Thursday, March 8, 2018

MAKALA: MZEE MILLINGA MUASISI WA TANU AMEZIKWA LEO MBINGA TUTAMKUMBUKA DAIMA

Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete akiwa kwenye picha ya pamoja na Muasisi wa TANU Mzee Costantine Millinga (Enzi ya uhai wake) mwaka 2010 walipokutana mjini Mbinga Mkoani Ruvuma, mara baada ya kuhutubia Mkutano mkubwa wa kampeni ya uchaguzi Mkuu Mbinga mjini katika mwaka huo.

Mwili wa Mwanasiasa Mkongwe, Marehemu Costantine Millinga ukiingizwa kaburini leo na vijana wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) tayari kwa mazishi katika makaburi yaliyopo katika maeneo ya nyumbani kwake mtaa wa Mhekela Mbinga mjini.

Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Taifa, Rodrick Mpogolo akiweka shada la maua katika kaburi la Muasisi wa TANU, Marehemu Costantine Millinga mara baada ya mazishi yake kufanyika leo Mbinga mjini.


Na Kassian Nyandindi,      

SIKU zote binadamu anapozungumzia jambo la kimaendeleo kuelekea Uhuru wa Tanganyika, amekuwa akitoa taswira au picha ya mchango wa watu mbalimbali ambao wamefanya kazi hiyo, hadi kufikia kilele cha mafanikio ambapo ndani yake wapo wanasiasa na jamii ya kawaida ambao walivuma na wengine wasiovuma.

Aidha katika kundi hilo wapo wake kwa waume, wametangulia mbele ya haki ambao ni wengi na wachache ndiyo waliobaki ambapo kwa maana hiyo, wapo Waasisi wa siasa ya nchi hususan katika chama chetu cha Tanganyika African National Union (TANU) ambacho ndicho kimebeba chimbuko la Uhuru na maendeleo ya Tanganyika na baadaye tukaipata Tanzania.

Katika makala haya mmoja wa hao yupo Mzee Costantine Oswald Millinga (96) huyu ni Mwanasiasa mkongwe na Mtanzania, mwenye historia ndefu katika kuasisi vyama vya Tanganyika African Association (TAA) na Tanganyika African National Union (TANU) akiwa mkazi wa baadhi ya miji iliyokuwa nguzo za vyama hivyo hapa nchini.

Mvuto huo ndiyo uliomfanya Rais mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete wakati alipokuwa madarakani, kumualika Mzee Millinga kuwa mmoja wa watu katika uzinduzi wa sherehe ya miaka 50 ya Uhuru zilizofanyika kwenye viwanja vya Mnazi mmoja, jijini Dar es salaam mwezi Julai mwaka 2011 na akawa kivutio kikubwa.


Mzee Millinga alionesha kuwa na uwezo mkubwa na kumbukumbu ya kusimulia kwa ufasaha historia ya TAA na TANU licha ya umri wake kuwa mkubwa, huku akiibua mambo ambayo wengi wao hawakuyajua au hayapo katika maandishi ya historia.

Katika vyama vyote vya TAA na TANU Mzee huyo anayo “mikono yake” ambapo safari hiyo ilianza katika simulizi ya mwaka 1952 akiwa mjini Ngudu Wilayani Kwimba, Mwanza kwa baba yake mdogo aliyekuwa Inspekta wa Polisi ambaye alikuwa akifanya mipango ajiunge na Shirika la Posta.

Hapo walitembelewa na rafiki wa baba yake mdogo alitokea mjini Masasi, Mtwara aliyemtambua kwa jina la Frederick Mchauro ambapo mgeni huyu alikuja na mawazo ya kumshawishi aachane na kazi za Posta na badala yake ajiunge na ajira ya Ofisi ya Maendeleo ya Jamii huko Masasi.

Pamoja na mambo mengine, baadaye kulikuwepo mawazo mbadala ambapo alipata ajira hiyo mjini Tabora wakati huo kukiwa na vuguvugu kubwa la mchakato wa kuanzishwa kwa TAA, kikiwa ndiyo chama kilichojumuisha Wakulima na Wafanyakazi wazalendo.

Pia Mzee Millinga anamkumbuka kiongozi wake wa kazi kwa wakati huo aliyemtaja kwa jina la Leonard Kunambi, ambaye huyu alimshawishi kujiunga na TAA lakini ndani ya kipindi kifupi mchango wake uliwavutia wanachama wengine hata akachaguliwa kuwa Katibu.

Hapo ndipo mwanzo wa ushiriki wake kikamilifu wa Mzee huyu katika siasa ulipoanza wakati huo akiwa kijana mwenye umri wa miaka 26 tu, katika zama hizo kasi ya kujijenga na TAA ilipamba moto mjini Dar es Salaam, Tabora na maeneo mengine hapa nchini.

Joto la siasa kwa Watanganyika kutaka haki ya kujitawala wakati huo lilikuwa juu, wakati TAA ikilenga kudai usawa kati ya jamii ya Waasia, Wazungu na Waafrika.

Katika hali isiyokuwa ya kawaida jambo hili liliwakera Serikali ya Kikoloni ya Mwingereza chini ya Gavana Edward Twining huku Wakoloni hao wakikerwa na msukumo huo wa Waafrika na kusababisha kupiga marufuku wafanyakazi wa Serikali kushiriki siasa za chama cha TAA.

Mzee Millinga akiwa Tabora waliandika barua kwa Serikali ya kikoloni wakitaka watumishi wa Serikali waendelee kushiriki katika siasa za chama hicho na kwamba ombi hilo lilikubaliwa kwa kupewa miezi sita ikiwa ni kipindi cha angalizo.

Kufikia mwaka 1953 alifahamishwa na Mwenyekiti wake aliyemtaja kwa jina la Mwalimu Said Haroub, kwamba wangetembelewa na Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambaye ni kiongozi mkubwa wa TAA kutoka Dar es Salaam ikiwa ni muda mfupi tu tangu aliporejea kutoka masomoni, Chuo kikuu cha Edinburg Uingereza.

Mwalimu Haroub alikuwa akifundisha katika Sekondari ya Tabora na huko nyuma alikwisha mfundisha Mwalimu Nyerere katika shule hiyo.

Mzee huyo anataja wajumbe wengine wa Kamati ya TAA huko Tabora kuwa ni pamoja na Walimu wa shule hiyo ya Tabora ambao ni Stephen Mhando na Erasto Mangenya.

Wengine ni Mshairi maarufu, Abdul Saadan Kandoro, Sheikh Amri Abeid Kaluta anayetajwa na Mzee Millinga kwamba “alikuwa maarufu sana” na Sheikh Abdallah Kivuruga ambaye anamtaja alikuwa “alwatani wa mjini”.

Mwingine katika safu hiyo ni Germanus Pacha aliyekuwa mtendaji mkuu wa Baraza la Machifu Tabora na mwanasiasa aliyejulikana baadaye, Balozi Tebandebage.

Wakati huo kwamba Mwalimu Nyerere alifika na kuwahutubia, hata hivyo katika kufunga kikao Mwenyekiti wa TAA Tabora alitamka kwamba “ndicho kikao cha mwisho cha Katibu” yaani Mzee Millinga anahama.

Mwalimu Nyerere akauliza anakwenda wapi?, ambapo Mzee Millinga katika tukio hilo ambalo ilikuwa mara ya kwanza kwake kuonana ana kwa ana na Nyerere, ambapo Nyerere alijibiwa kwamba Katibu (Millinga) anahamishiwa Dar es Salaam.

Mzee Millinga alipoingia Dar es Salaam

Mzee huyu wakati anasoma Januari mwaka 1954, tayari alikwisha ripoti jijini Dar es Salaam, kituo chake cha kazi kikiwa katika idara ya Maendeleo ya Jamii jengo la Arnatoglu, akiwajibika chini ya kiongozi wake aliyemtaja kwa jina la Denice Ombea.

Anasema Mwalimu Nyerere alikuwa na kawaida ya kufika mjini Dara es Salaam mara kwa mara akitokea Pugu hasa kwa siku za Jumamosi na kwamba walipokutana na Nyerere jirani na jengo hilo Dar es Salaam alimtamkia kwamba; “Millinga umekuja, nilivutiwa sana na maneno aliyoyasema Mwenyekiti wa (TAA-Tabora) juu yako”. Hapo Mzee Millinga alimjibu akisema; “na mimi nasema chama ni hicho hicho”.

Jambo hilo walikubaliana na Mwalimu Nyerere aliyemuahidi kwamba atawashawishi wenzake wamuingize katika Kamati ya TAA Dar es Salaam na hatimaye walikubali, katika hali ambayo Mzee huyu anasema ndivyo alivyoingia katika Kamati hiyo.

Katika vikao vyao vya TAA Mkoa wa Dar es Salaam, walianza kujenga hoja ya kuibadili ili iwe na sura ya kisiasa kwa kuwa iliyokuwapo haikuwa na nguvu na waliafikiana kufanya hivyo.

Vilevile mjadala ulikuwa mkali na walitaka kuondoa neno “Association” katika jina la chama hicho, hiyo ilimaanisha Ushirika jambo ambalo waliona waachane nalo na kukipatia jina la “Union” ikimaanisha “Umoja” wakiamini lina ushirikishaji wa wengi.

Kwa maana hiyo walipata pendekezo katika kikao chao cha TAA kwamba chama kiitwe Tanganyika African Union (TANU) na hasa neno Union liliwekwa kwa nia ya kujumuisha watu wote, lakini hilo wakalitafakari na waliona kwamba kwa kuwa nchi ya Kenya kuna Kenya African Union (KAU) chini ya Jomo Kenyatta, iliyopingwa marufuku na Uganda ambapo kulikuwepo Uganda African Congress (UAC) ikizingatiwa kwamba maeneo hayo kulikuwa na makoloni ya Mwingereza.

Hatua hiyo ilifanya Wajumbe wa TAA wagawanyike kwa makundi ya kanda, ambapo kila kundi walikuwa wakitafakari ni jina gani linafaa kwa ajili ya kuanzisha chama kipya cha siasa.

Kanda hizo ni Mashariki yaani Dar es Salaam, Pwani na Morogoro na kwamba Magharibi kulikuwa na Kigoma, Tabora na Mpanda huku kukiwa na kanda ya Mwanza na Bukoba pamoja na ya Kaskazini yaani Arusha na Moshi.

Wakati huo waliokuja na wazo la TANU ni wenzetu wa kutoka Mwanza ambao ni akina Saddan Kandoro, Lameck Makaranga na Walter Bugoke au kwa jina lingine maarufu alikuwa anaitwa “Kenyatta wa Tanganyika”.

Mnamo mwaka 1954 hapo ndipo Chama cha TANU kilizaliwa na kuandikishwa rasmi ikiwa ni chama kipya cha kisiasa kuchukua nafasi ya TAA.

Wakati huo, Serikali ya Kikoloni ilipiga marufuku watumishi wa Serikali (Umma) kushiriki kwenye masuala ya siasa, jambo ambalo lililomfanya aendelee kushiriki katika mikutano ya siasa za TANU kwa siri bila kuwa na kadi ya chama ili kuweza kulinda ajira yake, tofauti na wana – TANU wengine waliokuwa katika ajira ya Serikali kama vile Mwalimu Nyerere wao waliamua kujitosa kikamilifu na kuwa huru katika shughuli za chama.

Lakini maisha ya Mzee Millinga binafsi nimebaini yana mengi katika siasa za nchi na utumishi wa umma kwa ujumla, ikiwemo kujenga urafiki mkubwa na wanasiasa waandamizi nchini kama vile Hayati Rashid Kawawa.

Mzee huyo alifikia hatua ya kujikita katika masuala ya siasa na utumishi baada ya kupitia uzoefu muda mrefu wa kusaka maisha hadi Ughaibuni yenye simulizi na vitimbi vingi baada ya kukerwa na mfumo wa uongozi wa kikoloni nchini.

Mbali na kushiriki siasa hasa katika harakati za kuanzisha TAA na TANU pia ni kinara katika utumishi wa umma ambapo baada ya Uhuru amekuwa katika idara ya Maendeleo ya Jamii hadi alipostaafu akiwa mzoefu hasa.

Baada ya Uhuru alikuwa daima mkimya kuhusiana na masuala ya siasa huku akijikita zaidi katika utumishi wa umma ingawa mapenzi yake makubwa kwa TANU hakuweza kuyaweka pembeni, aliyaweka rasmi alipojiunga na chama hicho kwa kukata kadi baada ya Uhuru ambapo huko nyuma alihofia angeachishwa kazi na Serikali ya kikoloni ambayo ilipiga marufuku watumishi wote wa umma kushiriki siasa.

Tangu zama hizo alikuwa pia ni rafiki wa karibu wa Muasisi wa Taifa la Tanganyika, Kleist Sykes na vilevile ni rafiki wa karibu wa hayati Mzee Rashid Mfaume Kawawa.

Tunamkumbuka Kawawa alivyoshiriki katika harakati za Uhuru wa Tanganyika kwa namna mbalimbali.

Wasifu kama huo na mengi umemfanya Mzee Millinga awe mtu anayeheshimika miongoni mwa wanaomfahamu, hasa kwa hulka yake ni vigumu kujikweza na ndilo jambo linalomfanya asifahamike.

Miongoni mwa wanaomtambua na kumheshimu kwa hadhi anayostahili ni aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Mbinga, Kanali Mstaafu Edmund Mjengwa ambaye amekuwa akimtambua kwa staili ya kipekee kwenye shughuli muhimu za kitaifa ambapo huwa hakosi kufanya hivyo.

Hilo ndilo lililotokea wakati Rais Jakaya Kikwete alipozuru Wilayani Mbinga June 4 mwaka 2011 katika sherehe ya kumtawaza Askofu wa Kanisa Katoliki, Jimbo la Mbinga John Ndimbo ambapo alikuwa miongoni mwa wazee waalikwa wakibadilishana mawazo na Rais Kikwete.

Mazungumzo hayo yaliweza kumuongezea elimu ya ziada Rais Kikwete juu ya mengi kuhusu maisha binafsi ya hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere, tangu zama hizo akiishi Magomeni, Dar es Salaam.

Kumbe kumtambua ni Muasisi wa TANU, suala hilo lilimgusa Rais Kikwete na hata kuagiza uongozi wa chama kufanya utaratibu wa kuhakikisha kwamba anakuwa miongoni mwa wageni rasmi wa kuzindua sherehe za miaka 50 ya Uhuru iliyofanyika Julai 7 mwaka 2011, na kwamba bila kujua kinachoendelea alipewa taarifa na uongozi wa Wilaya kwa kushirikiana na wa Mkoa wa Ruvuma walimsafirisha hadi Dar es Salaam.

Kuhusu mchakato wa Uhuru  

Mzee Millinga ana mengi kuhusu kipindi hicho, wakati huo Kawawa akiwa tayari ni Katibu Mkuu na mwanaharakati mwandamizi wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TFL).

Wakati huo vuguvugu la TANU iliyoshirikiana kwa karibu na TFL mwaka 1958 katika uchaguzi mkuu ulitokea mgogoro mkubwa, juu ya ama TANU ikubali kushiriki au wakati huo Serikali ya kikoloni ilikuja na hoja kwamba uchaguzi utafanyika kwa utaratibu wa kura tatu ambazo ni za Mzungu, Mhindi na Mwafrika.

Mwalimu Nyerere alifanya jitihada ya kuwashawishi wana – TANU wakubali hoja hii kwa kutumia mkutano uliofanyika Tabora ulioongozwa na Sheikh Kihore, lakini wanachama wengine kama Bwana Zuberi Mtemvu hakukubaliana na hoja hiyo na wakati wa uchaguzi alijitoa TANU na kuanzisha chama kilichoitwa UTP.

Wakati huohuo wapo watu wengine waliosimama kama wagombea binafsi na walifanikiwa kama vile Chifu Amri Dodo wa Mbulu na Chifu Herman Sarawati wa Babati.

Walikuwepo pia wahindi walioshiriki uchaguzi wa kuiunga mkono TANU kama vile Bwana Karimjee Jivanjee na Amir Jamal, Mzungu Dereck Bryceson aliiunga mkono TANU na kwamba katika uchaguzi huo TANU iling’ara kwa kuwa hata wale waliosimama kama wagombea binafsi walikiunga mkono.

Licha ya upoinzani uliojitokeza hoja ya mwalimu Nyerere ilionekana ni ya msingi, kwani TANU iliibuka kinara na kuwa na hadhi ya kupewa haki ya kuongoza nchi.

Itakumbukwa kuwa baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia, Tanganyika ilikabidhiwa kwa wakoloni wa Kiingereza kutoka kwa Wajerumani kwa udhamini hadi itakapopata uwezo wa kujitawala.

Katika harakati hizi Mzee Millinga na wadau wengine muhimu wa Uhuru wa Tanganyika, John Rupia ambaye aliweza kutoa mchango wake wa shilingi 14,000 katika kumfahamisha safari hiyo ya Mwalimu Nyerere kwenda Umoja wa Mataifa.

Ambapo wakati huo wakoloni waliweza kuwakatisha tamaa jamii ya Wamisionari na walitumia nafasi zao kuwakejeli Watanganyika kuwa bado hawakuwa na uwezo wa kujitawala, lakini ndoto ya Watanganyika ilitekelezwa Disemba 9 mwaka 1961.

Maisha ya Mzee Millinga 

Mzee huyu alizaliwa Novemba 22 mwaka 1921 akiwa mtoto wa kwanza wa Mzee Oswald Millinga na mama yake Victoria katika kijiji cha Nkaya, Kata ya Lituhi Wilaya ya Nyasa (Zamani Mbinga) Mkoani Ruvuma.

Yeye ni mzaliwa wa kwanza katika uzao wa watoto watatu, baba yake alikuwa fundi cherehani na mdogo wake mmoja alifariki dunia angali mdogo. Dada ya Mzee Millinga ana umri wa miaka 93.

Mzee Millinga alianza masomo mwaka 1926 katika shule ya msingi Nkaya kuanzia ya awali na baadae shule ya msingi hadi darasa la nne, alisoma palepale kijijini kwao Nkaya.

Baadae aliendelea na masomo ya darasa maalum la Kiingereza kwa miaka miwili katika shule ya Mision Peramiho.

Mwaka 1936 hadi mwaka 1938 alipata mafunzo ya ualimu hapo hapo Mision ya Peramiho ilivyokuwa chini ya Wajerumani.

Alipohitimu, alianza kazi ya kufundisha katika shule ya maalum iliyokuwepo pale Mision Peramiho katika Seminari ya Kikatoliki ya Peramiho, akiwa hapo aliingia katika mgogoro na Mkuu wa shule ambaye alimtuhumu kuwa hafuati amri ya uongozi ya kukata nywele kila baada ya wiki mbili, ambapo Mzee huyu wakati wote alikuwa mtanashati na wakati huo alipenda kuchana nywele kwa mtindo wa “Way”.

Mgogoro huu ulisababishwa asimamishwe kazi kwa muda na kisha akahamishiwa kufundisha katika shule ya Nkaya alikosomea, aliweza kufundisha katika shule hiyo mpaka yalipotokea manyanyaso mengine ya kikoloni, ambapo Mwalimu Mkuu alimkera baada ya kumtukana mbele ya Wanafunzi na kumchapa makofi.

Sakata hilo liliamuliwa na Mkaguzi wa elimu kutoka Peramiho ambaye katika uamuzi wake alimhamishia katika kata ya Lituhi, jirani na Ziwa Nyasa ambako kulikuwa ni maili mbili kutoka alikokuwa huko alifanya kazi kwa mwaka mmoja na akaamua kuacha.

Mwaka 1942 Mzee Millinga aliibuka na uamuzi mwingine wa kuachana na kazi ya ualimu na akaamua kufanya safari ya kwenda Afrika Kusini kutafuta kazi, wakati huo nchi hiyo ilikuwa chini ya utawala wa Makaburu.

Alivyoianza safari ya kwenda huko akiwa na wenzake watatu, alikusanya nguo zake akizitaja kuwa ni Kaptura ya ziada (Mtindo wa vijana wakati huo ilikuwa kuvaa Kaptura) shati na shuka.

Wakati huo walipanda Mtumbwi, kutoka ukingoni mwa Ziwa Nyasa na waliweza kusafiri hadi Kyela na kisha wakaenda mji wa Karonga walikopanda meli ya MV Mpasa kwa nauli ya shilingi 30 wakati huo, mpaka Nkhata Bay na baadae walipanda gari Moshi hadi mji mkuu wa Blantyre.

Baada ya hapo safari iliendelea kwa gari Moshi kupitia Msumbiji na kuendelea hadi Zimbabwe, walipofika katika mji wa Salisbury wakiwa katika gari Moshi walikamatwa na askari waliowahoji kuhusu vibali vyao vya kusafiria.

Pamoja na mambo mengine, wakati huo walisafiria kwa kutumia nyaraka walizozitayarisha kwa maarifa yao zilizofanana na hati za kusafiria za wakati huo, lakini askari wale hawakuwaamini hivyo waliwekwa mahabusu na kuwafungulia mashitaka.

Wakiwa mahabusu walikutana na baadhi ya askari waliotokea Tanganyika ambao waliwasaidia kwa kuwaelekeza kwamba, ili wajinasue wajifanye hawajui Kiingereza wala Kiswahili bali wazungumze lugha ya Kimanda tu.

Mbinu hiyo ilileta utata mkubwa walipopelekwa Mahakamani, ilibidi Hakimu aliyekuwa anasikiliza kesi yao atafute mwendesha mashitaka anayejua Kiswahili ambapo pia iligundulika kuwa hawakijui Kiswahili.

Hivyo Mahakama iliwapa kibali cha kuwepo Zimbabwe kwa siku 14, waliishi huko wakihifadhiwa na Watanganyika wenzao na baadae waliendelea na safari ya kwenda Afrika Kusini, safari iliyowachukua siku tano huku wakivuka mbuga ya Transvaal kwa mguu wakiwa kundi la watu wapatao 10 walikabiliana na wanyama wakali na ukosefu wa maji ya kunywa, kuna wakati hawakulala huku baadhi ya maeneo walipofika walikuwa wakipeana zamu pale walipotaka kulala wengine wanakuwa macho wakijilinda na kukoka moto, kitu cha kustaajabisha ni kwamba baadhi ya wanyama wakali kama vile Faru waliuzunguka moto huo.

Walilazimika kuingia kwenye mashimo yaliyochimbwa na wanyama kutafuta maji, wakati mwingine walikuwa wakifukua mabonde ya mito ili kuweza kupata maji hatimaye safari yao ilifika katika mgodi wa Transvaal, ambako alienda kuomba kazi na akabahatika kupangwa katika stoo ya vyombo vya kuchimbia mgodi wa madini.

Alipewa kazi hiyo kutokana na kuwa na mwandiko mzuri na wenzake walipata kazi katika vitengo vingine vya uchimbaji.

Mzee Millinga na wenzake walipofika pale mgodini waliweza kuonana na Watanganyika wengine, waliokuwepo huko na hao ndiyo waliowapa mbinu za kuwaingia Makaburu na kufanikiwa kupata kazi mgodini.

Hata hivyo hakuridhika na kazi hiyo, hivyo baada ya miezi miwili aliamua kuondoka pale na kuelekea mjini Johannesburg na kisha Cape Town ambako alipata ajira, kazi hii ya sasa ilikuwa ngumu kwa kuwa alipata kazi ya kubeba vifaa vya wachimba migodi, alikuwa anaingia mgodini asubuhi na kutoka jioni wakati huo malazi yalikuwa katika hema.

Baada ya mwezi mmoja wafanyakazi wenzake kutoka Tanganyika walimnong’oneza kuwa kuna nafasi ya kazi ya kitengo cha Ofisini, wakamsihi aandike barua ya maombi ambapo aliandika barua kuomba kazi hiyo na katika usaili alifanya vizuri na hapo alifanikiwa kupanda cheo na kuongezewa marupurupu na kuna wakati alilipwa posho ya ziada kwa kufanya kazi ya watu wawili.

Mwanzoni mwa mwaka 1950 alirejea nyumbani Tanganyika baadae alipata habari kuwa baba yake mzazi alikuwa mjini Dodoma, aliamua kumfuata ili aweze kumshawishi arudi nyumbani Lituhi ambapo alikubali na akarejea nyumbani, lakini Mzee Millinga hakurudi nyumbani bali aliendelea na safari hadi Wilayani Ngudu kwa baba yake mdogo aliyekuwa Inspekta wa Polisi ambapo ilikuwa sasa ni chimbuko la kupata ajira katika Idara ya Maendeleo ya Jamii, kwa msaada wa rafiki wa Inspekta huyo aliyekuwa anafahamika kwa jina la Fredrick Mchauro.

Mzee Millinga alijiunga na chama cha TAA Mkoani Tabora, akiwa mtumishi wa Idara hiyo huko alipandishwa cheo kuwa katibu wa TAA Tabora katika kipindi hicho, Bwana Mchauro alikuwa amehama Tabora kabla ya hapo alikuwa Mwenyekiti wa TAA Tabora.

Baada ya safari ndefu ya utumishi wa Serikali na harakati za TAA na TANU, baada ya Uhuru Mzee huyo akiwa mkazi wa mtaa wa Lindi na baadae Temeke Wailesi Kota, Dar es Salaam na hapo baada ya Uhuru alijikita zaidi katika ajira yake ya Serikali.

Utumishi wake ulipitia katika sehemu tofauti, kuanzia Kilindi alikokuwa amehamia baada ya kutoka Dar es Salaam mara tu baada ya Uhuru na baadaye alihamia Morogoro na baada ya mizunguko ya muda mrefu, aliomba ahamishiwe kwao Mbinga ambako aliondoka miaka mingi na kustaafu utumishi rasmi mwaka 1976.

Mzee Millinga, ambaye ni kati ya Waasisi 17 wa TANU mwaka 1954 hapa nchini, amefariki dunia usiku wa kuamkia Machi 5 mwaka 2018 saa 7:40 Mbinga mjini akiwa nyumbani kwake amezungukwa na familia yake. 

Kabla ya kukutwa na umauti afya yake ilianza kutetereka kuanzia miaka saba iliyopita akisumbuliwa na Kiharusi, alikuwa akipata matibabu yake katika Hospitali ya Wilaya ya Mbinga, Peramiho iliyopo Songea na hatimaye alikuwa akitibiwa Muhimbili jijini Dar es Salaam.

Marehemu ameacha Mjane, watoto 10 wakiwemo Wanaume watano na Wanawake watano na kwamba watoto wanne wametangulia mbele ya haki, pia Marehemu ameacha Wajukuu 29 na Vitukuu 10.

Katika mazishi yake ambayo yameongozwa na Naibu Askofu wa Jimbo la Mbinga, Padri Josephat Malunda yamefanyika leo Machi 8 mwaka huu majira ya saa 10:00 jioni, katika makaburi yaliyopo mazingira ya nyumbani kwake mtaa wa Kihaha Mbinga mjini, viongozi mbalimbali wa Chama na Serikali waliweza kuhudhuria akiwemo Naibu Katibu Mkuu Taifa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rodrick Mpogolo na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Ruvuma, Oddo Mwisho na wa Wilaya ya Mbinga, Beda Hyera.  

Hata hivyo kwa upande wa Serikali alikuwa Mkuu wa Mkoa huo, Christine Mndeme na Wakurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga vijijini, Gombo Samandito na Mji wa Mbinga, Robert Mageni huku shughuli hiyo ya mazishi ikiwa imehudhuriwa na Wananchi wengi wa kutoka Mbinga na nje ya Wilaya hiyo. 

Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Marehemu mahali pema peponi……Amina.

No comments: