Thursday, May 3, 2018

WAKULIMA MBINGA WASHAURIWA KUWEKA AKIBA YA CHAKULA

Mkuu wa Wilaya ya Mbinga, Cosmas Nshenye.

Na Dustan Ndunguru,       
Mbinga.

SERIKALI Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma imewataka wakulima Wilayani humo kuachana na tabia ya kuuza mazao yao yote, badala yake wajenge tabia ya kuweka akiba ya chakula ili waweze kuepukana na njaa.

Agizo hilo lilitolewa na Mkuu wa Wilaya hiyo, Cosmas Nshenye alipokuwa akizungumza na Waandishi wa habari Ofisini kwake ambao walimtembelea kwa lengo la kupata taarifa mbalimbali za maendeleo.

Nshenye alisema kuwa Serikali Wilayani humo haitasita kuchukua hatua kali kwa wakulima wenye tabia ya kuuza mazao bila kufuata taratibu na sheria zilizowekwa, ikiwemo kuwataka kuweka akiba ya chakula ili kuwanusuru na balaa la njaa linaloweza kutokea hapo baadaye.


Alisema kuwa Serikali imekuwa ikibebeshwa mzigo mkubwa pale inapotokea janga la njaa kwa kutafuta chakula kwa ajili ya kuwasaidia watu waliokumbwa na tatizo hilo, licha ya wengi wao walishazalisha chakula kwa wingi ambapo kutokana na kuwa na tamaa ya fedha walijikuta wameuza chakula chote bila kukumbuka kuweka akiba kwa ajili ya matumizi ya familia zao.

“Ndugu zangu nimelazimika kulisemea hili  kwa kuwa limekuwa ni tabia iliyozoeleka kwa baadhi ya wananchi wamekuwa wanavuna mazao mengi ya chakula na biashara, lakini mwisho wa siku kutokana na kuwa na tamaa ya fedha wanajikuta hawana hata chakula kwa ajili ya kulisha familia zao sitaki hili lijitokeze katika Wilaya hii”, alisisitiza.

Mkuu huyo wa Wilaya Mbinga aliwataka wananchi Wilayani humo kutoendekeza matukio ya sherehe za ngoma zisizokuwa na msingi kwa kuwa zimekuwa zikitumia chakula kingi kwa wakati mmoja ili kupatasifa ambazo hazina maana yeyote kwao na mwisho wake hujikuta wakiendelea kuwa maskini.

Pamoja na mambo mengine aliongeza kuwa msimu wa mavuno unakaribia hivyo watendaji wa Serikali waliopo vijijini wanapaswa kuhakikisha kwamba wanawaelimisha wananchi juu ya umuhimu wa kujiwekea akiba ya chakula cha kutosha katika familia zao.

No comments: