuma)










Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

AFYA za wakazi wa kijiji cha Kigonsera kata ya Kigonsera wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, zipo mashakani kutokana na maji wanayotumia kwa ajili ya kuendeshea maisha yao ya kila siku kuwa machafu na kutofaa kwa matumizi ya binadamu.

Hali hiyo imesababisha wakazi hao kutoa tamko na kutishia kwamba siku ya ujio wa Rais Jakaya Kikwete, katika ziara ambayo anatarajia kuifanya hivi karibuni katika kipindi cha mwezi Mei mwaka huu mkoani humo hususani katika wilaya ya Mbinga, wapo tayari kulala barabarani kwa lengo la kushinikiza msafara huo usimame ili waweze kutoa kilio chao kwa kiongozi huyo wa kitaifa na kiweze kufanyiwa kazi haraka.

Walisema kufanya hivyo kunatokana na uongozi wa wilaya hiyo kuwa na kasi ndogo, ya uchukuaji wa hatua za kuwahamisha watu waharibifu katika eneo ambako chanzo cha maji kimejengwa na kugharimu mradi mzima wa maji uliosambazwa kijijini hapo kufikia shilingi milioni 479 kwa ufadhili wa benki ya dunia.

Tuesday, March 11, 2014

TANROADS RUVUMA YAENDELEA KUNYOSHEWA KIDOLE

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.


SERIKALI mkoani Ruvuma imeombwa kuchukua hatua za haraka juu ya ujenzi wa barabara ya kutoka Mbinga mjini, kwenda hospitali ya Litembo iliyopo wilayani humo, kutokana na barabara hiyo kuwa katika hali mbaya.

Rai hiyo ilitolewa na Wananchi wa wilaya ya Mbinga mkoani humo walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tofauti, ambapo walieleza kuwa kutokana na barabara hiyo kuwa na mashimo mengi ambayo ni makubwa, magari ya abiria na yale yanayobeba wagonjwa yamekuwa yakikwama na kuleta adha kubwa kwao.

Walisema wamechoshwa na ahadi hewa ambazo zimekuwa zikitolewa mara kwa mara na viongozi wa serikali wa mkoa huo, kwamba wataifanyia matengenezo na hakuna matokeo mazuri yanayoonekana kuzaa matunda juu ya kumaliza tatizo hilo ambalo limedumu kwa miaka mingi.

"Tunachohitaji hapa waifanyie matengenezo tumechoka na kauli zao ambazo hazina utekelezaji sisi ni wananchi kama walivyo wenzetu katika maeneo mengine ambayo serikali inawapelekea huduma za msingi",
walisema.

Monday, March 10, 2014

WANAWAKE MKOANI RUVUMA WALALAMIKIA UKATILI UNAOSABABISHWA NA HISIA ZA KIMAPENZI

Kutoka kulia ni Diwani wa viti maalum tarafa ya Mbinga mjini, Grace Millinga akifurahia jambo pamoja na Wanawake wenzake kwenye sherehe za maadhimisho ya siku ya mwanamke duniani, ambazo mkoani Ruvuma zilifanyika katika kijiji cha Kihereketi wilayani Mbinga.


Akina mama wa mkoa wa Ruvuma, wakiendelea kwa pamoja kufurahia maadhimisho ya sherehe za siku ya mwanamke Duniani.

Joseph Mkirikiti Mkuu wa wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, akipokea maelezo mafupi kutoka kwa mjasiriamali ambaye anatengeneza kinywaji cha asili aina ya "Wine". {Picha zote na Gwiji la matukio Ruvuma}


Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

WANAWAKE mkoani Ruvuma wamelalamikia na kupinga vikali vitendo vinavyoendelea kushamiri, ambavyo hufanyiwa miongoni mwao mkoani humo ikiwemo ukatili, kupigwa na kuuawa kutokana na hisia za kimapenzi.

Aidha wamesema kuwa upande wa watoto wa kike kumekuwa na ukosefu wa usawa katika kupata elimu, hivyo kusababisha watoto wengi kuishi katika mazingira hatarishi.

Kilio hicho kilitolewa na Wanawake hao kupitia risala yao iliyosomwa mbele ya mgeni rasmi Mkuu wa wilaya ya Songea Joseph Mkirikiti, katika sherehe za maadhimisho ya kilele cha siku ya wanawake duniani kilichofanyika katika mkoa huo kijiji cha Kihereketi kata ya Nyoni wilayani Mbinga.

