Tuesday, March 13, 2018

VIKUNDI VYA WANAWAKE MBINGA WAPEWA MKOPO MILIONI 10


Afisa wa idara ya maendeleo ya jamii Halmshauri ya mji wa Mbinga Mkoani Ruvuma, Alphonce Njawa akitoa maelezo mafupi kwa Mkuu wa Mkoa huo, Christine Mndeme (aliyevaa kitambaa rangi ya njano kichwani) juu ya bidha mbalimbali zinazotengenezwa na vikundi vya wanawake wajasiriamali katika Halmashauri hiyo.

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme (aliyevaa kitambaa rangi ya njano) akipata maelezo mafupi kutoka kwa mjasiriamali juu ya faida ya ulaji wa matunda ya asili.



Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

KATIKA kukuza maendeleo ya mwanamke, Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga Mkoani Ruvuma imefanikiwa kusajili vikundi 50 vya wanawake ambao ni Wajasiriamali, wakiwa wanajishughulisha na biashara ndogondogo.

Aidha vikundi hivyo vimekuwa vikijishughulisha na shughuli za kilimo na ufugaji na kuweza kujipatia kipato cha kuendeleza maisha yao.

Hayo yalisemwa hivi karibuni na Paschal Ndunguru ambaye ni Mkuu wa idara ya maendeleo ya jamii Wilayani humo, siku ya maadhimisho ya wanawake duniani yaliyofanyika Wilayani hapa.


Alisema kuwa katika sehemu ya vikundi hivyo, 18 vimefanikiwa kuanzisha SACCOS ya wanawake kwa lengo la kusimamia utoaji mikopo na marejesho katika hali ya usawa ambapo ina jumla ya wanachama 300.

“Halmashauri yetu imefanikiwa kutoa mikopo ya mzunguko kwa vikundi vya wanawake kumi, yenye jumla ya shilingi Milioni 10 ambazo zimetolewa kwa kupitia SACCOS hiyo kwa mujibu wa mwaka wa fedha wa 2016/2017”, alisema Ndunguru. 

Ndunguru alieleza pia kwa kushirikiana na asasi mbalimbali zilizopo Wilayani Mbinga, wameweza kuendelea kujenga uelewa kwa jamii juu ya haki ya mwanamke na mtoto wa kike hasa katika mazingira ya vijijini na kwamba, kipindi cha mwaka 2016/2017 idadi ya viongozi wapatao 53 wameweza kushika nyadhifa mbalimbali za uongozi.

Hata hivyo kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo VETA na SIDO pamoja na asasi za kiraia Wilayani humo wameweka vipaumbele vya kuwainua wanawake hasa waliopo vijijini, ambapo vikundi saba vya wanawake ambavyo vimeanza kutekeleza dhamira ya Tanzania ya viwanda kwa kujishughulisha na kazi ya usindikaji wa bidhaa na kuongeza thamani.

No comments: