Sunday, March 29, 2015

MEYA MANISPAA SONGEA ABURUTWA MAHAKAMANI NA TAKUKURU

Charles Mhagama, Meya wa Manispaa ya Songea.
Na Mwandishi wetu,
Songea.

CHALRES Mhagama, ambaye ni Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, ameburutwa katika Mahakama ya Hakimu mkazi mfawidhi wilaya ya Songea mkoani humo kwa kosa la kutoa rushwa, ikiwa ni lengo la kupora kiwanja cha Ofisa mtendaji wa kata ya Matogoro.

Akisomewa shitaka hilo mbele ya Hakimu, Elizabeth Missana na Mwendesha mashtaka wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Greigory Joseph alisema mwaka 2010 katika kata hiyo, Mhagama alitoa shilingi 250,000 na kumpatia Shaibu Ngonyani kama kishawishi cha kumwandikia mkataba feki wa mauziano ya kiwanja hicho.

MKURUGENZI MBINGA APUUZA AGIZO LA RAIS KIKWETE

Rais Jakaya Kikwete.
Na Kassian Nyandindi,

AGIZO lililotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete juu ya kutoondolewa kwa vifaa vya thamani katika shule ya sekondari ya wasichana Mbinga mkoani Ruvuma, limepuuzwa na vifaa husika vimeendolewa katika majengo ya shule hiyo.

Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Hussein Ngaga ndiye anayenyoshewa kidole kutumia nguvu kwa cheo alichonacho na kuchukua vifaa hivyo huku akijua fika, Rais Kikwete alikwisha toa agizo vitu vilivyomo ndani ya majengo ya shule hiyo visiondolewe.

Hivi karibuni, Rais Kikwete mnamo Julai 19 mwaka 2014 alikuwa katika ziara yake ya kikazi wilayani Mbinga, ambapo alitoa agizo hilo akilenga vifaa hivyo viweze kuwasaidia walimu na wanafunzi ambao wanasoma katika shule hiyo.

Saturday, March 28, 2015

WALIMU MBINGA WALIA WAITAKA SERIKALI IWALIPE MADAI YAO

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

CHAMA Cha Walimu Tanzania (CWT) tawi la Mbinga mkoa wa Ruvuma, kimesema kwamba walimu wake waliopo wilayani humo, wanaidai serikali shilingi milioni 238,777,267.30 kwa muda mrefu sasa jambo ambalo linawafanya walimu washindwe kuwajibika ipasavyo mashuleni.

Imeelezwa kuwa deni hilo ni la madai mbalimbali ambayo ni malimbikizo, uhamisho, matibabu, likizo, masomo na kujikimu hivyo wameitaka serikali kuhakikisha deni linalipwa mapema ili kuondoa malalamiko miongoni mwao.

Hayo yalisemwa na Katibu mkuu wa CWT wilayani Mbinga, Werner Mhagama alipokuwa akisoma taarifa ya utendaji kazi za chama kwa kipindi cha mwezi Julai 2013 hadi Disemba 2014 kwenye mkutano mkuu wa wilaya, uliofanyika ukumbi wa Uvikambi uliopo mjini hapa.

Mhagama alifafanua kuwa chama pia kimebaini kuwepo kwa tatizo la kutopandishwa vyeo walimu wilayani humo, hasa kwa wale ambao wanasifa ambapo mpaka sasa waliostahili ni 521 lakini waliopandishwa ni 470 tu.

Tuesday, March 24, 2015

UKOSEFU WA FEDHA WASABABISHA MRADI WA MAJI KUTOKAMILIKA KWA WAKATI

Na Julius Konala,
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa kutokamilika kwa wakati, ujenzi mradi wa maji Kihongo uliopo katika kijiji cha Kihongo, kata ya Mapera wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, unatokana na ukosefu wa fedha hivyo serikali imeombwa kutekeleza hilo ili mradi huo, uweze kujengwa kwa haraka na wananchi waweze kuondokana na adha ya ukosefu wa maji.

Hayo yalisemwa kupitia taarifa fupi iliyosomwa na Afisa mtendaji wa kijiji cha Kihongo, Danstan Hyera kwenye maadhimisho ya kilele cha wiki ya maji yaliyofanyika kimkoa katika kijiji hicho wilayani Mbinga.

Aidha Hyera alisema kuwa, hivi sasa hata kazi za ujenzi zimesimama hivyo kuna kila sababu kwa serikali kuona umuhimu wa kuwezesha mradi huo uweze kukamilika kwa wakati ili wananchi wapate huduma bora ya maji.

KIGONSERA WAMLALAMIKIA MKURUGENZI WA MBINGA KUTUMIA NGUVU KUCHUKUA MALI ZAO, WASEMA AMEKOSA UTAWALA BORA WATAKA SERIKALI KUINGILIA KATI

Rais Jakaya Kikwete, wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania.
Na Kassian Nyandindi,

HUSSEIN Ngaga, ambaye ni Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, analalamikiwa na Wakazi wa kijiji cha Kigonsera kata ya Kigonsera wilayani humo akidaiwa kutumia mabavu kwa cheo alichonacho na kuchukua mali kadhaa za kijiji hicho, kinyume na utaratibu.

Kitendo alichofanya Mkurugenzi huyo kimeelezwa kuwa ni wizi, kutokana na kile walichoeleza kwamba hakuna kikao chochote kilichoketi kijijini hapo na kuridhia achukue mali zao, ambavyo ni vifaa vya thamani walivyokabidhiwa na mkandarasi wa ujenzi wa barabara kiwango cha lami kutoka pacha ya Peramiho hadi Mbinga mjini, jambo ambalo limekuwa likizua malalamiko miongoni mwa jamii.

Ngaga ananyoshewa kidole na wakazi wa kijiji cha Kigonsera kwamba ametumia nguvu, na kulazimisha kuchukua vifaa hivyo ambavyo walikabidhiwa na mfuko wa barabara wa Millenium Challenge Account (MCA – Tanzania) mara baada ya Mkandarasi, ambaye ni kampuni ya kichina ya Sinohydro Corporation Limited kukamilisha kazi ya ujenzi wa barabara hiyo.

Mkandarasi huyo ambaye alikuwa ameingia mkataba na kijiji (nakala tunayo) inaonesha na kuthibitisha kuwa alikuwa ametumia sehemu ya ardhi ya kijiji hicho, kwa ajili ya kuweka kambi na kujenga majengo ambayo yalikuwa yakitumika kulala wataalamu wa ujenzi wa barabara hiyo.

Sunday, March 22, 2015

PENGO NI KIGEUGEU AU HATAMBUI JUKWAA LA WAKRISTO TANZANIA?

Padre Baptiste Mapunda.
Na Padre Baptiste Mapunda,

NI hivi majuzi tu, gazeti la Mwananchi liliamua kuweka mbele ujumbe uliokuwa ukisomeka TAIFA NJIA PANDA. Kichwa hiki cha habari kilisindikizwa na vitu vitatu vilivyo chagiza habari kuu kuwa ni mashine za BVR, Mahakama ya Kadhi na Upigaji wa kura ya maoni kuhusu katiba inayopendekezwa.

Hakika mhariri wa gazeti hili aliitendea haki, juu ya habari iliyobeba kwenye gazeti hilo kwa kutoa habari kwa kina na kuonyesha kwa nini, taifa lipo njia panda sasa. Leo nasi wakristo wakatoliki tunaweza kujihesabu kuwa tupo njia panda kuhusiana na tamko la Jukwaa la kikristo Tanzania, lililotutaka wakristo wote kuungana na kujitokeza kwa wingi kujiandikisha na hatimaye kujitokeza siku ya kupiga kura ya kuipitisha katiba inayopendekezwa, kwa kuipigia kura ya hapana.

Hii siyo kwa chuki tu, bali sababu zenye mashiko zimetolewa na Baraza au Jukwaa hilo karibu kila aliyemkristu alizikubali sababu hizo na kuona kwamba, zina mashiko makubwa.

Tukiwa katika hali ya umoja wa wakristo wote katika hili, ghafla bin vuuu, Baba yetu ambaye tunamtegemea na kumwamini, Kadinali Pengo, anajitokeza wazi kupinga sauti ya wengi ambayo sote tunaamini ni sauti ya Mungu na kutoa maelekezo tofauti kabisa na maamuzi ya Jukwaa hili na kubaki tunamshangaa!!. Hapa ndipo msingi wa swali langu kwenu wadau, PENGO NI KIGEUGEU au HATAMBUI JUKWAA LA KIKRISTO TANZANIA?

MAHAKAMA YA KADHI KULETA MACHAFUKO HAPA NCHINI, KURA YA HAPANA IPO PALE PALE

Padre Baptiste Mapunda.
Na Padre Baptiste Mapunda,

KWANZA ni lazima ieleweke kwamba, Wakristo kupitia Maaskofu wao hawaipingi Mahakama ya kadhi kama mahakama ya kadhi, ila wanachopinga ni uanzishwaji kwa mamlaka ya serikali.

Swali ni kwa nini serikali ijishughulishe na mahakama ya dini, wakati katiba imekataa? Watanzania  wengi wanajiuliza kuna agenda gani  ya siri iliyopo nyuma ya hii mahakama? Kwa mantiki hiyo na kwa kuzingatia tamko la Maaskofu wa Jukwaa la Wakristo na sababu nzito iliyotolewa, wakristo tujiandae kuipigia kura ya hapana katiba mpya kama tulivyoelekezwa na wala siyo kulazimisha kama wengine wanavyotafsiri tamko hilo.

Toka kuundwa kwa taifa letu la Tanganyika-Tanzania nchi yetu inajulikana kwamba serikali yake si ya kidini ila wananchi wake wanadini. Katiba ya mwaka 1977 inatamka hivyo na kila mtu anajua na hivyo basi masuala yote ya kidini  yanapaswa kuendeshwa na dini husika.

Waumini wa imani tofauti mathalani Wakristo na Waislamu, walikuwa wamekaa kwa amani hadi miaka ya 90  katika kipindi cha Rais wa awamu ya pili, Ally Hassan Mwinyi maarufu kama mzee wa “Ruksa” ndipo choko choko za kidini zilipoanza  kujitokeza.

Choko choko hizi ziliambatana na madai kwamba, Waislamu walikuwa wanaonewa, kunyanyaswa na kubaguliwa chini ya mfumo wa kikristo.

Kikaja kipindi cha Benjamini  Mkapa madai yalijitokeza, lakini yeye alifuata katiba ya nchi hivi hakuweza kuyapa nafasi hata ya kujadiliwa bungeni. Lakini leo cha ajabu ni kwamba Chama Cha Mapinduzi (CCM) ililiweka suala la mahakama ya kadhi katika ilani yake ya uchaguzi ya mwaka 1995.

CWT YAITAKA MANISPAA SONGEA KUMALIZA KERO ZA WALIMU

Na Amon Mtega,
Songea.

CHAMA Cha Walimu Tanzania (CWT) tawi la Songea mkoani Ruvuma, kimeutaka uongozi wa Manispaa hiyo kushughulikia matatizo ya walimu, ikiwemo kuwapandisha madaraja kwa wakati wale wote wanaostahili ili kuondoa malalamiko kwa baadhi yao, ambao ni muda mrefu sasa umepita hawajapandishwa.

Mwenyekiti wa CWT katika tawi hilo, Mathias Mwanjisi alitoa rai hiyo juzi alipokuwa kwenye mkutano mkuu wa uchaguzi viongozi wa chama hicho, akieleza kuwa licha ya wengi wao kuwa na vigezo vinavyostahili kupandishwa madaraja lakini hakuna kilichotekelezwa hadi sasa.

Kadhalika Mwanjisi ambaye alikuwa akitetea nafasi yake ya uenyekiti katika chama hicho, aliweza kushinda kwa kupata kura 84 huku mpinzani wake Edimund Nditi akipata kura 18 huku idadi ya wapiga kura wote ilikuwa  102.

Saturday, March 21, 2015

ASHIKILIWA KWA KOSA LA UBAKAJI

Na Amon Mtega,
Songea.

MKAZI mmoja ambaye anaishi mtaa wa Changalae kata ya Mletele Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, Hamis Milanzi (68) anashikiliwa na jeshi la polisi mkoani humo, kwa tuhuma za kumbaka mwanafunzi mwenye umri wa  miaka (13) anayesoma shule ya msingi Luhila seko iliyopo mjini hapa.

Akizungumza na Waandishi wa habari, Kaimu kamanda wa polisi wa mkoa huo, Yahaya Athumani alisema tukio hilo lilitokea majira ya jioni katika mtaa huo ambapo mtuhumiwa huyo alitenda kosa hilo, baada ya kumtishia mtoto huyo kwamba akikataa kufanya naye mapenzi atamfanya kitu kibaya huku akimrubuni kwa kumpatia shilingi 30,000.

Yahaya alisema kuwa mwanafunzi huyo, ambaye jina lake linahifadhiwa anaishi kata ya Mletele ambapo alikwenda nyumbani kwa mtuhumiwa huyo kumdaifedha za kuni ambazo alimkopesha na alipowasili huko, aliambiwa na mtuhumiwa huyo aingie ndani ili apewe fedha hizo.

MWAMBUNGU: AMKENI NA KUKUZA KIWANGO CHA ELIMU RUVUMA

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu akisisitiza jambo katika kikao hicho mjini Tunduru mkoani humo.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

MKUU wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu amewataka Wakuu wa wilaya na Wakurugenzi wa Halmashauri za mkoa huo, kuamka kutoka usingizini na kuanza kazi ya kukabiliana na changamoto ya utoro na mdondoko mkubwa wa wananfunzi ambao wamekuwa hawaendelei ipasavyo na masomo, katika shule za msingi na sekondari.

Mwambugu alitoa agizo hilo wakati alipokuwa akifungua mkutano wa Wadau wa tathimini ya elimu mkoni Ruvuma, uliofanyika kwenye ukumbi  wa Klasta ya walimu tarafa ya mlingoti mjini Tunduru na kuhakikisha watoto wote wanaoandikishwa, wanamaliza elimu ya msingi na kundelea na masomo ya sekondari.  

Kwa mujibu wa mkuu huyo wa mkoa, takwimu zinaonesha kuwa mkoa huo unakabiliwa na mdondoko wa kutisha ambapo mwaka 2008 ulindikisha wanafunzi wa darasa la kwanza 41,789 lakini takwimu za wanafunzi waliofanya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi, mwaka 2014 walikuwa 27,771 sawa na asilimia 66. 

PADI YAWAPIGANIA WAZEE KUTENGEWA BAJETI WAWEZE KUONDOKANA NA CHANGAMOTO MBALIMBALI KATIKA MAISHA YAO

Mkurugenzi wa PADI Iskaka Msigwa, akipokea tuzo ya kutoa huduma bora kwa wazee, na kuweza kutoa fedha za matibabu kwa wazee walioko mkoa wa Ruvuma kupitia shirika hilo Novemba 26, 2011. 
Na Julius Konala,
Songea.

HALMASHAURI ya wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, imetakiwa kutenga fedha katika bajeti yake kila mwaka, kwa ajili ya kuwahudumia wazee wasiojiweza ambao wamepoteza nguvu zao kutokana na kupigania taifa hili, katika mambo mbalimbali hususani ya kimaendeleo.

Mkurugenzi mtendaji wa shirika la kuhudumia wazee Tanzania (PADI) Iskaka Msigwa, alisema hayo alipokuwa akizungumza na timu ya wataalamu wa Halmashauri ya wilaya hiyo, kwenye mkutano wenye lengo la kuhamasishana juu ya masuala ya wazee kuingizwa kwenye bajeti, uliofanyika mjini Songea.

Msigwa alisema kuwa hatua hiyo, imefikiwa baada ya kuona kwamba kundi hilo limesahaulika kwa muda mrefu huku likikabiliwa na changamoto lukuki ikiwemo kushindwa kumudu gharama za maisha, na kubeba mzigo mzito wa kuwatunza watoto yatima ambao wameachwa na wazazi wao baada ya kufariki dunia kutokana na ugonjwa wa ukimwi au ajali, hivyo ameiomba serikali na jamii kwa ujumla kuwajibika katika kuwatunza.

Kufuatia hali hiyo, taasisi mbalimbali za kifedha nazo zimeombwa kuangalia uwezekano wa kuyasaidia makundi hayo kwa kuyakopesha hata fedha, kwa madai kwamba wazee wanakopesheka kutokana na kuwa waaminifu lakini pia serikali ione umuhimu wa kuwalipa pensheni, kwa ajili ya kuwapunguza ukali na ugumu wa maisha.

Friday, March 20, 2015

MFUKO WA BIMA YA AFYA WASHUSHA LAWAMA KWA WATENDAJI WA SERIKALI

Baadhi ya wajumbe waliohudhuria mkutano huo, wakifuatilia hoja mbalimbali kwa umakini.
Na Steven Augustino,
Tunduru.

IMEELEZWA kuwa mkoa wa Ruvuma, umekuwa ukikosa shilingi milioni 250 kila mwaka, kutokana na kuanzishwa utaratibu wa kutoa huduma za matibabu kupitia mfuko wa bima ya Afya ya jamii (NHIF) endapo viongozi wa halmashauri za mkoa huo wangeomba kupatiwa dawa kupitia mfumo huo, huku hali imetokana na kuwepo kwa michango ya wanachi kutoka katika kaya 26,058 ambazo huchangia fedha zao, huku wakikosa huduma waliyokusudia kuipata.

Meneja wa mfuko huo wa bima ya afya ya jamii mkoani Ruvuma, Slively Mgonza alisema hayo wakati alipokuwa akitoa taarifa ya maendeleo ya mfuko huo, katika mkutano wa tathimini ya elimu, uliofanyika kimkoa katika ukumbi wa Klasta ya walimu tarafa ya mlingoti, wilayani Tunduru mkoani humo.

“Nikituko cha ajabu, kwani endapo wangeomba fedha hizo zingesaidia kuondoa matatizo mbalimbali yanayozikabili hospitali, vituo vya afya  na zahanati katika utoaji wa huduma kwa jamii”, alisema Mgonza. 

Kwamujibu wa Mgonza, kati ya fedha hizo shilingi milioni 48  zilichangwa kutoka katika kaya 4,882 katika Manispaa ya Songea, milioni 56 kutoka katika kaya 5,699 zilizopo halmashauri ya wilaya songea na milioni 77 katika kaya 7,782 zilizopo Halmashauri ya wilaya ya Tunduru.

Wednesday, March 18, 2015

PROFESA SIGALLA ALIA NA WATUMISHI MANISPAA YA SONGEA

Na Julius Konala,
Songea.

MKUU wa wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, Profesa Norman Sigalla amewataka watumishi wa Halmashauri ya wilaya hiyo kumpa ushirikiano wa kutosha, ikiwa ni lengo la kuimarisha utendaji kazi kwa manufaa ya jamii, na upambanaji wa vita dhidi ya watu wenye tabia chafu ya kukatisha maendeleo ya wanafunzi masomo darasani hususani kwa watoto wa kike, kuwapa ujauzito.

Sigalla alitoa kauli hiyo juzi, alipokuwa akizungumza na watumishi wa kada mbalimbali, wakiwemo pia na wakuu wa idara  wa halmashauri hiyo kwenye ukumbi wa mikutano uliopo, ofisi ya mkuu wa wilaya hiyo kwa lengo la kufamihana.

Alisema hatakuwa na huruma wala kumfumbia macho, mtumishi yeyote atakayebainika anaendesha vitendo viovu, huku akiapa kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake, sambamba na kufikishwa kwenye vyombo vya kisheria.

“Natoa onyo hata kwa wazazi na walezi, ambao watakabainika kushindwa kutoa ushirikiano kwa serikali yetu katika kuwafichua watu ambao wamewapa ujauzito watoto waliokatika wakati wa kwenda shule, kwa sababu ya kurubuniwa na fedha au kitu fulani kwa lengo la kupoteza ushahidi, hatua kali za kisheria  zitachukuliwa dhidi yao”, alisema Sigalla.

MKURUGENZI MBINGA ANAMATATIZO NI VYEMA ACHUNGUZWE, ADAIWA KUWAIBIA MAMILIONI YA FEDHA WAKULIMA WA KAHAWA

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Na Kassian Nyandindi,

BUNDI ameendelea kumsakama Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Hussein Ngaga ambapo sasa ameingia katika kashfa mpya akidaiwa kuwaibia wakulima wa kahawa wilayani humo, zaidi ya shilingi milioni 783,399,412 baada ya kahawa yao kuuzwa mnadani Moshi.

Wakulima hao ni wale ambao walikopeshwa fedha, shilingi bilioni 2 na Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF) kupitia vyama vyao vya ushirika (AMCOS) vilivyopo wilayani humo, lengo la fedha hizo kutolewa na shirika hilo lilikuwa ni kutoa mikopo yenye gharama nafuu kwa wakulima wadogo wadogo, ambao wamejiunga kisheria katika vikundi hatimaye waweze kujikwamua kiuchumi na kuondokana na umasikini.

Hayo yamebainika kufuatia uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi, ambapo wakulima kutoka vyama vinne vya ushirika Mahilo, Ngaka, Ngima na Pilikano ambao hujishughulisha na uzalishaji wa zao la kahawa ndio walioibiwa fedha hizo.

Tuesday, March 17, 2015

HALMASHAURI MANISPAA YA SONGEA KUBURUTWA MAHAKAMANI


Na Julius Konala,
Songea.

KAMPUNI ya Majembe Auction Mart Limited, inakusudia kuifikisha Mahakamani Halmashauri ya Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, kwa kile kilichoelezwa kuwa imevunja mkataba wa ukusanyaji ushuru (Service Levy) kinyume na utaratibu, jambo ambalo limeisababishia kampuni hiyo, hasara zaidi ya shilingi milioni 70.

Mkurugenzi wa kanda katika kampuni hiyo, Nelson Mwasomola alisema hayo alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, juu ya kitendo cha uvunjwaji wa mkataba huo ambao umefanywa na Halmashauri hiyo.

Mwasomola alisema kusimamishwa kwa kampuni yake, kutoendelea na kazi ya ukusanyaji wa ushuru huo kumesababisha kushindwa kufikia malengo ya ukusanyaji wa fedha kwa kiwango husika kilichowekwa kwa kila mwezi, na kusababisha kuwepo kwa hasasra kubwa. 

WAUMINI NAMTUMBO WAMPONGEZA MWEKEZAJI KWA KUWAJENGEA MSIKITI




Na Julius Konala,
Namtumbo.

WAUMINI wa dini ya Kiislam, katika kijiji cha Likuyu Sekamaganga wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, wamempongeza na kumshukuru mwekezaji wa kampuni ya Game Frontiers Tanzania (GFT) inayojihusisha na uwindaji wilayani humo, Sheni Abdalah kwa jitihada zake za kujitolea kusaidia ujenzi wa msikiti wa kisasa kijijini hapo, kwa gharama ya shilingi milioni 40.

Pongezi hizo zilitolewa juzi na baadhi ya waumini wa dini hiyo, walipokuwa wakizungumza kwa nyakati tofauti na mwandishi wa habari hizi kijijini hapo, wakidai kwamba kufanikiwa kwa ujenzi huo, kumewaondolea adha pale wanapohitaji eneo la kufanyia ibada.

Immam wa msikiti huo, Omary Kudelega alisema kuwa kukamilika kwa ujenzi huo kumetokana na maombi ya kujengewa msikiti , yaliyotolewa na waumini wa dini ya kiislam wa kijiji cha Likuyu Sekamaganga kwa mwekezaji huyo.

Monday, March 16, 2015

CCM TUNDURU WATOFAUTIANA JUU YA KALOLO KUWA MGOMBEA PEKEE

Na Steven Augustino,
Tunduru.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, kimetofautiana na tamko la vijana wa chama hicho, katika tarafa ya Matemanga juu ya maamuzi yao  ya kukishinikiza kumtawaza Omary Ajili Kalolo, kuwa mgombea pekee kwa nafasi ya ubunge Jimbo la Tunduru Kaskazini kwenye uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.

Hilo linakuja pia, kwa chama hicho kuwataka wabunge, madiwani na viongozi wengine waliochaguliwa na wananchi kutimiza ahadi walizoahidi wakati wa kampeni ya uchaguzi uliopita, ili kujiwekea akiba ya kuchaguliwa tena vinginevyo wasitegemee kubebwa ili waweze, kushinda katika uchaguzi ujao.

Kauli hiyo ilitolewa na Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Tunduru, Hamisi Kaesa alipokuwa akizungumza na maelfu ya wananchi, ambao walikusanyika na kuhudhuria sherehe za ushindi wa chama hicho, katika kijiji cha Mtengashari kata ya Ligunga wilayani hapa.

Sunday, March 15, 2015

MICHANGO YA WAZAZI MBINGA YACHOTWA KIAINA, YADAIWA KUINGIZWA KWENYE AKAUNTI YA MZABUNI ALIYEPATIKANA BILA KUFUATA TARATIBU

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WAKATI serikali ikiwataka viongozi wake katika Halmashauri mbalimbali hapa nchini kufanya kazi kwa uwazi na kufuata taratibu husika, hali hiyo imekuwa kinyume kwa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, ambapo inadhihirisha pale agizo lililotolewa na Kaimu Afisa elimu msingi wa wilaya hiyo, Alphonce Mwamwile juu ya michango wanayochanga wazazi kwa ajili ya kuendeshea mitihani ya kata na shule mwishoni mwa mwezi na kuingizwa kwenye akaunti ya Rukwa Computer Training Centre, imezua mapya kufuatia baadhi ya Madiwani na Wenyeviti wa shule za msingi wa wilaya hiyo, kudai kuwa hakuna kikao kilichoketi na kujenga makubaliano kwamba fedha hizo zipelekwe huko.

Madiwani na wenyeviti hao walidai kwa nyakati tofauti kuwa, hata mchakato wa zabuni haujafanywa juu ya kumpata mzabuni huyo ambaye hafahamiki ni wa kutoka mkoa au wilaya gani na amepewa jukumu la kuchapa mitihani ya watoto wao, badala yake wanashangaa kuona waratibu elimu kata na walimu wakuu mashuleni wakiagizwa kukusanya michango hiyo na kuiingiza kwenye jina la akaunti hiyo. 

Imeelezwa kuwa agizo hilo lililotolewa na Ofisa elimu huyo linatekelezwa baada ya kuagizwa na Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri hiyo, Hussein Ngaga kwamba afanye hivyo na fedha ziingizwe kwenye jina la akaunti hiyo jambo ambalo wamesema, kitendo hicho ni wizi wa fedha za wananchi hivyo ni vyema zikafuatwa taratibu husika za kumpata mzabuni kwa kufuata taratibu zenye uwazi na sio vinginevyo, hivyo kutozingatia hilo ni kukosa utawala bora na kuleta migogoro isiyokuwa ya lazima katika jamii.

Mwandishi wa habari hizi amefanikiwa kupata barua yenye kumbukumbu namba W/E/MB/10/VOL.111/66 ya Januari 15 mwaka huu, ambayo inawaagiza waratibu na walimu wakuu wote shule za msingi wilayani Mbinga, kukusanya michango hiyo ya wazazi kwa ajili ya kuendeshea mitihani hiyo na kuiingiza kwenye akaunti namba 62101600263 benki ya NMB, ambayo ni ya Rukwa Computer Training Centre.

Sehemu ya barua hiyo inaagiza kwamba itafanyika mitihani sita ya wilaya kwa darasa la saba mwaka huu, mitihani minne fedha zitatoka kwa wananchi na miwili itatoka kwenye akaunti ya Capitation Grant, hivyo mwanafunzi mmoja kwa mtihani mmoja anapaswa kuchangia shilingi 1,500 kwa masomo ya Hisabati, Kiswahili, Sayansi, Historia, Uraia, Jiografia na Kiingereza.

Saturday, March 14, 2015

MAASKOFU JUKWAA LA WAKRISTO WAKOLEZA MOTO KUIKATAA KATIBA MPYA

Padre Baptiste Mapunda.
Na Padre Baptiste Mapunda,

GAZETI la mwananchi, ijumaa iliyopita, Machi 13 mwaka huu lilikuwa limebeba ujumbe mzito kwa Watanzania wenzangu, katika kichwa cha habari,  “Maaskofu: Pigieni Katiba kura ya hapana.”

Maaskofu wa Jukwaa la Wakristo ambao ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Kikristo (CCT) Askofu Dokta Alex Malasusa, Mwenyekiti wa Baraza la Maaskofu katoliki Tanzania (TEC) Askofu Tarcicius Ngalalekumtwa  na Mwenyekiti wa Kanisa la Pentekoste Tanzania (CPCT) Askofu Daniel Awet kwa sauti moja, wamewataka waumini wao kujiandikisha kwa wingi katika daftari la wapiga kura, kuisoma vyema katiba pendekezwa na hatimaye kuikataa “kata kata” kwa kuipigia kura ya hapana.

Sababu kuu za kuwahamasisha waumini wao na Watanzania kuikataa katiba pendekezwa ni mbili.

WATANZANIA WATAKIWA KUISHI KWA KUZINGATIA SHERIA

Na Amon Mtega,
Songea.

WATANZANIA wakati wote wa maisha yao ya kila siku, wametakiwa kuishi kwa kuzingatia sheria zilizowekwa, ili kuepusha migogoro ambayo inaweza kujitokeza baadaye katika jamii hasa pale inapotokea kundi moja au jingine, hukiuka taratibu na kutozingatia miongozo ya sheria.

Naibu Askofu wa Jimbo kuu la Songea mkoani Ruvuma, Padre Camillius Haulle alitoa rai hiyo alipokuwa kwenye sherehe ya kuwaaga wahitimu wa mafunzo ya msaada wa kisheria (Paralegle) yaliyofanyika katika kituo cha  kisheria cha, African Institute for Comparative and International Law (AICL) kilichopo Mahenge mjini hapa.

Haulle alisema kuwa kama watanzania watatambua umuhimu huo, huenda hata migogoro ambayo hujitokeza mara kwa mara katika jamii ikapungua au kwisha kabisa na kulifanya taifa, kuwa na watu ambao ni mfano bora mbele ya mataifa mengine.

RUVUMA NAO WAPINGA MAUAJI YA ALBINO, WASEMA SERIKALI IWEKE MIKAKATI MADHUBUTI KUDHIBITI VITENDO HIVYO

Na Kassian Nyandindi,   
Songea.

KUTOKUWEPO kwa matukio ya mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi Albino mkoani Ruvuma,  wananchi wa mkoa huo wameendelea kulaani vitendo hivyo vya ukatili dhidi ya kundi hilo tete, ambavyo vimekuwa vikiendelea kujitokeza katika maeneo ya kanda ya ziwa hapa nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, Katibu msaidizi wa chama cha watu wenye ulemavu wa ngozi mkoani hapa, Fatuma Jumbe alisema kundi hilo la watu wenye ulemavu wa ngozi linahitaji uangalizi wa hali ya juu na kuitaka serikali, kuweka mikakati madhubuti ambayo itaweza kufanikisha katika kupambana na kuwakamata watu wenye kushiriki kwa namna moja au nyingine kuua albino.

Lakini alipongeza uamuzi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete kukutana na wawakilishi wa kundi hilo, pamoja na kuahidi kuunda tume ya kushughulikia vitendo hivyo vya kikatili, dhidi ya watu hao wenye ulemavu wa ngozi.

TEKINOLOJIA MPYA YA UHIFADHI MAZAO YAZINDULIWA RUVUMA

Na Nathan Mtega,
Songea.

KITUO cha hifadhi ya taifa ya chakula (NFRA) cha Songea mkoani Ruvuma, kwa kushirikiana na kampuni ya uhifadhi wa chakula ya AGRA kimezindua teknolojia mpya ya uhifadhi wa mazao, ambao utasaidia kwa kiasi kikubwa kudhibiti uharibifu wa mahindi ambayo zaidi ya tani 78,000 yamehifadhiwa nje ya maghala, huku mengine yakiendelea kuharibika kutokana na kituo hicho kuelemewa na wingi wa zao hilo ambayo huzalishwa na wakulima mkoani humo.

Maghala ya kituo hicho, yana uwezo wa kuhifadhi tani 26.000 na kwa mujibu wa Mkurugenzi wa hifadhi ya chakula taifa, Charles Warwa alisema zaidi ya tani 78.000 yameshindwa kuhifadhiwa ndani ya maghala na kulazimika kuyaweka nje, ambapo baadhi ya magunia ya mahindi yameanza kuharibika na kuliwa na wadudu, kutokana na teknolojia duni ya uhifadhi wa chakula unaofanywa katika kituo hicho.

Alisema hali hiyo inawafanya wafanyakazi wa hifadhi ya chakula katika ngazi ya mikoa na taifa, kuwakosesha usingizi lakini ujio wa teknolojia mpya ya uhifadhi wa chakula iliyoletwa na kamuni washirika ya AGRA, itakuwa ni ufumbuzi tosha wa changamoto hiyo ambapo kwa kituo cha Songea kuna tani zaidi ya 78,000 zimehifadhiwa nje kwa kutumia telnolojia ya zamani, ambayo hudhoofisha ubora wa mazao na kuharibu soko la ndani na nje.

Friday, March 13, 2015

TUFANYE NINI MWAKA HUU KUWA NA UCHAGUZI HURU NA WA HAKI?

Padre Baptiste Mapunda. 
Na Padre Baptiste Mapunda,

HOFU ya kukataliwa kwa katiba  mpya kumeifanya serikali ya awamu ya nne ivunje kabisa makubaliana na TCD, kwamba kura ya maoni ingesitishwa hadi  baada ya uchaguzi 2016.

Hadi sasa hatujui nani atakuwa madarakani ni mpinzani au  mwanaCCM mwenzao, hivi wanaona afadhali waendelee kulazimisha  kura ya maoni kwa mtindo ule ule wa kulazimisha. Watanzania tunaelekea pabaya  hii ni alama ya chama hiki tawala kukata tamaa na kuanguka.

Matokeo yake inafanya kila hila, ili daftari la kudumu la wapiga kura lisiboreshwe na waweze kuchota kura kirahisi,  na ushahidi ukosekane.

ZAHANATI ILIYOWEKWA JIWE LA MSINGI NA KIONGOZI WA MBIO ZA MWENGE KITAIFA TUNDURU YATELEKEZWA

Na Steven Augustino,
Tunduru.

WANANCHI wa kijiji cha Mtengashari, wilayani Tunduru Ruvuma, wamewataka viongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani humo, kutimiza ahadi yao ya kuwajengea zahanati ya kijiji hicho.

Kilio cha wananchi hao, kilitolewa kwa njia tofauti ikiwemo kupitia nyimbo zao walizoimba kwa mtindo wa kwaya, pamoja na maoni ya mtu mmoja mmoja wakati walipokuwa kwenye sherehe za kukipongeza chama hicho, kupata ushindi katika uchaguzi wa serikali za mitaa ambao umefanyika hivi karibuni.

Wakifafanua taarifa hiyo, walisema wamechukua uamuzi huo wa kufikisha kilio chao katika sherehe hizo kutokana na CCM kuwa na furaha kubwa kupata ushindi huo wa asilimia 75, huku kijiji chao kikipata ushindi wa asilimia 100 kwa wagombea wa nafasi zote, ikiwa ni tofauti na chaguzi zilizopita ambapo walikuwa wakiongozwa na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) pamoja na Chama Cha Wananchi (CUF).

“Tunajua kuwa ahadi ya kujengewa zahanati hiyo imekuwa ikififia kwa muda mrefu sasa, hivyo tunahitaji kujengewa zahanati hii, ili tuondokane na adha tunayoendelea kuipata sasa juu ya matibabu pale tunapougua”, walisema.

TUNDURU KASKAZINI WAPENDEKEZA MBUNGE WAO

Na Steven Augustino,
Tunduru.

WAPIGA kura wa Jimbo la Tunduru kaskazini mkoani Ruvuma, wamechukua jukumu la kumpendekeza Omary Kalolo, kuwa mgombea pekee kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika jimbo hilo, kwa nafasi ya ubunge katika uchaguzi mkuu ambao unatarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu.

Shirikisho la umoja wa vijana la CCM wilayani Tunduru katika jimbo hilo, ndilo ambalo limempendekeza mgombea huyo, kwa madai kuwa wanaimani naye katika utendaji wa kazi zake.

Aidha vijana hao wamemtaka Kalolo kutoa tamko ambalo litaunga mkono juu ya maamuzi na msimamo uliotolewa na shirikisho hilo, wakidai kuwa yeye ndiye chaguo la wengi.

Msimamo wa kumtaka Kalolo kugombea, umejitokeza kupitia risala yao iliyosomwa na Ally Nyama kwenye sherehe za ushindi wa asilimia 75 katika matokeo ya uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika hivi karibuni mjini Tunduru.

Monday, March 9, 2015

SIASA BILA DINI NI UWENDAWAZIMU

Padre Baptiste Mapunda.
Na Padre Baptiste Mapunda,

HISTORIA ya siasa duniani, haitengani sana  na  historia ya dini. Vitu hivi  viwili kwa maisha ya mwanadamu, vimekuwa sambamba na vyenye mafao kwa jamii yoyote ile duniani ambapo kwa upande mwingine dini na siasa vimeleta matatizo makubwa hapa duniani.

Uhusiano mzuri usipojengwa kati ya siasa na dini, hakika katika dunia hii na nchi yetu kwa ujumla tutaendelea kushuhudia machafuko na uharibifu mkubwa wa  mali, pamoja na mauti dhidi ya binadamu kama yalivyowahi kutokea hapa nchini hasa katika kampeni za kisiasa. Mara nyingi maovu hayo, yanasababishwa na uelewa mdogo juu ya mahusiano ya siasa na dini.

Na hivi sasa Tanzania imezalisha ugonjwa mpya unaojulikana kwa jina la “udini.” Unapoanza kuingiza udini katika ajira, elimu, afya  na siasa ujue kwamba  usalama wa nchi huenda ukawa hatarini.

Kutenganisha kabisa siasa na dini ni kitu ambacho hakiwezekani katika dunia ya leo, bali kinachotafutwa ni kila taasisi kuielewa vyema inahusiana vipi na nyingine, na kutengeneza mipaka yake na leo hii ndiyo ninaandika kwamba; “siasa bila dini ni uwenda wazimu.”

Thursday, March 5, 2015

NSSF RUVUMA YATOA MSAADA KWA SHULE YA MSINGI KIHURUKU



Na Julius Konala,

Mbinga.

SHIRIKA la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF)mkoa wa Ruvuma, limechangia kiasi cha shilingi milioni 2.5 kwa ajili ya ukarabati wa majengo ya shule ya msingi Kihuruku, iliyopo wilayani Mbinga mkoani humo, kutokana na majengo hayo kuwa katika hali mbaya ya uchakavu.

Mchango huo ulitolewa hivi karibuni na Meneja wa shirika hilo mkoani hapa, Dickson Hawanga baada ya kujionea mazingira magumu ya shule hiyo ikiwemo ukosefu wa choo, jambo ambalo linasababisha watoto kujisaidia vichakani.

Akizungumza mara baada ya kukabidhi hundi hiyo, kwa mwalimu mkuu wa shule hiyo, Edmund Hyera Meneja huyo alisema anataka kuona fedha hizo zinatumika ipasavyo kwa kazi iliyokusudiwa na sio vinginevyo.

Hawanga ameyaomba mashirika mbalimbali ya serikali na yasiyokuwa ya kiserikali, watu binafsi pamoja na wahisani toka nje na ndani ya nchi kumuunga mkono katika kuichangia shule hiyo, kwa kuipatia fedha au vifaa vya ujenzi ili ukarabati uweze kukamilika kwa wakati.

Awali akisoma taarifa fupi ya shule hiyo mbele ya Meneja huyo wa NSSF, mwalimu mkuu wa shule hiyo, Edmund Hyera alifafanua kuwa shule yake inakabiliwa pia na tatizo la ukosefu wa maji safi na salama ya bomba.

Wednesday, March 4, 2015

WAANDISHI WA HABARI RUVUMA, LINDI NA MTWARA WANOLEWA

Waandishi wa habari wakiwa katika picha ya pamoja.
Na Kassian Nyandindi,

Aliyekuwa Mtwara.

MTANDAO wa kutetea haki za binadamu Tanzania (THRDC) umewataka waandishi wa habari nchini, kuzingatia usalama wa kazi zao pindi wanapokuwa kazini ili kuweza kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza baadae, hasa katika kipindi kijacho kuelekea uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika, Oktoba mwaka huu.

Imeelezwa kuwa mwaka huu ni mwaka ambao unahekaheka nyingi, hivyo ni kipindi ambacho si salama kwa waandishi wa habari, na kwamba wanakumbushwa kuzingatia usalama wa kazi zao kwa kutambua hatari, vitisho pamoja na udhaifu katika usalama.

Hayo yalisemwa na Mkurugenzi wa THRDC, Onesmo Olengurumwa kwenye mafunzo ya usalama na tathimini ya athari kwa watetezi ambayo yametolewa kwa waandishi wa habari 28, toka nyanda za juu Kusini ambayo inajumuisha mikoa ya Ruvuma, Lindi na Mtwara.

Alisema kuwa kipindi hiki cha kuelekea kwenye uchaguzi mkuu ujao ni kipindi kigumu sana kwa waandishi wa habari, hivyo wanatakiwa kutambua mazingira ya kufanyia kazi kutokana na kukabiliwa na hatari kubwa kipindi cha kufanya kazi.