Akisoma taarifa hiyo kwa niaba ya wanawake wenzake, Cosma Mbawala ambaye ni mkazi wa kijiji hicho alisema wanawake ni kichocheo kikubwa katika harakati za kuleta maendeleo lakini inasikitisha kuona wamekuwa wakinyanyaswa na kunyimwa haki zao za msingi.

Friday, March 7, 2014

WANAFUNZI WAJISAIDIA PORINI KUTOKANA NA SHULE KUKOSA VYOO



Na Kassian Nyandindi,

Nyasa.

SHULE ya msingi Ndingine iliyopo katika kata ya Ngumbo wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, inakabiliwa na tatizo la ukosefu wa vyoo kwa muda mrefu sasa jambo ambalo lina hatarisha usalama wa afya kwa walimu na watoto wanaosoma shuleni hapo.

Mwandishi wa habari hizi amebaini na kushuhudia pia wanafunzi wakijisaidia pori lililopo jirani na shule hiyo, huku walimu wao nao wakiomba msaada katika vyoo vya wakazi wanaoishi jirani na shule hiyo.

Huenda hatua zisipochukuliwa mapema hususani katika kipindi hiki cha masika magonjwa ya mlipuko kama vile kipindupindu na homa zingine za matumbo, zinaweza kujitokeza na kuleta madhara makubwa kwa binadamu.

Ndingine ni shule ambayo ina jumla ya wanafunzi 306 wakiwemo wavulana   163 na wasichana 143 ambapo hata mazingira ya shule hiyo sio mazuri hivyo jitihada za makusudi zinahitajika katika kunusuru hali hiyo isiweze kuendelea.

HOSPITALI YAPEWA MSAADA WA VIFAA TIBA



Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

HOSPITALI ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, imepewa msaada wa vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 5,530,000 kwa lengo la kusaidia utoaji wa huduma bora za matibabu kwa wagonjwa.

Vifaa hivyo vilitolewa na Mbunge wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo wakati alipokuwa ametembelea hospitalini hapo, kwa lengo la kujionea changamoto mbalimbali ambazo zinakwamisha utoaji wa huduma za matibabu.

Kayombo alikabidhi vifaa vya kitengo cha maabara ambavyo ni Darubini mbili, mashine za kupimia magonjwa ya sukari na moyo ambapo hospitali hiyo inakabiliwa na upungufu wa vifaa hivyo.

Monday, February 24, 2014

MAFUNZO YA UTENGENEZAJI VITO VYA THAMANI MBINGA YAKAMILIKA, WASHIRIKI WAIOMBA SERIKALI KUUNGA MKONO

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
WASHIRIKI wa mafunzo ya kutengeneza vito vya thamani wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wameiomba serikali wilayani humo kuendelea kuunga mkono mafunzo waliyoyapata ili yaweze kuleta faida kwa kizazi cha sasa na kijacho.
 
Kauli hiyo ilitolewa kupitia risala yao iliyosomwa na mmoja kati ya washiriki hao, Editha Komba mbele ya mgeni rasmi Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga wakati wa kufunga mafunzo hayo ya wiki mbili yaliyofanyika katika chuo cha maendeleo ya wananchi (FDC) kilichopo mjini hapa.
 
Aidha katika risala hiyo washiriki hao walisema wameweza kujifunza kutengeneza ukataji wa vipande vya aluminiamu na shaba, kutengeneza mapambo mbalimbali kama vile heleni, cheni na bangili.
 
Walieleza kuwa wameweza kujifunza kutumia vitu vya asili kama vile mbegu za maembe, kahawa, maboga na manyoya ya kuku kutengeneza mapambo ya asili.

Friday, February 21, 2014

POLISI WAFANIKIWA KUKAMATA JAMBAZI LILILOKUWA LIKITESA WANANCHI WA MBINGA KWA MUDA MREFU

Jambazi linalodaiwa kuwa sugu Roster Ndunguru (katikati) akiwa chini ya ulinzi wa polisi katika hospitali ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, ambako amelazwa baada ya kuambulia kipigo kutoka kwa Polisi wakati akijaribu kutoroka.

Jambazi linalodaiwa kuwa sugu Roster Ndunguru (27) mkazi wa kijiji cha Mbangamao akiwa amefungwa pingu katika hospitali ya wilaya ya Mbinga ambako amelazwa baada ya kuambulia kipigo kikali kutoka kwa Polisi wakati akijaribu kutoroka mikononi mwao. (Picha zote na Kassian Nyandindi)



Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

JESHI la Polisi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, limefanikikwa kumkamata Roster Ndunguru mkazi wa kijiji cha Mbangamao wilayani humo ambaye anadaiwa kuwa ni jambazi sugu na amekuwa akifanya matukio mengi ya kiuhalifu ikiwemo kuwajeruhi watu na kunyang’anya mali zao.

Aidha Jambazi hilo lilikuwa likitafutwa kwa muda mrefu baada ya kumjeruhi Mratibu elimu kata ya Mbangamao, Florence Kowelo kwa kumjeruhi sehemu mbalimbali za mwili wake na kumpiga na kitu kizito kichwani.

Tukio hilo imeelezwa kuwa lilitokea majira ya usiku wakati Mratibu huyo akiwa nyumbani kwake amelala na familia yake, ambapo baada ya kupiga kelele majirani walijitokeza na jambazi hilo lilitokomea kusikojulikana.

Kwa mujibu wa chanzo cha uhakika kutoka Jeshi la Polisi wilayani Mbinga ambacho hakikutaka jina lake litajwe katika mtandao huu, kilisema kuwa Roster amekuwa na matukio mengi ya kiujambazi ambayo amekuwa akiyafanya katika maeneo mbalimbali wilayani humo.

Tuesday, February 18, 2014

HALMASHAURI YA MBINGA YAINGIA MKATABA WA MAFUNZO YA KUTENGENEZA VITO VYA THAMANI, WAKOREA KUJENGA KIWANDA

Mbunge wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo(aliyesimama) akisisitiza jambo wakati wa kumkaribisha mtaalamu wa madini kutoka Korea, Dokta Kim (katikati) ambaye ana lengo la kupanua soko la madini kwa wachimbaji wadogo wadogo wa madini na kutangaza fursa za kimaendeleo kwa mataifa mengine wilayani Mbinga. Kushoto ni mtaalamu mwenzake aitwaye Changlee.



Mtaalamu wa madini ambaye ni wa kwanza kutengeneza vito vya thamani Korea kusini Dokta Kim, (kushoto) akiweka sahihi katika mkataba aliotiliana nao na Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma katika hafla fupi iliyofanyika ukumbi wa chuo cha maendeleo uliopo mjini hapa, Upande wa kushoto kwa Dokta Kim ni mkuu wa chuo cha maendeleo ya jamii (FDC) wilayani Mbinga Aidan Mchawa naye akiweka sahihi katika mkataba huo wa kutoa mafunzo ya kutengeneza vito hivyo na kujenga kiwanda cha kutengeneza vito vya thamani wilayani humo, kiwanda hicho kinatarajiwa kujengwa na wakorea hao miaka mitano ijayo. Wanaoshuhudia kutoka kushoto ni Askofu wa jimbo la Mbinga John Ndimbo na anayefuatia ni Mbunge wa jimbo la Mbinga Gaudence kayombo. (Picha na Kassian Nyandindi)

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
HALMASHAURI ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma kupitia chuo chake cha maendeleo ya jamii (FDC) kilichopo mjini hapa, kimeingia mkataba na mtaalamu wa madini ambaye anafahamika kwa jina la Dokta Kim kutoka nchi ya Korea kusini, kwa ajili ya kutoa mafunzo ya wiki mbili ya utengenezaji wa vito vya thamani.
 
Pia mkataba huo unalenga miaka mitano ijayo mtaalamu huyo ataweza kujenga kiwanda cha kutengeneza vito vya thamani wilayani humo, jambo ambalo litaweza kupanua soko la ajira kwa wananchi wa wilaya hiyo.
 
Akizungumza katika hafla fupi ya kutiliana sahihi katika ukumbi wa chuo cha maendeleo uliopo Mbinga mjini, Dokta Kim alisema yeye ni mtu wa kwanza katika nchi hiyo ya Korea kusini ambaye anaongoza kwa utengenezaji wa vito vya thamani, hivyo anawaomba washiriki walioteuliwa kujiunga na mafunzo hayo kuwa makini wakati watakapo kuwa darasani.
 
Dokta Kim alisema kuwa wazo hili la kuja Mbinga na kutaka kufanya hayo ni jitihada zilizofanywa na Mbunge wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo, ambapo mafunzo hayo yataweza kuwafungua vijana wa wilaya hiyo waweze kufanya shughuli za utengenezaji wa vito hivyo na kuweza kuondokana na umasikini.

Monday, February 17, 2014

WAZAZI WILAYANI MBINGA WASHAURIWA KUPELEKA WATOTO WAO KATIKA CHUO CHA UFUNDI PILIKANO

Kibao kikionyesha mwelekeo wa chuo cha ufundi Pilikano, ambacho kipo umbali wa kilometa 18 kutoka Mbinga mjini mkoani Ruvuma.

Wanafunzi wakijifunza ufundi wa umeme wa majumbani.

Baadhi ya wanafunzi wakiwa darasani wakijifunza fani ya ushonaji.

Mkurugenzi wa chuo cha ufundi Pilikano, Bruno Kapinga, akizungumza na mwandishi wa habari hizi (Hayupo pichani) wakati wa mahojiano yaliyofanywa juu ya maendeleo ya chuo hicho. (Picha zote na Gwiji la matukio Ruvuma)



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WADAU wa elimu wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wametakiwa kuwa na mwamko wa kupeleka watoto wao katika vyuo vya ufundi hususani kwa vile ambavyo vipo karibu na maeneo yao, ili waweze kupata ujuzi wa aina mbalimbali.

Aidha imeleezwa kuwa watoto wanaomaliza darasa la saba wilayani humo, wamekuwa wengi wakizurula mitaani hivyo ni vyema sasa wakapelekwa katika vyuo hivyo ili waweze kuwa na maendeleo katika fani za ufundi kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.

Wito huo ulitolewa na Mkurugenzi wa chuo cha ufundi Pilikano Bruno Kapinga, kilichopo katika kata ya Mkumbi wilayani Mbinga wakati alipokuwa akihojiwa na mwandishi wa habari hizi juu  ya maendeleo ya chuo hicho.

Kapinga alisema kuwa chuo hicho kimesajiliwa na VETA na kilianza rasmi kutoa mafunzo ya ufundi mwaka 2012 katika fani ya ushonaji, magari na umeme.

Mkurugenzi huyo alisema kwamba wazo la kujenga chuo alilipata baada ya kupata ufadhili kutoka Uholanzi, ambapo wafadhili kutoka katika nchi hiyo waliweza kumsaidia vifaa vya ufundi katika fani hizo.

Tuesday, February 11, 2014

MBINGA NAKO KWA CHAFUKA WAFANYABIASHARA WAGOMA

Jakaya Kikwete, Rais wa Tanzania.

 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
HALI  si shwari  katika  mji  wa Mbinga mkoani Ruvuma, kufuatia  kuanza kwa mgomo  usio na kikomo wa wafanyabiashara kama njia ya  kufikisha ujumbe  kwa Waziri wa viwanda na biashara   na  serikali ya  Rais Jakaya  Kikwete,  juu ya gharama za mashine za kutolea risiti (EFD) wakidai kwamba gharama hizo ni kubwa na ni sawa na kumtishwa mzigo mfanyabiashara ambao hauna tija kwake.  


Mgomo huo umeanza leo  asubuhi  hii  huku  makundi ya wafanyabiashara wakiwa wamekusanyika katika maeneo mbalimbali ya mji huo, huku wakipanga kufanya maandamano  kuwaadhibu wenzao wanaokiuka mgomo huo ambao wataonekana wamefungua maduka.


Hali kwa upande wa wakazi wa Mbinga mjini  na wale wa maeneo ya vijijini ambao  wanakuja kwa ajili ya kupata huduma mbalimbali imewafanya wawe katika wakati mgumu kutokana na mgomo huo, hivyo kujikuta wakiambulia makufuri katika maduka hayo.


Wafanyabiashara  hao  wametoa onyo kwa  wenzao iwapo  watafungua  maduka yao  watakiona cha moto  na  kuanzia  wakati  wowote sasa,  wataanza msako wa duka moja hadi jingine kwani wamesema mgomo  huo ni wa nchi nzima na wao  wametii uamuzi wa  wafanyabiashara wenzao katika mikoa yote iliyopo hapa nchini.

Saturday, February 8, 2014

OFISA ELIMU SHULE ZA SEKONDARI MBINGA AVULIWA MADARAKA, WAZIRI ASEMA NIMEMSHUSHA MADARAKA AKAFUNDISHE AKIWA MWALIMU WA KAWAIDA

Naibu Waziri Elimu na Mafunzo ya Ufundi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Kassim Majaliwa, akiwasili wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma baada ya kupokelewa na Mkuu wa wilaya hiyo (Kulia kwake) Senyi Ngaga katika eneo la Kanisa Katoliki (Jimboni) lililopo mjini hapa.

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Kassim Majaliwa akiweka sahihi katika vitabu vya wageni baada ya kuwasili kwenye ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Ngaga ambaye yupo mbele yake akishuhudia.

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi Kassim Majaliwa akizungumza na Walimu hawapo pichani wa wilaya hiyo katika ukumbi wa UVIKAMBI uliopo Mbinga mjini, upande wa kulia mwanzo kwake Waziri ni Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga na wa mwisho kutoka kwa Mkuu wa wilaya hiyo ni Katibu tawala wa wilaya hiyo Stephano Ndaki. (Picha zote na Gwiji la Matukio Ruvuma)


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

NAIBU Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Ofisi ya Waziri mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Kassim Majaliwa amemvua madaraka kwa kumshusha cheo Ofisa elimu shule za sekondari wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Hanji Yusuph Godigodi kwenda kuwa mwalimu wa kawaida wa sekondari kutokana na Ofisa huyo kushindwa kutekeleza majukumu yake ya kazi na kufanya ubadhirifu wa shilingi milioni 268 za maendeleo ya elimu ya sekondari wilayani humo.

Aidha amewashusha vyeo Wakuu wa shule za sekondari sita za wilaya hiyo kwenda kuwa walimu wa kawaida, kutokana na walimu hao wakidaiwa
kushirikiana na Ofisa huyo wa sekondari kufanya ubadhirifu wa fedha hizo.

Hatua ya Naibu Waziri huyo kuwashusha vyeo viongozi hao ilifikiwa katika kikao ambacho alikuwa akizungumza na Walimu wa shule za msingi na sekondari wilayani humo, ambacho kiliketi kwenye ukumbi wa Uvikambi uliopo mjini hapa na kwamba Waziri huyo yupo katika ziara yake ya kikazi wilayani Mbinga kwa muda wa siku mbili.

Waziri Majaliwa aliwataja wakuu wa shule za sekondari wilayani Mbinga ambao wameshushwa madaraka kuwa ni William Hyera ambaye ni wa shule ya
sekondari Maguu, Clemence Sangana anatoka shule ya sekondari Mkuwani, Method Komba Langilo sekondari, John Tillia Ukilo sekondari, Leonard Juma Luli Sekondari huku akimtaja kwa jina moja mwalimu Konga ambaye yupo sekondari ya Kihangimahuka.

Wednesday, January 29, 2014

DOKTA KAMANI AFUNGUKA AWATAKA WAFANYAKAZI WASIOENDANA NA KASI YAKE WAJIONDOE MAPEMA




Na Mwandishi wetu,


WAZIRI  wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi Dokta Titus Kamani, amesema ili kwenda na kasi ya maboresho ya wizara hiyo, inahitajika dhana ya uwajibikaji na uwazi sambamba na kujitolea kwa nguvu zote katika kufanya kazi.

Kamani, aliyasema hayo juzi katika mkutano wa kwanza uliowakutanisha wafanyakazi wote wa wizara hiyo, wakiwemo wastaafu wa mwaka jana katika ofisi ya wizara hiyo ilizopo Temeke jijini Dar es Salaam.

Alisema kama kuna mtu ambaye ni kikwazo katika kukwamisha shughuli za wizara, ni bora akawapisha mapema na kwamba kila mtumishi kwa nafasi yake, anatakiwa kuifanya kazi kwa uwazi na akaitaka wizara kufanya kazi na vyombo vya habari kwani ndio njia pekee ya kuwafanya watanzania wajue wizara inafanya nini.

“Wewe upo ofisini, halafu unaogopa ogopa vyombo vya habari, kwani unatatizo gani kuweni wazi mambo yenu yawe hadharani watanzania wa Mbeya wayajue, Rufiji mpaka Pemba, hakuna kuficha ficha jambo katika wizara yangu.” alisistiza Dokta Kamani.

Alisema wizara ya maendeleo ya mifugo na uvuvi ndio moyo wa taifa kwani huwajumuisha watanzania wengi wenye maisha ya kawaida, lakini amesikitishwa kwa jinsi ambavyo wizara hiyo imekuwa ikichukuliwa na baadhi ya watu kama ni wizara yenye migogoro na kuleta hasara maeneo mengine.

GUNINITA AMRUSHIA KOMBORA NAPE


Na Mwandishi wetu,
Dar es Salaam.

KITENDO cha Katibu mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Nape Nnauye cha kupinga uteuzi wa Mawaziri uliofanywa na Mwenyekiti wa chama hicho ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni mwendelezo wa tabia zake za ukosefu wa nidhamu kwa viongozi wake.

Hayo yamo katika taarifa yake kwa vyombo vya habari aliyoitoa hivi karibuni, ambapo aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Dar es salaam, John Guninita  amesema Nape ni mkiukwaji wa maadili, asiyeheshimu wakubwa ambao wamemteua kushika nafasi hiyo.

Alisema ni kiongozi ambaye anatakiwa kufanya kazi kwa  kuzingatia mipaka yake hivyo ni vema akafahamu kuwa madaraka ya kuteua Baraza la mawaziri ni kazi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano na sio vinginevyo.

Guninita alisema hata kama ingetokea Rais akashauriwa na washauri zaidi ya mia moja, bado uamuzi wake unapaswa kuheshimiwa na hakuna mtu anayeweza kuingilia au kubeza.

Wednesday, January 15, 2014

CHAMA CHA WALIMU MBINGA KWA CHAFUKA, NAIBU KATIBU MKUU TAIFA APOKELEWA KWA MABANGO

Baadhi ya Wanachama wa CWT wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakiwa wameshika mabango yenye ujumbe wa aina mbalimbali ambayo yanawashutumu Katibu wao wa mkoa huo Zebedayo Mwasandungila na wa wilaya hiyo Samwel Mhaiki, ambapo Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho kwa hasira alikataa kuyasoma na kuwaambia Wajumbe wa mkutano huo twendeni kwanza ndani kwenye ukumbi tukafanye mkutano.



Bado Wajumbe wa mkutano huo wakiwa ndani ya ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa ambako mkutano huo ulikuwa ukifanyika, wakiwa na hasira na kuendelea kushika mabango yenye ujumbe wa aina mbalimbali ambao ulikuwa ukiwashutumu baadhi ya viongozi wao wa mkoa na wilaya ya Mbinga .

Katibu Mkuu wa Chama Cha Walimu Tanzania, Ezekiah Oluoch, akihutubia katika ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa, mara baada ya Wanachama wa chama hicho kutuliza jazba zao. Upande wa kulia ni Mbunge wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo na kushoto ni Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo Hussein Ngaga. (Picha zote na Kassian Nyandindi) 



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) Ezekiah Oluoch amejikuta akiwa katika wakati mgumu, baada ya kupokelewa na wanachama wa chama hicho wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kwa malalamiko ya hapa na pale na mabango yaliyobeba ujumbe wa aina mbalimbali ambayo yalikuwa yakiwashutumu Katibu wa CWT wa mkoa huo na Wilaya hiyo.

Waliokuwa wakishutumiwa ni Zebedayo Mwasandungila ambaye ni Katibu wa CWT mkoa wa Ruvuma na Samwel Mhaiki, Katibu wa chama hicho wilayani Mbinga ambao wanalalamikiwa kutengeneza makundi ndani ya chama.

Vilevile Mhaiki alikuwa akinyoshewa kidole kwamba yeye na kamati yake ya chama wilayani humo, wameshindwa kukiongoza chama na badala yake makato wanayokatawa wanachama ya asilimia 15 katika mishahara yao hawarejeshewi katika matawi yao, hivyo hawaoni sababu ya kuendelea kubaki na viongozi hao na kuwataka wajiuzuru mara moja.

Walisema wamekwisha mpatia Bw. Mhaiki notisi ya siku 30 kwa lengo la kusudio la kumfikisha Mahakamani ili haki zao ziweze kupatikana.

“Tumekwisha mwona mwanasheria kwa lengo la kusudio la kumfikisha Mahakamani ndugu Samwel Mhaiki, na sasa tumempatia notisi ya siku 30 atuambie fedha zetu za makato ya kila mwezi zipo wapi”, walisikika wakisema kwa sauti.

Wednesday, January 8, 2014

WATUHUMIWA MAUAJI YA MLINZI WA GAPCO WAPANDISHWA KIZIMBANI

Watuhumiwa wanaodaiwa kumuua mlinzi wa kampuni ya GAPCO inayouza mafuta wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakipandishwa katika Karandika la Polisi baada ya kusomewa mashtaka yao katika Mahakama ya wilaya hiyo leo. (Picha na Kassian Nyandindi)










Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WATU watano wakazi wa Mbinga mjini mkoani Ruvuma, wameburutwa katika Mahakama ya wilaya ya Mbinga mkoani humo kwa tuhuma ya mauaji ya mlinzi wa kituo cha kuuza mafuta GAPCO, kilichopo mjini hapa.

Mwendesha mashtaka wa Polisi Inspekta Nassib Kassim alidai mbele ya Hakimu wa Mahakama ya wilaya hiyo, Joackimu Mwakyolo kuwa tukio hilo lilitokea Desemba 31 mwaka huu majira ya usiku.

Kassim aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Thito Turuka (30), Boniface Nombo (40), Ally Aman Chinga (29), Egno Nchimbi (24) na Felix Turuka (38).

Monday, January 6, 2014

TUNDURU WATAKIWA KUJENGA MSHIKAMANO NA UPENDO



Aliyesimama Diwani wa kata ya Majengo Athuman Nkinde akisisitiza jambo kabla ya kugawa vifaa vya kutengeneza batiki na sabuni za maji na vipande, kwa vikundi vya Majengo A na B wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma. Ambao wameketi ni viongozi wengine wa kata hiyo.  


Na Steven Augustino,
Tunduru.

WANACHAMA na wakereketwa wa chama cha Mapinduzi (CCM) katika kata ya Majengo wilayani Tunduru Ruvuma, wamehimizwa kudumisha muungano na upendo miongoni mwao na kuhakikisha wanapata ushindi wa  chama chao katika chaguzi zijazo za serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika mwaka huu.

Mariwani Athumani Nkinde wa Kata hiyo na  Diwani waviti maalumu wa tarafa ya Mlingoti Bi. Atingala Mohamed walisema hayo kwa nyakati tofauti  wakati wa  uzinduzi wa mradi wa maji safi ya bomba ugawaji wa vifaa vya kutengenezea Batiki, mafuta ya kupaka, sabuni za maji, na vipande katika kata hiyo.

Madiwani hao walisema kuwa endapo wanaCCM hawatashikamana katika ujenzi na uimarishaji wa chama chao ipo hatari ya mamluki kuingia miongoni mwao, na kuwavuruga kwa lengo la kuvipatia ushindi vyama pinzani.
 
Akifafanua taarifa ya ujenzi wa mtandao wa bomba la maji hayo na vifaa hivyo Diwani Athuman Nkinde, alisema kuwa hadi kukamilika kwake miradi hiyo imegharimu shilingi 400,000 na akatumia nafasi hiyo kuwaomba waitumie na kuitunza.

WAKAZI WA MBINGA MJINI WASHAURIWA KUTOA MSAADA KWA WAGONJWA

Mganga wa zamu wodi ya watoto (kulia) katika hospitali ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma,  Revina Kayombo akipokea msaada wa sabuni za kufulia wagonjwa, kutoka kwa Philiberth Hyera (aliyevaa suti nyeusi ambaye amekaa) mkazi wa Mbinga mjini. Hyera alitoa wito kwa wakazi wengine waliopo mjini hapa kupenda kuwasaidia wagonjwa.

Aliyevaa suti nyeusi ni Philiberth Hyera mkazi wa Mbinga mjini akitoa msaada wa sabuni za kufulia, kwa wagonjwa ambao wamelazwa katika wodi ya akina mama hospitali ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, hivi karibuni. (Picha zote na Kassian Nyandindi)

Thursday, January 2, 2014

UWT MBINGA YAWATAKA AKINA MAMA KUEPUKANA NA MAKUNDI YA ANASA

Wanachama wa UWT wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kukabidhi zawadi zao walipokwenda kuwataka hali akina mama wenzao ambao wamelazwa katika hospitali ya wilaya hiyo iliyopo mjini hapa.


Upande wa kushoto aliyevaa shati la kijani ni Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, Pendo Ndumbaro akifurahia jambo baada ya kushika mtoto mchanga ambaye alizaliwa usiku wa kuamkia mwaka mpya (2014) alipokuwa ametembelea jana wodi ya akina mama katika hospitali ya wilaya hiyo iliyopo mjini hapa kwa lengo la kuwataka hali, na wanaoshuhudia ni baadhi ya akina mama ambao wamelazwa katika hospitali hiyo. (Picha zote na Kassian Nyandindi).



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
WANAWAKE wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma wametakiwa kuwa makini katika kuendesha maisha yao kwa kujishughulisha na kilimo, biashara na kujiunga na vyama vya akiba na mikopo ili waweze kuepukana na kujiingiza kwenye anasa ambazo zinachangia maambukizi ya virusi vya ukimwi.
 
Sambamba na hilo wameshauriwa kushirikiana na kuchukua hatua katika kukabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili katika maisha yao ya kila siku kwa kufanya kazi kwa bidii.

Rai hiyo ilitolewa  jana na Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) wilayani Mbinga Pendo Ndumbaro, alipokuwa akizungumza na akina mama waliolazwa katika hospitali ya wilaya hiyo iliyopo mjini hapa ambao aliwatembelea kwa lengo la kuwataka hali na kuwapa zawadi mbalimbali.

Pia Mwenyekiti huyo alikuwa ameambatana na wanachama wenzake wa umoja huo ambao walishiriki kwa pamoja kwenda kuwaona wagonjwa hao waliokuwa wamelazwa katika hospitali hiyo.

GAUDENCE KAYOMBO ASIKITISHWA NA UJENZI WA BARABARA KIWANGO CHA LAMI KUTOKA SONGEA KWENDA MBINGA

Gaudence Kayombo.



















Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MBUNGE wa jimbo la Mbinga Gaudence Kayombo amesema, ujenzi wa  barabara kiwango cha lami kuanzia eneo la Likuyufusi pacha ya Peramiho wilaya ya Songea hadi Mbinga, katika baadhi ya maeneo umejengwa kwa kiwango kisichoridhisha kutokana na barabara hiyo kuanza kuwekwa viraka kabla ya kukabidhiwa rasmi mikononi mwa serikali.

Kayombo alisema hayo alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini hapa, huku akisisitiza kuwa hali hiyo huenda ikatokana na wataalamu husika kutozingatia ipasavyo vipimo vya kimaabara na ndio maana barabara hiyo hubomoka na kulazimika kuweka viraka.

Alisema uzembe huo uliofanywa wa kutozingatia viwango husika ni hasara kubwa kwa serikali kutokana na fedha nyingi iliyotumika kujengea barabara hiyo kutofanya kazi yake kama ilivyokusudiwa.

MLINZI AUAWA NA MAJAMBAZI KWA KUKATWA KOROMEO


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MLINZI wa kituo cha kuuza mafuta GAPCO kilichopo Mbinga mjini mkoani Ruvuma, amekutwa akiwa ameuawa kikatili na watu wasiojulikana kwa kukatwa koromeo na kujeruhiwa vibaya sehemu mbalimbali za mwili wake.

Kwa mujibu wa taarifa zilizolifikia gazeti hili imeelezwa kuwa aliyeuawa ni Kelvin Mapunda(52) mkazi wa mjini hapa, ambapo mwili wake ulikutwa ukiwa umetelekezwa karibu na eneo la kituo hicho cha mafuta.

Mwandishi wa habari hizi alipofika katika eneo la tukio hilo, alikuta umati mkubwa wa watu ukiwa umezunguka mwili wa marehemu huyo huku wakionekana kuchukizwa na kitendo hicho cha kinyama.

WAKIMBIA FAMILIA ZAO WAKIHOFIA KUKAMATWA NA POLISI


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

BAADHI ya Wanaume wa kijiji cha Mbangamao kati, kata ya Mbangamao wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma wamezikimbia familia zao wakihofia kukamatwa na polisi baada ya kuvamia nyumba ya Mratibu elimu wa kata hiyo Florence Kowelo, na kumjeruhi kwa kumpiga nondo kichwani.

Watu hao wanadaiwa kufanya kitendo hicho na kutishia usalama wa Watumishi wengine wa serikali, katika kata hiyo baada ya kuwatuhumu wamekuwa na tabia ya kufanya mapenzi na wake zao.

Tukio hilo lilitokea usiku wa Desemba 27 mwaka huu na kwamba vibaka hao ambao wanatamba kijijini hapo kwa jina la M 23, kuwa wameapa kupambana na Watumishi wote waliopo katika kata ya Mbangamao.