Monday, September 30, 2013

KAMPUNI YA BAM YAPONGEZWA KWA KAZI YA USAMBAZAJI WA PEMBEJEO ZA KILIMO MKOANI RUVUMA

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Juma Simai, akifungua jengo(Ghala) la kampuni ya BAM ambalo hutumika kuhifadhia pembejeo za kilimo.

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru, Juma Simai akiwa ndani ya ghala la kuhifadhia pembejeo, akisisitiza jambo mara baada ya kupokea taarifa ya maendeleo ya kampuni ya BAM juu ya usambazaji wa pembejeo za kilimo mkoani Ruvuma.

Uongozi wa kampuni ya BAM ukiwa katika picha ya pamoja na kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Juma Simai.(aliyeshika Mwenge)

Hizi ni moja kati ya pembejeo za kilimo ambazo husambazwa na kampuni ya BAM kwa wakulima mkoani Ruvuma.

Mkurugenzi mkuu wa BAM, Bernad Malila. (Picha zote na Kassian Nyandindi)



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KIONGOZI wa mbio Mwenge  wa Uhuru Juma Simai ameipongeza kampuni ya BAM (LTD) inayojishughulisha na usambazaji wa pembejeo za kilimo katika maeneo mbalimbali ya mkoa wa Ruvuma, kutokana na kuwa na mipango thabiti inayolenga kupanua shughuli za kilimo na kuongeza uzalishaji wa chakula hapa nchini hatua ambayo inaweza kuinua uchumi wa wakulima na nchi kwa jumla.

Simai alitoa pongezi hizo hivi karibuni mjini  Mbinga, wakati akifungua jengo la ghala la kuhifadhi pembejeo za kilimo lenye uwezo wa kuhifadhi zaidi ya tani 600 za mbolea aina mbalimbali na kuiagiza serikali ya wilaya ya Mbinga, kuunga mkono juhudi kubwa iliyoonyeshwa na kampuni hiyo kwani inalenga kuwakomboa na kuwasaidia wakulima.

Alisema iwapo viongozi watashirikiana na BAM katika mkakati wa kitaifa wa kukifanya kilimo kiwe ni kati ya maeneo makubwa ya kiuchumi, kuna uwezekano mkubwa wa wilaya hiyo kupiga hatua za haraka za maendeleo kufuatia kuwepo kwa eneo kubwa la ardhi inayofaa kwa ajili ya shughuli za kilimo ikilinganishwa na maeneo mengine hapa nchini.

Alieleza kuwa kitendo cha kampuni hiyo kupunguza bei za pembejeo ni faraja kubwa siyo kwa wakulima pekee, bali hata kwa serikali kwani nayo imepania kukifanya kilimo kiwe ni eneo lingine la kibiashara zaidi kwa kuajiri maafisa ugani wengi na kupunguza ruzuku na kodi katika vifaa vya kilimo, hivyo ni vyema kila mmoja wakiwemo viongozi kushiriki na kuiunga mkono kampuni hiyo ambayo  imeleta unafuu mkubwa kwa wakulima wa wilaya ya Mbinga, mkoa na taifa kwa ujumla.

“Viongozi wa Mbinga, wapeni ushirikiano hawa watu  wanaokuja  kuleta maendeleo hapa wilayani kwenu, narudia kulisema hili kwa sababu viongozi katika maeneo mengi tumekuwa watu wa kujisahau sana, hakuna maendeleo ya kweli yanayokuja bila ya kushirikiana na wadau”, alisema Simai.

Awali akitoa taarifa ya kampuni hiyo Meneja mkuu wa kampuni ya BAM Suzo Komba alieleza kuwa lengo  kubwa la mradi huo ni kuleta huduma za usambazaji wa pembejeo kwa wakulima wakubwa na wadogo katika maeneo ya karibu zaidi mkoani Ruvuma,  ili kuwarahisishia upatikanaji wa pembejeo na mahitaji mengine ya wakulima badala ya kutembea umbali mrefu kufuata pembejeo za kilimo.

Komba alitaja walengwa wakuu katika mpango huo ni wakulima wa mazao ya mahindi, kahawa, mpunga na mazao mengine ya chakula na biashara ambayo kwa kiasi kikubwa yanazalishwa katika wilaya ya Mbinga na kuwa na kituo kikubwa  cha usambazaji na kitakacholinda ubora wa mbolea zitakazouzwa kupitia kampuni  hiyo.


Alisema hadi sasa kampuni hiyo imeweza kujenga ghala kubwa la kuhifadhia mbolea ambalo limegharimu zaidi ya shilingi milioni 235.7 fedha ambazo zimetokana na mfuko wa kampuni hiyo kutokana na faida kidogo wanazopata baada ya kuuza pembejeo za kilimo, wanazozisambaza na kwamba aliishukuru serikali chini ya wizara ya kilimo na chakula kwa ushirikiano mkubwa wanaouonyesha kwa wasambazaji wa pembejeo za kilimo.



MAPENDEKEZO YA WILAYA TATU YASABABISHA MVUTANO KATI YA MADIWANI NA WATAALAMU


Na Steven Augustino,
Tunduru.

BARAZA la Madiwani katika Halmashauri ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, limepitisha mapendekezo ya uundwaji wa mji mdogo, mgawanyo wa eneo la utawala na kuridhia kuundwa kwa mkoa mpya utakaoziunganisha wilaya ya hiyo na Namtumbo.

Mapendekezo hayo yalipitishwa katika kikao maalum kilichoketi kwenye ukumbi wa Klasta mjini humo, na kwamba Madiwani hao walifikia makubaliano hayo  baada ya majadiliano ya muda mrefu ambapo awali, baadhi yao walipendekeza uwepo wa mgawanyiko wa Wilaya mbili wakilenga kusogeza huduma na kuharakisha maendeleo kwa wananchi.

Kwa mujibu wa mapendekezo hayo ambayo yalionekana kutoendana na mapendekezo ya wataalamu ambao walienda na mapendekezo ya mgawanyo wa wilaya mbili, Wilaya ya kwanza walitaka iundwe na tarafa za Matemanga na Nampungu wilaya ya pili iundwe na tarafa za Nakapanya, Mlingoti na Namasakata na wilaya ya tatu  nayo ikitajwa kuundwa na tarafa za Nalasi na Lukumbule.

Akifafanua maelezo ya mgawanyo huo Diwani wa kata ya Ligunga Kazembe Said alisema kuwa, kutakuwa na faida mbalimbali kwani katika kupatikana kwa wilaya hizo tatu kutapanua huduma na kuiwezesha serikali kufikisha huduma kwa wananchi wake kwa haraka, na kuyafikia malengo husika iliyojipangia kuwafikia wananchi wake ifikapo 2020 na kwamba  endapo watapendekeza mgawanyo wa  wilaya mbili watakuwa wameshiriki kulitenga eneo kubwa ambalo bado litakuwa  halifikiwi wa uirahisi kiutawala.

Tuesday, September 24, 2013

MAKABIDHIANO YA MWENGE WA UHURU LIGANGA: KIONGOZI WA MBIO HIZO KITAIFA, AWATAKA WANAFUNZI KUZINGATIA MASOMO

Msafara wa Mwenge wa Uhuru ukiwasili katika kijiji cha Liganga wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, tayari kwa makabidhiano ukitokea wilayani Mbinga.

 Mwenge wa Uhuru ukipelekwa katika eneo maalum, kwa ajili ya maandalizi ya kukabidhiwa wilaya ya Songea.

Wanafunzi wa shule ya Msingi Liganga, wakiwa wameshika mabango yenye ujumbe wa aina mbalimbali wa mbio za Mwenge wa Uhuru.


Burudani ngoma za asili, nazo hazikuwa nyuma katika kijiji cha Liganga.

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Juma Alli Simai, akizungumza na wanafunzi wa shule ya msingi Liganga ambapo aliwasisitiza watoto hao, kuzingatia masomo wanapokuwa shuleni.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga(aliyeshika Maiki) akizungumza jambo wakati akiwa katika hatua ya kumkabidhi kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa Juma Alli Simai (aliyekuwa upande wa kushoto) kwenda wilaya ya Songea, kwa ajili ya kuendelea na mbio hizo mkoani Ruvuma. Upande wa kushoto ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi wilayani Mbinga Christantus Mbunda.

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Juma Alli Simai, akiveshwa Skavu baada ya Mkuu wa wilaya ya Mbinga kumkabidhi kwa wananchi wa wilaya ya Songea.


Mkuu wa wilaya ya Songea Joseph Mkirikiti, akikumbatiana na kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa mara baada ya kukamilika kwa zoezi la kuveshwa Skafu, ikiwa ni ishara ya kukaribishwa kwa kiongozi huyo wa kitaifa wilaya ya Songea.

Senyi Ngaga Mkuu wa wilaya ya Mbinga, akitoa heshima(maelezo) kabla ya kuukabidhi Mwenge wa Uhuru kwa Mkuu wa wilaya ya Songea.

Mkuu wa wilaya ya Songea Joseph Mkirikiti, akiwa ameushika Mwenge wa Uhuru mara baada ya kukamilika kwa makabidhiano kutoka kwa Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Ngaga ambaye ameonyesha mgongo(amevaa trakisuti nyeusi)

Tayari Mwenge wa Uhuru ukiwa katika eneo maalum, kwa ajili ya kuendelea na mbio zake wilayani Songea mkoa wa Ruvuma. (Picha zote na Kassian Nyandindi)


Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

HATIMAYE Mwenge wa Uhuru uliokuwa ukiendelea kufanya kazi zake wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, sasa umemaliza kazi husika salama na kukabidhiwa leo kwa uongozi wa wilaya ya Songea.

Makabidhiano hayo yamefanyika katika kijiji cha Liganga wilayani humo, ambapo Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga alifanya kazi ya kumkabidhi kiongozi mwenzake ambaye ni Mkuu wa wilaya ya Songea Joseph Mkirikiti.

Wakati makabidhiano hayo yakifanyika kijijini hapo shamra shamra na burudani za hapa na pale, zilikuwa zikiendelea kutolewa ambapo vikundi vya ngoma za asili navyo havikuwa nyuma, katika makabidhiano hayo.

Kiongozi wa mbio hizo za Mwenge wa Uhuru kitaifa,  Juma Alli Simai naye hakuwa mbali katika kutoa ujumbe wa mbio hizo, ikiwemo lile la kuwataka Watanzania kuendelea kuheshimu, kulinda amani na utulivu huu tulionao.

Pamoja na mambo mengine Simai pia alisisitiza kwa wazazi kuhakikisha watoto wao wanawapeleka shule, na sio kuwaacha majumbani.

Alisema jukumu la mzazi kumpeleka mtoto shule ni jambo la lazima na sio hiari, hivyo linapaswa kuzingatiwa wakati wote kwa kuhakikisha pia mtoto husika anapata mahitaji yake muhimu, awapo shuleni.

Mwenge wa Uhuru wilayani Mbinga, umeweza kufanya kazi kwenye miradi 11 yenye jumla ya thamani ya shilingi bilioni 1,061,881,200.

Monday, September 23, 2013

WATANZANIA WATAKIWA KUWABEZA NA KUEPUKA VIONGOZI WANAOTUMIA MAJUKWAA KUVURUGA AMANI YA NCHI YETU

Kikundi cha Ngoma aina ya Mganda kikitumbuiza mara baada ya Mwenge wa Uhuru, kuwasili katika kijiji cha Mpapa wilayani Mbinga.

Mwenge wa uhuru mara baada ya kuwasili ukitokea wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, ukipelekwa katika eneo maalum tayari kwa maandalizi ya makabidhiano kwa wilaya ya Mbinga mkoani humo.

Mkuu wa wilaya ya Nyasa(Aliyeshika maiki) Ernest Kahindi, akizungumza, kutambulisha/kukabidhi wageni waliokuwa wakikimbiza Mwenge kwa ngazi ya kitaifa, mkoa na wilaya hiyo.

Senyi Ngaga Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, akisalimiana na Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Juma Ally Simai wakati wa utambulisho na makabidhiano ya viongozi wa mbio za mwenge kitaifa mara baada ya mwenge huo ukitokea wilayani Nyasa.

Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa, Juma Ally Simai akisalimiana na Mwenyekirti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Mbinga, Christantus Mbunda.

Mkuu wa wilaya ya Nyasa Ernest Kahindi, akijiandaa kuukabidhi Mwenge wa Uhuru kwa Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga akiupokea Mwenge wa uhuru kutoka kwa Mkuu wa wilaya ya Nyasa Ernest Kahindi. (Picha zote na Kassian Nyandindi)


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WATANZANIA wametakiwa kuwabeza, kuepukana na Viongozi wa dini au siasa  ambao hutumia majukwaa kuhutubia wananchi, kwa nia ya kuchochea maneno yenye kujenga kuvuruga amani iliyopo hapa nchini, badala yake wawe na mshikamano, upendo na utulivu ili kuimarisha amani hiyo isiweze kuvurugika.

Rai hiyo iliotolewa na Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa Juma Ally Simai, alipokuwa akitoa ujumbe wa Mwenge huo wakati akizungumza na baadhi ya wananchi wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, katika kijiji cha Mpapa kata ya Mpapa wilayani humo.

Simai alitoa kauli hiyo mara baada ya kumaliza kufanya makabidhiano ya Mwenge huo kijijini hapo, ambapo awali msafara wa mwenge ulikuwa ukitokea katika wilaya mpya ya Nyasa mkoani humo.

 “Ndugu zangu amani ndio msingi mkuu wa maendeleo, kwa umoja wetu tulionao tuendelee kuudumisha tuachane na mambo ya itikadi za kisiasa au dini, sisi sote ni wa moja”

“Tuepukane na viongozi wa dini au siasa wenye nia mbaya ya kuvuruga umoja huu, taifa letu halikujengwa kwa misingi ya kiubaguzi”, alisisitiza Simai.

Thursday, September 19, 2013

BALOZI WA PAPA AWATAKA WAKRISTO KUTOJIINGIZA KATIKA MACHAFUKO

Kanisa la Mtakatifu Killian lililopo Mbinga mjini mkoani Ruvuma.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma Senyi Ngaga, naye hakuwa mbali katika kushiriki maadhimisho ya misa takatifu ya kuwapaka watoto mafuta ya Kipaimara.

 Balozi wa Papa nchini Askofu mkuu Francisco Montecillo Padilla, akiendelea na maadhimisho ya misa katika Kanisa la Mtakatifu Killian lililopo Mbinga mjini mkoani Ruvuma. (Picha zote na Kassian Nyandindi)


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WAUMINI wa dhehebu la Kikristo, wameshauriwa kutojiingiza katika matukio yenye kuhatarisha na kuvuruga amani ya nchi yetu, na badala yake waungane kwa pamoja kupinga matukio maovu yanayoendelea kutokea katika maeneo mbalimbali hapa nchini.

Wito huo ulitolewa na Balozi wa Papa hapa nchini, Askofu mkuu Francisco Montecillo Padilla alipokuwa akizungumza na Waumini wa Kanisa la Mtakatifu Killian Jimbo la Mbinga mkoani Ruvuma, katika maadhimisho ya sherehe za misa takatifu ya kuwapaka mafuta ya daraja la kipaimara, watoto  waliokuwa wakipatiwa daraja hilo.

Balozi huyo alisema itakuwa si busara kwa waumini wa dhehebu hilo kujihusisha na matendo yasiyompendeza Mungu, hivyo ni vyema wajiepushe ili taifa liendelee kuwa na amani.

“Ndugu zangu matukio ya ajabu yamekuwa yakiendelea kutokea, mapadri wamekuwa wakifanyiwa vibaya kule Zanzibar, makanisa yetu yanachomwa moto, kwa kweli matukio kama haya hayavumiliki na   haya mpendezi Mungu”, alisema Padilla.

Aidha wakati wa maadhimisho ya misa hiyo ulinzi mkali ulikuwa umetanda kuzunguka kanisa hilo ndani na nje, ambao ulijumuisha maofisa usalama wa taifa na askari polisi huku waumini wa kiislamu ambao walionekana kutaka kuingia katika eneo la kanisa hilo, walizuiwa kuingia.

BARAZA LA TAIFA LAISIMAMISHA KAMPUNI KUENDELEA NA KAZI YA UCHIMBAJI WA MAKAA YA MAWE

Rais Jakaya Kikwete.





















Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

BARAZA la taifa la hifadhi na usimamizi  wa mazingira limeisimamisha kampuni ya Tancoal Energy, inayochimba makaa ya mawe katika wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma  kufanya kazi ya kupakia na kusafirisha makaa ya  mawe katika kituo cha Amani Makolo na Bandari ya Ndumbi,  kwa muda wa siku saba kutokana na kukiuka maagizo ya baraza hilo.

Kampuni hiyo imesimamishwa baada ya timu ya baraza hilo la taifa la hifadhi na usimamizi wa mazingira, kukagua na kutoa maelekezo mara kadhaa ya namna ya kupunguza athari za vumbi kwa wananchi,  uchafuzi wa vyanzo vya maji, kujenga vyoo na mifereji ya kupitisha taka vimiminika na kampuni hiyo kutotekeleza maagizo hayo.

Dokta Madoshi Makene alisema maeneo yaliyofungiwa kufanya kazi ni eneo la Amani Makolo Mbinga  na bandari ya  Ndumbi, katika wilaya ya Nyasa mkoani humo, ambako kunazalishwa kiasi kikubwa cha vumbi kutokana na shughuli ya upakiaji na usafirishaji wa makaa hayo ya mawe na kushindwa kuzuia vumbi lisisambae katika makazi ya watu.

Katika eneo la Ndumbi timu hiyo haijakuta vyoo vilivyojengwa kwa ajili ya wafanyakazi, na hakuna mifereji kwa ajili ya kupitisha maji machafu yanayotoka kwenye eneo hilo ili yasiende kuchafua maji ya mito na ya ziwa Nyasa ambayo hutumika na wananchi katika shughuli za maisha yao ya kila siku.

Kwa upande wao wakazi wa kijiji cha Amani makolo wilaya ya Mbinga wanaomba serikali iwasaidie ili waweze kulipwa na  kuhama, sasa wanashindwa kuishi katika makazi yao kutokana na mazingira ya nyumba zao kuzungukwa na vumbi na kusababisha watoto kuugua mafua na kikohozi.

Meneja wa mazingira na usalama wa kampuni ya Tancoal Felix Fida, amekiri kuwa ni kweli wanafahamu matatizo ya vumbi katika vituo hivyo, lakini kuna juhudi zinazofanyika ili kupunguza ama kuondoa kabisa kero hiyo.