Wednesday, September 11, 2013

UKAGUZI HALMASHAURI YA WILAYA YA MBINGA WAUMIZA VICHWA WAFANYAKAZI WA HALMASHAURI HIYO

Ludovick Utouh, Mkaguzi na mdhibiti mkuu wa hesabu za serikali.                                   (Picha kwa hisani ya mtandao)

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

BAADHI ya wakazi wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wameishukuru serikali kwa kuchukua hatua ya kumleta Mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali hapa nchini(CAG) kufanya ukaguzi, katika halmashauri yao ya wilaya hiyo.

Walisema hatua hiyo ni ya busara, na inapaswa kuungwa mkono kutokana na halmashauri hiyo kuwepo malalamiko mengi miongoni mwa jamii, juu ya utekelezaji mbovu wa miradi mbalimbali ya wananchi.

Baadhi ya miradi ya wananchi wilayani Mbinga, imetekelezwa kwa kiwango kisichokubalika ikiwemo ujenzi wa barabara za wananchi vijijini, miradi ya kilimo cha umwagiliaji, majosho ya kuogeshea mifugo na hata nyumba za watumishi vijijini.

Wakazi hao kwa nyakati tofauti walieleza kuwa hata kwa upande wa kitengo cha manunuzi wilayani humo wanamashaka nacho, hivyo wameiomba serikali kuwa makini na kitengo hicho wakati wanapokifanyia ukaguzi.

“Ukarabati wa  majengo ya halmashauri hiyo kwenye idara mbalimbali nao umekuwa ukifanywa kwa kutokidhi viwango, ambapo kuna tetesi kwamba majengo mengine yamekuwa yakitengewa fedha na ukarabati wake umekuwa haufanyiki, sasa tunahoji fedha husika zinapelekwa wapi?”, walisema.


Pamoja na mambo mengine Mwandishi wa habari hizi alipozungumza kwa nyakati tofauti na baadhi ya wafanyakazi wa halmashauri ya Mbinga, baadhi yao walisema ukaguzi huo umekuwa ni changamoto kubwa kwao.

Wengine walisikika wakisema; “vichwa vimekuwa vikituuma, matumbo joto juu ya ukaguzi huu, sijui hapa kama tutapona…..”.

Hata hivyo vyanzo mbalimbali vya habari vimeeleza kwamba ukaguzi huu ni wa muda mfupi na hautachukua siku nyingi, hivyo wanachosubiri ni kuona serikali inawatendea haki wananchi wa wilaya ya Mbinga kwa kuibua ukweli uliopo na pale itakapobaini kuna matatizo wameitaka serikali ichukue hatua mara moja, ili iwe fundisho katika jamii.

No comments: