Friday, March 13, 2015

TUNDURU KASKAZINI WAPENDEKEZA MBUNGE WAO

Na Steven Augustino,
Tunduru.

WAPIGA kura wa Jimbo la Tunduru kaskazini mkoani Ruvuma, wamechukua jukumu la kumpendekeza Omary Kalolo, kuwa mgombea pekee kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika jimbo hilo, kwa nafasi ya ubunge katika uchaguzi mkuu ambao unatarajiwa kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu.

Shirikisho la umoja wa vijana la CCM wilayani Tunduru katika jimbo hilo, ndilo ambalo limempendekeza mgombea huyo, kwa madai kuwa wanaimani naye katika utendaji wa kazi zake.

Aidha vijana hao wamemtaka Kalolo kutoa tamko ambalo litaunga mkono juu ya maamuzi na msimamo uliotolewa na shirikisho hilo, wakidai kuwa yeye ndiye chaguo la wengi.

Msimamo wa kumtaka Kalolo kugombea, umejitokeza kupitia risala yao iliyosomwa na Ally Nyama kwenye sherehe za ushindi wa asilimia 75 katika matokeo ya uchaguzi wa serikali za mitaa uliofanyika hivi karibuni mjini Tunduru.


Walisema wameamua kutoa msimamo huo mapema kutokana na kukosa imani na wagombea wengine (majina tunayo) ambao wanataka kujitokeza kugombea katika jimbo hilo huku wakiwa hawana maaadili ya kichama.

Katika kuhakikisha kuwa nia yao hiyo inafanikiwa, vijana hao walimkabidhi mgeni rasmi katika sherehe hizo, ambaye Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Tunduru Hamis Kaesa kiasi cha shilingi 100,000 ili zikae huko, ambazo zitamwezesha mteule wao kwenda kuchukua fomu ya kuwania ubunge huo wakati utakapowadia.

Taarifa hiyo iliyoonekana kuungwa mkono kwa zaidi ya asilimia 60 ya wananchi walioshiriki katika sherehe hizo, vikiwemo vikundi vya kwaya ambavyo viliendelea kufafanua katika nyimbo zao kuwa, Kalolo anao uwezo mkubwa wa kuwaongoza kutokana na uzowefu alioupata wakati akiwa katibu wa chama hicho ngazi ya wilaya na mkoa.

Huku akishangiliwa na maelfu ya wanachama na wakereketwa wa Chama Cha Mapinduzi ambao walihudhuria sherehe hizo, Nyama aliendelea kufafanua kuwa maamuzi hayo hayatafanywa kwa kukurupuka, bali wameyafanyia uchunguzi wa kina na kujiridhisha kuwa wagombea wote wanaotajwa kuwania nafasi hiyo hawana sifa zinazomfikia mteule huyo.

“Sisi wanajimbo la Kaskazini kupitia tamko letu hili kwa dhati na tunakuomba utoe tamko litakalojibu leo ombi letu hili, ambalo litatuhakikishia ushindi katika jimbo letu kwani wewe ni hitaji la wengi”, alisisitiza Nyama.


Alisema maamuzi hayo yametokana na mtazamo wa vijana wengi katika Jimbo hilo, kuamini kuwa vijana ndiyo nguvu kazi hivyo ni bora nafasi hiyo wampatie kijana mwenzao.

No comments: