Tuesday, March 27, 2018

WAJAWAZITO TUWE MACHO TUNDURU WAISHUKURU TASAF KUWAJENGEA ZAHANATI

Na Muhidin Amri,    
Tunduru.

WANAWAKE Wajawazito katika kijiji cha Tuwe Macho kata ya Tuwe Macho Wilayani Tunduru Mkoa wa Ruvuma, wameishukuru Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) Wilayani humo kwa kujenga Zahanati ambayo hivi sasa inawasaidia kupata tiba na ushauri juu ya masuala ya afya na uzazi, hivyo kuweza kupunguza idadi ya vifo vya akina mama Wajawajazito kabla na wakati wa kujifungua.

Walisema kuwa kabla ya TASAF kujenga Zahanati hiyo, walikuwa wakilazimika kutembea umbali mrefu na kutumia muda mwingi kwenda kutafuta huduma husika Hospitali ya Wilaya Tunduru iliyopo mjini hapa, jambo ambalo liliwafanya kwa kiasi kikubwa kukosa hata muda wa kushiriki kikamilifu katika shughuli zao za maendeleo.

Aidha wameiomba Serikali kuboresha mfumo wa utoaji huduma za afya ikiwemo kuwaletea waganga, vitanda vya kujifungulia sambamba na baadhi ya vifaa tiba ambavyo vitawezesha kupata huduma bora hasa wakati wa kujifungua.


Wakizungumza kwa nyakati tofauti walisema kuwa licha ya Serikali kupitia mfuko huo kujenga Zahanati hiyo katika kijiji hicho, kwa ajili ya kurahisisha upatikanaji wa  huduma za matibabu jirani na makazi yao bado huduma za afya zimekuwa duni kwa sababu ya ukosefu wa Daktari na hivi sasa wamekuwa wakimtegemea Mhudumu mmoja tu wa afya.

Zabib Ameir na Hadija Issa walisema Mhudumu huyo tangu kufunguliwa kwa Zahanati hiyo mwaka mmoja uliopita, amekuwa anafanya kazi ya kutoa huduma mbalimbali za afya peke yake bila ya Wataalam wa afya, ambao wangeweza kusaidiana pamoja huku kukiwa na idadi kubwa ya wagonjwa wanaokwenda kupata matibabu.

Walisema kuwa licha ya TASAF kuonesha uzalendo na huruma kubwa kwa wakazi wa kijiji cha Tuwe Macho bado changamoto kubwa waliyonayo sasa ni ya upatikanaji wa baadhi ya huduma kwani Mhudumu aliyepo hawezi kutoa huduma ambazo zinahitaji mtaalamu ambaye ataweza kufahamu matatizo ya mgonjwa.

Kwa upande wake Muuguzi pekee anayefanya kazi katika zahanati hiyo Sada Lusenga, alisema hali ya upatikanaji wa huduma za afya katika Zahanati hiyo ni nzuri kwani kuna dawa za kutosha na wananchi wanaendelea kupata matibabu.

Hata hivyo aliongeza kuwa changamoto kubwa iliyopo ni uhaba wa watumishi kwani aliyekuwa sasa ni mmoja tu, ambapo ameiomba Serikali kuangalia uwezekano wa kupeleka watumishi wengine akiwemo Daktari ambaye ataweza kushirikiana na wenzake katika kuhudumia wagonjwa ipasavyo.

No comments: