Sunday, March 22, 2015

MAHAKAMA YA KADHI KULETA MACHAFUKO HAPA NCHINI, KURA YA HAPANA IPO PALE PALE

Padre Baptiste Mapunda.
Na Padre Baptiste Mapunda,

KWANZA ni lazima ieleweke kwamba, Wakristo kupitia Maaskofu wao hawaipingi Mahakama ya kadhi kama mahakama ya kadhi, ila wanachopinga ni uanzishwaji kwa mamlaka ya serikali.

Swali ni kwa nini serikali ijishughulishe na mahakama ya dini, wakati katiba imekataa? Watanzania  wengi wanajiuliza kuna agenda gani  ya siri iliyopo nyuma ya hii mahakama? Kwa mantiki hiyo na kwa kuzingatia tamko la Maaskofu wa Jukwaa la Wakristo na sababu nzito iliyotolewa, wakristo tujiandae kuipigia kura ya hapana katiba mpya kama tulivyoelekezwa na wala siyo kulazimisha kama wengine wanavyotafsiri tamko hilo.

Toka kuundwa kwa taifa letu la Tanganyika-Tanzania nchi yetu inajulikana kwamba serikali yake si ya kidini ila wananchi wake wanadini. Katiba ya mwaka 1977 inatamka hivyo na kila mtu anajua na hivyo basi masuala yote ya kidini  yanapaswa kuendeshwa na dini husika.

Waumini wa imani tofauti mathalani Wakristo na Waislamu, walikuwa wamekaa kwa amani hadi miaka ya 90  katika kipindi cha Rais wa awamu ya pili, Ally Hassan Mwinyi maarufu kama mzee wa “Ruksa” ndipo choko choko za kidini zilipoanza  kujitokeza.

Choko choko hizi ziliambatana na madai kwamba, Waislamu walikuwa wanaonewa, kunyanyaswa na kubaguliwa chini ya mfumo wa kikristo.

Kikaja kipindi cha Benjamini  Mkapa madai yalijitokeza, lakini yeye alifuata katiba ya nchi hivi hakuweza kuyapa nafasi hata ya kujadiliwa bungeni. Lakini leo cha ajabu ni kwamba Chama Cha Mapinduzi (CCM) ililiweka suala la mahakama ya kadhi katika ilani yake ya uchaguzi ya mwaka 1995.


Kuanzia hapo basi Waislamu nchini, wameendelea na madai yao ya kubaguliwa kwa misingi kwamba nchi inaendeshwa kwa “mfumo wa kikristo” sielewi hata maana yake ni nini.

Rais Kikwete yeye anajitetea anasema siyo yeye aliyeliweka katika  ilani ya uchaguzi ya mwaka l995, kwani yeye hakuhusika katika utengenezaji wa ilani hiyo. Je madai hayo ni ya kweli?

Maaskofu wa madhehebu ya kikristo wameshamwambia bayana  Rais Kikwete kwamba suala hilo ni la kiimani na hivi halifai kuingizwa katika katiba na wala halitawezekana. Lakini bado serikali ya Rais  Kikwete inaendelea kulipigania kiaina aina. Sasa limeingizwa katika agenda ya katiba mpya, swali je, Rais  Kikwete atafanikiwa kuwapatia Waislamu  mahakama ya kadhi kabla hajaondoka ikulu?

Kwa upande wangu naliona suala la mahakama ya kadhi ni kama sehemu ya utekelezaji wa Tamko la Abuja la mwaka 1990 juu ya ustawi wa dini ya Kiislamu barani Afrika. Inasemekana  lengo mojawapo kubwa la tamko hilo, ni kufuta imani zisizo za kiislamu barani Afrika katika nchi wanachama na hivi kuanzisha dola ya kiislamu itakayotawala kwa kutumia sharia.

Kama kuna mtu anabisha juu ya hili basi aende tu kusearch katika  mitandao, “ABUJA DECLARATION” na atembelee  http//eaclj.org/component/content/article 25-religion-feature-article/… atapata elimu kubwa sana juu ya jambo hili.

Suala la mahakama ya kadhi hata kama linawahusu waislamu tu katika ndoa na mirathi linabaki kuwa la kidini (imani). Bunge la katiba linapata wapi mamlaka ya kulijadili jambo la kidini wakati katiba yetu imesema mambo ya dini yatakuwa nje ya katiba? Je, bunge letu sasa limegeuka la kidini? Hawa Maaskofu na wachungaji  waliomo katika bunge hili wanajisikiaje juu ya suala hili?

Kwa kweli hii ni alama kwamba kama vile Mungu alivyoufanya moyo wa Farao ukawa mgumu, basi  hata  leo anaendelea kumpa Rais Kikwete na serikali yake ya CCM  ugumu wa kuelewa na hivi mwishowe Mungu atashinda tu. Spika wa Bunge la katiba anasema ameunda kamati ya watu kumi kuangalia suala la mahakama ya kadhi je, wataliangalia kwa misingi ipi? Sasa ni wazi kwamba Bunge hili limepotoka vibaya sana na hivi linapaswa kusitishwa haraka sana.

Serikali ya CCM  na Rais Kikwete  lazima ijiepushe na kujihusisha na masuala ya kidini ndani ya Bunge la katiba na katika maeneo mengine, nasema hivi kwa sababu hii ni kinyume cha sheria kabisa na serikali inajua hilo. Rais Kikwete hachoki bado anaendelea  kulipigania suala hilo ingawaje anajificha asionekane lakini kwa sababu ni suala linalohusu haki kwa dini nyingine,  suala hili na mipango yote ya siri inajulikana. Kwa Mungu hakuna siri yeyote ile  kuna siku itafumuka tu.

Nataka  kuihakikishia serikali ya CCM kwamba mpango huu hautafanikiwa kamwe katika nchi hii na ukifanikiwa kitakuwa chanzo kikubwa sana cha machafuko katika nchi, huu ni utabiri wangu. Ninawasihi wanaCCM kuachana na mpango huu mara moja kwani tutaomba  usiku na mchana na Mungu atasikia tu. Kama CCM ina uwingi wa wabunge katika nchi hii, basi sisi Wakristo tuna uwingi wa maaskofu, mapadre, wachungaji, wainjilisti, makatekista na waumini na hata vichaa na wavuta bangi wataunga mkono jitihada zetu serikali ya CCM lazima ijue haiwezi kushindana na nguvu za Mungu iulize Kenya kilitokea nini?

Mpango wa kuifanya Tanzania nchi ya Kiislamu kwa njama za mahakama ya kadhi  umechelewa. Tunaungana na Maskofu na viongozi wote wa kikristo  walioshauri tayari kwamba mahakama ya kadhi ianzishwe nje ya katiba, kama yalivyo mahakama ya kanisa katoliki na madhehebu mengine. Kwa nini kutafuta nguvu ya katiba? Je, watu  wakishawishika kutumia mahakama  ya kadhi vibaya itakuwaje? Mahakama ya kadhi haina maslahi kwa Watanzania labda Mashekhe wachache.

Hata ndani ya waislamu  wenyewe, mahakama ya kadhi italeta  mgawanyiko kati ya Bakwata na Ansar Sunnar. Hawa ni wale wanaoendesha shuura ya Maimam wakiwa na ushawishi mkubwa katika jamii ya waislamu wakisaidiwa na vyombo vyao vya mawasiliano kama Radio Imani, Times FM, na gazeti la  An-Nuur na Nasaha.

Suala la mahakama ya kadhi inaonekana ni la kimaslahi zaidi yaani; ajira kwa wachache. Lakini swali la msingi ni hili, je  watalipwa na fedha za nani? Kama mahakimu na watendaji wa mahakama za kadhi watalipwa na fedha za walipakodi yaani Watanzania wote basi huu ni unyanyasaji na ubaguzi ambao unageuka kuwa udini na wala si haki kwa madhehebu mengine.

Ili kuleta usawa kwa dini zote  na kwa sababu serikali ina pesa nyingi  basi kila dini iingize mahakama zake ndani ya katiba na watendaji wake walipwe, namna nyingine halitawezekana. Hivi itawezekana vipi Wakristo wakubali mahakama za kadhi zitoe ajira kwa Waislamu kuanzia ofisi ya Mtaa, Kata, tarafa, Wilaya, Mkoa na Taifa kwa malipo ya pesa ya walipa kodi wa Tanzania wakiwamo Wakristo. Hii ni haki kweli?

Wakristo wote wa Bara na Zanzibari wanahaki ya kupinga mahakama ya kadhi (MK). Kuna uvumi kwamba maoni ya katiba mpya juu ya mahakama ya kadhi   yamechakachuliwa kasoro Mbeya na Mwanza. Sasa najiuliza hivi mkoa wa Ruvuma Wakristo ndiyo walioipitisha mahakama ya kadhi au ni nani maana idadi ya Waislamu mkoani Ruvuma ni ndogo sana, ukilinganisha na ya  Wakristo.

Wanaodai uwepo wa ubalozi wa Vatikani nchini, kwamba ni kinyume cha katiba basi hawaelewi kitu. Ni vyema serikali ikalitolea jambo hili maelezo ya kina bila kuogopa kundi lolote lile na kuonyesha wazi kwamba, ubalozi huo unaendeshwa kwa pesa ya Wakatoliki na si pesa ya umma.

Ni upendeleo serikali kutumia pesa ya walipakodi kwa masilahi ya dini moja, suala la mahakama ya kadhi litaleta mgogoro wa kidini na machafuko nchini kama ilivyotokea katika suala la “nani ana haki na mamlaka ya kuchinja.” Namna nyingine Wakristo wote tutaungana ili kuikataa katiba mpya kwa sababu imebeba masilahi ya dini moja.

Mwandishi wa makala haya anapatikana kwa barua pepe; frmapunda91@gmail.com

No comments: