Saturday, February 27, 2016

DEREVA ASOMBWA NA MAJI WAKATI AKIOGA MTONI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

DEREVA mmoja wa kampuni ya Synohdryo, inayojenga barabara kiwango cha lami kutoka Tunduru mjini kwenda tarafa ya Nakapanya wilayani humo mkoa wa Ruvuma, amefariki dunia baada ya kusombwa na maji.

Dereva huyo ambaye hufahamika kwa jina la, Ally Ramadhani (31) mzaliwa wa  mkoa wa Tanga  alikumbwa na mkasa huo Februari 25 mwaka huu, majira ya saa 11.30 jioni wakati akiwa anaoga katika eneo la mto huo.

Taarifa za tukio hilo zinasema kuwa marehemu huyo alienda kuoga katika mto Muhuwesi, baada ya muda wa kazi kwisha na kwamba aliteleza na kutumbukia mtoni hatimaye kusombwa na mkondo mkali wa maji na kumpeleka kusikojulikana.

MKURUGENZI HALMASHAURI YA SONGEA ASIMAMISHWA KAZI KWA UBADHIRIFU



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MKURUGENZI  Mtendaji Halmashauri ya wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, Sixbert Valentine Kaijage amesimamishwa kazi, kwa sababu ya kushindwa kusimamia kikamilifu miradi ya maendeleo ya wananchi na kuisababishia serikali hasara kubwa kutokana na miradi husika katika wilaya hiyo, kutokamilika kwa wakati na kujengwa chini ya kiwango.

Benson Mpesaya ambaye ni Mkuu wa wilaya ya Songea, alisema kuwa Mkurugenzi huyo alienda kuaga Ofisini kwake na kusema kuwa amepewa barua kutoka Wizarani, juu ya kusimamishwa kazi ili apishe uchunguzi kuanzia siku ya Jumatano Februari 24 mwaka huu.
Sixbert Valentine Kaijage.

Mpesya alifafanua kuwa kwa mujibu wa sheria ya utumishi wa umma, mtumishi yeyote akibainika kufanya ubadhirifu au kukiuka taratibu za kiutumishi anasimamishwa kazi hadi pale uchunguzi utakapokamilika na endapo akibainika kuwa amehusika katika tuhuma zinazomkabili, huchukuliwa hatua za kisheria kwa mujibu wa kanuni za utumishi wa umma.

Aidha baadhi ya Madiwani ambao waliomba majina yao yasitajwe, walisema katika vikao vya baraza la madiwani katika Halmashauri hiyo walibaini kuwepo kwa ubadhirifu wa fedha katika miradi ya maji, barabara na ujenzi wa majengo.

ITS MY FAULT SASA IPO SOKONI WADAU WATAKIWA KUUNGA MKONO




Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

KWA mara ya kwanza vijana waigizaji kutoka wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wameweza kutoa filamu yao mpya yenye picha kali ambayo inatamba mtaani kwa jina la “IT’S MY FAULT” hivyo wadau mbalimbali, wametakiwa kukaa mkao wa kula na kuipokea albamu hiyo kwa kuendelea kuwaunga mkono wasanii hao kwa kazi hiyo waliyoifanya.
Erick Kapinga.

Filamu hiyo imebeba maudhui mazuri, yenye kulenga kuelimisha jamii ikiwa na picha nzuri zenye ubora unaokubalika.

Kazi kubwa ya ‘Production’ ya filamu hiyo, imefanywa na kijana mmoja maarufu mkazi wa Mbinga mjini anayefahamika kwa jina la Erick Kapinga, akishirikiana na timu ya vijana wenzake  kadhaa.

Vijana hao kwa ujumla wameweza kuanzisha kampuni yao ya filamu inayotambulika kwa jina la, Amaizing Films Company (AFC) iliyopo mjini hapa.

Friday, February 26, 2016

SONGEA NA MADABA WAPONGEZWA KUGAWANA MALI BILA MVUTANO



Na Stephano Mango,
Songea.

MADIWANI wa Halmashauri ya wilaya ya Songea na Madaba mkoani Ruvuma, wamepongezwa kwa kuridhia mgawanyo wa mali kwa pande zote mbili, bila kuwepo na mvutano kama ilivyo kwa baadhi ya halmashauri zingine mkoani humo.

Pongezi hizo zilitolewa na Katibu tawala wa mkoa huo, Hassan Bendeyeko alipokuwa akizungumza  kwenye kikao maalumu cha baraza la madiwani wa halmashauri ya wilaya ya Songea na Madaba kilichokuwa kikijumuisha mgawanyo wa mali, rasilimali na madeni kilichofanyika mjini hapa.

Bendeyeko alisema kuwa madiwani wa halmashauri hizo mbili, wanapaswa kuwa mfano wa kuigwa na halmashauri zingine mkoani humo na kuwataka kuendeleza zaidi mahusiano na kuheshimu makubaliano waliyotiliana sahihi, kwenye mkataba wa mgawanyo wa mali hizo.

HALMASHAURI MJI WA MBINGA YAAZIMIA KUNUNUA MTAMBO WA KUSAGA TAKA




Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

HALMASHAURI ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, imeazimia kununua mitambo maalum ya kusaga takataka, ili kuondokana na hatari ya kukumbwa na magonjwa ya milipuko yanayotokana na uchafu ikiwemo kipindupindu.

Akizungumza katika kikao cha baraza la Madiwani, Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri hiyo Oscar Yapesa alisema kuwa takataka hizo pia zitakuwa zikisagwa kwenye mitambo hiyo, na kutumika kama mbolea kwenye mashamba ya wakulima.
Oscar Yapesa.

Kadhalika Mkurugenzi huyo alisema kwamba, wanakabiliwa na changamoto ya gari la kuzoa taka hizo ambapo hivi sasa wanagari moja tu ambalo halitoshelezi mahitaji halisi.

Naye Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Ngaga kwa upande wake aliwataka Madiwani hao kuhakikisha wanawaelimisha wananchi ya juu ya utunzaji wa mazingira, ili kuepukana na ugonjwa huo wa kipindupindu.

Kwa ujumla Halmashauri ya mji wa Mbinga, inazalisha takataka tani 18 kwa siku na ina uwezo wa kuzoa tani tatu tu kwa siku jambo ambalo linatishia afya za wakazi wa mji huo, wakihofia kukumbwa na magonjwa ya mlipuko yanayotokana na uchafu.

Thursday, February 25, 2016

HALMASHAURI YA MBINGA VIJIJINI NA MJINI WAGAWANA MALI


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KATIBU Tawala mkoa wa Ruvuma, Hassan  Bendeyeko ameziagiza Halmashauri za wilaya ya Mbinga vijijini na mjini zilizopo katika wilaya ya Mbinga mkoani humo, kuhakikisha kwamba zinakamilisha mchakato wa kugawana mali, rasilimali na madeni kwa kufuata miongozo ya serikali, kama ilivyokubaliwa katika mkutano wa baraza la Madiwani. 

Aidha Bendeyeko alitoa onyo kali akisema, hataki kusikia Halmashauri mama ya Mbinga vijijini inaleta vikwazo kwamba, haitaki kutoa rasilimali husika kwa ajili ya kuendeshea Halmashauri mpya ya Mbinga mjini na endapo Ofisi yake itapata taarifa kama kutakuwa na mfarakano juu ya jambo hilo, yupo tayari kumchukulia hatua kali za kinidhamu Mkurugenzi atakayeonekana anakiuka taratibu na makubaliano ya mkutano huo.
Madiwani wakiwa katika mkutano huo wa kugawana mali.

Rai hiyo ilitolewa jana na Katibu tawala huyo, ambaye pia ni Mwenyekiti anayesimamia mgawanyo wa mali katika halmashauri hizo mbili, kwenye kikao maalum cha baraza la Madiwani, kilichoketi ukumbi wa Jimbo kuu Katoliki la Mbinga uliopo mjini hapa.

“Kuanzia sasa mali zote zianze kugawanywa kwenda halmashauri mpya, lengo la serikali tunataka kazi za kuwatumikia wananchi zianze mara moja, tusipofanya maamuzi sahihi halmashauri hii mpya ya Mbinga mjini haitaweza kutekeleza majukumu yake”, alisema Bendeyeko.

Wednesday, February 24, 2016

MKURUGENZI WA HALMASHAURI YA KONDOA HUSSEIN NGAGA AKALIA KUTI KAVU

Hussein Issa Ngaga, Mkurugenzi mtendaji Halmashauri ya wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma.


Na Dany Tibason,
Dodoma.

SELEMAN JAFO, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) amebaini upotevu wa shilingi milioni 180 katika Halmashauri ya wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma.

Kutokana na kubainika kwa upotevu wa fedha hizo, Jafo ametoa masaa 48 kwa Hussein Issa Ngaga ambaye ni Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo, ahakikishe anapeleka maelezo ya kina katika Ofisi ya TAMISEMI juu ya kuibiwa kwa fedha hizo ambazo ni za walipakodi Watanzania.

Agizo hilo la Naibu Waziri huyo, lilitokana na ziara yake ya kikazi aliyoifanywa jana sambamba na kufanyika kwa kikao cha ndani, katika Halmashauri hiyo.

Alisema kuwa, serikali ya awamu ya tano haitavumilia kiongozi yeyote ambaye atafanya ubadhirifu wa fedha za umma au jambo lolote ambalo linaonekana kuwepo na harufu ya ufisadi.

Tuesday, February 23, 2016

BARAZA LA MADIWANI HALMASHAURI MJI WA MBINGA LA PITISHA RASIMU YA BAJETI SHILINGI BILIONI 33.4



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

HALMASHAURI ya Mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, katika rasimu yake ya bajeti ya mwaka 2016/2017 inatarajia kukusanya na kutumia kiasi cha shilingi bilioni 33.4 kwa ajili ya utekelezaji na kuboresha, shughuli mbalimbali za maendeleo ya wananchi wa mji huo.

Katika fedha hizo shilingi bilioni 17.8 zinalenga kulipa mishahara ya wafanyakazi wake, bilioni 2.2 matumizi mengineyo, bilioni 12.3 ni fedha za utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

Oscar Yapesa, Mkurugenzi mtendaji Halmashauri ya mji wa Mbinga.
Aidha imekisia kukusanya na kutumia shilingi bilioni 1.7 ambazo ni fedha zitakazotokana na makusanyo ya ndani, katika halmashauri ya wilaya hiyo. 

Hayo yalisemwa na Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri hiyo, Oscar Yapesa alipokuwa akiwasilisha umbile la makisio hayo ya matumizi ya fedha katika rasimu ya bajeti, kwa mwaka wa fedha wa 2016/2017.

Yapesa alikuwa akiiwasilisha leo kwenye kikao cha kawaida, cha baraza la Madiwani kilichoketi kwenye ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa.

ASKOFU MKUU JIMBO LA MBINGA AWATAKA WATENDAJI WA SERIKALI KUENDANA NA KASI YA UTAWALA WA MAGUFULI

Na Kassian Nyandindi,

Mbinga.

ASKOFU Mkuu wa Jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma, John Ndimbo ameeleza kuwa Watendaji waliopo katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani humo, wametakiwa kuwa tayari kupokea majukumu yanayoendana na nafasi walizonazo ikiwemo, kasi ya utawala wa serikali ya awamu ya tano kwa manufaa ya jamii na Taifa kwa ujumla.

“Kumbukeni, vigezo vya Rais wetu John Magufuli anavyovitaka katika nchi yetu ili iweze kusonga mbele ni kuwa wazalendo kwa mali zetu, kwa manufaa ya wananchi”, alisema Ndimbo.

Askofu John Ndimbo.
Kadhalika alibainisha kuwa viongozi wanapopanga mambo ya kimaendeleo, wanapaswa kushirikisha watu waliopo katika eneo husika na sio kufanya peke yao kwa kukaa mezani na kutengeneza mambo ambayo siku ya mwisho, yamekuwa yakileta kero na kuzua migogoro isiyokuwa na tija.

Askofu Ndimbo alieleza hayo jana alipokuwa akihutubia kwenye kikao cha baraza la Madiwani wa Halmashauri ya mji wa Mbinga, lililofanyika mjini hapa katika ukumbi wa Umati huku akiongeza kuwa kiongozi ambaye hatimizi majukumu yake ipasavyo, anapaswa kujiondoa mapema kabla ya kutokea madhara kwa watu anaowatawala.

Pia alitolea mfano kwa kueleza kwamba, kuna baadhi ya watendaji wa vijiji na kata ambao wamepewa dhamana ya kuongoza wananchi katika maeneo yao wamekuwa hawatekelezi na kufuata taratibu za nchi kama zinavyotaka, hivyo alishauri wachukuliwe hatua mapema ili iwe fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo.

Monday, February 22, 2016

WATAKAO HUJUMU VIFAA VYA KUTENGENEZA MADAWATI TUNDURU KUKIONA CHA MOTO



Na Steven Augustino,
Tunduru.

IMEELEZWA kuwa watu watakaojaribu kuhujumu malighafi au vifaa vya kutengenezea madawati, kwa ajili ya matumizi ya wanafunzi shuleni wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, watachukuliwa hatua kali za kisheria ikiwemo kufikishwa Mahakamani.

Walimu, mafundi na wananchi wameonywa na wametakiwa kuondokana na mawazo hayo, badala yake wanapaswa kujenga ushirikiano kwa umoja wao ili kazi hiyo ya utengenezaji wa madawati iweze kukamilika kwa wakati.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa.
Onyo hilo limetolewa na Mkuu wa wilaya ya Tunduru, Agnes Hokororo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake juu ya maendeleo ya wilaya hiyo, huku akisisitiza kuwa utaratibu huo hautachakachuliwa vinginevyo endapo litatokea tatizo ameunda kikosi kazi na kamati inayofuatilia suala hilo ili kila dawati, liweze kukamilika na kukabidhiwa shuleni kwa ajili ya kuanza kutumika.

"Ofisi yangu imejipanga kikamilifu katika usimamizi wa zoezi hili, nimeunda kikosi kazi na kuteua kamati zinazosimamia ili kudhibiti uchakachuaji wowote unaoweza kujitokeza, wakati wa utekelezaji wa jambo hili", alisema Hokororo. 

Hokororo alisema hayo wakati alipokuwa akijibu pia tuhuma, juu ya uwepo wa taarifa kwamba wapo baadhi ya mafundi wanaoshirikiana na watu wasiokuwa waaminifu, kuhujumu juhudi za maendeleo ya utengenezaji wa madawati ya kukali wanafunzi wilayani humo.

JELA MIEZI 12 KWA KUKUTWA NA NYARA ZA SERIKALI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

MKAZI mmoja wa kijiji cha Chiungo wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, Rashid Selemani (41) amehukumiwa kwenda jela kutumikia kifungo cha miezi 12, baada ya kupatikana na hatia katika makosa matatu yaliyokuwa yakimkabili.

Hukumu hiyo ilitolewa na Hakimu mfawidhi wa Mahakama ya wilaya ya Tunduru, Gradys Barthy baada ya Mahakama hiyo, kujiridhisha na ushahidi uliotolewa na upande wa mashtaka.

Awali akisoma mashtaka hayo mbele ya Hakimu huyo, Mwendesha mashtaka mkaguzi msaidizi wa Polisi Inspekta Songelaele Jwagu alisema mtuhumiwa huyo ambaye alikuwa anakabiliwa na makosa matatu, kosa la kwanza  bila halali alipatikana na nyara za serikali, kinyume na kifungu namba 86 (1) na kifungu cha 2 (b) cha sheria ya kuhifadhi wanyamapori namba 5 ya mwaka 2009. 

Akifafanua maelezo ya kosa hilo, alisema mnamo Juni 27 mwaka jana majira ya mchana katika hifadhi ya Mwambesi wilayani Tunduru mkoani hapa, mshitakiwa huyo alikamatwa akiwa na nyama ya ngorombwe, ngozi na nyama ya sungura bila kibali.

MKUU WA WILAYA YA MBINGA AWATAKA MADIWANI HALMASHAURI YA MJI WA MBINGA KUTEKELEZA MAJUKUMU YA WANANCHI



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MADIWANI katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, wametakiwa kuondoa itikadi zao za vyama vya kisiasa na kutekeleza majukumu ya kufanya kazi kwa umoja wao, ambayo yataleta manufaa kwa wananchi wanaowazunguka katika maeneo yao.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa wilaya hiyo, Senyi Ngaga alipokuwa akitoa salamu za serikali katika kikao cha baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo, kilichofanyika leo kwenye ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa.

“Hatuna sababu hivi sasa kuendeleza malumbano ya kisiasa, Madiwani tunapaswa kufanya kazi za wananchi mambo ya vyama wekeni pembeni, kuendelea kulumbana hakutatufikisha mbali”, alisema Ngaga.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Simon Ngaga.
Aidha Mkuu huyo wa wilaya, akizungumzia suala la maendeleo katika sekta ya elimu aliwataka pia madiwani hao katika mipango yao wafikirie kujenga majengo mapya ya shule za msingi na sekondari, ili waweze kuwa na shule ambazo zitaweza kutosheleza mahitaji ya watoto waliopo sasa.

Ngaga alisema kuwa licha ya Halmashauri ya mji wa Mbinga, kuwa na upungufu wa madarasa ya kusomea wanafunzi, pia inakabiliwa na tatizo kubwa la uhaba wa madawati ya kukalia watoto hao.

Saturday, February 20, 2016

BENKI YA POSTA TANZANIA YAPONGEZWA KWA KUKARABATI VYOO VYA SHULE YA MSINGI MAKAMBI SONGEA


Ofisa uhusiano wa Benki ya Posta Tanzania, Noves Mosses   akifanya ufunguzi na makabidhiano ya vyoo vya shule ya msingi Makambi iliyopo Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma. Ofisa huyo alisema kuwa  benki  hiyo imekuwa ikiunga mkono juhudi zinazofanywa na wananchi na serikali kwa ujumla katika kutatua changamoto mbalimbali kwenye sekta ya elimu, afya na ustawi wa jamii.
Na Kassian Nyandindi,

Songea.

BENKI ya Posta Tanzania (TPB), imepongezwa kwa hatua iliyochukua ya kufanya ukarabati wa vyoo vya wanafunzi wanaosoma shule ya msingi Makambi, iliyopo katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma.
Wanafunzi shule ya msingi Makambi, wakifurahia.

Ukarabati huo uliofanywa, umeelezwa kuwa ni msaada mkubwa kwa watoto hao na kwamba itasaidia waweze kuwa na vyoo bora na kuepukana na magonjwa mbalimbali.
Shule ya msingi Makambi ina wanafunzi 850, ambapo imepata ufadhili wa kukarabatiwa vyoo hivyo, vyenye matundu 12 kwa thamani ya shilingi milioni 4.7. 

Ofisa uhusiano wa Benki ya Posta hapa nchini, Noves Mosses amekabidhi vyoo hivyo  kwa Mwalimu mkuu msaidizi  wa shule hiyo, Kanisius Ngongi baada ya kukamilika ukarabati wake.

Wanafunzi wa shule hiyo wamefurahia kukarabatiwa kwa vyoo hivyo, ambapo awali walisema kuwa walikuwa wakitumia choo kimoja wanafunzi wengi jambo ambalo lilikuwa ni hatari kwao kwa maambukizi ya magonjwa mbalimbali, hasa kwa watoto wa kike.

WANANCHI WATAKIWA KUJIKINGA NA MAGONJWA YALIYOSAHAULIKA

Wakurugenzi na viongozi wa kutoka katika Halmashauri za mkoa wa Ruvuma, wakishiriki semina ya kampeni ya kumeza vidonge kwa magonjwa yaliyosahaulika mjini Songea.
Na Mwandishi wetu,

Songea.

WANANCHI wanaoishi katika mkoa wa Ruvuma na nje ya mkoa huo, wametakiwa kujikinga kwa kujenga mazoea ya kumeza dawa, ambazo huzuia kuenea kwa magonjwa yaliyosahaulika.
 
Imeelezwa kuwa endapo watazingatia hilo, wataweza kuepukana na magonjwa ya matende, usubi, kichocho, trakoma na minyoo.

Mratibu wa magonjwa hayo hapa nchini, Dkt. Edward Kirundi aliyasema hayo mjini hapa na kuongeza kuwa magonjwa hayo  yanatibika, na kwamba jambo muhimu kila mtu anapaswa kuzingatia tiba au kinga.

Vilevile alisisitiza kwa kuitaka jamii hapa nchini, kushiriki kikamilifu katika kampeni ya kutokomeza magonjwa hayo na wataalamu wa afya wazingatie kutoa elimu sahihi kwa wananchi, ili kuifanya jamii iweze kuwa na uelewa juu ya madhara yatokanayo na magonjwa hayo.