Sunday, March 22, 2015

CWT YAITAKA MANISPAA SONGEA KUMALIZA KERO ZA WALIMU

Na Amon Mtega,
Songea.

CHAMA Cha Walimu Tanzania (CWT) tawi la Songea mkoani Ruvuma, kimeutaka uongozi wa Manispaa hiyo kushughulikia matatizo ya walimu, ikiwemo kuwapandisha madaraja kwa wakati wale wote wanaostahili ili kuondoa malalamiko kwa baadhi yao, ambao ni muda mrefu sasa umepita hawajapandishwa.

Mwenyekiti wa CWT katika tawi hilo, Mathias Mwanjisi alitoa rai hiyo juzi alipokuwa kwenye mkutano mkuu wa uchaguzi viongozi wa chama hicho, akieleza kuwa licha ya wengi wao kuwa na vigezo vinavyostahili kupandishwa madaraja lakini hakuna kilichotekelezwa hadi sasa.

Kadhalika Mwanjisi ambaye alikuwa akitetea nafasi yake ya uenyekiti katika chama hicho, aliweza kushinda kwa kupata kura 84 huku mpinzani wake Edimund Nditi akipata kura 18 huku idadi ya wapiga kura wote ilikuwa  102.


Matokeo hayo yalitangazwa na msimamizi mkuu wa uchaguzi huo, Efigenia Nzota ambapo alitetea nafasi yake hiyo na mafanikio yake alisema kuwa changamoto kubwa ni kwa baadhi ya walimu, ambao wanastahili kupandishwa madaraja kushindwa kufanyiwa hivyo kwa wakati na hatimaye kutengeneza malalamiko dhidi yao.

Alisema kuwa ili kuondoa dhana hiyo ya malalamiko  ni lazima viongozi wa kitengo husika cha Manispaa ya Songea, kupeleka taarifa zote za walimu wanao stahili kupanda madaraja katika ofisi husika za makao makuu na kufanyiwa kazi kwa haraka.

Mwenyekiti huyo  akitoa neno la shukrani kwa wajumbe waliohudhuria mkutano huo wa uchaguzi, alisema kazi kubwa ni kushikamana na kukijenga chama kwa kuepusha migogoro ambayo inaweza kuwagawa bila sababu za msingi.

“Naomba tushikamane kukijenga chama chetu, tusiposhikamana tutakiharibu chama na matokeo yake chama kitaingia kwenye migogoro ambayo inaweza ikatugharimu baadaye, jambo ambalo siyo jema mbele ya jami”, alisema.


Hata hivyo katika uchaguzi huo nafasi mbalimbali ziligombewa ikiwemo ya mweka hazina ambapo Emmnuel Kayuza alipita bila kupingwa, kutokana na mpinzani wake Ananias Mbilinyi kujitoa mapema huku nafasi ya uwakilishi walimu wanawake aliibuka kidedea, Sophia Luoga ambaye aliwabwaga wapinzani wake watano.

No comments: