Wednesday, March 14, 2018

DC APONGEZA USIMAMIZI NA MATUMIZI SAHIHI YA FEDHA ZA SERIKALI MADABA

Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Madaba Mkoani Ruvuma, Shafi Mpenda (aliyevaa suti rangi nyeusi) akimuonesha Mkuu wa Wilaya ya Songea Mkoani humo, Pololet Mgema baadhi ya vitanda vilivyowekwa katika moja kati ya bweni lililojengwa na Serikali kupitia mpango wa P4R katika shule ya Sekondari Mahanje iliyopo Madaba.

Na Kassian Nyandindi,      
Madaba.

MKUU wa Wilaya ya Songea Mkoani Ruvuma, Pololet Mgema ameipongeza Halmashauri ya Wilaya ya Madaba Mkoani humo kwa usimamizi na matumizi sahihi ya fedha za Serikali ambazo zinapelekwa katika Halmashauri hiyo, kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo na kuboresha maisha ya wananchi.

Mgema alitoa kauli hiyo juzi alipotembelea na kujionea mradi wa ujenzi wa mabweni mawili, madarasa mawili na matundu sita ya vyoo katika shule ya Sekondari Mahanje iliyopo kata ya Mahanje ndani ya Halmashauri hiyo ambayo inajengwa kupitia mpango wa P4R.

Serikali imeipatia Halmashauri ya Madaba, shilingi milioni 196.6 kwa ajili ya kukamilisha kazi hiyo ambapo mabweni hayo mawili yenye uwezo wa kuchukua watoto 80 kila moja, madarasa na matundu ya vyoo yamekwisha kamilika.


“Hapa lazima niseme kweli, Mkurugenzi na uongozi wenu wa shule mmenifurahisha sana na miradi yenu mliyoijenga, kimsingi imeendana na gharama halisi ya fedha ambazo Serikali ilileta kwa ajili ya kazi hii, mnastahili pongezi na kuwa mfano wa kuigwa na Wakurugenzi wengine katika Wilaya yangu”, alisema Mgema.

Vilevile ameutaka uongozi wa shule hiyo na wanafunzi wake kutunza miradi hiyo ambayo imetumia fedha nyingi za walipa kodi wa nchi hii, ili iweze kuwa endelevu na itumike kuongeza kiwango cha taaluma katika shule hiyo.

Alibainisha kuwa Serikali imejenga miundombinu hiyo kwa lengo la kuboresha mazingira mazuri ya kujifunzia na kufundishia, hivyo haitakuwa na maana kama kiwango cha ufaulu kitaendelea kushuka.

Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya Madaba, Shafi Mpenda mbali na kuishukuru Serikali ya awamu ya tano kutoa fedha hizo kwa ajili ya kuboresha miundombinu hiyo, ameahidi pia kupeleka baadhi ya vifaa ikiwemo meza na viti kwa ajili ya matumizi ya walimu ili shule iweze kuendana na ubora wake.

Kwa upande wao nao baadhi ya walimu wa shule hiyo, wameiomba Serikali kujenga ukumbi wa chakula ili uweze kutumika kwa ajili ya wanafunzi pale wanapokula chakula.

No comments: