Friday, March 30, 2018

WAPIGWA FAINI KWA KUKATAA KUCHANGIA FEDHA ZA USAFI WA MAZINGIRA


Na Muhidin Amri,   
Songea.

BAADHI ya Wakazi kumi wanaoishi katika maeneo mbalimbali Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, wamepigwa faini ya shilingi Milioni moja kwa ujumla wao baada ya kubainika wamekataa kulipa shilingi 2,000 ambayo inatozwa kila mwezi kwa kila kaya, kwa ajili ya kuchangia huduma za usafi wa mazingira katika Manispaa hiyo.

Mahakama ya Mwanzo Mfaranyaki iliyopo mjini hapa, ndiyo iliyowahukumu adhabu hiyo na kwamba Wakazi hao ni wale wa kutoka katika kata ya Majengo, Misufini, Bombambili na Matarawe.

Philipo Beno ambaye ni Mkuu wa masuala ya usafi wa mazingira katika Mnispaa ya Songea akizungumza juzi na Waandishi wa habari, alisema kuwa wameamua kuanza kuwapeleka Mahakamani Wananchi wote wanaonekana kukaidi kulipa mchango huo, ili iweze kuwa fundisho kwa wengine wenye tabia kama hiyo na hatimaye waweze kuchangia kwa urahisi bila usumbufu wowote kwa kufuata taratibu na sheria ndogo zilizowekwa.

UJENZI MACHINJIO YA KISASA SONGEA KUKAMILIKA NDANI YA MKATABA


Na Albano Midelo,     
Songea.

KATIKA Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, Mradi wa machinjio ya kisasa unaofadhiliwa na Benki ya Dunia kwa gharama ya shilingi zaidi ya bilioni tatu, unatarajiwa kukamilika kabla ya mwezi Juni 30 mwaka huu.

Mradi huo unajengwa katika kata ya Tanga iliyopo kwenye Manispaa hiyo hadi sasa umefikia karibu ya asilimia 80 ujenzi wake, ambapo Mkandarasi wa ujenzi wa mradi huo ni Kampuni ya Giraffe ambayo imeahidi kukamilisha kazi hiyo kabla ya tarehe ya mwisho wa mkataba ambao umeanzia Julai 2017 na kukamilika Julai 2018 mwaka huu.

“Imebakia mistari michache kukamilisha kuzungusha jengo lote kisha tunaanza kazi ya kuezeka machinjio, hadi mwishoni mwa mwezi Mei tunatarajia kazi itakuwa katika hatua za mwisho”, alisema.

Thursday, March 29, 2018

TBA YAKABIDHI BWENI SEKONDARI YA WASICHANA SONGEA

Na Kassian Nyandindi,     
Songea.
 
WAKALA wa Majengo Tanzania (TBA) wamekabidhi jengo moja, ambalo ni bweni la kulala wanafunzi katika shule ya Sekondari ya Wasichana Songea iliyopo Mkoani Ruvuma, ambalo limekarabatiwa kwa zaidi ya shilingi Milioni 102.

Kabla ya kukabidhi jengo hilo umefanyika ukaguzi wa bweni hilo ambalo ni la ghorofa likiwa na uwezo wa kuchukua Wanafunzi 110.

Ukaguzi huo uliwashirikisha watalaamu kutoka Manispaa ya Songea wakiwemo na mwakilishi wa Mkurugenzi wa Manispaa hiyo Frowin Komba, Mhandisi wa ujenzi Karoline Kandonga, Mkuu wa shule hiyo Tupoke Ngwala, Mwakilishi wa TBA Mhandisi Eugenics Thomas na viongozi wa Serikali ya wanafunzi katika shule ya Sekondari ya Wasichana Songea.

Tuesday, March 27, 2018

WAJAWAZITO TUWE MACHO TUNDURU WAISHUKURU TASAF KUWAJENGEA ZAHANATI

Na Muhidin Amri,    
Tunduru.

WANAWAKE Wajawazito katika kijiji cha Tuwe Macho kata ya Tuwe Macho Wilayani Tunduru Mkoa wa Ruvuma, wameishukuru Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) Wilayani humo kwa kujenga Zahanati ambayo hivi sasa inawasaidia kupata tiba na ushauri juu ya masuala ya afya na uzazi, hivyo kuweza kupunguza idadi ya vifo vya akina mama Wajawajazito kabla na wakati wa kujifungua.

Walisema kuwa kabla ya TASAF kujenga Zahanati hiyo, walikuwa wakilazimika kutembea umbali mrefu na kutumia muda mwingi kwenda kutafuta huduma husika Hospitali ya Wilaya Tunduru iliyopo mjini hapa, jambo ambalo liliwafanya kwa kiasi kikubwa kukosa hata muda wa kushiriki kikamilifu katika shughuli zao za maendeleo.

Aidha wameiomba Serikali kuboresha mfumo wa utoaji huduma za afya ikiwemo kuwaletea waganga, vitanda vya kujifungulia sambamba na baadhi ya vifaa tiba ambavyo vitawezesha kupata huduma bora hasa wakati wa kujifungua.

HOMA YA NGURUWE BADO TISHIO IMEUA 864 SONGEA

Ugonjwa wa Nguruwe, unavyoteketeza Nguruwe Songea Mkoani Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,     
Songea.

KATIKA Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, wamesitisha uchinjaji wa Nguruwe katika maeneo yote ya Manispaa hiyo, tangu mwezi Februari mwaka huu, kufuatia kuibuka kwa homa ya Nguruwe ambayo haina kinga wala tiba.

Takwimu ambazo zimetolewa na Afisa Mifugo na Uvuvi wa Manispaa ya Songea, Bilaly Mwegeni zinaonesha kuwa homa hiyo ambayo inafahamika kwa jina la “African Swine Fever” katika kipindi cha kuanzia Januari 31 hadi Machi 14 mwaka huu imeua Nguruwe 864.

Mwegeni alisema kuwa takwimu hizo za vifo ni matukio ambayo yameripotiwa katika idara yake, ambapo uchunguzi umebaini kuwa zaidi ya nusu ya Nguruwe waliopo katika Manispaa hiyo wamekufa kutokana na ugonjwa huo, hali ambayo inahatarisha kuteketeza Nguruwe katika Manispaa hiyo.

Sunday, March 25, 2018

MANISPAA SONGEA YAINGIA MKATABA UJENZI WA STENDI MPYA YA KISASA

Hili ni eneo la kata ya Tanga ambalo ujenzi wa Stendi ya kisasa katika Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma unatarajiwa kuanza kujengwa.

Na Kassian Nyandindi,         
Songea.

KAMPUNI ya Serikali ya China, inayoitwa China Sichuan International Cooperation imesaini mkataba wa miezi 18 na Halmashauri ya Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, kwa ajili ya ujenzi wa Stendi mpya ya mabasi katika eneo la Tanga kuanzia Aprili Mosi mwaka huu.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa hiyo, Mhandisi Samwel Sanya alisema kuwa Mkataba huo unaanzia Machi 25 hadi Septemba 30 mwaka 2019.

Alisema kuwa zaidi ya Shilingi Bilioni sita zitatumika katika awamu ya kwanza ya ujenzi wa stendi hiyo ya kisasa na kwamba lengo la kufanya hivyo ni kuendana na kasi ya ukuaji wa mji, hivyo Manispaa iliamua kutenga eneo la kituo kikuu cha mabasi kuwa katika mtaa huo wa Tanga ikiwa ni umbali wa takribani kilometa 14 toka mjini Songea.

TASAF TUNDURU YATUMIA BILIONI 946.3 UTEKELEZAJI MIRADI KAYA MASKINI


Na Muhidin Amri,        
Tunduru.

MFUKO wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) katika Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma, umepokea jumla ya Shilingi Bilioni 946,388,947.40 kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali iliyopangwa kutekelezwa katika mwaka wa fedha wa 2017/2018.

TASAF katika Wilaya hiyo hadi kufikia mwezi Machi mwaka huu imeweza kutekeleza sehemu tatu ya mpango huu wa kunusuru kaya maskini ambapo ni wa Uhawilishaji wa Fedha (CCT) kwa awamu 25 tangu kuanzishwa kwake, Utekelezaji wa Miradi ya Ajira za Muda (PWP) kwa miaka miwili, Ujenzi wa miundombinu ya Barabara pamoja na ujenzi wa zahanati ya kijiji cha Tuwemacho.

Mratibu wa Mfuko huo Wilaya ya Tunduru, Muhidin Shaibu alisema hayo wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu juu ya mapokezi ya fedha hizo.

MNADA WAINGIZA MAMILIONI YA FEDHA MANISPAA SONGEA

Baadhi ya mitambo mbalimbali na  magari yaliyopigwa mnada na Manispaa Songea Mkoani Ruvuma.

Na Kassian Nyandindi, 
Songea.

HALMASHAURI ya Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, Machi 24 mwaka huu imeuza kwa njia ya mnada wa hadhara mitambo yake 16 ikiwemo magari, pikipiki na mitambo mingine chakavu na kufanikiwa kukusanya zaidi ya Shilingi Milioni 87.75.

Mitambo hiyo ambayo imeuzwa katika mnada huo ni Mitsubishi Bozer, Toyota land Cruiser station wagon mbili, Nissan station wagon, Nissan station wagon tipper, Isuzu tipper mbili, Hyster Roller, pikipiki sita aina ya Suzuki 125, pikipiki aina ya Honda 110 na Hysosung.

Fedha hizo taslimu ambazo zimekusanywa katika mnada huo uliofanyika kwenye Karakana ya Manispaa ya Songea na kusimamiwa na Kampuni ya YONO Auction Mart chini ya dalali mahiri, Zuberi Lumbizi ni shilingi zaidi ya milioni 26.

Thursday, March 22, 2018

MCHINA KUENDELEA NA UKARABATI BARABARA MANISPAA SONGEA

Moja kati ya barabara za Manispaa ya Songea ya FFU Matogoro ambayo inafanyiwa ukarabati.
Na Albano Midelo,      
Songea.

HATIMAYE Kampuni ya kimataifa ya Serikali ya China, inayoitwa China Sichuan International Co-operation, kufikia Machi 25 mwaka huu itaanza rasmi ukarabati wa barabara za Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, kwa kiwango cha lami nzito.

Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Songea Mkoani humo, Mhandisi Samwel Sanya alisema hayo leo kuwa Kampuni hiyo tayari imesaini mkataba baina yake na Halmashauri ya Manispaa hiyo.

Alifafanua kuwa mkataba unaonesha kuwa, ukarabati wa barabara hizo zenye urefu wa kilometa 10.3 utaanza Machi 25 mwaka huu na unatarajia kukamilika Septemba 30 mwaka 2019.

Tuesday, March 20, 2018

MAJALIWA ATAKA SULUHISHO MAGONJWA YASIYOAMBUKIZA


Na Mwandishi wetu,

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amewataka Mawaziri wa Afya kutoka nchi tisa za Afrika kutoa mapendekezo ya namna ya kutokomeza magonjwa yasiyo ambukiza, kwa wakuu wa nchi hizo ili yafanyiwe kazi haraka.

Aliyasema hayo jana Machi 19 mwaka huu wakati alipokuwa akifungua Mkutano wa 65 wa Mawaziri wa Afya, kutoka nchi tisa wanachama wa Jumuiya ya Afya kwa nchi za Afrika Mashariki, Kati  na Kusini (ECSA-HC).

Alisema kuwa magonjwa yasiyo ambukiza ni miongoni mwa magonjwa ambayo yameendelea kuwatesa wananchi kwa kiasi kikubwa, katika nchi nyingi za Bara la Afrika hivyo vyema mawaziri hao wakatoa mapendekezo ya namna ya kuyatokomeza.

WALIOPORA VIWANJA UWT MBINGA KUKIONA CHA MOTO

Upande wa kulia ni Katibu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Wilaya ya Mbinga, Martina Katyale akikabidhi taarifa fupi ya maendeleo ya umoja huo Wilayani humo kwa Katibu Mkuu wa UWT Taifa, Amina Makillagi alipokuwa juzi Katibu huyo katika ziara yake ya siku mbili Wilayani hapa. 
Aliyesimama upande wa kulia ni Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Amina Makillagi akizungumza na baadhi ya Wanawake wa Wilaya ya Mbinga, ambao walikusanyika katika uwanja wa Masumuni uliopo mjini hapa ambapo alisisitiza kuwa kwa wale watu waliopora viwanja vya UWT wahakikishe wanavirudisha haraka kabla hawajachukuliwa hatua kali za kisheria.

Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

KATIBU Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Amina Makillagi amesema kwamba, Viwanja vyote ambavyo vina migogoro na ni mali ya umoja huo Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma, wale wote ambao wamekuwa wakivitaka wakidai kuwa ni vya kwao wavirudishe mapema kabla hawajachukuliwa hatua kali za kisheria.

Alisisitiza kuwa yeyote aliyepora mali za Umoja huo, Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Rais Dokta John Pombe Magufuli atapelekewa ripoti ili waweze kushughulikiwa. 

“Popote walipo hao ambao wamepora viwanja vyetu warudishe mara moja hatutaki utani, niwasihi na kuwaomba waachane na ubinafsi warudishe mali zetu”, alisisitiza Makillagi.

MAKILLAGI ATAKA UWT KUWA KIMBILIO LA WANAWAKE


Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

JUMUIYA ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) imesema kuwa wanataka kuona kwamba inakuwa kimbilio kubwa kwa Wanawake, katika kuanzisha vikundi vya ujasiriamali ambavyo vitaweza kuwakomboa waweze kuondokana na umaskini.

Vikundi hivyo imesisitizwa kuwa viundwe na kusajiliwa kisheria ili kuweza kukuza uchumi wa akina mama na kujenga mshikamano wa pamoja utakaowafanya waache tabia ya kuwa na makundi ambayo hapo baadaye yanawagawa wao na chama kwa ujumla.

Amina Makillagi ambaye ni Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) alisema hayo juzi, alipokuwa katika ziara yake ya siku mbili Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma akitembelea kujionea maendeleo ya umoja huo.

DC ATAKA WATUMISHI WADANGANYIFU MADABA WASHUGHULIKIWE


Na Muhidin Amri,    
Madaba.

MKUU wa Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma, Pololet Mgema amemuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Madaba, Shafi Mpenda kuwachukulia hatua za kinidhamu Watumishi wake waliopo katika Halmashauri hiyo ambao wamehusika na kufanya udanganyifu katika ujenzi wa vyumba vya madarasa shule ya msingi Kibulang’ombe iliyopo kata ya Likalangiro Wilayani hapa.

Udanganyifu huo umefanyika kwenye ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa katika shule hiyo na kusababisha ujenzi kusimama kwa muda kufuatia watu waliopewa dhamana ya kusimamia hilo kukiuka taratibu husika hasa katika manunuzi vifaa ikiwemo bati geji 32 badala ya geji 30 kama ilivyoagizwa na Serikali jambo ambalo Mkuu huyo wa Wilaya amesimamisha ujenzi huo kwa muda mpaka tatizo hilo litakapokwisha.

“Nimewatuma watu wangu kufuatilia kila mradi unaotekelezwa katika Halmashauri yako, walipofika pale shule ya msingi Kibulang’ombe kwa kweli  ni masikitiko makubwa kwani bati zilizonunuliwa ni geji 32 badala ya geji 30, kwa hiyo nakuagiza wewe na wataalamu wako lazima mfuatilie hili ili kujiridhisha ni nani aliyehusika kufanya udanganyifu”, alisema Mgema.

WANAFUNZI 60 WA KIKE MBINGA WASHINDWA KUENDELEA NA MASOMO


Na Kassian Nyandindi,   
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa katika shule za Sekondari zilizopo Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma, Wanafunzi 60 wa kike wanaosoma katika shule hizo wameshindwa kuendelea na masomo mwaka jana 2017 kutokana na kuwa na ujauzito.

Wazazi, walezi na jamii ndiyo wamenyoshewa kidole katika suala zima la malezi ya watoto wa kike, ambapo wamekuwa hawatoi ushirikiano wa kutosha hata pale mtoto huyo anapokuwa amepata ujauzito hususan Serikali inapotaka kuchukua hatua dhidi ya watuhumiwa wanaohusika na tatizo hilo.

Joseph Kapere ambaye ni Afisa elimu Sekondari wa Wilaya hiyo alisema hayo hivi karibuni, wakati alipokuwa akizungumza kwenye kikao cha tathimini ya elimu kilichofanyika mjini hapa.

Monday, March 19, 2018

WAHUDUMU WA AFYA MKAKO MBINGA WAZALISHA MAMA WAJAWAZITO KWA KUTUMIA MWANGA WA SIMU ZA MKONONI

Amina Makillagi.

Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

WAHUDUMU wa Afya wanaofanya kazi katika Zahanati ya Mkako iliyopo Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma, wamefikisha kilio chao kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Amina Makillagi wakilalamikia kwamba kutokana na kukosa mwanga wa umeme kwenye zahanati hiyo, nyakati za usiku wamekuwa wakizalisha akina mama wajawazito kwa kutumia mwanga wa simu za mkononi huku wakiwa wameziweka mdomoni.

Aidha walisema kuwa kwa kulinda hadhi ya mwanamke wanahitaji Serikali iboreshe mazingira ya zahanati hiyo, ikiwemo chumba cha kujifungulia akina mama hao ambacho hivi sasa hakina mazingira rafiki hasa pale wanapotoa huduma husika.

“Tumekuwa tukipata tatizo la mwanga tunapotoa huduma nyakati za usiku, tunazalisha akina mama 10 hadi 15 kwa mwezi kwa kutumia mwanga wa simu za mkononi tumeahidiwa kwa muda mrefu kuletewa umeme, lakini tunaomba tuharakishiwe ili tufanye kazi zetu kwa ufanisi zaidi”, walisema.

Sunday, March 18, 2018

DED MADABA AMTUMBUA AFISA MANUNUZI


Na Muhidin Amri,         
Madaba.

UKIUKAJI wa taratibu za manunuzi katika Halmashauri ya Wilaya ya Madaba Mkoani Ruvuma, ambako kumefanywa na Mkuu wa idara ya Manunuzi katika Halmashauri hiyo, Boniface Soko kumemfanya Mkurugenzi Mtendaji wa Wilaya hiyo Shafi Mpenda kumsimamisha kazi mtumishi huyo.

Mpenda alisema kuwa, Soko amekuwa akifanya hivyo kwa makusudi na kwamba Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) imekuwa ikisisitiza na kutoa miongozo mara kwa mara namna ya kutumia mfumo wa Force Account, lakini yeye hazingatii hilo.

Alisema kuwa mfumo huo umekuwa mzuri kwani unalenga kutumia mafundi wanaopatikana katika jamii, badala ya kutumia Makandarasi ili kuweza kuepuka gharama kubwa ambazo Serikali imekuwa ikitumia katika utekelezaji wa miradi mbalimbali.

Wednesday, March 14, 2018

SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WAFUGAJI WALIOVAMIA HIFADHI MADABA


Na Kassian Nyandindi,      
Madaba.

WAFUGAJI waliovamia katika hifadhi ya Gesi Masowa, katika kijiji cha Kipingo kata ya Lituta Halmashauri ya Wilaya ya Madaba Mkoani Ruvuma, wanatakiwa kuondoka mara moja kabla Serikali haijatumia nguvu na kuwachukulia hatua kali za kisheria.

Hayo yalisemwa juzi na Mkuu wa Wilaya ya Songea, Pololet Mgema wakati alipokuwa akizungumza na Wawakilishi wa wafugaji hao, Wenyeviti wa vijiji, Maafisa mifugo pamoja na viongozi wa Wilaya ya Madaba.

Mgema alisema kuwa Serikali inayo taarifa kuwa baadhi ya wafugaji wameingia katika jimbo la Madaba na kwenda moja kwa moja katika hifadhi zilizotengwa kwa ajili ya makazi ya wanyama na kufanya shughuli zao za ufuagaji, ambapo amewataka baada ya wiki moja kuanzia sasa wawe wameondoka na kwenda katika ranchi ya Ngadinda iliyopo Wilayani humo ambayo imetengwa na Wizara ya mifugo kwa ajili ya shughuli hizo za ufugaji.

DC APONGEZA USIMAMIZI NA MATUMIZI SAHIHI YA FEDHA ZA SERIKALI MADABA

Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Madaba Mkoani Ruvuma, Shafi Mpenda (aliyevaa suti rangi nyeusi) akimuonesha Mkuu wa Wilaya ya Songea Mkoani humo, Pololet Mgema baadhi ya vitanda vilivyowekwa katika moja kati ya bweni lililojengwa na Serikali kupitia mpango wa P4R katika shule ya Sekondari Mahanje iliyopo Madaba.

Na Kassian Nyandindi,      
Madaba.

MKUU wa Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma, Pololet Mgema ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Madaba Mkoani humo kwa usimamizi na matumizi sahihi ya fedha za Serikali ambazo zinapelekwa katika Halmashauri hiyo, kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo na kuboresha maisha ya wananchi.

Mgema alitoa kauli hiyo juzi alipotembelea na kujionea mradi wa ujenzi wa mabweni mawili, madarasa mawili na matundu sita ya vyoo katika shule ya Sekondari Mahanje iliyopo kata ya Mahanje ndani ya Halmashauri hiyo ambayo inajengwa kupitia mpango wa P4R.

Serikali imeipatia Halmashauri ya Madaba, shilingi milioni 196.6 kwa ajili ya kukamilisha kazi hiyo ambapo mabweni hayo mawili yenye uwezo wa kuchukua watoto 80 kila moja, madarasa na matundu ya vyoo yamekwisha kamilika.

UWT TUNDURU WAONESHA MSIMAMO WAO


Na Muhidin Amri,      
Tunduru.

JUMUIYA ya Wanawake Tanzania (UWT) Wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma imepata Mwenyekiti wake, Zuhura Maftari baada ya kumchagua kwa ushindi wa kishindo kuongoza jumuiya hiyo.

Msimamizi wa  uchaguzi huo ambao ni wa marudio uliofanyika kwenye ukumbi wa UWT Wilayani humo, ambaye ni Mjumbe wa Kamati tendaji ya Mkoa huo, Maristela Mapunda akitangaza matokeo ya uchaguzi huo alisema kuwa Maftari alishinda kwa kupata kura 367.

Alifafanua kuwa katika ushindi huo, Maftari aliongeza idadi ya kura na kwamba katika uchaguzi uliofanyika hapo awali wagombea walioshindwa, walikata rufaa huku akiwa na ushindi wa kura 346.

ACT WAZALENDO TUNDURU WAPATA PIGO WANACHAMA WAKE 1,630 WAHAMIA CHAMA TAWALA


Na Muhidin Amri,         
Tunduru.

VIONGOZI na Wanachama 1,630 wa Chama cha ACT– Wazalendo katika Wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma, wamefunga milango ya chama chao na kukihama chama hicho huku wakijiunga na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Wanachama hao walifikia maamuzi hayo juzi mbele ya Naibu Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Rodrick Mpogoro katika kijiji cha Mtina Wilayani Tunduru Mkoani hapa kwa kile walichodai kwamba wanaunga mkono juhudi za Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dokta John Pombe Magufuli ambaye amekuwa akionesha kupambana kwa vitendo hasa katika matukio ya ufisadi, rushwa wizi na dhuluma.

Akizungumza kwa niaba ya Wanachama wenzake Afisa wa ACT, Amani Ramadhan Kawawa alisema kuwa yeye na wanachama wenzake katika Wilaya hiyo wamefikia maamuzi hayo, baada ya kubaini kuwa viongozi wa vyama vya upinzani wamekuwa wakiwatumia wao kama daraja la kuweza kufikia mafanikio yao binafsi.

Tuesday, March 13, 2018

SERIKALI KUTUMIA TRILIONI 32.4 MWAKA WA FEDHA 2018/2019



Na Mwandishi wetu,
Dodoma. 

IMEELEZWA Serikali imepanga kukusanya na kutumia shilingi trilioni 32.476 kwa mwaka ujao wa fedha wa 2018/2019.
Dokta Philip Mpango.

Akiwasilisha mapendekezo ya Serikali ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa na kiwango cha ukomo wa bajeti kwa mwaka 2018/2019, Waziri wa Fedha na Mipango, Dokta Philip Mpango alisema kuwa ukomo wa bajeti umezingatia upatikanaji wa mapato.

Dokta Mpango alisema katika mwaka huo Serikali imepanga kutumia shilingi trilioni 20.468 kwenye matumizi ya kawaida sawa na asilimia 63 ya bajeti yote.

Matumizi hayo alifafanua kuwa yanajumuisha shilingi trilioni 10 zitakazolipa deni la Taifa na shilingi trilioni 7.369 mishahara ya watumishi wakati shilingi trilioni 3.094 zikielekezwa kwenye matumizi mengine.

VIKUNDI VYA WANAWAKE MBINGA WAPEWA MKOPO MILIONI 10


Afisa wa idara ya maendeleo ya jamii Halmshauri ya mji wa Mbinga Mkoani Ruvuma, Alphonce Njawa akitoa maelezo mafupi kwa Mkuu wa Mkoa huo, Christine Mndeme (aliyevaa kitambaa rangi ya njano kichwani) juu ya bidha mbalimbali zinazotengenezwa na vikundi vya wanawake wajasiriamali katika Halmashauri hiyo.

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme (aliyevaa kitambaa rangi ya njano) akipata maelezo mafupi kutoka kwa mjasiriamali juu ya faida ya ulaji wa matunda ya asili.



Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

KATIKA kukuza maendeleo ya mwanamke, Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma imefanikiwa kusajili vikundi 50 vya wanawake ambao ni Wajasiriamali, wakiwa wanajishughulisha na biashara ndogondogo.

Aidha vikundi hivyo vimekuwa vikijishughulisha na shughuli za kilimo na ufugaji na kuweza kujipatia kipato cha kuendeleza maisha yao.

Hayo yalisemwa hivi karibuni na Paschal Ndunguru ambaye ni Mkuu wa idara ya maendeleo ya jamii Wilayani humo, siku ya maadhimisho ya wanawake duniani yaliyofanyika Wilayani hapa.

Sunday, March 11, 2018

DOKTA MAGUFULI AWATAKA WAMILIKI WA VIWANDA VYA NDANI KUAJIRI WAZAWA



Na Mwandishi wetu,

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dokta John Pombe Magufuli amemwagiza Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage kuhakikisha kwamba wamiliki wote wa viwanda vya ndani wanaajiri wazawa.

Dokta Magufuli ametoa agizo hilo leo Machi 11 mwaka huu wakati alipokuwa akizindua kiwanda cha kufua vyuma cha Kahama Oil Mill kilichopo mjini Kahama Mkoa wa Shinyanga.

Alisema kuwa wananchi wazawa ndio waliompigia kura, hivyo ni lazima wapewe kipaumbele cha ajira katika viwanda hivyo.

RC RUVUMA AWATAKA VIJANA BODABODA KUJIUNGA MAFUNZO YA MGAMBO



Na Mwandishi wetu,    
Songea.

MKUU wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme amewataka Vijana ambao wanajihusisha na biashara ya kuendesha Pikipiki maarufu kwa jina la Bodaboda Mkoani humo kujiunga na mafunzo ya Mgambo ili waweze kukabiliana na vitendo vya uhalifu, hasa wanavyofanyiwa na watu wenye nia mbaya ambao wamekuwa wakitumia nafasi hiyo kuwanyang’anya Pikipiki zao ikiwa ndiyo njia rahisi ya kutekeleza uhalifu wao.
Christine Mndeme.

Mndeme alisema kuwa Serikali ya Mkoa itahakikisha kwamba inatoa mafunzo ya mgambo kwa vijana wote watakaokuwa tayari, ili kuweza kuwapata vijana wengi ambao watakuwa na mchango mkubwa katika masuala ya ulinzi na usalama ndani ya Mkoa na nchi kwa ujumla.

Alitoa kauli hiyo jana akiwa katika uwanja wa michezo wa Majimaji mjini Songea, wakati alipokutana na kuzungumza na vijana hao zaidi ya 200 waendesha Bodaboda kutoka maeneo mbalimbali ya Manispaa ya Songea, huku akiwataka waachane na tabia ya ulevi na matendo maovu ambayo hayafai katika jamii.

BODABODA MKOA WA RUVUMA WAPEWA ONYO KALI



Na Kassian Nyandindi,  
Songea.

KATIKA kipindi cha mwaka 2017 Mkoani Ruvuma, imeelezwa kuwa jumla ya watu 32 wamefariki dunia na wengine 41 kujeruhiwa vibaya, kutokana na ajali zilizosababishwa na waendesha Pikipiki maarufu kwa jina la Bodaboda.

Vifo hivyo imefafanuliwa kuwa ni ongezeko la vifo 11 vilivyotokea katika kipindi cha mwaka 2016 Mkoani humo.

Gemin Mushy ambaye ni Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo alisema hayo jana, alipokuwa akitoa taarifa ya ajali za barabarani ambazo zimetokana na waendesha Pikipiki.

WAKULIMA MBINGA WALIA NA UENDESHAJI KILIMO CHA ZAO LA KAHAWA

Kahawa ambayo ipo shambani kama hii, ikikosa pembejeo za kilimo kama vile madawa na mbolea huwa kama hivi baada ya kukosa virutubisho halisi na kushambuliwa na wadudu waharibifu.


Na Kassian Nyandindi,       
Mbinga.

BAADHI ya Wakulima wanaozalisha zao la Kahawa Wilayani Mbinga Mkoa wa Ruvuma, wamesema kwamba hivi sasa wanashindwa kuendesha kilimo cha zao hilo kutokana na mfumo uliowekwa na Serikali wa vyama vya ushirika, kushindwa kuwakopesha pembejeo za kilimo wakulima hao kama vile madawa na mbolea.

Aidha kwa nyakati tofauti walisema kuwa ni vyema wakati Serikali inajipanga kutekeleza hilo, wangeruhusu kwanza Makampuni binafsi ambayo yalikuwa yakiwawezesha pembejeo hizo yangeendelea kusambaza kwa wakulima hao, huku wakisubiri mfumo wa ushirika ukiendelea kuimarishwa.

Walidai kuwa mfumo wa vyama vya ushirika sio kwamba wanaupinga, lakini imekuwa ni haraka mno kuyasitisha Makampuni hayo ambayo yalikuwa ni msaada mkubwa kwao, hivyo ni vyema ungetolewa muda kwanza na masharti kadhaa namna ya kuweza kusaidia wakulima hao.

Saturday, March 10, 2018

JAJI MKUU ATAKA NAKALA ZA HUKUMU ZITOLEWE KWA WAKATI



Profesa Ibrahimu Juma.
Na Ferdinand Shayo,    
Arusha.

JAJI Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahimu Juma ameonesha kutoridhishwa kwake na mfumo wa utoaji wa taarifa mbalimabli za Kimahakama ikiwa ni pamoja na matamshi ya lugha, urasimu unaofanywa na baadhi ya Watumishi wa Mahakama katika utoaji wa nakala za hukumu.

Profesa Juma ametoa kauli hiyo leo jijini Arusha katika ufunguzi wa kikao kazi cha watendaji na wataalamu wa Mahakama, kwa lengo la kutathimini utekelezaji wa mpango mkakati wa miaka mitano na utekelezaji wa mradi wa maboresho wa utoaji wa huduma za Mahakama hapa nchini.

Katika kikao hicho Jaji Mkuu, alitolea mfano andiko la benki ya dunia linalozungumzia ukosefu wa taarifa kwa umma kuhusu mashauri na kasi ndogo ya kuchapishwa kwa nakala za hukumu, huku nakala hizo zikichapishwa kwa lugha ya kiingereza na wakati mwingine kisheria zaidi.

MWENYEKITI AOMBA MSAADA DAKTARI WA KUITIBU MAJIMAJI SONGEA



Na Kassian Nyandindi,     
Songea.

MWENYEKITI wa Chama cha Soka Mkoa wa Ruvuma, Golden Sanga amesema kuwa hali ya maendeleo ya timu ya soka ya Majimaji Mkoani humo, hivi sasa imeyumba na kwamba hawana uhakika wa kufanya vizuri kwenye michezo ya ligi. 

Aidha Sanga amefafanua kuwa hawako vizuri kifedha, jambo ambalo linasababisha kukosekana kwa matokeo mazuri ndani ya timu yao, ambayo ipo mwisho wa msimamo wa ligi ya VPL.

Alieleza kuwa timu haijasimama vizuri kutokana na baadhi ya wachezaji kusimamishwa, ambao hawajatajwa na sababu za kusimamishwa kwao hazijawekwa wazi.

WANAOANZISHA CHOKOCHOKO WAMCHUKIZA DOKTA MAGUFULI



Na Mwandishi wetu,

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dokta John Pombe Magufuli amewapongeza Wizara ya Ujenzi na Mkandarasi aliyefanikisha ujenzi wa barabara ya Uyovu – Bwanga na kudai kuwa watu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) sio ndiyo wanawahi kwenda kuandamana.

Dokta Magufuli alisema hayo leo Machi 10 mwaka huu akiwa kwenye ufunguzi wa barabara hiyo, Bukombe Mkoani Geita na kusema kuwa Serikali imefanya maendeleo makubwa ujenzi wa barabara hapa nchini na kudai hayo ndiyo mambo ambayo yeye anayahitaji kwenye Serikali yake.

Kadhalika Rais Magufuli alidai kuwa kuna watu hawafurahii maendeleo ya Tanzania, ndiyo maana wamekuwa wakijitahidi kufanya chokochoko.

AFARIKI DUNIA BAADA YA KUGONGANA USO KWA USO PIKIPIKI WALIZOKUWA WAKIENDESHA


Na Kassian Nyandindi,    
Tunduru

MTU mmoja aliyejulikana kwa jina la Masudi Namurumi (28) amefariki dunia, katika tukio la ajali ambayo ilihusisha Pikipiki mbili kugongana uso kwa uso.
 
Mashuhuda wa tukio hilo walieleza kuwa lilitokea katika eneo la makutano ya barabara iendayo kijiji cha Nandembo na Kitalo Wilayani Tunduru Mkoa wa Ruvuma.

Pamoja na ajali hiyo kusababisha kifo hicho, watu watatu wamelazwa katika Hospitali ya Wilaya hiyo ambao walikuwa abiria katika Pikipiki hizo.

Imeelezwa kuwa hali zao ni mbaya, baada ya kupata majeraha sehemu mbalimbali za miili yao.

TATIZO LA UKATILI WA KIJINSIA CHANGAMOTO KUBWA WILAYA YA MBINGA

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme ambaye amefunga kitambaa rangi ya njano kichwani akifurahi kwa pamoja mbele ya kundi la Wanawake wa Wilaya ya Mbinga Mkoani humo, siku ya maadhimisho ya Wanawake duniani ambapo katika Mkoa huo yalifanyika katika kijiji cha Lipumba kata ya Kihangimahuka Wilayani Mbinga. 

Upande wa kushoto aliyevaa kitambaa rangi ya njano kichwani ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme akikagua moja kati ya mabanda ya maonesho siku ya maadhimisho ya Wanawake duniani ambapo katika Mkoa huo yaliadhimishwa Kimkoa katika kijiji cha Lipumba kata ya Kihangimahuka Wilaya ya Mbinga, na kwamba banda hilo ambalo ni la Dawati linaloshughulikia masuala ya ukatili wa kijinsia Wilayani humo amelitaka kuhakikisha kwamba linatekeleza majukumu yake ipasavyo, ili kuweza kudhibiti matatizo ya ukatili wa kijinsia katika jamii.


Na Kassian Nyandindi,    
Mbinga.

KUHUSU tatizo la Ukatili wa kijinsia unaofanywa dhidi ya wanawake, imeelezwa kuwa ni miongoni mwa changamoto kubwa inayoongoza katika Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma ambapo wanawake wamekuwa wakipigwa, kubakwa, kutelekezwa na kunyang’anywa mali zao hasa pale waume zao wanapofariki dunia.

Tatizo hilo hivi sasa limeongezeka na kukua kwa kasi ambapo katika mwaka 2016 kulikuwa na malalamiko ya ukatili wa kijinsia 232 ikiwemo miongoni mwao kesi za kubakwa 30 na kupigwa 105.

Imefafanuliwa kuwa wanawake wamekuwa hawashirikishwi katika kupanga mipango ya miradi ya maendeleo, katika familia na kupewa fursa ya kufanya maamuzi hivyo kufanya changamoto hiyo kuendelea kuwa kubwa.

Friday, March 9, 2018

HALMASHAURI MADABA KUKAMILISHA UJENZI WA MIUNDOMBINU MBALIMBALI

Mkuu wa Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma, Pololet Mgema akizungumza na baadhi ya Wanafunzi wa kidato cha pili, Cosma Mwageni (Katikati) na Happy Hyera wa shule ya Sekondari Mahanje Halmashauri ya Wilaya Madaba Mkoani humo, wakati alipotembelea kukagua ujenzi ambao unaendelea wa mradi wa mabweni, vyumba vya madarasa na matundu ya vyoo ambapo upande wa kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri hiyo, Shafi Mpenda.
Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Madaba Mkoani Ruvuma, Shafi Mpenda aliyevaa suti akimuonesha Mkuu wa Wilaya ya Songea Mkoani humo, Pololet Mgema baadhi ya vitanda vilivyowekwa katika moja ya bweni ambalo limejengwa na Serikali kupitia mpango wa P 4 R katika shule ya Sekondari Mahanje iliyopo Wilayani hapa.

MLEMAVU WA MIGUU KICHANGANI TUNDURU APEWA MSAADA WA BAISKELI MAGURUDUMU MATATU

Mkurugenzi wa Kampuni ya D&G Export Company Limited, Geofrey Kalamba (kushoto) akikabidhi Baiskeli ya magurudumu matatu yenye thamani ya shilingi 320,000 kwa Fatma Kaluma ambaye ni Mlezi wa mwanafunzi Shaibu Mpoto aliyeketi kwenye Baiskeli hiyo, anayesoma darasa la saba shule ya Msingi Kichangani Wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma.


Na Mwandishi wetu,      
Tunduru.

MWANAFUNZI wa darasa la saba, Shaibu Mpoto ambaye ni wa shule ya Msingi Kichangani kata ya kichangani Wilaya ya Tunduru Mkoani Ruvuma, anashindwa kuendelea na masomo katika shule hiyo baada ya kuugua ugonjwa wa kupooza miguu kwa muda mrefu.

Tatizo hilo ambalo limempata mwanafunzi huyo ni miaka minne sasa imepita, lakini baada ya kupata msaada wa Baiskeli yenye magurudumu matatu hivi sasa inamsaidia kwenda shuleni kuhudhuria vipindi vya masomo na kurudi nyumbani kwake Kichangani ambako anaishi na ndugu zake.

Kampuni ya D&G Export Limited inayojishughulisha na kazi ya ununuzi wa mazao na utunzaji wa Korosho Tunduru na Liwale Mkoa wa Lindi, ndiyo ambayo imeweza kumpatia Baiskeli hiyo na kuondoa adha aliyokuwa akiipata kwa muda mrefu mwanafunzi huyo.

PICHA ZA MATUKIO MAZISHI YA MUASISI WA TANU MAREHEMU COSTANTINE MILLINGA

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme akiweka shada la maua kwenye kaburi la Muasisi wa TANU, Marehemu Costantine Millinga mara baada ya mazishi yake kufanyika jana katika maeneo ya nyumbani kwake Marehemu, Mtaa wa Mhekela Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani humo. 

Mkuu wa Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma, Cosmas Nshenye akiweka shada la maua kwenye kaburi la Muasisi wa TANU, Marehemu Costantine Millinga mara baada ya mazishi yake kufanyika jana katika maeneo ya nyumbani kwake Marehemu, Mtaa wa Mhekela Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani humo. 



Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Ruvuma, Oddo Mwisho akiweka shada la maua kwenye kaburi la Muasisi wa TANU, Marehemu Costantine Millinga mara baada ya mazishi yake kufanyika jana katika maeneo ya nyumbani kwake Marehemu, Mtaa wa Mhekela Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani humo. 

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma, Beda Hyera akiweka shada la maua kwenye kaburi la Muasisi wa TANU, Marehemu Costantine Millinga mara baada ya mazishi yake kufanyika jana katika maeneo ya nyumbani kwake Marehemu, Mtaa wa Mhekela Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani humo.      

Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga vijijini Mkoani Ruvuma, Gombo Samandito akiweka shada la maua kwenye kaburi la Muasisi wa TANU, Marehemu Costantine Millinga mara baada ya mazishi yake kufanyika jana katika maeneo ya nyumbani kwake Marehemu, Mtaa wa Mhekela Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani humo. 
Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani Ruvuma, Robert Mageni akiweka shada la maua kwenye kaburi la Muasisi wa TANU, Marehemu Costantine Millinga mara baada ya mazishi yake kufanyika jana katika maeneo ya nyumbani kwake Marehemu, Mtaa wa Mhekela Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani humo. 
Meya wa Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, Abdul Mshaweji akiweka shada la maua kwenye kaburi la Muasisi wa TANU, Marehemu Costantine Millinga mara baada ya mazishi yake kufanyika jana katika maeneo ya nyumbani kwake Marehemu, Mtaa wa Mhekela Halmashauri ya Mji wa Mbinga Mkoani humo. (Picha zote na Kassian Nyandindi)