Monday, October 30, 2017

KIPINDUPINDU CHAINGIA DODOMA MTU MMOJA AFARIKI DUNIA

Ummy Mwalimu Waziri wa afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto.

Na Mwandishi wetu,
Dodoma.

MTU mmoja amefariki dunia na wengine nane kuugua ugonjwa wa kipindupindu mkoani Dodoma, ambapo inadaiwa kuwa ugonjwa huo uliwapata wakiwa kwenye sherehe ya harusi iliyofanyika katika kijiji cha Mlowa barabarani wilayani Chamwino.

Dokta Charles Kiologwe ambaye ni Mganga mkuu wa Mkoa wa Dodoma alisema kuwa ugonjwa huo uliingia mkoani humo Oktoba 19 mwaka huu huku akizitaja wilaya zilizokumbwa na ugonjwa kuwa ni Bahi, Chamwino na Kongwa.

Alisema ugonjwa wa kipindupindu umeingia katika mkoa wa Dodoma ambapo baadhi ya watu wameugua na mmoja amepoteza maisha wilayani Bahi.

WASIMAMIZI MTIHANI KIDATO CHA NNE WAPEWA ONYO KALI

Katibu Mtendaji wa Baraza la mitihani Tanzania, Dokta Charles Msonde.
Na Mwandishi wetu,

WAKATI Watahiniwa 385,938 wanatarajiwa kuanza mtihani wa kumaliza kidato cha nne mwaka huu leo, Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA) limetoa onyo kali kwa wasimamizi wa mtihani huo.

Baraza hilo limesema kuwa halitasita kuchukua hatua kali dhidi ya wasimamizi hao wa mitihani, pale itakapobainika kuna udanganyifu wa aina yoyote ile.

Katibu Mtendaji wa baraza hilo, Dokta Charles Msonde alitoa onyo hilo jana jijini Dar es Salaam wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ambapo alisema watahiniwa wa shule watakuwa 323,513 na wa kujitegemea 62,425.

Friday, October 27, 2017

BREAKING NEWS: KIKAO BARAZA LA MADIWANI MJI WA MBINGA CHAVUNJIKA MKURUGENZI MTENDAJI AKALIA KUTI KAVU AJIKUTA AKIWA KATIKA WAKATI MGUMU

Baadhi ya Madiwani wa Halmashauri ya mji wa Mbinga leo wakiwa wamekusanyika nje ya ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa wa kufanyia kikao chao cha baraza la Madiwani, kabla ya kikao hicho cha baraza kuanza kufanyika.

Aliyesimama ni Diwani wa kata ya Mpepai halmashauri ya mji wa Mbinga, Benedict Ngwenya akichangia hoja ya kukataa kuendelea na kikao cha baraza la Madiwani wa mji huo, wakitaka mpaka Mkurugenzi mtendaji Robert Kadaso Mageni atoke nje ya kikao ndipo waendelee na kikao ambapo hata hivyo kikao hicho kilivunjika hawakuweza kuendelea nacho. 

Madiwani wa Halmashauri ya mji wa Mbinga na baadhi ya waalikwa wakitoka nje ya ukumbi baada ya kikao cha baraza la Madiwani hao kuvunjika.
Na Kassian Nyandindi,    
Mbinga.

KATIKA hali isiyokuwa ya kawaida, kikao cha baraza la Madiwani wa Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, kimeshindwa kufanyika na badala yake kimevunjika kufuatia Madiwani hao kumkataa Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Robert Kadaso Mageni wakidai kuwa hawataki kufanya naye kazi tena kutokana na Mkurugenzi huyo kushindwa kusimamia kikamilifu miradi ya maendeleo ya wananchi wa halmashauri hiyo.

Madiwani hao walichukua maamuzi hayo magumu leo katika kikao hicho ambacho walitakiwa kupokea taarifa za maendeleo ya wananchi, robo ya kwanza ya mwaka kilichoketi kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa.

Aidha maamuzi hayo yalifikiwa baada ya Mwenyekiti wa Madiwani hao, Kipwele Ndunguru kufungua kikao cha baraza hilo na kuwataka Madiwake wake wapokee agenda za kikao, ambapo kwa pamoja walimkatalia kupokea agenda hizo huku wakieleza kuwa wapo tayari kuzipokea endapo Mkurugenzi huyo hatakuwepo katika baraza hilo.

Thursday, October 26, 2017

WANANCHI MBINGA WAITAKA SERIKALI KUWAJIBISHA WAHUSIKA UPOTEVU WA MAPATO MSITU WA MBAMBI

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dokta Binilith Mahenge.
Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

BAADA ya taarifa ya Kamati maalum iliyofanya kazi ya kuchunguza uvunaji msitu wa Mbambi uliopo katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, kuwasilisha taarifa ya kazi iliyofanya na kubaini hasara ya mapato ya shilingi milioni 800 ambayo ilibidi yapatikane kutokana na uvunaji huo, baadhi ya wananchi wamesema kuwa usimamizi wa kazi hiyo ungekuwa mzuri fedha hizo zingepatikana na kuweza kuboresha huduma muhimu katika hospitali ya wilaya ya Mbinga iliyopo mjini hapa.

Kadhalika walieleza kuwa hospitali hiyo ambayo hivi sasa baadhi ya majengo yake ni chakavu likiwemo jengo la upasuaji ambalo halijafanyiwa ukarabati kwa miaka mingi huku hali ya huduma ikiwa mbaya hivyo wanaiomba serikali kuchukua hatua ili kuweza kunusuru hali hiyo.

“Hata dawa za kuhudumia akina mama wajawazito pale wanapofikia hatua ya kujifungua wakati mwingine hazipatikani kwenye hii hospitali yetu na kusababisha baadhi yao kupoteza maisha lakini fedha hizi zingepatikana zingeweza kuhudumia jamii”, walisema.

WOFMAIZE YASHINDA ZABUNI YA KUKUSANYA USHURU SONGEA

Meya wa Manispaa ya Songea, Abdul Mshaweji akisaini mikataba kati ya Manispaa hiyo na Kampuni ya WOFMAIZE kwa ajili ya kampuni hiyo kuanza kazi ya kukusanya ushuru wa shilingi milioni 610 baada ya kushinda zabuni. 
Na Albano Midelo,    
Songea.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, imesaini mkataba wa ukusanyaji ushuru wa mazao wa shilingi milioni 610 na kampuni ya WOFMAIZE iliyopo hapa Songea.

Makubaliano ya kusaini mkataba huo yamekamilika Oktoba 24 mwaka huu katika Ofisi ya Mstahiki Meya wa Manispaa ya Songea, Abdul Hassan Mshaweji huku yakishuhudiwa na wawakilishi wa kampuni hiyo pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Manispaa ya Songea Injinia Samwel Sanya.

Katika mikataba hiyo kampuni hiyo itahusika na ukusanyaji ushuru wa mazao ya vyakula vilivyosindikwa na visivyosindikwa katika maeneo ya SODECO, Manzese na maeneo mengine ya Manispaa hiyo.

KAYA MASKINI SONGEA WAWEZESHWA MILIONI 175


Baadhi ya wananchi waliopo kwenye mpango wa kunusuru kaya maskini katika Manispaa ya Songea wakipata huduma.
Na Albano Midelo,    
Songea.

MFUKO wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Euvuma, imeweza kuwasaidia wanufaika 4,881 waliopo kwenye mpango wa kunusuru kaya maskini katika halmashauri hiyo kwa kuwapatia shilingi milioni 175 ili ziweze kuwasaidia na hatimaye waweze kuondokana na umaskini.

Christopher Ngonyani ambaye ni Mratibu wa mfuko huo katika halmashauri hiyo alimweleza mwandishi wetu kuwa fedha hizo zimetolewa katika kipindi cha mwezi Septemba hadi Oktoba mwaka huu.

Alisema malipo hayo yamefanyika na kukamilika ndani ya wiki hii katika mitaa 53 ambayo ina wanufaika hao.

Wednesday, October 25, 2017

SAKATA LA MSITU WA MBAMBI LAENDELEA KUMSAKAMA MKURUGENZI HALMASHAURI MJI WA MBINGA

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dokta John Pombe Magufuli.
Na Kassian Nyandindi,         
Mbinga.

SAKATA la tuhuma wizi wa mamilioni ya fedha za mradi wa uvunaji wa msitu wa Mbambi katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, limeibua sura mpya baada ya wananchi wa kata ya Matarawe mjini hapa kuitaka halmashauri hiyo iwalipe asilimia 10 ya fedha za mapato yaliyotokana na msitu huo.

Asilimia hiyo ya mapato wanayodai wananchi hao imeelezwa kuwa ni makubaliano yaliyofanywa katika vikao halali vilivyopita na kupitishwa na baraza la Madiwani wa halmashauri ya mji huo.

Walisema wanamshangaa Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya mji wa Mbinga, Robert Kadaso Mageni kwa kutosimamia kikamilifu fedha za msitu huo na kusababisha wizi huo ufanyike na wao kukosa sehemu ya mapato yao.

WAMPONGEZA RAIS MAGUFULI KWA KUWABANA MAFISADI

Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

WANANCHI wa kijiji cha Lukalasi kitongoji cha Ngembambili kijiji cha Mkako wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wamempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dokta John Pombe Magufuli kwa kazi anayoendelea kuifanya ya kuwaibua mafisadi na kuwachukulia hatua wakiwemo wezi wa madini.

Pongezi hizo zimetolewa hivi karibuni na wachimbaji wadogo wa madini ambao wanaishi katika maeneo hayo mbele ya mkutano wa hadhara ambao ulihudhuriwa na Mkuu wa mkoa huo, Dokta Binilith Mahenge.

Masha Mussa na Silvano Challe wakazi wa Ngembambili kwa nyakati tofauti walisema kuwa kitendo anachokifanya Magufuli na kuwabana mafisadi hao ambao walikuwa wanadhoofisha uchumi wa nchi, ni ujasiri wa hali ya juu hivyo wamemwomba aendelee kukaza kamba zaidi ili kuweza kudhibiti vitendo hivyo viovu visiweze kuendelea kutokea.

Tuesday, October 24, 2017

TFDA MANISPAA SONGEA YAKAMATA DAWA AMBAZO HAZIFAI KWA MATUMIZI YA BINADAMU

Mratibu wa Udhibiti wa Chakula na Dawa (TFDA) katika Manispaa ya Songea, Vitalis Mkomela akionesha dawa za aina mbalimbali kwa waandishi wa habari ambazo zimepita muda wake wa matumizi. 
Na Albano Midelo,
Songea.

MAMLAKA ya Udhibiti wa Chakula na Dawa (TFDA) katika Manispaa ya Songea Mkoa wa Ruvuma, imekamata dawa za binadamu ambazo zilikuwa zinaendelea kuuzwa zikiwa zimepita muda wake katika baadhi ya maduka ya dawa muhimu yaliyopo mjini hapa.

Mratibu wa TFDA katika Manispaa hiyo, Vitalis Mkomela alisema kuwa dawa za aina mbalimbali zenye thamani ya shilingi 244,000 zilikamatwa katika operesheni maalum ambayo ilifanywa na watalaamu wa idara ya afya.

Mmiliki wa duka moja ambalo lilikutwa na dawa hizo amekiri kuuza dawa hizo zilizomalizika muda wake na kwamba tayari amepigwa faini ya shilingi 600,000.

Sunday, October 22, 2017

MKURUGENZI HALMASHAURI MJI WA MBINGA NA WENZAKE WATUHUMIWA KUTAFUNA MAMILIONI YA FEDHA ZA MSITU

Baraza maalum la Madiwani Halmashauri ya mji wa Mbinga likiwa limeketi katika kikao chake kujadili ubadhirifu wa fedha za mavuno ya msitu wa Mbambi katika halmashauri hiyo.
Mwenyekiti wa Kamati maalum ya kuchunguza msitu wa Mbambi halmashauri mji wa Mbinga, Kelvin Mapunda akikabidhi taarifa ya uchunguzi kwa Mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Ndunguru Kipwele.
Na Kassian Nyandindi,         
Mbinga.

BARAZA la Madiwani la Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, limetoa mapendekezo yake ya kumkataa Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo Robert Kadaso Mageni kwamba hawataki kufanya naye kazi tena, wakimtuhumu ametafuna fedha za mauzo ya mbao zilizopasuliwa katika msitu wa Mbambi uliopo mjini hapa ambao ni mali ya halmashauri ya mji huo.

Robert Kadaso Mageni.
Aidha imeelezwa kuwa Mkurugenzi huyo amelipotosha baraza hilo katika kikao walichoketi Novemba 2 hadi 3 mwaka jana na kutoa taarifa za uongo kwamba msitu huo una jumla ya miti 5,4040 ambayo inafaa kupasuliwa mbao wakati ukweli ni kwamba msitu ulikuwa na miti 8,470.

Kufuatia taarifa hizo ambazo hazikuwa sahihi wakati anazitoa kwenye baraza hilo juu ya uvunaji wa msitu huo, hali hiyo imesababisha halmashauri kupata hasara ya shilingi milioni 888,000,000.

Baada ya baraza hilo la Madiwani kutoa mapendekezo hayo ya kumkataa, walimtaka Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Cosmas Nshenye kufikisha kilio chao kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dokta John Pombe Magufuli ili aweze kuchukua hatua zaidi za kinidhamu dhidi ya mtumishi huyo.

SERIKALI YAPONGEZWA KWA KUBORESHA ELIMU KATIKA SHULE ZA MSINGI, SEKONDARI NA VYUO VIKUU

Na Kassian Nyandindi,   
Songea.

MJUMBE wa Kamati tendaji Taifa ya Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) mkoani Ruvuma, Sabina Lipukila ameipongeza Serikali ya awamu ya tano ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais Dokta John Pombe Magufuli kwa kuona umuhimu wa kuboresha shule za msingi, sekondari na vyuo vikuu hapa nchini ikiwa ni lengo la kuhakikisha vijana wote wanapata elimu bora.

Hayo yalisemwa juzi na Mjumbe huyo katika mahafali ya tatu ya kuhitimu wanafunzi wa kidato cha nne, katika sekondari ya kutwa ya Mahanje iliyopo Madaba wilayani Songea mkoani hapa.

Alisema kuwa kufuatia hali hiyo wananchi wanapaswa kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali katika kuboresha maendeleo ya sekta ya elimu hapa nchini ili watoto wanaosoma katika shule hizo waweze kuwa katika mazingira mazuri.

Wednesday, October 18, 2017

MANISPAA SONGEA YATOA MILIONI 49 KUWEZESHA WAJASIRIAMALI WAKE

Kutoka kulia aliyesimama ni Mbunge wa Jimbo la Songea mjini, Leonidas Gama akisisitiza jambo juu ya namna ya kuwajali na kuthamini vikundi vya wajasiriamali vya vijana na wanawake na upande wa kushoto aliyeketi ni Meya wa Manispaa ya Songea Abdul Mshaweji.
Na Mwandishi wetu,        
Songea.

IMEELEZWA kuwa Wajasiriamali wadogo wadogo waliopo katika halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, watanufaika na mkopo wa shilingi milioni 49 ambao umetolewa na halmashauri hiyo, kwa ajili ya kuwawezesha wasonge mbele kimaendeleo katika shughuli zao za ujasiriamali.

Mkuu wa idara ya Maendeleo ya Jamii katika Manispaa hiyo, Naftari Saiyoloi alitoa taarifa hiyo juzi mjini hapa, katika uzinduzi wa mfuko wa vijana na wanawake.

Saiyoloi alibainisha kuwa shilingi milioni tisa zitakopeshwa kwa vikundi kumi vya vijana na shilingi milioni 40 zitakopeshwa vikundi 39 vya wanawake.

Sunday, October 15, 2017

WATU 2,458 MANISPAA SONGEA HAWAJUI KUSOMA NA KUANDIKA

Mkuu wa wilaya ya Songea, Palolet Mgema akikagua zana za kufundishia katika Manispaa ya Songea.
Na Albano Midelo,
Songea.

IMEELEZWA kuwa Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, ina Watu Wazima 2,458 ambao hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu.

Afisa elimu ya Watu Wazima, Faraja Yonas alisema hayo juzi ambapo alifafanua kuwa kati yao wanaume ni 661 na wanawake ni 1,797.

Yonas alibainisha kuwa kwa mujibu wa takwimu za usajili mwezi Januari hadi Machi mwaka huu, Manispaa hiyo ina jumla ya Watu Wazima 119,328 ambapo kati yao wanaume ni 58,049 na wanawake ni 61,279.

Friday, October 13, 2017

TFDA SONGEA YAKAMATA MAFUTA FEKI YA ALBINO NA VYAKULA VILIVYOHARIBIKA

Mganga Mkuu wa Manispaa ya Songea, Mameritha Basike akionesha kwa waandishi wa habari mafuta feki ya Albino ambayo yalikamatwa katika moja ya duka linalouza vipodozi mjini hapa.
Baadhi ya vyakula vilivyoharibika na mafuta feki ya albino ambavyo vilikamatwa hivi karibuni na Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) Songea.
Na Albano Midelo,    
Songea.

IDARA ya Afya katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, kwa kushirikiana na watalaamu wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) wamefanya Operesheni katika maduka ya vipodozi katika mji wa Songea mkoani humo na kufanikiwa kukamata mafuta ya Albino yakiuzwa kinyume cha sheria na taratibu husika.

Mganga Mkuu wa Manispaa hiyo Dokta Mameritha Basike alisema mafuta hayo yalikamatwa juzi katika duka la Godluck Mranga ambayo yalikuwa yanauzwa shilingi 4,500.

“Hairuhusiwi mafuta ya kupaka Albino aina ya Sunblock Cream UV40 kuwepo kwenye maduka ya vipodozi badala yake mafuta haya yanaruhusiwa kuwepo kwenye maduka ya dawa (Pharmacy)”, alisema Dokta Basike.

MANISPAA SONGEA YAVUNJA MKATABA NA MKANDARASI

Hii ni moja kati ya sehemu ya barabara mtaa wa FFU kwenda Matogoro yenye urefu wa kilometa 3.2 inayojengwa kwa kiwango cha lami nzito katika Manispaa ya Songea.
Na Mwandishi wetu,     
Songea

HATIMAYE Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, imevunja rasmi Mkataba ujenzi wa lami nzito kati yake na Kampuni ya Lukolo yenye makao makuu yake Jijini Dar es salaam.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa hiyo, Mhandisi Samwel Sanya alisema kuwa wamechukua maamuzi hayo baada ya muda wa Mkataba wa kumaliza kazi kwa Mkandarasi huyo ulimalizika tangu Juni 30 mwaka huu.

Alisema kuwa baada ya muda huo kumalizika Mkandarasi huyo aliingizwa kwenye tozo (Liquidated Damage) na kwamba iwapo atashindwa kumaliza kazi kwa siku 100 hatua za kisheria za kuvunja mkataba zitafanyika.

Thursday, October 12, 2017

MWANSASU MWENYEKITI MPYA WA CHAMA CHA MAPINDUZI NAMTUMBO

Na Yeremias Ngerangera,
Namtumbo.

WANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma wamemchagua, Aggrey Mwansasu kuwa Mwenyekiti mpya wa CCM wilayani humo baada ya kumbwaga chini aliyekuwa Mwenyekiti wa chama hicho Benjamini Nindi.

Uchaguzi wa kumpata Mwenyekiti huyo ulifanyika juzi kwenye ukumbi wa shule ya Sekondari Namtumbo, ambayo inamilikiwa na Jumuiya ya wazazi ya Chama Cha Mapinduzi iliyopo mjini hapa.

Katika uchaguzi huo awali uliingia dosari baada ya msimamizi wa uchaguzi huo, Zena Mijinga kujisahau kwa kutosoma kanuni ya ushindi wa uchaguzi huo ambapo mgombea ni sharti apate kura zaidi ya nusu ya wapiga kura waliopo kwenye uchaguzi huo.

FUMANIZI LADAIWA KUSABABISHA GARI KUTEKETEZWA MOTO

Gari aina ya Noah linalodaiwa kuteketea kwa moto eneo la Peramiho wilayani Songea baada ya fumanizi.  
Na Albano Midelo,   
Songea.

GARI aina ya Noah limeteketea kwa moto katika eneo la Peramiho wilayani Songea mkoa wa Ruvuma.

Taarifa za awali za mashuhuda waliohojiwa katika eneo la tukio walidai kuwa gari hilo liliteketezwa, kutokana na sababu za fumanizi la mke wa mtu ambaye inadaiwa kuwa mwenye mume aliamua kuteketeza gari hilo.

Uchunguzi umebaini kwamba ubavuni mwa gari hilo ambalo limeteketea yameandikwa maneno kwa rangi nyeusi, kuwa mke wa mtu ni sumu ambapo akinamama wanne waliokutwa katika eneo hilo walidai kuwa tukio hilo lilisababishwa na fumanizi.

WANANCHI MITENDEWAWA NA CHANDARUA SONGEA KUNUFAIKA NA MRADI WA MAJI SAFI NA SALAMA

Mhandisi wa maji Manispaa ya Songea, Samwel Sanya aliyesimama katikati akitoa maelezo mafupi juu ya maendeleo ujenzi mradi wa maji safi na salama katika mtaa wa Mitendewawa na Chandarua katika Manispaa hiyo kwa Mkuu wa wilaya ya Songea, Palolet Mgema aliyesimama upande wa kushoto ambaye amevaa suti rangi nyeusi.
Na Albano Midelo,
Songea.

MTAA wa Mitendewawa na Chandarua iliyopo katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wananchi wake wanatarajia kunufaika na kuondokana na adha ya upatikanaji wa maji safi na salama, baada ya serikali kuanza kujenga mradi wa maji wenye thamani ya shilingi milioni 517.

Samwel Sanya ambaye ni Mhandisi wa Maji katika Manispaa hiyo alisema hayo mbele ya Mkuu wa wilaya ya Songea, Palolet Mgema wakati Mkuu huyo wa wilaya alipofanya ziara yake ya ukaguzi wa mradi huo.

Alisema kuwa utekelezaji wa mradi huo ulitakiwa kuanza mwaka wa fedha wa 2014/2015 lakini utekelezaji wake haukufanikiwa kutokana na fedha hizo kuchelewa kuwafikia kutoka Serikali kuu.

Sunday, October 8, 2017

MATUKIO KATIKA PICHA SIKU YA MAHAFALI DARASA LA SABA DE PAUL SONGEA

Mgeni rasmi katika mahafali ya wanafunzi wa darasa la saba shule ya De Paul Msamala Manispaa ya Songea Kamishina wa elimu Tanzania, Dokta Edicome Shirima akiangalia vifaa vya masomo ya sayansi kwa wahitimu wa darasa la saba wa shule hiyo.

Wahitimu wa darasa la saba shule ya De Paul Msamala wakionesha umahili wao wa kucheza muziki wakati wa mahafali yao ya kumaliza elimu ya msingi shuleni hapo.

Kamishina wa elimu Tanzania Dokta Edicome Shirima akimzawadia mwanafunzi Amri Mmanja ambaye alifanya vizuri katika michezo na taaluma wakati wa mahafali yao ya kuhitimu darasa la saba katika shule ya De Paul Msamala iliyopo Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma.

Mama mzazi wa Amri Mmanja Farida Komba, akimpatia zawadi mtoto wake Amri Mmanja baada ya kuhitimu elimu ya msingi wakati wa mahafali yake ya darasa la saba iliyofanyika juzi katika shule ya De Paul iliyopo Msamala katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma.

NAMSWEA MBINGA WAFANYA TAMASHA LA MICHEZO KUHAMASISHA MAENDELEO

Upande wa kushoto mdhamini wa tamasha la michezo ikiwemo nyimbo za asili katika tarafa ya Namswea wilayani Mbinga, Thotnant Ezekiel Kayombo ambaye alikuwa mgeni rasmi katika tamasha hilo akiwa na diwani wa kata ya Namswea wilayani humo, Angelus Mbilinyi ambaye yupo katikati amevaa suti rangi nyeusi.
Washiriki wa mchezo, mpira wa miguu wakiwa katika picha ya pamoja siku ya tukio la tamasha la michezo katika tarafa ya Namswea wilayani Mbinga.
Na Mwandishi wetu,
Mbinga.

KATIKA kuenzi utamaduni wa kiafrika, Wananchi wanaoishi katika tarafa ya Namswea wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma wamefanya tamasha la michezo mchanganyiko ndani ya tarafa hiyo, ikiwa ni lengo la kuhamasisha shughuli mbalimbali za maendeleo.

Tamasha hilo lilizinduliwa hivi karibuni katika viwanja vya michezo Namswea likiwa limebeba kauli mbiu “Ujana ni hazina tuutumie vizuri kwa manufaa ya sasa na baadae” ambapo lilifadhiliwa na Thotnant Ezekiel Kayombo ambaye alikuwa mgeni rasmi huku michezo iliyokuwa ikichezwa siku hiyo ni mpira wa miguu na ngoma mbalimbali za asili.

Akizungumza na mwandishi wetu, Kayombo alifafanua kuwa lengo la tamasha hilo ni kufikisha ujumbe huo kwa jamii hasa vijana juu ya wajibu wao katika kushiriki kwenye shughuli za kimaendeleo katika maeneo yao wanayoishi.

Saturday, October 7, 2017

MANISPAA SONGEA YAFAULISHA KIDATO CHA SITA KWA ASILIMIA 97

Mstahiki Meya wa Manispaa ya Songea, Abdul Hassan Mshaweji.
Na Albano Midelo,
Songea. 

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma imeendelea kufanya vizuri katika mtihani wa Taifa kidato cha sita, baada ya kufaulisha kwa asilimia 97.2.

Kwa mujibu wa matokeo hayo, shule tano za Serikali kidato cha sita wanafunzi ambao walipata daraja la kwanza ni 62 na kwamba kati yao wavulana ni 34 na wasichana ni 28.

Daraja la pili lina jumla ya wanafunzi 471 kati yao wavulana ni 174 na wasichana 297 ambapo daraja la tatu wapo jumla ya wanafunzi 507 kati yao wavulana ni 179 na wasichana 328.

Friday, October 6, 2017

WATUMISHI SONGEA WAPATA MAFUNZO YA KUANDAA BAJETI KWA MFUMO WA MTANDAO

Christopher Ngonyani mwezeshaji wa mafunzo ya kuandaa bajeti kwa mfumo wa mtandao akitoa elimu kwa watumishi wa halmashauri ya Manispaa ya Songea namna ya kutumia mfumo huo.
Watumishi wakiwa katika mafunzo ya mfumo wa kuandaa bajeti kwa njia ya kieletroniki. 
Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WATUMISHI 49 waliopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wamepata mafunzo ya siku tano ya Mfumo wa kieletroniki ambayo yatapunguza gharama za uendeshaji katika maandalizi, uwasilishaji na utekelezaji wa mipango ya bajeti mpya katika shughuli mbalimbali za halmashauri.

Mafunzo hayo yamefunguliwa juzi na Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Manispaa hiyo, Injinia Samwel Sanya katika ukumbi wa halmashauri hiyo uliopo mjini hapa.

Christopher Ngonyani ambaye ndiye mwezeshaji wa mafunzo hayo alisema kuwa mfumo huo mpya ambao umeanza kutumika rasmi hapa nchini kuanzia mwezi Septemba mwaka huu, utaweza kupunguza gharama za safari kwa Wakuu wa idara na wahasibu ndani ya halmashauri zote hapa nchini.

MILIONI 127 KUTUMIKA UJENZI WA DARAJA MATARAWE SONGEA

Upande wa kushoto, Mkuu wa wilaya ya Songea Palolet Mgema akitoa msisitizo juu ya ujenzi wa daraja la Matarawe alipofanya ziara yake juzi.
Na Mwandishi wetu,
Songea.

MKUU wa Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma, Palolet Kamando Mgema amefanya ziara ya kushitukiza kukagua ujenzi wa daraja la mto Matarawe lililopo katika Manispaa ya Songea mkoani humo.

Ziara hiyo imefanyika juzi ambapo daraja hilo limekuwa ni kiungo muhimu kwa wananchi wa Kata ya Matarawe, Mjimwema na kata nyingine jirani mjini hapa.

Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Songea Injinia Samwel Sanya alisema kuwa zaidi ya shilingi milioni 127 zimetengwa kwa ajili ya kazi ya kukamilisha ujenzi wa daraja hilo.

OFISI YA KATA MJIMWEMA SONGEA YAGHARIMU UJENZI WAKE MILIONI 25.5

Ofisi ya kata Mjimwema Songea.
Na Albano Midelo,
Songea.

MRADI wa ujenzi Ofisi ya Kata Mjimwema iliyopo katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma umegharimu shilingi milioni 25.56 ambapo ujenzi huo umetokana na fedha zilizotolewa na michango ya wananchi na serikali.

Afisa Mtendaji wa kata hiyo, Stan Kibiki alisema kuwa kati ya fedha hizo nguvu ya wananchi ni shilingi 556,000 na gharama ya serikali ni shilingi milioni 25.

Vilevile alisema mradi wa ujenzi ya ofisi hiyo ulianza tangu mwaka wa fedha wa 2012/2013 ambapo amezitaja shughuli ambazo zilifanyika katika kipindi hicho kuwa ni pamoja na kusafisha eneo la mradi, kujenga msingi na kunyanyua ujenzi wa jengo husika.

Wednesday, October 4, 2017

WIZARA YA AFYA YATOA TAHADHARI UWEPO UGONJWA WA TAUNI MADAGASCAR



Imeelezwa kuwa kati ya wagonjwa 104 walioripotiwa, 20 wamefariki dunia, ambapo taarifa iliyotolewa jana Jumanne na Ofisa Habari wa Wizara hiyo, Catherine Sungura imesema kuwa Shirika la Afya Duniani (WHO) limeeleza nchini Madagascar mikoa minane  imeripotiwa kuwepo wagonjwa ukiwemo mji mkuu wa nchi hiyo, Antananarivo.

Ugonjwa huo ulianza kuripotiwa Agosti 23 hadi Septemba 28 mwaka huu.

“Wengi walioripotiwa wameonyesha kuwa na uhusiano kwa njia moja au nyingine na mgonjwa wa kwanza jambo linalothibitisha yapo maambukizi ya ugonjwa wa tauni kati ya binadamu na binadamu.

Hivyo kwa mujibu wa WHO, ipo hatari ya wastani (Moderate risk) ya ugonjwa huo kusambaa katika nchi jirani na Madagascar,” imesema taarifa hiyo.

VITUO VYA ELIMU VISIVYOSAJILIWA SONGEA MARUFUKU KUTOA HUDUMA

Ofisi za Halmashauri Manispaa ya Songea.
Na Albano Midelo,
Songea.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea mkoani hapa, imewaandikia barua wamiliki wote wa vituo vya kutolea elimu yoyote bila kusajiliwa kuacha mara moja tabia hiyo, kwa kuwa ni kinyume cha sheria za nchi na endapo kutakuwa na mtu anafanya hivyo atachukuliwa hatua kali ikiwemo kufikishwa Mahakamani.

Idara ya elimu katika Manispaa hiyo imetoa agizo hilo juzi kwa Waratibu elimu kata wote waliopo kwenye Manispaa ya Songea kusimamia ipasavyo utekelezaji wake ambapo kuanzia mwezi uliopita Septemba mwaka huu imepigwa marufuku hairuhusiwi mmiliki wa shule au kituo chochote kile cha kutolea mafunzo ya tuition kutoa masomo bila kusajiliwa.

Imebainisha kuwa kumeibuka taasisi zisizokuwa rasmi na watu binafsi kuanzisha vituo vya elimu na kujitangaza kwa njia mbalimbali kwamba wanatoa masomo ya ngazi mbalimbali ya elimu kuanzia elimu ya chekechea, msingi, sekondari na vyuo.

WAZEE MANISPAA SONGEA WALIA NA MATIBABU

Eliezer Nyoni Mwenyekiti Baraza huru la wazee Manispaa ya Songea.
Na Albano Midelo,
Songea.

WAZEE katika Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma wameiomba Serikali kutatua kero ya kupata matibabu bure, ambayo inaongoza kwa wazee wa Manispaa hiyo hali ambayo inasababisha wengi wao kukosa matibabu.

Akisoma risala ya maadhimisho ya siku ya wazee duniani Oktoba Mosi mwaka huu, Makamu Mwenyekiti wa Baraza Huru la Wazee wa Manispaa ya Songea Sophia Hasara, alisema ni muhimu sasa kwa Serikali kuwapatia wazee hao kadi za matibabu bure kama ilivyoelekezwa hapo awali ili waweze kuondokana na kero hiyo pale wanapokwenda kupatiwa matibabu katika vituo vya serikali.

Hasara alisema kuwa kuna umuhimu kwa Manispaa hiyo kuharakisha mchakato wa upatikanaji wa kadi hizo kwa wazee wote ili kuweza kumaliza kero hiyo ambayo imedumu kwa muda mrefu na sasa inasababisha baadhi ya wazee kupoteza maisha kutokana na wakati mwingine wanashindwa kugharamia matibabu.

Monday, October 2, 2017

SHEIKH PONDA AINGILIA KATI SAKATA LA WATU WASIOJULIKANA

Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislam Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda amemkosoa Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robert Boaz akieleza kuwa vyombo vya ulinzi na usalama vimeshindwa kuchunguza matukio ya uhalifu yanayotokea nchini.

Akiwa nchini China kuhudhuria mkutano mkuu wa 86 wa Taasisi ya Polisi ya Kimataifa (Interpol), Boaz alikaririwa na gazeti moja la Serikali akisema kuwa vyombo vya ulinzi na usalama vina uwezo wa kuchunguza matukio ya uhalifu, yakiwamo mauaji na utekaji bila kusaidiwa na vyombo vya nje.

Hata hivyo, Sheikh Ponda aliyempigia simu jana mwandishi wetu, alisema kauli iliyotolewa na DCI haina ukweli.

WADAU MBINGA WATAKIWA KUCHANGIA MAENDELEO SHULE YA SEKONDARI MKINGA

Na Mwandishi maalum,      
Mbinga.

MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wazazi Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, Sostenes Nchimbi amewaomba Wadau mbalimbali waliopo wilayani humo kujitokeza kwa wingi na kuchangia maendeleo ya shule ya sekondari ya wazazi Mkinga iliyopo katika wilaya hiyo. 

Ombi hilo lilitolewa juzi na Mwenyekiti huyo wakati alipokuwa ametembelea shule hiyo huku akiwa ameambatana na viongozi wengine wa jumuiya hiyo kwa lengo la kujionea maendeleo yake na changamoto mbalimbali.

“Tumeingia madarakani kwa lengo la kuweza kuisaidia jamii iweze kusonga mbele kimaendeleo siku zote umoja ni nguvu utengano ni udhaifu, napenda kueleza kwamba nipo tayari kuunga mkono katika maendeleo ya shule hii”, alisema Nchimbi.