Saturday, February 20, 2016

DAVINA MAKETTA AITAKA JAMII KUWAJALI WATU WENYE ULEMAVU



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

JAMII hapa nchini, imetakiwa kuacha tabia ya kuwatumikisha watoto wadogo kwa kuwapa ajira ambazo zinawarudisha nyuma kimaendeleo, badala yake ihakikishe inawapa  ulinzi na haki zao za msingi sambamba na kuwapeleka shule ili waweze kusonga mbele kimaendeleo.

Rai hiyo ilitolewa na Ofisa ustawi wa jamii wilaya ya Mbinga, Davina Maketta anayeshughulikia kitengo cha watu wenye ulemavu wilayani humo, alipokuwa akifungua kongamano la kupinga ukatili kwa wanawake na watoto walio chini ya umri wa miaka mitano, ambalo liliandaliwa na Chama Cha Walemavu Tanzania (CHAWATA) tawi la Mbinga wilayani humo.

Alifafanua kuwa ni kweli hivi sasa jamii inakabiliwa na wimbi kubwa la  ongezeko la watoto wa mitaani, linalotokana na yenyewe kushindwa kuwapatia mahitaji muhimu, hata hivyo inatakiwa isitumie nafasi hiyo kuwakandamiza watoto  hao kwa kuona kama ni watu wasiostahili kuishi vizuri kama wenzao.

Mbali na  agizo hilo, Maketta amewataka wazazi wilayani humo kujiepusha  kuzaa watoto wengi kwa kuwa huchangia kutowapatia mahitaji  yao ya msingi na matokeo yake wazazi mwisho wa siku, hujikuta wakielemewa na mzigo mkubwa wa  kutunza  watoto hao jambo  ambalo pia linasababisha ongezeko la kaya maskini kwa baadhi ya familia zenye idadi kubwa ya watoto.


Kwa mujibu wa takwimu zilizopo wilayani Mbinga, inakadiriwa kuwa na watoto zaidi ya 100 wa mitaani wenye umri kuanzia miaka  saba hadi 18 wanaoishi katika mazingira magumu, bila ya uangalizi  mzuri wa wazazi wao mbali na wale waliopelekwa katika vituo vya kulelea watoto yatima na wenye mahitaji maalumu.

Maketa alisema kwamba uzazi wa mpango, unasaidia kupata idadi ndogo ya watoto ambao wazazi na walezi watakuwa na uwezo wa kuwahudumia kwa kuwapatia mahitaji ya lazima, lakini hali hiyo ni tofauti  kwa familia zenye watoto wengi.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa CHAWATA tawi la Mbinga wilayani humo, Martin Mbawala ametoa wito kwa jamii kuhakikisha kwamba inasaidia kutoa uangalizi wa kutosha kwa watoto wanaozagaa hovyo mitaani, badala ya kuwanyanyapaa na kuwaita majina mabaya ambayo yanasababisha watoto hao mwisho wa siku, kuathirika kisaikolojia na kuamua kushiriki katika matendo maovu.

Mbawala alieleza kuwa kuna baadhi ya watu wamekuwa ni chanzo cha kuongezeka kwa watoto wa mitaani, wanapowaona badala ya kuwaita  ili kufahamu chanzo cha tatizo walilonalo huishia kuwapa manyanyaso na kuwaita majina ambayo hayapendezi hata kidogo kuitwa binadamu.

No comments: