Sunday, September 25, 2016

DC SONGEA AWAKALIA KOONI WASIOFANYA USAFI

Na Kassian Nyandindi,        
Songea.

AGIZO limetolewa kwa Watendaji wote wa Halmashauri za wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, kuhakikisha kwamba wanawapiga faini wananchi ambao wataonekana kutotii amri ya kufanya usafi kila Jumamosi ya mwisho wa mwezi ili iweze kuwa fundisho kwa wengine na kuleta mabadiliko chanya, kwa jamii kujenga tabia ya kufanya usafi katika maeneo yao.

Mkuu wa wilaya ya Songea, Palolet Mgema alitoa agizo hilo juzi wakati alipokuwa akizungumza na wakazi wa mtaa wa Miembeni kata ya Bombambili mjini hapa, ambako shughuli za usafi wa mazingira kiwilaya zilikuwa zikifanyika na kuongozwa naye.

Kwa ujumla wilaya hiyo inaundwa na halmashauri tatu ambazo ni Manispaa ya Songea, halmashauri ya wilaya ya Songea na ile ya Madaba.

Mgema alisema kuwa watu wote ambao hawataki kufanya usafi wa mazingira kuanzia sasa watozwe faini ya shilingi 50,000 na kwamba anataka ripoti ya watu hao pale wanapotozwa ifikishwe ofisini kwake haraka, ili aweze kutambua ni nani wenye tabia ya kugoma kufanya usafi ili waweze kuchukuliwa hatua zaidi.

WATUMISHI WA SERIKALI RUVUMA WENYE KUFANYA KAZI KWA MAZOEA KUKIONA CHAMTEMAKUNI

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge akisisitiza jambo katika sehemu ya vikao vyake vya kikazi na chama mkoani hapa.
Na Julius Konala,       
Songea.

WATUMISHI wa Serikali waliopo katika sekta mbalimbali mkoani Ruvuma, wametakiwa kujiepusha na vitendo vya utoaji huduma kwa wananchi kwa mtindo wa upendeleo au kujenga tabia ya kuendekeza vitendo vya rushwa, itikadi za dini na ukabila.

Aidha kwa mtumishi yeyote atakayebainika kufanya hivyo atachukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kufukuzwa kazi, ili iweze kuwa fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge alisema hayo juzi alipokuwa akizindua Baraza la Wafanyakazi la watumishi kutoka Ofisi ya Mkuu wa mkoa huo lililofanyika kwenye ukumbi wa mikutano, Ikulu ndogo mjini Songea.

Dkt. Mahenge alieleza kuwa serikali haitasita kumchukulia hatua za kinidhamu mtumishi yeyote atakayebainika kwenda kinyume cha sheria, taratibu na kanuni za utumishi wa umma badala yake wanapaswa kuwahudumia Watanzania wote kwa kufuata usawa.

Saturday, September 24, 2016

POLISI MKOANI RUVUMA WASEMA KIFO CHA MWANAFUNZI MAKITA SEKONDARI KUZAMA MAJI ZIWA NYASA KIMESABABISHWA NA UZEMBE WA WALIMU WAKE

Wavuvi wakiwa katika ziwa Nyasa mkoani Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,       
Songea.

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma limesema kuwa tukio la kufa maji mwanafunzi wa kidato cha tatu, Yahaya Rashid (19) katika ziwa Nyasa mkoani humo limesababishwa na uzembe wa Walimu ambao walikuwa wameambatana na wanafunzi wenzake waliokwenda katika ziwa hilo kujifunza mambo ya utalii.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Zubery Mwombeji alisema kuwa tukio hilo lilitokea Septemba 23 mwaka huu majira ya saa 11 jioni katika mji mdogo wa Mbamba bay wilaya ya Nyasa.

Alisema kuwa mwanafunzi huyo ambaye amekutwa na umauti ni mkazi wa Mbinga mjini, ambapo anasoma shule ya Sekondari Makita iliyopo halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani hapa.

Mwombeji alisema kuwa Rashid alikuwa ameambatana na wanafunzi wenzake pamoja na walimu wa shule hiyo ambao walikwenda wilayani Nyasa, kwa lengo la kwenda kujifunza masuala ya utalii, mawimbi ya ziwani pamoja na mipangilio ya miamba iliyopo katika ziwa hilo.

GAMA: UMEME GRIDI YA TAIFA SONGEA KUUNGANISHWA 2018

Na Kassian Nyandindi,           
Songea.

IMEELEZWA kwamba ifikapo mwaka 2018, mji wa Songea ambao ni makao makuu ya mkoa wa Ruvuma unatarajiwa kuunganishwa na umeme wa gridi ya taifa kutoka Makambako mkoa wa Njombe.

Leonidas Gama.
Hayo yalisemwa na Mbunge wa Songea mjini, Leonidas Gama alipokuwa akizungumza na wananchi wa kata ya Misufuni mjini hapa na kuongeza kuwa serikali imekwisha anza mchakato wa kukamilisha kazi hiyo, ili utekelezaji wake uweze kuanza mara moja.

“Nataka kuwahakikishia kwamba mkandarasi ameanza kazi mwaka huu kwa ajili ya upembuzi yakinifu wa kuweza kuleta umeme huu wa gridi ya taifa, kutoka Makambako ambao utapitia Madaba hadi Songea mjini makao makuu ya mkoa wetu wa Ruvuma”, alisema Gama.

Wednesday, September 21, 2016

ASKOFU AWANYOSHEA KIDOLE WANASIASA HAPA NCHINI

Na Mwandishi wetu,      
Tunduru.

ASKOFU wa Kanisa la Anglikana Dayosisi ya Masasi mkoani Mtwara, Dkt. James Almasi amekemea tabia ya baadhi ya wanasiasa hapa nchini kutumia migongo ya waumini kupitia mashirika ya dini, kwa ajili ya manufaa yao binafsi na kuwataka kuacha mara moja tabia hiyo kwa kile alichoeleza kuwa kufanya hivyo ni dhambi na kumchukiza mwenyezi Mungu.

Badala yake alifafanua kuwa ni vyema wanasiasa wakatafuta njia nyingine mbadala ambayo itawafanya waweze kuwa salama mbele ya Mungu, kwa kutumia kipato wanachopata kwa ajili ya kuchangia na kusaidia shughuli mbalimbali za maendeleo ya wananchi katika maeneo yao.

Dkt. Almasi alitoa kauli hiyo hivi karibuni wakati alipokuwa akikabidhi  vifaa tiba, vitanda pamoja na baiskeli za magurudumu matatu  kwa ajili ya zahanati, vituo vya afya na hospitali katika vijiji 66 kwa Mkuu wa wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, Juma Homera.

Alisema kuwa Dayosisi hiyo imekuwa mstari wa mbele kutekeleza shabaha yake kuu ya pili ya kumwezesha na kumwendeleza kila binadamu kujikomboa kifikra na kuondokana na umaskini, ikiwemo kuboresha maisha yake kwa kutumia rasilimali zinazomzunguka katika mazingira yake.

CCM WAPONGEZA UJENZI WA BARABARA NYANDA ZA JUU KUSINI

Na Muhidin Amri,          
Tunduru.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, kimeishukuru serikali kwa kutekeleza ahadi yake ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kwa wananchi wa wilaya hiyo na ukanda wote wa mikoa ya nyanda za juu Kusini.

Chama hicho kimesema kwamba kukamilika kwa ujenzi wa barabara hiyo kutoka Songea hadi wilaya ya Nanyumbu mkoani Mtwara, kupitia Tunduru ambayo ilikuwa na mateso makubwa kwa wananchi kutokana na kupitika kwa shida nyakati za masika hivi sasa ujenzi huo utasaidia kufungua fursa za kiuchumi, mawasiliano na hata kuongezeka kwa uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara.

Hayo yalisemwa jana mjini  hapa na Katibu wa CCM wa wilaya hiyo Mohamed Lawa wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake juu ya hatua ambazo serikali ya awamu ya tano imeanza kutekeleza kwa wananchi wa wilaya ya Tunduru.

JAMII YATAKIWA KUHAKIKISHA INAPELEKA WATOTO WAO SHULE

Kutoka kulia ni Makamu Mwenyekiti wa halmashauri wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Kassim Ntara akisisitiza jambo katika sehemu ya ziara zake za kikazi wilayani humo.
Na Mwandishi wetu,          
Namtumbo.

JAMII hapa nchini imetakiwa kuhakikisha kwamba watoto wao wanawapeleka shule na kuhakikisha kwamba wanahudhuria masomo yao kikamilifu, ukizingatia kwamba elimu ndiyo urithi uliobora maishani mwao na wenye manufaa makubwa hasa katika ulimwengu wa sasa wa sayansi na teknolojia.

Mwenyekiti wa Kamati ya elimu, afya na maji baraza la Madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Kassim Ntara alisema hayo wakati alipokuwa akizungumza na madiwani wenzake wa halmashauri hiyo katika hafla fupi ya kupokea msaada wa madawati  90 yaliyotolewa na benki ya CRDB tawi la Songea kwa ajili ya shule za wilaya hiyo.

Ntara alisema kuwa kutokana na mabadiliko ya ulimwengu wa sasa ni muhimu kwa wazazi na walezi wilayani humo, wakati wote kuwekeza zaidi katika elimu kwa watoto wao, badala ya kuwarithisha vitu ambavyo baadaye vitakuwa tatizo na kuleta mifarakano katika  familia zao.

Tuesday, September 20, 2016

SUMATRA NA KIKOSI CHA USALAMA BARABARANI WALALAMIKIWA TUNDURU

Na Muhidin Amri,
Tunduru.

BAADHI ya Wananchi wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wamelalamikia hatua ya wamiliki wa mabasi yanayofanya safari zake kati ya Tunduru mjini kwenda Masasi mkoani Mtwara, kuendelea kutoza nauli kubwa licha ya kukamilika kwa ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami.

Dkt. Binilith Mahenge Mkuu wa mkoa wa Ruvuma.
Aidha wameilalamikia Mamlaka ya Udhibiti na Usimamizi wa Usafiri wa  nchi kavu na Majini (SUMATRA) mkoani Ruvuma, kwa kushindwa kuchukua hatua za haraka dhidi ya tatizo hilo ambalo sasa limefikia hatua ya kuwa kero katika jamii.

Walisema kuwa SUMATRA imeshindwa kuyachukulia hatua Makampuni husika yanayosafirisha abiria, ambayo yanaendelea kuwakandamiza wananchi na kuwa kero kubwa kwao.

Wakizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti wananchi hao walisema kuwa ni jambo la kusikitisha kuona wamiliki  wa mabasi hayo, kuendelea na mchezo huo mchafu wa kutoza nauli ya shilingi 12,000 kutoka Tunduru hadi  Masasi badala ya shilingi 7,000 hadi 8,000.

BASI LA NEW FORCE LAPATA AJALI LAUA 12 NA KUJERUHI 30

Na Kassian Nyandindi,         
Songea.

WATU 12 wamefariki dunia na wengine 30 kujeruhiwa vibaya kufuatia ajali ya basi la Kampuni ya New Force, linalofanya safari zake kati ya Dar es Salaam na Songea mkoani Ruvuma kuacha njia na kupinduka mara tatu katika kata ya Kifanya wilaya ya Njombe mkoani Njombe.

Tukio hilo lilitokea jana majira ya usiku katika kijiji cha Lilombwi kata ya Kifanya wilaya ya Njombe mkoani  Njombe, kabla ya kufika mpakani mwa mikoa ya Njombe na Ruvuma.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Njombe Pudenciana Protas amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kusema kuwa  lilitokea Septemba 19 mwaka huu majira ya saa 1.40 usiku, huku chanzo cha ajali hiyo kikielezwa kuwa ni uzembe wa dereva kutokana na kuendesha kwa mwendo kasi.

Kwa mujibu wa Kamanda huyo wa Polisi alifafanua kuwa gari lililohusika na ajali hiyo ni lenye namba za usajili T 429 aina ya Zongtong, ambalo lilikuwa likitoka Dar es Salaam kuelekea Songea mkoani Ruvuma likiwa linaendeshwa na dereva aliyetambuliwa kwa jina la Charles Chilwa ambaye amekimbia na kutokomea kusikojulikana.

MANISPAA SONGEA YATUMIA MILIONI 448 UJENZI MRADI WA MAJI RUHUWIKO

Na Muhidin Amri,            
Songea.

MANISPAA ya Songea mkoani Ruvuma, inatarajia kutumia zaidi ya shilingi milioni 448 kwa ajili ya kufanya kazi ya ujenzi wa mradi wa maji katika mtaa wa Ruhuwiko kanisani ili kuweza kuwaondolea kero wananchi ya ukosefu wa maji, ambayo imedumu kwa muda mrefu sasa.

Samwel Sanya ambaye ni Mhandisi wa maji katika Manispaa hiyo, alimweleza mwandishi wa habari hizi kuwa tayari wamekwisha ingia mkataba na mkandarasi wa Kampuni ya Giraf Investment, kwa ajili ya kuanza kazi ya ujenzi huo.

Alifafanua kuwa upembuzi yakinifu kwa mradi huo, umefikia asilimia 95 ambapo ulifanywa mwaka wa fedha wa 2012/2013 na kwamba ujenzi wake hivi sasa ambao unaendelea kutekelezwa, umefadhiliwa na benki ya dunia.

SONGEA PRIVATE DISPENSARY YAFUNGIWA KUTOA HUDUMA

Na Muhidin Amri,            
Songea.

UONGOZI wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, kupitia idara yake ya afya, umeifungia zahanati moja inayomilikiwa na mtu binafsi mjini hapa kutokana na kutoa huduma za matibabu chini ya kiwango.
Damas Kayera Mganga Mkuu mkoa wa Ruvuma.

Zahanati hiyo ambayo inafahamika kwa jina moja maarufu la Songea Private Dispensary, ilifungiwa juzi kuendelea kutoa huduma hizo kutokana na kukiuka miongozo ya Wizara ya afya.

Ofisa habari wa Manispaa hiyo, Albano Midelo alisema hayo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, ambapo alifafanua kuwa hatua hiyo ilifikiwa baada ya timu ya wataalamu wa afya kubaini dosari husika.

Midelo alizitaja baadhi ya sababu zilizosababisha kufungwa kwa zahanati hiyo kuwa ni kufanya kazi ambazo haziendani na miongozo ya Wizara ya afya Ustawi wa Jamii Wanawake, Jinsia, Wazee na Watoto, kutokuwa na ikama ya watumishi ya kutosha na kukosa watumishi wenye sifa ya kutoa huduma za afya.


“Zahanati hii imefungiwa kutoa huduma hadi hapo mmiliki husika atakapokamilisha na kukidhi vigezo vya kuendesha kutoa huduma ya afya, kulingana na miongozo ya Wizara husika”, alisema Midelo.

Monday, September 19, 2016

RC RUVUMA AWATAKA WADAU WA MAENDELEO KUENDELEA KUSHIRIKIANA NA SERIKALI

Na Kassian Nyandindi,           
Namtumbo.

MKUU wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge amewataka Wadau mbalimbali katika mkoa huo kuona umuhimu wa kuendelea kushirikiana na Serikali katika shughuli za maendeleo ya wananchi, ili kuweza kuharakisha ukuaji wa uchumi ndani ya mkoa huo.

Dkt. Mahenge alitoa kauli hiyo juzi mjini Namtumbo mkoani hapa, wakati alipokuwa akifungua kikao maalumu kwa ajili ya uanzishaji wa Benki ya wananchi wa mkoa wa Ruvuma, kilichofanyika mjini hapa.

Alisema kuwa kuazishwa kwa benki hiyo ni agizo lililotolewa na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, katika kikao chake na Wakuu wa mikoa mjini Dodoma kwamba kila mkoa unapaswa kuona umuhimu wa kuanzisha  benki ya wananchi ili iweze kusaidia kukua kwa uchumi na kusogeza huduma za kifedha kwa karibu zaidi katika eneo husika.

Saturday, September 17, 2016

BENKI YA CRDB YAKABIDHI MSAADA WA MADAWATI NAMTUMBO

Meneja wa benki ya CRDB tawi la Songea mkoani Ruvuma, Enock Lugenge upande wa kushoto akikabidhi madawati 90 yenye thamani ya shilingi milioni 5 kwa Makamu Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani hapa, Titus Ng'oma ikiwa ni msaada uliotolewa na benki hiyo kwa ajili ya kunusuru wanafunzi wa shule za msingi  wilayani humo wasiweze kukaa chini.
Na Muhidin Amri,          
Namtumbo.

BENKI ya CRDB tawi la Songea mkoani Ruvuma, imetoa msaada wa madawati 90 yenye thamani ya shilingi milioni 5 kwa halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani humo, ili yaweze kusaidia kukabiliana na tatizo la upungufu wa madawati kwa watoto wa shule za msingi wilayani humo.

Akikabidhi madawati hayo juzi Meneja wa tawi hilo, Enock Lugenge alisema kuwa msaada huo uliotolewa ni utaratibu waliojiwekea benki hiyo ambapo  kila mwaka inagawa faida inayopatikana kwa wanahisa wake na sehemu ya faida inayobaki inarudishwa katika nyanja mbalimbali kwa kuchangia huduma za afya, elimu, maji na shughuli nyingine za maendeleo hapa nchini.

Lugenge alifafanua kuwa katika kusogeza huduma karibu na wananchi pia benki hiyo ya CRDB imefungua tawi dogo mjini Namtumbo, ambapo  hutoa huduma za kifedha wakati wote wa masaa ya kazi.

BENKI YA NMB YAJIVUNIA MAFANIKIO YAKE WAJASIRIAMALI WAPIGWA MSASA SONGEA

Meneja wa benki ya Nmb tawi la Songea mkoani Ruvuma, Colman Kiwia akizungumza na Wajasiriamali wadogo na wa kati katika kikao kati ya benki hiyo na Wajasiriamali hao kilichofanyika kwenye ukumbi wa hoteli ya Heritage Cottage mjini Songea.

Mjasiriamali mdogo kutoka wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Sarah Komba ambaye ni mteja wa benki ya NMB akizungumza wakati wa kikao hicho cha pamoja kati ya wateja wa benki hiyo na uongozi wa NMB tawi la Songea pamoja na wa kutoka makao makuu ya Kanda Mtwara.
Na Muhidin Amri,    
Songea.

WAJASIRIAMALI wadogo na wakati kutoka katika wilaya tano za mkoa wa Ruvuma, wameipongeza benki ya NMB  kwa kuwa na mipango thabiti inayolenga kupunguza umaskini kwa wananchi wengi, ikiwemo kutoa mikopo yenye riba nafuu hatua ambayo itasaidia kuharakisha ukuaji wa uchumi.

Pongezi hizo zilitolewa na Wajasiriamali hao wa kutoka wilaya ya Tunduru, Namtumbo, Mbinga, Songea na Nyasa mkoani humo wakati walipokuwa juzi kwenye kikao chao na uongozi wa benki hiyo Kanda ya kusini, kinachojulikana kwa jina la NMB BUSINESS CLUB ambacho kilihudhuriwa pia na maafisa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania, Jeshi la zimamoto na Maafisa biashara wa Manispaa ya Songea  katia ukumbi wa Heritage Cottage mjini hapa.

Aidha wameiomba serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Dkt. John Magufuli kuiunga mkono benki hiyo ambayo imeonekana kuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi wengi, hasa wenye kipato kidogo ambao wameanza kunufaika na huduma mbalimbali zinazotolewa na benki ya NMB ikiwemo zile za mikopo ambayo huwawezesha kuanzisha biashara ndogo ndogo na shughuli nyingine za kimaendeleo.

Thursday, September 15, 2016

WATAKIWA KUTUMIA UTAJIRI WALIONAO KUPELEKA WATOTO WAO SHULE

Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

WAZAZI na Walezi wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma wametakiwa kutumia utajiri walionao wa kilimo cha zao la kahawa wilayani humo, kwa kuwapeleka watoto wao shule kwani ndiyo msingi mzuri wa maisha yao ya sasa na baadaye badala ya  kuwarithisha mali walizonazo.

Aidha hakuna ufahari kuwarithisha watoto mali au mashamba, kwani yanaweza yasiwasaidie maishani mwao na kuwafanya washindwe kusonga mbele kimaendeleo kutokana na kukosa elimu itakayowasaidia waweze kuondokana na adui ujinga, maradhi na umaskini.

Ofisa elimu msingi wa wilaya ya Mbinga, Samwel Komba alitoa rai hiyo juzi alipokuwa akizungumza na wananchi wa kijiji cha Ruanda kata ya Ruanda  wilayani humo juu ya umuhimu wa kuchangamkia fursa ya mpango wa upimaji ardhi, kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) na suala zima la kuwapatia watoto wao elimu bora ili iweze kuwasaidia kukabiliana na changamoto mbalimbali katika maisha yao.

MBINGA YATENGA MBEGU TANI SITA ZA MBAAZI KWA AJILI YA WAKULIMA

Na Kassian Nyandindi,           
Mbinga.

HALMASHAURI ya  wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, imetenga mbegu tani sita za zao la mbaazi kwa wakulima wa wilaya hiyo sawa na kilo 6,000 kwa lengo la kuwataka wakulima hao, kufufua zao hilo ili waweze kuinua uchumi wao na kuacha kutegemea zaidi zao la kahawa na mahindi.

Kwa mujibu wa Ofisa kilimo wa wilaya hiyo, Yohanes Nyoni alisema kuwa kilo hizo 6,000 zitapandwa katika ekari 2,000 ambapo kila ekari moja itapandwa kilo tatu za mbegu za mbaazi na kwamba zitasambazwa katika maeneo yanayostawi vizuri ili wakulima waanze kuzalisha katika msimu ujao wa 2016/2017.

Nyoni alisema kuwa usambazaji wa mbegu hizo kwa wakulima wilayani Mbinga ni mkakati pia wa kuboresha na kuongeza vyanzo vya mapato, hususani kwenye mazao ya chakula na biashara yanayozalishwa wilayani humo.

Wednesday, September 14, 2016

RC RUVUMA APONGEZA UFYATUAJI TOFARI

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge akishiriki na wananchi katika zoezi la ufyatuaji tofari katika kata ya Nyoni wilaya ya Mbinga mkoani humo.
Na Kassian Nyandindi,           
Mbinga.

MKUU wa Mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge amewapongeza wananchi kata ya Nyoni wilayani Mbinga mkoani humo kwa jitihada wanazozifanya za ufyatuaji wa matofari kwa ajili ya ujenzi wa nyumba mbili za walimu na zahanati ya kijiji cha Likwera zilizopo katika kata hiyo.

Dkt. Mahenge alitoa pongezi hizo juzi wakati alipokuwa katika ziara yake ya kikazi wilayani humo, kukagua miundombinu ya ujenzi wa barabara na maendeleo mbalimbali yanayofanywa na wananchi wa wilaya hiyo.

“Nawapongeza wananchi wa kata hii ya Nyoni kwa moyo huu mlionao wa kujitolea katika shughuli za maendeleo nawaomba endeleeni kufanya hivi, ili tuweze kufikia malengo ya kuwa na nyumba za kutosha za walimu na zahanati zetu za kutolea huduma ya afya kwa kila kijiji”, alisema Dkt. Mahenge.

Tuesday, September 13, 2016

WATENDAJI TUNDURU WATAKIWA KUTEKELEZA MAAGIZO WALIYOPEWA

Na Kassian Nyandindi,             
Tunduru.

MAAFISA Watendaji wa kata katika halmashauri ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, wametakiwa kuhakikisha kwamba zoezi la kufyatua tofari kwa kila kijiji wilayani humo linatakiwa liwe limekamilika mapema iwezekanavyo Septemba 15 mwaka huu.

Aidha wamesisitizwa kusimamia ukusanyaji wa mapato katika maeneo yao ya utendaji kazi, ambapo kila mnunuzi wa mazao mchanganyiko anatakiwa kuwa na kibali cha ununuzi kutoka halmashauri ya wilaya hiyo na leseni hai ya biashara husika.

Agizo hilo lilitolewa na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Tunduru, Abdallah Mussa alipokuwa katika kikao cha kazi juzi akizungumza na Watendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo mjini hapa.

AFARIKI DUNIA BAADA YA LORI KUPARAMIA NYUMBA

Na Kassian Nyandindi,          
Songea.

MTU mmoja mkazi wa kijiji cha Myangayanga Tanga pachani halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Anna Ndunguru (40) amefariki dunia baada ya lori lililokuwa limebeba shehena ya magunia ya mahindi, kuacha njia na kuparamia nyumba waliyokuwa wanaishi wakati akiwa amekaa ndani ya nyumba hiyo na wenzake wakipata mlo wa mchana.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo walieleza kuwa, lilitokea Septemba 8 mwaka huu majira ya saa 6:32 mchana ambapo lori hilo lenye namba za usajili T 231 BCH mali ya mfanyabiashara mmoja maarufu mjini hapa, Medson Ulendo lilikuwa likitokea katika kijiji cha Kilindi kata ya Matiri wilayani hapa.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Festo Sangana ambaye ndiye mmiliki wa nyumba ambayo lori hilo liliparamia na kubomoa sehemu kubwa ya kuta za nyumba hiyo alisema kuwa, ajali hiyo ilisababishwa na uzembe wa dereva kutokana na kuwa katika mwendo kasi ambapo gari lilimshinda kukata kona ndipo alisababisha ajali hiyo.

Sunday, September 11, 2016

SASAWALA NAMTUMBO HAWANA VYOO BORA VYA KUJISAIDIA WANAFUNZI

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge akiwa katika ziara yake ya kikazi juzi wilayani Namtumbo. (Picha na Yeremias Ngerangera)
Na Julius Konala,      
Namtumbo.

MKUU wa mkoa wa Ruvuma Dkt. Binilith Mahenge, amefanya ziara ya kushitukiza katika shule ya msingi Sasawala iliyopo wilayani Namtumbo mkoani humo na kubaini shule hiyo kuwa na ukosefu wa vyoo bora vya kisasa kwa ajili ya kujisaidia wanafunzi.

Mahenge alikumbana na changamoto hiyo juzi baada ya kufanya ziara hiyo iliyolenga kuhamasisha shughuli mbalimbali za maendeleo, ikiwemo kuhimiza suala la ufyatuaji wa matofali 100,000 kwa kila kijiji kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa zahanati, madarasa, matundu ya vyoo, nyumba za walimu pamoja na vyumba vya maabara.

Alisema kuwa hali hiyo inaweza kusababisha magonjwa ya mlipuko kwa wanafunzi wa shule hiyo ambapo ameutaka uongozi wa wilaya hiyo, kuhakikisha kwamba unaanza mchakato wa ujenzi wa vyoo shuleni hapo haraka iwezekanavyo ili kuweza kunusuru afya za watoto hao.

“Kwa kweli nimesikitishwa sana kuona karne hii ya leo bado kuna baadhi ya shule za msingi wanafunzi wake, wanatumia vyoo vilivyojengwa kwa kuzungushiwa nyasi na havina milango jambo hili nasema ni udhalilishaji mkubwa hasa kwa watoto wa kike”, alisema Dkt. Mahenge.

WAKULIMA RUVUMA WAFURAHIA UTARATIBU WA UNUNUZI MAHINDI ULIOPANGWA NA SERIKALI

Na Julius Konala,         
Songea.

BAADHI ya wakulima mkoani Ruvuma, wamefurahia utaratibu uliopangwa na serikali kupitia kitengo chake cha Wakala wa Taifa Hifadhi ya Chakula Tanzania (NFRA) kanda ya Songea mkoani humo, kwa kufungua vituo vya ununuzi wa mahindi katika vijiji mbalimbali kwa kile walichoeleza kuwa kufanya hivyo kumeweza kutoa fursa kwa wakulima wadogo wadogo, kuuza mazao yao pamoja na kuondoa malalamiko yasiyokuwa na msingi.

Pongezi hizo zilitolewa na wakulima hao mwishoni mwa wiki mbele ya Mkuu wa mkoa huo, Dkt. Binilith Mahenge alipokuwa katika ziara yake ya kikazi kutembelea vituo hivyo vilivyotengwa kwa ajili ya ununuzi wa mahindi msimu wa mwaka 2016/2017 mkoani hapa.

Walisema kuwa awali utaratibu huo ulikuwa ukiwanufaisha walanguzi na wafanyabiashara wakubwa na sio kwa wakulima wadogo kama ilivyo sasa.

Saturday, September 10, 2016

POLISI SONGEA WAMSAKA MWENDESHA BODABODA ALIYEUA MWANAFUNZI

Na Kassian Nyandindi,      
Songea.

JESHI la Polisi mkoani Ruvuma linamsaka mwendesha bodaboda ambaye jina lake limehifadhiwa kwa tuhuma za kumgonga mtembea kwa miguu, ambaye ni Mwanafunzi wa darasa la kwanza shule ya msingi Lilondo halmashauri ya wilaya ya Madaba, Martha Mussa (7) na kumsababishia kifo papo hapo.

Zubery Mwombeji.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi ofisini kwake, Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma Zubery Mwombeji alisema kuwa tukio hilo lilitokea Septemba  8 mwaka huu majira ya saa  3:45 asubuhi, katika eneo la kitongoji cha Mabanda barabara ya kutoka Mateteleka kwenda Maweso katika kijiji cha Lilondo kata ya Wino wilayani humo.

Mwombeji alifafanua kuwa siku ya tukio hilo mwendesha bodaboda huyo akiwa anaendesha pikipiki yake aina ya SANLG ambayo namba zake za usajili hazikupatikana, alimgonga mwanafunzi huyo ambaye ni mkazi wa kijiji cha Lilondo na kumsababishia apoteze maisha yake.

Alieleza kuwa mtuhumiwa huyo baada ya kumgonga Martha alikimbia na kutokomea kusikojulikana ambapo Polisi kwa kushirikiana na wananchi wanaendelea kumsaka na mara tu atakapopatikana atafikishwa mahakamani kujibu shitaka hilo linalomkabili.

Kamanda Mwombeji alifafanua kuwa chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi aliokuwa nao mwendesha bodaboda huyo, ambapo alishindwa kumudu usukani wa pikipiki yake na kupelekea kumgonga mtembea kwa miguu ambaye alikuwa kandokando mwa barabara hiyo.

Thursday, September 8, 2016

WANUSURIKA KUPOTEZA MAISHA BAADA YA LORI KUPARAMIA NYUMBANI KWAO


Lori hili lenye namba za usajili T 231 BCH ndilo ambalo limesababisha maafa hayo. (Picha na Kassian Nyandindi)
Na Kassian Nyandindi,           
Mbinga.

WATU watatu wakazi wa Tanga pachani kata ya Mbinga mjini mkoani Ruvuma, wamenusurika kupoteza maisha yao baada ya lori lililokuwa limebeba shehena ya magunia ya mahindi, kuacha njia na kuparamia nyumba wakati wakiwa wamekaa ndani ya nyumba hiyo wakipata mlo wa mchana.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo walieleza kuwa lilitokea Septemba 8 mwaka huu, majira ya saa 6:32 mchana ambapo lori hilo lenye namba za usajili T 231 BCH mali ya Mfanya biashara mmoja maarufu mjini hapa, Medson Ulendo lilikuwa likitokea katika kijiji cha Kilindi kata ya Matiri wilayani hapa.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, Festo Sangana ambaye ndiye mmiliki wa nyumba ambayo lori hilo liliparamia na kubomoa sehemu kubwa ya kuta za nyumba hiyo alisema kuwa, ajali hiyo ilisababishwa na uzembe wa dereva kutokana na kuwa katika mwendo kasi ambapo gari lilimshinda kukata kona ndipo alisababisha ajali hiyo.

Tuesday, September 6, 2016

UPIMAJI MASHAMBA YA KAHAWA MBINGA KUWANEEMESHA WAKULIMA

Na Kassian Nyandindi,            
Mbinga.

MASHAMBA ya wakulima wanaozalisha zao la kahawa wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, yamewekwa katika mpango wa kupimwa kisheria ili wakulima hao waweze kuwa na hati miliki za kimila, ambazo zitawasaidia waweze kusonga mbele kimaendeleo.

Aidha upimaji huo wa mashamba unalenga pia kuifanya serikali iweze kutambua ni wakulima wangapi wilayani humo wanamashamba ya kahawa, ili hapo baadaye iweze kutengeneza takwimu zake halisi zitakazowatambua wazalishaji wake wa zao hilo.

Hayo yalisemwa na Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya hiyo, Gombo Samandito alipokuwa akitolea ufafanuzi juu ya faida za upimaji ardhi katika kikao cha wadau wa kahawa kilichofanyika juzi mjini hapa.

Monday, September 5, 2016

RC RUVUMA: WATUMISHI WA SERIKALI WANAOJIONA HAWAENDANI NA KASI YA AWAMU YA TANO WAJIONDOE MAPEMA



Na Kassian Nyandindi,          
Mbinga.

WATUMISHI wa serikali katika mkoa wa Ruvuma, wametakiwa kuacha kufanya kazi kwa mazoea badala yake wanapaswa kuendana na kasi ya serikali ya awamu ya tano, ili kuweza kuwaletea maendeleo wananchi kwa faida ya kizazi cha sasa na baadaye.


Kadhalika kwa wale ambao wanajiona kwamba hawawezi kuendana na kasi hiyo wameshauriwa wajiondoe mapema, kabla mkono wa sheria haujawafikia ili waweze kuepukana na madhara yanayoweza kuwapata hapo baadaye.

Kauli hiyo ilitolewa na Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge wakati alipokuwa akizungumza na wakuu wa idara wa halmashauri ya mji wa Mbinga na wilaya ya Mbinga mkoani humo, katika kikao cha kazi kilichofanyika mjini hapa.

MAKAMPUNI YA KAHAWA MBINGA YAPEWA SIKU 14 KUKAMILISHA MALIPO YA WAKULIMA

Cosmas Nshenye, Mkuu wa wilaya ya Mbinga.


Na Kassian Nyandindi,          
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Cosmas Nshenye ametoa amri kwa Makampuni yanayonunua kahawa wilayani humo kuhakikisha kwamba ndani ya siku 14 kuanzia sasa, yawe yamekamilisha malipo ya awamu ya pili ya fedha za wakulima wa kahawa na kwamba kampuni itakayoshindwa kutekeleza amri hiyo itachukuliwa hatua za kisheria ikiwemo kufikishwa Mahakamani.

Aidha ametoa agizo kwa wafanyabiashara wote wanaojishughulisha na biashara ya zao hilo, kuandaa takwimu za malipo na mauzo ya kahawa ambapo mara baada ya msimu wa mauzo kwisha, takwimu hizo ziwasilishwe ofisini kwake ili serikali iweze kuzifanyia kazi.

Nshenye alitoa agizo hilo jana alipokuwa akizungumza kwenye kikao cha Wadau wa kahawa wilayani hapa, ambacho kilishirikisha wafanyabiashara, vikundi vya wakulima na makampuni ambayo hujishughulisha na ununuzi wa zao hilo wilayani humo.

“Ndugu zangu hili sio ombi, takwimu hizi tukishazipata zitaisaidia serikali kutambua ni nani ameuza kahawa hasa kwa wale watu wajanja wasiokuwa na mashamba, ambao hupita vijijini kwa wakulima na kuendelea kumnyonya mkulima abaki kuwa maskini’, alisema Nshenye.

DOKTA MAHENGE: HAKIKISHENI HUDUMA YA MAJI SAFI NA SALAMA INATOSHELEZA KATIKA MJI WA MBINGA

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge akisisitiza jambo katika kikao cha kazi kilichofanyika mjini hapa, wakati alipokuwa akizungumza juzi na Wakuu wa idara wa halmashauri ya mji wa Mbinga na wilaya ya Mbinga mkoani humo.


Na Kassian Nyandindi,              
Mbinga.

MAMLAKA ya Maji safi na Usafi wa Mazingira (MBIUWASA) halmashauri ya mji wa Mbinga mkoa wa Ruvuma, imetakiwa ihakikishe kwamba huduma ya upatikanaji wa maji safi na salama katika mji huo inatosheleza wakati wote kwa ajili ya matumizi ya wananchi.

Agizo hilo lilitolewa na Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge alipokuwa akizungumza na wakuu wa idara wa wilaya hiyo katika kikao cha kazi kilichofanyika mjini hapa.

“Nataka kuona maji yanatosheleza katika mji huu ili tuweze kuwaondolea adha wananchi wetu kutafuta maji umbali mrefu, boresheni mindombinu ya maji na kukusanya madeni ya ankra za maji kwa wakati”, alisisitiza Dkt. Mahenge.

MKUU WA MKOA RUVUMA AZITAKA HALMASHAURI KUWATUMIA JKT KWA AJILI YA UJENZI WA MIUNDOMBINU MBALIMBALI

Kaimu mkuu wa kikosi cha 842 Kj -Mlale JKT Meja Absolomon Shausi kulia, akimkaribisha mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge kikosini hapo kwa ajili ya kufunga mafunzo ya miezi mitatu kwa vijana 1,365 kwa mujibu wa sheria, Operesheni Magufuli mwaka 2016.
Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Dkt. Binilith Mahenge akikagua gwaride rasmi la vijana 1,365 waliojiunga na mafunzo ya  kijeshi ya miezi mitatu katika kikosi cha 842 Kj- Mlale JKT kwa mujibu wa sheria Operesheni Magufuli mwaka 2016 wilayani Songea mkoani humo.



Na Kassian Nyandindi,        
Songea.

MKUU wa mkoa wa Ruvuma, Dkt. Binilith Mahenge amezitaka Halmashauri za wilaya mkoani humo, mpaka kufikia mwishoni wa mwezi Disemba mwaka huu zihakikishe kwamba zimekamilisha zoezi la ujenzi wa vyoo katika shule za msingi na sekondari.

Aidha ameagiza utekelezaji wa kuboresha miundombinu ya sekta ya afya ambapo kila kijiji na kata wataalamu husika, wanatakiwa kusimamia na kutekeleza ujenzi wa majengo ya zahanati na vituo vya afya.
 
Dkt. Mahenge alitoa agizo hilo juzi alipokuwa mgeni rasmi katika sherehe za kufunga mafunzo ya miezi mitatu kwa mujibu wa sheria, Operesheni Magufuli kwa vijana waliomaliza kidato cha sita katika maeneo mbalimbali hapa nchini katika kikosi cha Jeshi Mlale 842KJ zilizofanyika mkoani hapa.

“Pia naagiza halmashauri zote katika mkoa huu, watumie jeshi hili kwa ajili ya kufanya shughuli mbalimbali za ujenzi wa majengo ya maabara, shule na hata ujenzi wa matundu ya kisasa ya vyoo ili tuweze kuwafanya watoto wetu mashuleni waweze kuepukana na magonjwa ya mlipuko”, alisema Dkt. Mahenge.

Friday, September 2, 2016

MKOA WA RUVUMA WATUMISHI NANE WASIMAMISHWA KAZI

Na Julius Konala,    
Songea.

SERIKALI mkoani Ruvuma imewasimamisha kazi watumishi nane kutoka halmashauri za wilaya nne za mkoa huo ikiwemo katika wilaya zake za Tunduru, Nyasa, Mbinga na Namtumbo kwa lengo la kupisha uchunguzi baada ya kubainika wameshindwa kuzingatia weledi wa utumishi wa umma ikiwemo kufanya vitendo vya ubadhirifu wa fedha.

Hayo yalisemwa na Katibu tawala wa mkoa huo, Hassan Bendeyeko alipokuwa akitoa taarifa kwa waandishi wa habari katika ukumbi wa mipango uliopo kwenye Ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Ruvuma.

Bendeyeko aliwataja watumishi waliosimamishwa kazi kuwa ni Fortunatus Mlokozi Kakiko, ambaye ni mkaguzi wa ndani Alan Ansigali Mbunda ni Afisa ugavi na Juma Kassim Kasalo ambaye ni Mweka Hazina wote wanatoka halmashauri ya wilaya ya Tunduru.