Monday, September 16, 2013

KITUO CHA SHERIA NA HAKI ZA BINADAMU CHA WATAKA MADIWANI NA WATENDAJI WA HALMASHAURI KUJENGA UWAJIBIKAJI NA UWAZI KATIKA SHUGHULI ZA MAENDELEO YA WANANCHI

Rosemary Manase, Wakili wa kituo cha Sheria na Haki za binadamu hapa nchini, akitoa ufafanuzi wa mambo mbalimbali alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wilayani Mbinga, mkoa wa Ruvuma.(Picha na Kassian Nyandindi)



Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.

MADIWANI na watendaji katika halmashauri hapa nchini, wametakiwa kujenga uwajibikaji na uwazi katika shughuli mbalimbali za maendeleo ya wananchi, ili kuweza kuleta ufanisi na kukuza uelewa katika jamii.

Aidha kwa upande wa Madiwani wamesisitizwa kufanya mikutano na wananchi wao mara moja kwa kila mwezi na kutoa elimu juu ya haki za binadamu, hususani kwa wananchi walioachwa nyuma katika nyanja mbalimbali.

Rai hiyo imetolewa na Rosemary Manase, Wakili wa kituo cha Sheria na Haki za binadamu hapa nchini, wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari juu ya malengo mahususi ya mafunzo ya siku tatu ya haki za binadamu, yanayotolewa na kituo hicho katika wilaya ya Nyasa na Mbinga mkoani Ruvuma.


Manase alisema mafunzo hayo yameshirikisha Madiwani na Watendaji wa halmashauri za wilaya hizo, lengo hasa ikiwa ni kukuza uelewa wa sheria na haki za binadamu kwa jamii, uwajibikaji na uwazi katika shughuli za halmashauri.

“Vitu vyote tunavyo wafundisha hawa wenzetu, tunahitaji wavifikishe kwa wananchi, ni vizuri Madiwani wakayafikisha huko katika maeneo yao ya kazi”, alisisitiza.

Aidha alifafanua kuwa wamekuwa wakielimisha juu ya masuala ya  rasimu ya katiba mpya,  ambapo wamekuwa wakisisitiza juu ya wao kupendekeza uwepo  wa serikali moja katika katiba ijayo.

“Sisi kwa upande wa kituo cha haki za binadamu, tunapendekeza uwepo wa serikali moja katika katiba ijayo, vilevile tunataka watu ambao watakuwa kwenye bunge la katiba wawe ni raia au watu wa kawaida, mashirika mbalimbali(NGO’S) na wanasiasa wawe wachache wasiwe wengi”, alisema Manase.

Kadhalika alisema kituo cha sheria na haki za binadamu wanatoa msaada wa kisheria na elimu kwa ujumla, ili watu waweze kuwa na uelewa wa kupata haki zao za msingi.

Pamoja na mambo mengine mada kuu ambazo zimekuwa zikitolewa katika mafunzo hayo ni sheria ya ajira na mahusiano kazini, haki za binadamu, katiba, rushwa, haki kazi na wajibu wa madiwani, kanuni kuhusu maadili ya madiwani na kukuza uelewa wa madiwani juu ya dhana kuu ya uwajibikaji na uwazi wa shughuli za halmashauri.

No comments: