Wednesday, March 18, 2015

MKURUGENZI MBINGA ANAMATATIZO NI VYEMA ACHUNGUZWE, ADAIWA KUWAIBIA MAMILIONI YA FEDHA WAKULIMA WA KAHAWA

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Na Kassian Nyandindi,

BUNDI ameendelea kumsakama Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Hussein Ngaga ambapo sasa ameingia katika kashfa mpya akidaiwa kuwaibia wakulima wa kahawa wilayani humo, zaidi ya shilingi milioni 783,399,412 baada ya kahawa yao kuuzwa mnadani Moshi.

Wakulima hao ni wale ambao walikopeshwa fedha, shilingi bilioni 2 na Shirika la Hifadhi ya Jamii (NSSF) kupitia vyama vyao vya ushirika (AMCOS) vilivyopo wilayani humo, lengo la fedha hizo kutolewa na shirika hilo lilikuwa ni kutoa mikopo yenye gharama nafuu kwa wakulima wadogo wadogo, ambao wamejiunga kisheria katika vikundi hatimaye waweze kujikwamua kiuchumi na kuondokana na umasikini.

Hayo yamebainika kufuatia uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hizi, ambapo wakulima kutoka vyama vinne vya ushirika Mahilo, Ngaka, Ngima na Pilikano ambao hujishughulisha na uzalishaji wa zao la kahawa ndio walioibiwa fedha hizo.


Wizi huo unadhihirisha pale mkurugenzi huyo, badala ya kuwalipa wakulima hao shilingi bilioni 4,104,748,612 yeye aliwalipa shilingi bilioni 3,321,349,200 na kuficha mwenendo mzima wa fomu ya mauzo ya kahawa (Account Sell) ili wakulima hao wasiweze kujua juu ya ukweli wa kahawa zao namna gani zilivyouzwa huko mnadani, jambo ambalo analalamikiwa hadi sasa.

Gazeti hili limefanikiwa kupata nakala ya fomu ya mauzo ya kahawa kutoka Bodi ya Kahawa Tanzania (TCB) ambayo inaonesha uhalisia wa mauzo yote ya jumla kwa kahawa zilizouzwa na vyama hivyo vya ushirika  msimu wa mwaka 2014/2015  hivyo inadhirisha wazi wakulima hao wameibiwa fedha hizo, huku wengine wakisema wanaiomba serikali kuingilia kati ili waweze kupata fedha zao.

Wakulima hao wamekuwa wakimtaka kwa muda mrefu mkurugenzi huyo awapatie fomu hiyo ya mauzo ya kahawa, lakini hadi leo hii hajawapatia na wamegonga mwamba.

Kadhalika habari zilizopatikana kutoka kwenye vyanzo vyetu mbalimbali vinaeleza kuwa, hivi sasa baadhi ya wakulima wanampango wa kwenda kuuona uongozi wa NSSF, ili wafikishe kilio chao na kuwataka watume wakaguzi kwa ajili ya kukagua mwenendo wa matumizi ya fedha hizo walizokopeshwa, huku wakidai kuwa katika mkopo huo kuna zaidi ya shilingi milioni 300 zilibakia wakati wa mchakato wa manunuzi ya kahawa zao na hawajui zimeenda wapi.

Walisema kuwa wananyimwa hata kupewa fomu yenye kuonyesha mwenendo wa matumizi ya fedha hizo walizokopeshwa katika akaunti zao za vyama vya ushirika (Bank Statement) ambazo zilingizwa huko, ili waweze kujua zilitumikaje na hili linatokana na mkurugenzi Ngaga kupangia matumizi fedha hizo na kuzuia viongozi wa AMCOS hizo kutozifanyia matumizi wakati wa msimu wa manunuzi ya kahawa ulipofanyika, mpaka ruhusa itoke kwake jambo ambalo limefafanuliwa kwamba ni ukiukwaji wa sheria na taratibu za vyama vya ushirika.  

Walifafanua kwamba kitendo hicho kilichofanywa na mkurugenzi huyo   amemdanganya Rais Jakaya Kikwete, kwa kauli yake aliyoitoa hivi karibuni mbele yake kwamba fedha hizo watakabidhiwa walengwa wa vyama hivyo na kukopeshana wenyewe, kwa mujibu wa taratibu husika ili waweze kunufaika nazo na hatimaye waondokane na umasikini.

Rais Kikwete mnamo Julai 19 mwaka jana, alikabidhi mfano wa hundi kwa viongozi wa vyama hivyo vinne vya ushirika wilayani Mbinga, ambavyo vilikopeshwa fedha hizo na shirika hilo alipokuwa katika ziara yake ya kikazi wilayani humo, mkurugenzi huyo alimhakikishia Rais Kikwete mbele ya umma katika mkutano wa hadhara uliofanyika stendi kuu ya magari ya abiria mjini hapa kwamba taratibu zitazingatiwa.

Mahilo, Ngaka, Ngima na Pilikano ni vyama vya ushirika ambavyo hujishughulisha na uzalishaji wa zao la kahawa wilayani hapa na kila kimoja kilipewa shilingi milioni 500 lakini mkurugenzi Ngaga, alitengeneza utaratibu anaoujua yeye na kuvipatia fedha kidogo kidogo kulingana na kiasi cha kahawa, inayoingizwa kiwandani kwa ajili ya kukobolewa na ndio maana leo analalamikiwa.

Hata baadhi ya watumishi wa halmashauri ya wilaya hiyo (majina tunayo) walionekana muda mwingi wakitumia magari ya halmashauri kutia mafuta ambayo ilibidi yakafanye shughuli nyingine za maendeleo ya wananchi vijijini, wakilipana posho na kufanya ufuatiliaji kuhakikisha kwamba vikundi vinapeleka kahawa kiwandani ndipo vinakopeshwa fedha hiyo, jambo ambalo watu wengi walikuwa wakihoji inakuwaje halmashauri inaingia katika biashara ya kahawa?

Pia wakulima wa vyama hivyo vya ushirika kwa nyakati tofauti, walidai kuwa huenda mkurugenzi huyo alifanya hivyo akiwa na makusudi yake binafsi, ili fedha hizo aweze kunufaika nazo kwa namna moja au nyingine na sio mkulima, kama shirika la NSSF lilivyolenga.

Walidai kuwa pamoja na fedha hizo kulenga kumpunguzia mkulima wa kahawa makali ya maisha, bado hawaoni tofauti kama ilivyo kwa makampuni binafsi ambayo yalikuwa yakinunua kahawa wilayani humo, kwa bei inayoridhisha.

Baadhi ya wakulima walio katika vikundi ambao walikopeshwa fedha hizo wamesikitishwa na kitendo hicho, huku wengine wakieleza kuwa wao wanachoelewa ni kwamba fedha hizo baada ya kuingizwa kwenye akaunti za vyama vyao vya ushirika na wanachama kupitia viongozi wao ilikuwa wajipangie utaratibu wao wenyewe wa kukopeshana kwa kuzingatia taratibu na sheria za ushirika, kulingana na kiasi cha kahawa walichonacho na sio utaratibu alioutumia mkurugenzi huyo kupangia matumizi wakati akijua fika anavunja sheria au kukiuka taratibu husika.

Lengo la NSSF kuwakopesha wakulima fedha hizo, lilikuwa waondokane na changamnoto ya kukosa uhakika wa huduma za afya, ununuaji wa pembejeo ili waongeze uzalishaji na uhakika wa kipato baada ya kufikia umri wa uzee, ambapo husababisha kushindwa kuendelea na shughuli za kilimo.

Jitihada ya kumpata Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Ngaga ofisini kwake ili aweze kutolea ufafanuzi juu ya malalamiko haya hazikufanikiwa na simu yake ya kiganjani ilikuwa haipatikani.


No comments: