Wednesday, August 31, 2016

BIHARAMULO WALILALAMIKIA SHIRIKA LA UGAVI WA UMEME TANZANIA

Waziri wa nishati na madini, Profesa Sospeter Muhongo.

Na Mwandishi wetu,

Kagera.

BAADHI ya Wateja ambao wamelipia huduma ya kuunganishiwa nishati ya umeme majumbani kwao wilaya ya Biharamulo mkoa wa Kagera, wamelinyoshea kidole Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (TANESCO) wilayani humo kwa kushindwa kutimiza majukumu yake kwa wakati na kuwafanya wateja hao, wapate hasara katika kuendesha shughuli zao za ujasiriamali.

Aidha imeelezwa kuwa wateja hao ambao ni wa maeneo ya mjini wamelilalamikia Shirika hilo wakidai kwamba, tokea walipolipia huduma ya kujengewa mita za umeme mwanzoni mwa mwezi wa sita mwaka huu, hakuna utekelezaji uliofanyika jambo ambalo linawafanya wawe na mashaka.

Wakizungumza na mwandishi wetu kwa nyakati tofauti, walisema kuwa shughuli zao za ujasiriamali ambazo zinategemea nishati hiyo ya umeme wanashindwa kuziendesha, hivyo wanaiomba serikali itatue kero hiyo mapema ili waweze kuondokana na adha kubwa wanayoipata sasa.

Kadhalika wamemuomba Waziri mwenye dhamana, Profesa Sospeter Muhongo kuona umuhimu wa kuingilia kati ili kuweza kumaliza tatizo hilo mapema ambalo hawajui litakwisha lini.

WAHAMIAJI HARAMU WAKAMATWA GUMBIRO SONGEA WAKITOKEA DAR ES SALAAM



Na Mwandishi wetu,           
Songea.

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma, kwa kushirikiana na Maofisa wa idara ya uhamiaji wamefanikiwa kuwatia mbaroni watu watatu ambao ni raia wa nchi ya Ethiopia wakiwa ndani ya basi la Super Feo, wakitokea Jijini Dar es Salaam kuelekea nchi ya Msumbiji kupitia Songea mkoani hapa.

Akizungumza na waandishi wa habari Ofisini kwake, Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Zubery Mwombeji alisema kuwa tukio hilo lilitokea Agosti 23 mwaka huu katika kijiji cha Gumbiro wilaya ya Madaba mkoani humo.

Mwombeji aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Halima Said Bachu (27) mkazi wa Oromo Ethiopia ambaye alikuwa anajishughulisha na shughuli za kibiashara huko Jijini Nairobi nchini Kenya.

TAHARUKI YAIBUKA MADENI YA MIKOPO ELIMU YA JUU NAMTUMBO

Na Mwandishi wetu,         
Namtumbo.

KUFUATIA kutolewa  kwa orodha  ya  majina ya wadaiwa sugu ya mkopo wa elimu ya juu, kumeibuka taharuki kwa baadhi ya watumishi wa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma kuingizwa kwenye orodha  ya wadaiwa hao, licha ya kutosoma elimu ya juu na kutohusika kuomba mkopo huo.

Kwa mujibu wa Ofisa habari wa wilaya hiyo, Yeremias Ngerangera amethibitisha kupokea malalamiko kutoka kwa walimu sita wa shule za msingi wilayani humo ambao wanadai kuwa hawajasoma elimu hiyo ya juu na hawakuomba fedha hizo kutoka bodi ya mikopo.

Aidha Ngerangera aliwataja walimu waliowasilisha malalamiko yao wilayani humo kuwa ni  mwalimu Thomas Komba ambaye anadaiwa shilingi 3,444,030, Joseph Chengura anayedaiwa 12,911,370 na mwalimu Michael Haulle anayedaiwa shilingi 2,733,099 na bodi ya mikopo elimu ya juu.

JESHI LA POLISI RUVUMA LINAWASAKA WALIOHUSIKA NA MAUAJI NYASA

Na Kassian Nyandindi,            
Songea.

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma linawasaka watu wanaodaiwa kuhusika kuwashushia kipigo kikali kwa kuwapiga kwa mapanga, mawe na marungu watu wawili sehemu mbalimbali za miili yao ambao ni wakazi wa kijiji cha Ndumbi na Lituhi, wilaya ya Nyasa mkoani humo na kuwasababishia vifo papo hapo.
Zubery Mwombeji.

Mauaji hayo yalitokana na watu hao wakituhumiwa kwamba ni washirikina ambapo walimpoteza kimazingara, kijana mmoja aliyefahamika kwa jina la Baraka Mahundi (28) katika ziwa Nyasa.

Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, Zubery Mwombeji amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba amewataja waliouawa kuwa ni Jackob Mahundi (90) mkazi wa kijiji cha Ndumbi na Vicent Ngatunga (63) wa kijiji cha Lituhi wilayani humo.

WANANCHI LITAPASWI SONGEA WANYWA TOGWA INAYODAIWA KUWA NA SUMU

Na Mwandishi wetu,          
Songea.

BAADHI ya wananchi wa kijiji cha Lyangweni kata ya Litapwasi wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, wamekumbwa na hali mbaya baada ya kuhofiwa kunywa kinywaji aina ya togwa kinachodaiwa kuwa na sumu.

Wananchi hao ambao ni 66 walikunywa kinywaji hicho wakati walipokuwa kwenye sherehe ya mwananchi mwenzao, ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja.

Habari zilizopatikana mjini hapa ambazo zimethibitishwa na Mganga mkuu wa wilaya hiyo Dkt. Yesaya Mwasubira, alisema kuwa tukio hilo lilitokea juzi majira ya mchana huko katika kijiji cha Lyangweni ambacho kipo umbali wa kilometa tisa kutoka Songea mjini.

Alisema kuwa wanakijiji hao walikuwa wamekwenda kwenye sherehe hiyo, ambako walipatiwa chakula pamoja na kinywaji aina ya togwa iliyotengenezwa kienyeji.

Kadhalika baadhi ya wananchi waliozungumza na mwandishi wetu kwa nyakati tofauti walisema kuwa togwa hiyo, ilikuwa imeandaliwa kwa wingi kwenye sherehe hiyo na kila aliyekunywa baada ya muda mfupi tu, alianza kulalamika kuuma tumbo.

CHADEMA RUVUMA YAPINGA KATAZO LA JESHI LA POLISI YASEMA MAANDALIZI OPARESHENI UKUTA YAMEKAMILIKA KWA ASILIMIA 99

Na Kassian Nyandindi,          
Songea.

CHAMA Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) mkoani Ruvuma kimesema kwamba kinapinga vikali katazo la vikao vya ndani vya chama, lililotolewa na Jeshi la Polisi hapa nchini kupitia kwa Mkuu wa Oparesheni na mafunzo  ya jeshi hilo, CP Nsato Marijani.

Akizungumza na mwandishi wetu jana ofisini kwake Mwenyekiti wa CHADEMA mkoani hapa, Ireneus Ngwatura alisema kuwa tayari maandalizi yao ya Oparesheni UKUTA mkoani hapa yamekamilika kwa asilimia 99.

“Kuhusu katazo hili la vikao vya ndani ambalo limetolewa na Jeshi la Polisi kwamba kuanzia Agosti 24 mwaka huu ni marufuku kufanya vikao vya ndani vya kisiasa kwa vyama vya siasa, jambo hili kwetu halikubaliki kabisa na wala hakuna mwanachama yeyote atakayeridhia katazo hili”, alisema Ngwatura.

Alieleza kuwa nchi haiendeshwi kwa kauli za Jeshi la Polisi bali inaendeshwa kwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na sheria zake mbalimbali, hivyo hakuna sheria yoyote ya Polisi au ya vyama vya siasa inayoruhusu kupiga marufuku vikao vya ndani na mikutano ya hadhara.

Monday, August 29, 2016

KAYA MASKINI SONGEA ZAIPONGEZA TASAF KWA KUBADILISHA MAISHA YAO

Felix Mkuruha mkazi wa mtaa wa Ruhuwiko shuleni Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, akionesha shamba lake alilozalisha vitunguu baada ya kuwezeshwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) mkoani humo.


Na Kassian Nyandindi,        
Songea.

RUZUKU ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF) inayotolewa kwa kaya maskini katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, imeweza kubadilisha maisha kwa baadhi ya kaya hizo na kuweza kuendesha maisha yao bila utegemezi.

Katika ziara ya kutembelea na kukagua kaya maskini ambayo ilihusisha maafisa wa mfuko huo na waandishi wa habari katika kata ya Mjimwema mjini Songea, baadhi ya wananchi waliopata ruzuku hiyo walisema kuwa maisha yao yamebadilika na kwamba hivi sasa, wamekuwa wakiendesha miradi ya aina mbalimbali ambayo imekuwa ikiwaingizia kipato.

Hawa Hassan (60) mkazi wa mtaa wa Kijiweni kata ya Mjimwema alisema kuwa kabla ya kuwezeshwa na TASAF, alikuwa na hali mbaya kimaisha baada ya kuachwa na mumewe kutokana na kuugua maradhi ya miguu lakini hivi sasa anao uwezo wa kumudu gharama za maisha yake.

“TASAF walinipatia ruzuku  ya shilingi 36,000 kila baada ya miezi mitatu nilianzisha biashara ndogondogo ya kuuza mafuta ya kula na nyanya na baadaye nikafanikiwa kuwa na mtaji wa shilingi laki moja, nilinunua kuku wa mayai 74 ambao ni wa kienyeji na sasa naendelea kuwafuga na wananipatia kipato cha kuendeshea maisha yangu”, alisema Hawa.

Hawa alisema pia anaouhakika wa maisha, hata kama serikali itasimamisha ruzuku inayotolewa na Mfuko huo wa maendeleo ya jamii miradi yake itaendelea vizuri na kwamba kuku wake wanataga mayai, ambayo huyauza na kujipatia fedha taslimu za kuendeshea maisha yake.

SHINDANO LA KUMSAKA MREMBO LAWANUFAISHA WAZEE SONGEA

Na Julius Konala,        
Songea.

WAANDAAJI wa shindano la kumsaka mrembo wa Miss Ruvuma mwaka huu, kutoka Rona Promotion ya Jijini Dar es salaam kupitia ufadhili wa Kampuni ya Bayauck ya nchini Japan, wametoa msaada wa nguo mbalimbali kwa baadhi ya wazee wasiojiweza katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 1,000,000.

Msaada huo ulitolewa juzi kwa wazee hao na washiriki wa shindano hilo kupitia shirika la kuhudumia wazee (PADI) lililopo mjini hapa ambapo Mkurugenzi mtendaji wa Kampuni ya Rona promotion Nassib Mahinya, alisema kuwa wameamua kufanya hivyo baada ya kuguswa na changamoto mbalimbali zinazowakabili wazee.

Mahinya alisema kuwa lengo kuu ni kuwafundisha washiriki wa mashindano ya warembo, kujitoa katika kusaidia jamii na makundi mengine yasiyojiweza huku akifafanua kuwa mapato yatakayopatikana siku ya shindano hilo litakalofanyika Agosti 27 mwaka huu, asilimia 10 itaelekezwa kusaidia jamii.

DIWANI ACHANGIA MAENDELEO KATIKA KATA YAKE AWATAKA WAZAZI KUSHIRIKIANA NA WALIMU

Na Julius Konala,      
Songea.

KATIKA kuhakikisha kwamba agizo la serikali linatekelezwa juu ya ujenzi wa vyoo bora vya kisasa katika shule za msingi na sekondari hapa nchini, diwani wa kata ya Msamala Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma Issack Lutengano kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) amechangia kiasi cha shilingi milioni 1,000,000 kwa ajili ya ukamilishaji wa ujenzi wa choo cha walimu, shule ya msingi Msamala iliyopo mjini hapa.

Mchango huo ulikabidhiwa juzi kwa Mwalimu mkuu wa shule hiyo, Mariam Kinyunyu baada ya kutoa ombi hilo kwa diwani huyo ambaye alikuwa mgeni rasmi katika mahafali ya 34 ya shule hiyo, ambapo alisema kuwa katika hatua ya kwanza ya ujenzi wa choo hicho tayari zimetumika shilingi milioni mbili huku makadirio yakiwa ni shilingi milioni tatu mpaka kukamilika kwake.

Akizungumza katika mahafali hayo diwani Issack alisema kuwa atahakikisha anashirikiana na halmashauri hiyo, wazazi na wananchi wa kata hiyo katika kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili shule yake ikiwemo pia ujenzi wa vyumba vya madarasa na matundu ya vyoo.

Sunday, August 28, 2016

RC RUVUMA ASEMA HALI YA USAFI SONGEA SIO YA KURIDHISHA

Na Kassian Nyandindi,          
Songea.

MKUU wa mkoa wa Ruvuma Dkt. Binilith Mahenge amesema kuwa hali ya usafi katika Manispaa ya Songea mkoani humo, sio ya kuridhisha hivyo ameutaka uongozi husika wa Manispaa hiyo kuchukua hatua za haraka kunusuru hali hiyo ili isiweze kuleta madhara, ikiwemo magonjwa ya mlipuko kama vile kipindupindu.

Mji wa Songea.
Dkt. Mahenge amemtaka Mkurugenzi mtendaji Tina Sekambo na Meya wake wa Manispaa hiyo Alhaj Abdul Mshaweji, kutumia sheria ndogo ndogo za mazingira ambazo zitaweza kusimamia suala hilo na kuufanya mji huo kuwa safi.

Dkt. Mahenge alisema hayo juzi kwenye kikao kilichohusisha watumishi wa serikali, taasisi za umma, madiwani, wafanyabiashara na wazee ambacho kilifanyika mjini hapa.

Alisema kuwa utunzaji wa mazingira na masuala ya usafi ni jambo la lazima ambalo kila mwananchi, anapaswa kulitekeleza ili kuweza kuzuia magonjwa ya mlipuko yanayoweza kujitokeza na kuleta madhara katika jamii.

NAMTUMBO KUZALISHA TANI 600 ZA TUMBAKU

Zao la tumbaku.
Na Yeremias Ngerangera,        
Namtumbo.

WAKULIMA wanaozalisha tumbaku katika kata ya Mgombasi wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma, katika msimu wa mwaka 2016/2017 wanatarajia kuzalisha tani 600 za zao hilo wilayani humo.

Hayo yalisemwa na diwani wa kata ya Mgombasi wilayani hapa, Mrisho Mbawala mbele ya Ofisa kilimo wa wilaya hiyo, Ally Lugendo wakati wa ziara ya kuhamasisha wakulima hao wazalishe tumbaku kwa wingi kwa kuzingatia mbinu za kilimo bora cha kisasa.

Mbawala alifafanua kuwa wataweza kuzalisha kiasi hicho katika msimu huo kutokana na uliopita, walikuwa wakizalisha tani 60 tu kufuatia wakulima wengi kukata tamaa juu ya uzalishaji huo.

Aidha alieleza kuwa sababu kuu ya ongezeko hilo linatokana na wakulima wengi kuhamasika kulima tumbaku, ambapo katika kipindi cha mwaka 2015/2016 kulikuwa na wakulima 150 na sasa wamefikia wakulima 400.

MKURUGENZI MADABA AFUNGA CHUO FEKI CHA UUGUZI

Na Kassian Nyandindi,      
Songea.

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma Shafii Mpenda amelazimika kukifunga chuo cha Noble College Tanzania Limited (NCTL) ambacho kilikuwa kinatoa mafunzo ya uuguzi baada ya kubaini kwamba chuo hicho, hakijasajiliwa kisheria na miundo mbinu yake sio rafiki kwa wanafunzi wanaosomea taaluma hiyo.

Shafii Mpenda.
Mpenda alisema kuwa amefikia uamuzi huo baada ya kujiridhisha kuwa katika halmashauri yake hakuna mtu yeyote ambaye amewahi kupeleka maombi kwa ajili ya uendeshaji wa mafunzo ya uuguzi, jambo ambalo limesababisha kuwepo kwa malalamiko ya muda mrefu kutoka kwa wananchi kwamba chuo hakina usajili unaotambuliwa na serikali.

Alifafanua kuwa kuanzia sasa NCTL hakitaruhusiwa kutoa mafunzo ya uuguzi na amewataka wanafunzi wamtafute mkuu wa chuo hicho, ili aweze kuwarejesha majumbani kwao kwani kuna baadhi ya wanafunzi wanatoka mikoa ya Kigoma, Shinyanga, Iringa, Njombe, Rukwa na Tabora hapa nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa chuo hicho Kelvin Sikamanga, alipohojiwa na mwandishi wa habari hizi kuhusiana na kufungwa kwa chuo chake alithibitisha kuwa Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya hiyo, Mpenda amekifunga chuo chake kwa madai kwamba hakina sifa na hakijasajiliwa, lakini amefafanua kuwa chuo hicho alikwisha kisajili chini ya mwamvuli wa chama cha msalaba mwekundu.

MTOTO AJINYONGA CHUMBANI KWAKE BAADA YA KUCHOSHWA NA KAULI MBAYA ZA MAMA YAKE MZAZI

Na Kassian Nyandindi,      
Songea.

MTOTO Zawadi Hassan (14) mkazi  wa kitongoji cha Majengo kijiji cha Mkongo wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma, amejinyonga kwa kutumia chandarua chake wakati akiwa chumbani kwake baada ya kuchoshwa  na kauli zisizokuwa na staha kutoka kwa  mama yake mzazi ambaye hakufahamika jina lake mara moja.

Tukio hilo limetokea  mwishoni mwa wiki ambapo mwili wa marehemu huyo ulikutwa chumbani kwake asubuhi siku ya Ijumaa, baada ya mama huyo kumtaka aamke na ndipo jitihada za kumwita mlangoni ziligonga mwamba ambapo alipochukua jukumu la kufungua mlango, aliukuta mwili wa mwanae ukiwa juu unaning’inia.

Mtendaji wa kata ya Mkongo, Whiclif Mtinda alikwenda katika eneo la tukio na kuthibitisha kifo cha kijana huyo kilichosababishwa na kujinyonga kwa kutumia chandarua kutokana na  kauli za kuudhi kutoka  kwa mama yake  mzazi.

Thursday, August 25, 2016

MANYANYA: SERIKALI ITAENDELEA KUSHIRIKIANA NA MADHEHEBU YA DINI AITAKA JAMII KUONA UMUHIMU WA KUPELEKA WATOTO SHULE

Na Kassian Nyandindi,              
Mbinga.

NAIBU Waziri wa Elimu, Sayansi na Tekinolojia Injinia Stella Manyanya amesema kwamba serikali hapa nchini, itaendelea kushirikiana na madhehebu yote ya dini katika kuhakikisha kwamba amani na utulivu ni jambo ambalo, linapaswa kuwepo wakati wote kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.

Aidha ameitaka jamii kuona umuhimu wa kupeleka watoto wao shule, ili waweze kusonga mbele kimaendeleo na kulifanya taifa liweze kuondokana na tabaka la watu maskini.

Injinia Stella Manyanya.
Vilevile alisisitiza kwamba, serikali haitasita kuwachukulia hatua wazazi ambao wataonekana wanakwamisha jitihada za maendeleo ya mtoto shuleni ikiwemo kufikishwa kwenye vyombo vya kisheria kama vile mahakamani.

Injinia Manyanya alisema hayo leo alipokuwa mgeni rasmi, wakati akizungumza kwenye maadhimisho ya Jubilei ya kutimiza miaka 25 ya Upadri jimbo la Mbinga, yaliyofanyika katika Kanisa la Mtakatifu Killian lililopo mjini hapa.

Maadhimisho hayo yalihusisha mapadri 11 wa kutoka Parokia mbalimbali zilizopo jimboni humo, tangu walipopata upadirisho wao Septemba 13 mwaka 1991 katika utumishi wao wa kuwatumikia wakristo wenzao.

Mapadri hao ni Philibert Mbunda, Alfredy Komba, Aidan Nchimbi, Mendrad Nyandindi, Thadei Kinyero, Christopher Mapunda, Amon Nchimbi, Addo Mapunda, Thimoth Ndunguru, Joackimu Lipanga na Bosco Ndiu.

DC MBINGA ASISITIZA UJENZI WA VYOO SHULE ZA MSINGI NA SEKONDARI

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Robert Mageni akizungumza juzi katika kikao cha baraza la madiwani wa mji huo kilichofanyika kwenye ukumbi wa jumba la maendeleo mjini hapa, katikati ni Mwenyekiti wa halmashuri hiyo Kipwele Ndunguru na wa mwisho kushoto ni Makamu wake Mwenyekiti Tasilo Ndunguru.
Na Kassian Nyandindi,          
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Cosmas Nshenye amewataka watendaji waliopo katika halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani humo kuhakikisha kwamba wanatekeleza kwa haraka zoezi la ujenzi wa vyoo bora mashuleni, ili wanafunzi waweze kuepukana na magonjwa ya mlipuko kama vile kipindupindu.

Zoezi hilo la ujenzi wa vyoo hivyo alisema kuwa anataka lianze mara moja kuanzia sasa, kwa shule za msingi na sekondari ambazo kuna tatizo la upungufu wa vyoo ili kuweza kuepukana na watoto kujisaidia vichakani.

Agizo hilo la Mkuu huyo wa wilaya lilitolewa juzi kwenye kikao cha baraza la madiwani wa halmashauri ya mji huo, kilichofanyika mjini hapa katika ukumbi wa Jumba la maendeleo.

WANANCHI MBINGA WAFURAHIA UPIMAJI ARDHI

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Gombo Samandito akizungumza juzi na wakazi wa kata ya Maguu wilayani humo wakati wa zoezi la uhamasishaji wananchi kwa ajili ya kazi ya kupima ardhi itakayofanywa na wataalamu wa idara ya ardhi katika vijiji, kata na miji midogo yote iliyopo wilayani hapa.
Na Kassian Nyandindi,          
Mbinga.

HATIMAYE zoezi la uhamasishaji upimaji ardhi ya wananchi katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, limepokelewa kwa mikono miwili katika vijiji, kata na miji midogo iliyopo wilayani humo ambapo wakazi waliopo katika maeneo husika kwa nyakati tofauti wamefurahia mpango huo na kuutaka uongozi wa wilaya hiyo kuanza mara moja kazi ya upimaji wa ardhi yao, ili waweze kunufaika nayo katika kusukuma mbele maendeleo yao.

Mafanikio hayo yametokana na elimu iliyokuwa ikitolewa na timu ya wataalamu ambayo iliundwa na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Gombo Samandito ambapo ilikuwa ikipita katika kila kijiji, kata na miji midogo iliyopo wilayani humo kuhamasisha juu ya umuhimu wa upimaji ardhi kisheria na kuwafanya wakazi waliopo katika maeneo husika wasiweze kujenga kiholela.

Zoezi hilo la uhamasishaji limetekelezwa kwa siku saba, ambapo lilianza rasmi Agosti 15 mpaka 21 mwaka huu likiongozwa na Mkurugenzi huyo, ambapo  imeelezwa kuwa hatua hiyo itasaidia wananchi kumiliki ardhi yao kisheria sambamba na kupewa hati ambazo watazitumia kwa ajili ya  shughuli mbalimbali za kiuchumi, kwa kupata mikopo kutoka taasisi za kifedha kama vile benki.

Jumla ya vijiji 118, kata 29 pamoja na miji minne ya Ruanda, Matiri, Kigonsera na Maguu ndiyo ambayo inatarajiwa kupimwa wilayani Mbinga ili wananchi hao waweze kunufaika na kwamba upimaji huo unatarajiwa kuanza kufanyika wakati wowote kuanzia sasa, kufuatia zoezi hilo la utoaji elimu kwa wananchi kukamilika taratibu zake.

Monday, August 22, 2016

MADIWANI WALALAMIKIA WIZI WA MADAWA HOSPITALI HALMASHAURI MJI WA MBINGA

Dkt. Robert Elisha Mganga Mkuu hospitali ya Halmashauri mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,             
Mbinga.

HALI ya upatikanaji wa madawa kwa ajili ya kutibu wagonjwa katika hospitali ya Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, imeelezwa kuwa ni tatizo sugu ambalo linaendelea kuitesa jamii hivyo serikali imeombwa kuingilia kati kutatua tatizo hilo ili wagonjwa wanaopata huduma katika hospitali hiyo waweze kuondokana na kero hiyo.

Kadhalika imefafanuliwa kwamba upungufu huo wa madawa unatokana na baadhi ya watumishi wa idara ya afya kutokuwa waaminifu, ambapo inadaiwa kuwa dawa hizo wamekuwa wakiiba na kuziuza kupitia maduka yao ya dawa muhimu yaliyopo mjini na vijijini huku wagonjwa wakilazimika kwenda kununua kwenye maduka hayo.

Hayo yalisemwa katika kikao cha baraza la madiwani wa halmashauri ya mji huo kilichofanyika juzi mjini hapa ambapo licha ya kuwepo kwa changamoto hiyo, madiwani hao pia walilalamikia baadhi ya wauguzi kuwatolea lugha mbaya wagonjwa ambao wanakwenda hospitalini hapo kupatiwa matibabu.

ASHIKILIWA NA POLISI KWA KUMILIKI SILAHA KINYUME CHA SHERIA

Na Kassian Nyandindi,          
Songea.

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma, linamshikilia Filbert Moyo (40) mkazi wa kijiji cha Tingi wilaya ya Nyasa mkoani humo kwa kukutwa na silaha mbili aina ya Gobole ambazo zimetengenezwa kienyeji.

Aidha Jeshi hilo linamsaka mtu mwingine ambaye jina lake halikuweza kufahamika mara moja, ambaye ni mkazi wa kijiji cha Malumba wilayani Tunduru mkoani hapa kwa kukutwa na silaha aina ya SMG ikiwa na risasi 23.

Zubery Mwombeji, Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake, Kaimu kamanda wa Polisi wa mkoa wa Ruvuma, Dismas Kisusi alisema kuwa tukio la kwanza lilitokea Agosti 13 mwaka huu majira ya saa 11:30 asubuhi huko katika wilaya ya Nyasa ambako askari Polisi walifanikiwa kumkamata mtuhumiwa huyo akiwa na silaha hizo.

Kisusi alisema kuwa silaha hizo alikuwa amezihifadhi kwenye mfuko katika eneo la Ngurumashamba kwenye hifadhi ya wanyama ya Liparamba iliyopo wilayani humo.

MADIWANI SONGEA WAPEWA ONYO KALI

Na Kassian Nyandindi,             
Songea.

MKUU wa wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, Palolet Mgema ameonya vikali dhidi ya kikundi cha baadhi ya Madiwani wa Manispaa ya Songea mkoani humo ambao walitaka kuleta fujo wakati wa kikao cha baraza la madiwani kilichoketi juzi mjini hapa, ambapo amesema kwamba endapo kama watarudia tena atawachukulia hatua za kisheria.

Aidha Mgema alisema kuwa kamwe hataweza kuvumilia kuanzia sasa kuona tabia hiyo inajirudia tena na kwamba, akijitokeza mtu yeyote na kusababisha kuleta vurugu zinazoashiria uvunjifu wa amani atakiona cha mtemakuni.

Mgema alisema hayo kwenye kikao cha baraza la madiwani kilichofanyika katika ukumbi wa Manispaa mjini Songea, kufuatia kutokea kwa mvutano mkali kati ya baadhi ya kikundi cha madiwani wachache wa Chama Cha Mapinduzi (CCM)  na Meya wa halmashauri hiyo, Abdul Mshaweji kuhusiana na hoja ya mabasi ya kupakia abiria kuanzia stendi kuu ya zamani iliyopo mjini hapa kwenda Msamala iliyopo mbali na mji huo.

Hali hiyo ilizua tafrani ndani ya kikao hicho na kuwafanya baadhi ya wananchi waliohudhuria kuwazomea madiwani ambao walikuwa wakipindisha hoja hiyo kwa nguvu na kuwaunga mkono, Meya Mshaweji pamoja na Mbunge wa Songea mjini Leonidas Gama ambao walionyesha wazi kuwasaidia wananchi kutatua kero hiyo ya muda mrefu ya ombi lao la mabasi kuanzia stendi hiyo ya zamani.

Sunday, August 21, 2016

CHIKAMBO AWATAKA WANAWAKE RUVUMA KUMPATIA USHIRIKIANO



Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

MBUNGE wa Viti maalum mkoani Ruvuma, Sikudhan Chikambo amezitaka Halmashauri za wilaya mkoani humo kutekeleza jukumu la kupeleka asilimia 10 ya fedha za mapato yake ya ndani katika vikundi vya ujasiriamali, kwa wanawake na vijana.

Aidha amewaagiza madiwani wa mkoa huo, kuhakikisha kwamba suala hilo wanalifuatilia kwa karibu ndani ya halmashauri zao kupitia vikao husika, ili fedha hizo zielekezwe kwa kundi hilo.

Chikambo alitoa agizo hilo juzi, alipokuwa akizungumza na akina mama wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) wilaya ya Mbinga, katika kikao cha baraza la wanawake kilichofanyika kwenye ukumbi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) mjini hapa.

Mbunge huyo alisema kuwa wanawake wanaweza kujituma kwa kila jambo la kimaendeleo, hivyo wanapaswa wakati wote kutetea haki zao pale wanapoona zinaporwa na watu wasiopenda maendeleo yao.

Saturday, August 20, 2016

NJOWOKA: WANACCM TUACHE KUTENGENEZA MAJUNGU

Kamanda wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma, Cassian Njowoka akikabidhi msaada wa mashine ya Fotokopi kwa Mwenyekiti wa CCM wa wilaya hiyo, Francis Homanga ambapo mashine hiyo aliikabidhi kwa ajili ya matumizi mbalimbali ya chama hicho wilayani humo.

Cassian Njowoka akikabidhi msaada wa Kompyuta kwa Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Nyasa, Francis Homanga kwa ajili ya matumizi ya chama hicho wilayani humo.


Na Kassian Nyandindi,       
Nyasa.

VIONGOZI na Wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma, wametakiwa kuacha kutengeneza majungu na mifarakano ndani ya chama hicho na kwamba endapo wataendekeza mambo hayo, huenda wakasababisha malumbano na kukigawa chama.

Cassian Njowoka.
Aidha viongozi wa CCM wameshauriwa kutembelea wananchi wao katika maeneo yao mara kwa mara, ili kukifanya chama kiweze kuwa endelevu katika kupigania haki na maendeleo husika katika jamii.

Hayo yalisemwa na Cassian Njowoka ambaye ni Kamanda wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) wilayani Nyasa, alipokuwa akizungumza na wananchi wa kata ya Kingirikiti wilayani humo katika hafla fupi ya kukabidhi msaada wa vifaa vya chama hicho.

WATENDAJI MBINGA WATAKIWA KUKUSANYA MAPATO IPASAVYO

Aliyesimama ni Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Gombo Samandito akisisitiza jambo katika kikao cha baraza la Madiwani wilayani humo ambacho kilifanyika hivi karibuni.
Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

WATENDAJI wa vijiji na kata katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wametakiwa kukusanya mapato ya halmashauri hiyo kwa kuhakikisha kwamba wanadhibiti mianya inayoweza kupoteza mapato hayo, ili fedha zitakazopatikana ziweze kwenda kufanya kazi za maendeleo ya wananchi.

Vilevile wameagizwa kuendelea kuimarisha mfumo wa ukusanyaji mapato hayo kwa kutumia mfumo wa mashine maalumu za kieletroniki (EFD’S) ili kuweza kudhibiti wizi unaoweza kutokea kwa wale watendaji wasiokuwa waaminifu ambao wamekuwa na mazoea ya kuiibia serikali.

Gombo Samandito ambaye ni Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, alisema hayo juzi alipokuwa akitoa maelekezo mbalimbali ya kikazi kwa watendaji hao katika kikao cha baraza la madiwani kilichofanyika mjini hapa.

Tuesday, August 16, 2016

NJOWOKA ATOA MSAADA WA TAIRI NNE ZA GARI KWA KITUO KIKUU CHA POLISI NYASA

Kutoka upande wa kulia ni Mkuu wa Polisi wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma, Shaban Mpwaga akipokea msaada wa tairi nne za gari la kituo kikuu cha Polisi wilayani humo kutoka kwa Kamanda wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) wa wilaya hiyo, Cassian Njowoka.

Kutoka kushoto Mkuu wa Polisi wilaya ya Nyasa, Shaban Mpwaga akipokea msaada wa mashine ya Printer kutoka kwa Kamanda wa Umoja wa Vijana Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) wilayani humo, Cassian Njowoka. Mashine hiyo ilipokelewa kwa ajili ya matumizi ya kituo kikuu cha Polisi wilaya ya Nyasa. (Picha zote na Gwiji la Matukio Ruvuma)
Na Kassian Nyandindi,        

Nyasa.

MKUU wa Polisi wilaya ya Nyasa mkoani Ruvuma, Shaban Mpwaga amemshukuru na kumpongeza Kamanda wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) wa wilaya hiyo, Cassian Njowoka kwa kutoa msaada wa tairi nne za gari la kituo kikuu cha Polisi wilayani humo zenye thamani ya shilingi milioni 4.4.

Aidha alisema kuwa gari la kituo hicho ambalo tairi zake zimekuwa kipara, wakati mwingine askari wake wanashindwa kutekeleza majukumu yao kikazi kutokana na tairi zilizopo kwisha muda wake wa matumizi.

Shukrani hizo zilitolewa jana na Mkuu huyo wa Polisi wilaya ya Nyasa kwenye hafla fupi ya makabidhiano ya msaada huo, iliyofanyika katika viwanja vya kata ya Kingirikiti wilayani hapa.

Mpwaga alifafanua kuwa licha ya kupewa msaada huo pia Njowoka siku za nyuma aliwahi kuwapatia msaada wa kompyuta, printa mbili za kisasa na karatasi rimu katoni mbili kwa ajili ya kuweza kusaidia kufanyia kazi za Polisi kama vile kuchapa barua za aina mbalimbali.

EPZA YALALAMIKIWA KUTOWALIPA FIDIA WANANCHI MWENGEMSHINDO SONGEA

Rais Dkt. John Magufuli.


Na Julius Konala,           
Songea.

BAADHI ya wananchi wa kata ya Mwengemshindo Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma ambao maeneo yao yametwaliwa na shirika la EPZA kwa kipindi cha miaka tisa iliyopita bila kuwalipa fidia yoyote, wamemuomba Waziri wa viwanda na biashara, Charles Mwijage kuingilia kati suala hilo ili waweze kupata haki yao ya msingi.

Ombi hilo lilitolewa juzi na wananchi hao mbele ya Mbunge wa jimbo la Songea mjini Leonidas Gama, katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa michezo wa kata hiyo na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa siasa na serikali.

Walisema kuwa tangu maeneo yao yachukuliwe wamekuwa wakiishi katika maisha magumu kutokana na kuzuiwa kuendesha shughuli yoyote ile, ikiwemo kilimo cha mazao ya chakula na biashara ili waweze kujipatia kipato katika maisha yao ya kila siku.

TUNDURU WALIA NA TEMBO WANAOVURUGA MAZAO YAO KAYA 2,000 ZIPO HATARINI KUKUMBWA NA NJAA

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge.


Na Steven Augustino,      
Tunduru.

ZAIDI ya kaya 2,000 zinazoishi katika vijiji vilivyopo kata ya Kalulu na Mbungulaji wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wapo hatarini kukumbwa na baa la njaa kutokana na mazao yao waliyolima shambani kushambuliwa na kuvurugwa na kundi la tembo waliojitokeza kutoka hifadhi ya taifa ya Selous.

Taarifa ya tukio hilo ilitolewa na Salum Bakari, Alli Amani na Abdalla Kindimba ambao ni wakazi wa maeneo hayo ambapo walimweleza hayo Mkuu wa wilaya hiyo, Juma Homera alipowatembelea kwenda kujionea juu ya uharibifu huo uliofanyika.

Wananchi hao waliendelea kusema kuwa hivi sasa wanaishi kwa hofu baada ya mazao yao ya mpunga, mahindi, migomba ya ndizi, maharage, ufuta, mihogo na vitunguu kushambuliwa na wanyama hao na kuwafanya waishi katika mazingira magumu.

DC MBINGA APANIA KUWASAKA WAFANYABIASHARA WAJANJA WANAOTOROSHA KAHAWA



Na Kassian Nyandindi,            
Mbinga.

SERIKALI wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma imesema kwamba, imeanza kuchukua hatua kali za kuwasaka wafanyabiashara wajanja ambao wamekuwa wakinunua na kutorosha zao la kahawa wilayani humo nyakati za usiku, kwa njia za panya kuelekea mkoani Mbeya bila kibali maalumu.

Aidha imeelezwa kuwa vitendo hivyo vimekuwa vikishamiri hasa kipindi hiki cha kiangazi, pale msimu wa mavuno ya zao hilo unapofanyika ambapo wafanyabiashara hao hupita vijijini kwa wakulima na kuwarubuni kununua zao hilo kwa njia zisizo halali.

Mkuu wa wilaya Mbinga, Cosmas Nshenye alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza kwenye mkutano wa baraza la madiwani la halmashauri ya wilaya hiyo, liloketi katika ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa.

LONGA WAKULIMA WALALAMIKIA KUIBIWA KAHAWA YAO



Na Kassian Nyandindi,         
Mbinga.

WANANCHI wa kijiji cha Longa kata ya Mkumbi wilaya ya Mbinga mkoa wa Ruvuma, wamelalamikia kitendo cha wizi wa kahawa zaidi ya magunia 100 ambao umefanyika kijijini humo na watu wasiojulikana.

Hali hiyo imeelezwa kwamba, kahawa iliyoibwa ni ile ambayo ilianikwa kwenye vichanja nje ya ghala la kuhifadhia kahawa tayari kwa kusafirishwa kwenda Kiwanda cha kukoboa kahawa Mbinga (MCCCO) kilichopo mjini hapa.

Kufuatia tukio hilo walinzi wawili ambao walikuwa wakilinda katika eneo la ghala la kuhifadhia kahawa hiyo, wanashikiliwa na mgambo katika mahabusu ya kata hiyo wakidaiwa kuiba kahawa ambayo ilianikwa kwenye vichanja hivyo.

Sunday, August 14, 2016

TAARIFA YA UMOJA WA VIJANA WA CCM KWA VYOMBO VYA HABARI KUFUATIA UCHUNGUZI NA MAAZIMIO YALIYOTOLEWA NA KIKAO CHA BARAZA KUU LA UVCCM TAIFA MJINI DODOMA




 VMMU.80Vol.1/46                             14/08/2016

Karibuni sana katika mkutano wetu muhimu tunaofanya leo tukiwa hapa Dodoma mara baada ya kumalizika kwa kikao cha juu cha Jumuiya yetu yaani Baraza Kuu la Umoja wa Vijana wa CCM Taifa.

Tarehe 10 Agost mwaka huu kilianza kikao cha Sekretarieti ya Baraza Kuu la UVCCM Taifa kikafuatia kikao cha  Kamati ya Maadili, kufuatia kikao cha Kamati ya Utekelezaji ya Baraza Kuu la UVCCM Taifa na baadaye Baraza Kuu la UVCCM Taifa. Jumla ya Agenda tisa (9) zilijadiliwa.

Baraza Kuu limeridhika na taarifa kadhaa kuhusiana na agenda mbali mbali na kupokea taarifa moja nyeti na muhimu kwa Jumuiya. “Ripoti ya uchunguzi wa Shamba la UVCCM Na. 454 MBYLR lenye ekari 210” lililopo Igumbilo Wilaya ya Iringa mjini Mkoani Iringa ambalo limeuzwa kwa Ndugu Suhail Ismail Thakore kinyume na taratibu pia viwanja hivyo kuuzwa kwa watu mbalimbali na kuwahusisha Viongozi kadhaa wenye dhamana ndani ya Jumuiya yetu.

Baada ya kupata taarifa za uuzaji wa shamba hilo Mali ya UVCCM, kwa Mamlaka iliyonayo Kamati ya Utekelezaji Taifa Ibara 91 (d), ilimwachia Mamlaka Mwenyekiti wa UVCCM Taifa kuunda na kuteua wajumbe watatu wa Kamati ya Utekelezaji ya Baraza Kuu la UVCCM Taifa kuenda kufanya uchunguzi wa kadhia hiyo.

Nichukue nafasi hii kuishukuru kwa dhati Kamati ya uchunguzi iliyoongozwa na;

Ndugu Mariam Chaurembo    -    Mwenyekiti
Ndg Juma Homela  - Katibu
Ndg Amir Mkalipa    Mjumbe
Ndugu Ally Nassor  Mjumbe

Kwa kufanikisha kazi waliyopewa na Jumuiya na hatimaye kuwasilisha ripoti yao ambayo ilibaini mambo kadhaa machafu kinyume na miongozo ya Chama na Jumuiya yetu.

Kikao cha Kamati ya Utekelezaji Mkoa wa Iringa kilichoketi Februari 27, 2015 kilipitisha agenda Namba saba kuhusu shamba la Igumbilo na kukubaliana kuuza ekari 20 hadi 30 kwa Shs. 3,000,000/= kwa eka moja, fedha zitakazopatikana zitumike katika Matumizi mbali mbali kwa ajili ya shamba hilo.

Machi 2, 2015 UVCCM Mkoa wa Iringa ilipokea barua toka kwa Ndugu Suhail Ismail Thakore kuomba kununua shamba hilo ekari 30 eneo la Igumbilo kwa bei ya Shs. 3,000,000/= kwa eka ambapo ni sawa na Shs. 90,000,000/=. Machi 4, 2015 Mkataba kati ya UVCCM Mkoa wa Iringa na mnunuzi ulisainiwa rasmi.

Mnamo April 13,17 na 24 Ndugu Suhail aliweka kiasi cha Shs. 90,000,000/= katika Akaunti ya UVCCM  Mkoa wa Iringa Tawi la CRDB.

Shamba la UVCCM Igumbilo ambalo lilikuwa na ekari 210, ekari 85 zilipimwa na kubaki ekari 125. Ekari 85 zilitoa viwanja 170 kwa ukubwa tofauti ambapo ukubwa wa chini sqm 319 na ukubwa wa juu sqm 32,007 ambapo katika viwanja 170 viwanja 25 vikawa miliki ya Ndugu Suhail ambavyo vimetokana na ekari 30 kufuatia mauziano ya sehemu ya shamba hilo kabla ya kupimwa.

Februari 27, 2015, Kamati ya Utekelezaji Mkoa wa Iringa iliketi na kupitisha ili ipatikane fedha kwa taratibu za upimaji na kuomba Hati iliyopo irejeshwe kwa ajili ya kuwasilishwa Halmashauri ya Mji wa Iringa.

Aidha Machi 9 mwaka 2015 UVCCM Mkoa wa Iringa iliandika barua kwenda Makao Makuu ya Umoja wa Vijana wa CCM kuomba kupatiwa Hati ya UVCCM ya umiliki wa shamba la Igumbilo kutoka Makao Makuu ambapo April mwaka 2015 aliyekuwa Katibu Mkuu Ndugu Sixtus Raphael Mapunda aliandika barua kwa Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini na kuipeleka nakala Ofisi ya Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi ili kuikabidhi Hati ya Shamba la Igumbilo.

Machi 29 mwaka 2015 “Special; Resolution Letter” ilisainiwa kati ya Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini Dk. Emmanuel Nchimbi na aliyekuwa Katibu Mkuu wa UVCCM Ndugu Sixtus Mapunda ili kuonesha “deed of surrender of right of occupancy”.

CHAMA CHA WALIMU MKOA WA RUVUMA CHAMPONGEZA RAIS DOKTA MAGUFULI



Na Muhidin Amri,
Songea.

CHAMA Cha Walimu Tanzania (CWT) mkoani Ruvuma, kimepongeza juhudi kubwa zinazofanywa na serikali ya wamu ya tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli kwa kukusanya kodi, kupambana na vitendo vya wizi, ufisadi na uzembe mahali pa kazi.

Aidha chama hicho kinaamini kwamba, hatua hiyo itasaidia kupatikana kwa fedha ambazo zitalipa madeni mbalimbali wanayoidai walimu serikali, ambapo kipindi cha nyuma ulipaji wake ulikuwa ukisuasua na kuwavunja moyo watumishi hao waliopo katika sekta ya elimu.
 
Hayo yalisemwa jana na Katibu wa CWT mkoani hapa, Shaibu Mohamed alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu ofisini kwake mjini Songea.

Mohamed alisema kuwa licha ya serikali kuanza kuchukua hatua dhidi ya watumishi wasiofaa ambao kwa muda mrefu wameliingizia taifa hili hasara kubwa, bado kuna umuhimu wa kuendelea na msako huo hata kwa watumishi wa ngazi ya juu ambao baadhi yao wanatumia vyeti na majina bandia kujipatia ajira katika idara na taasisi za umma.

WAUGUZI MBINGA WATISHIA KUISHITAKI MAHAKAMANI KURUGENZI SACCOS

Upande wa kulia ni Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini mkoani Ruvuma, Sixtus Mapunda akipeana mkono kwa lengo la kuagana na mganga mkuu wa hospitali ya halmashauri ya mji wa Mbinga, Elisha Robert mara baada ya kumaliza kuzungumza na wauguzi wa hospitali hiyo.


Na Kassian Nyandindi,          
Mbinga.

WAUGUZI wa idara ya afya, hospitali ya Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma wameulalamikia uongozi wa Chama cha akiba na mikopo, Kurugenzi SACCOS kilichopo mjini hapa kwa kushindwa kuwalipa madai yao ya fedha kwa miaka mingi huku wakieleza kuwa, watakwenda kuushtaki uongozi husika Mahakamani ili waweze kupata fedha zao.

Aidha walisema kuwa madai wanayodai ni yale ambayo yanatokana na makato mbalimbali wanayokatwa katika mishahara yao, hivyo hawaoni sababu ya kuendelea kuwa wanachama katika SACCOS hiyo kutokana na manyanyaso wanayoyapata.

Hayo yalisemwa na Wauguzi hao walipokuwa wakizungumza na Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini, Sixtus Mapunda katika kikao maalum kilichoketi jana katika jengo la hospitali hiyo mjini hapa.

Wednesday, August 10, 2016

WATUMISHI IDARA YA AFYA MBINGA WAITAKA SERIKALI KUWALIPA MADAI YAO


Sixtus Mapunda, Mbunge wa jimbo la Mbinga mjini akisisitiza jambo katika kikao alichoketi jana wakati akizungumza na watumishi wa idara ya afya katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.


Na Kassian Nyandindi,         
Mbinga.

WATUMISHI wa idara ya afya hospitali ya Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, wameutaka uongozi wa halmashauri hiyo kuwalipa madai yao ya aina mbalimbali ili waweze kutatua matatizo yao yanayowakabili katika maisha yao ya kila siku.

Watumishi hao wakichangia hoja mbalimbali.
Madai hayo walifafanua kuwa ni malimbikizo ya fedha za likizo, matibabu na safari ambapo hawajalipwa kwa muda mrefu sasa na hawajui hatima yake kwa kile walichoeleza kuwa wamekuwa wakifuatilia mara kwa mara, kwa uongozi husika na hakuna dalili zinazoonesha kuzaa matunda.

Hayo yalisemwa jana na watumishi hao walipokuwa wakizungumza na Mbunge wa jimbo la Mbinga mjini, Sixtus Mapunda ambaye aliwatembelea hospitalini hapo kwa lengo la kusikiliza na kupokea kero zao za aina mbalimbali ili ziweze kufanyiwa kazi.

Raymond Ngatunga ambaye naye ni muuguzi wa hospitali hiyo alieleza kuwa yeye na watumishi wenzake wamekuwa wakidai madai hayo kwa muda mrefu, hivyo kuna kila sababu kwa serikali kuona umuhimu wa kutekeleza jambo hilo mapema ili waweze kuondokana na mazingira magumu katika kusukuma mbele maisha yao.

LUMEME NYASA WALIA NA NAIBU WAZIRI WA ELIMU TEKINOLOJIA NA MAFUNZO YA UFUNDI WAMTAKA KUTEKELEZA AHADI ZAKE



Na Kassian Nyandindi,            
Nyasa.

WANANCHI wanaoishi katika kijiji cha Lumeme kata ya Lumeme wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma wamemtaka Naibu Waziri wa Elimu Tekinolojia na Mafunzo ya Ufundi, Injinia Stella Manyanya kutatua kero mbalimbali za wananchi wake katika sekta ya elimu wilayani humo, ili waweze kusonga mbele kimaendeleo.

Injinia Stella Manyanya.
Aidha Waziri huyo ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Nyasa, walisema hivi karibuni alitoa ahadi ya vifaa vya kiwandani kwa ajili ya ujenzi wa choo cha matundu manne kwa wanafunzi shule ya msingi Mbanga, iliyopo katika kata hiyo lakini ni muda mrefu umepita hakuna utekelezaji alioufanya mpaka sasa.

Walifafanua kuwa choo kilichopo sasa katika shule hiyo kimebomoka na kwamba wanafunzi wanapata shida pale wanapohitaji kujisaidia, ambapo hulazimika kutumia vyoo vya walimu au wakati mwingine huenda kujisaidia katika pori lililokuwa karibu na shule hiyo.