Sunday, March 4, 2018

WATANZANIA WATAKIWA KUJIEPUSHA NA VITENDO VINAVYOTISHIA USALAMA WA NCHI YETU

Mkuu wa Majeshi ya ulinzi na usalama, Jenerali Venance Mabeyo wa kwanza upande wa kulia akiangalia kaburi la chifu wa kabila la Wangoni, Mbano Songea ambaye alinyongwa na Wakoloni wa Kijerumani mwaka 1905 baada ya kukataa kuwa kibaraka wa Wakoloni hao, ambapo wa pili upande wa kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme na watatu yake ni Mkuu wa Wilaya ya Songea, Palolet Mgema.
Mkuu wa Majeshi ya ulinzi na usalama, Jenerali Venance Mabeyo akikata utepe kufungua rasmi kumbukumbu na historia ya Mashujaa wa Vita ya majimaji katika Makumbusho ya Taifa ya Mashujaa wa vita hivyo mjini Songea, ambapo anayeshuhudia ni Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Christine Mndeme.



Na Muhidin Amri,      
Songea.

MKUU wa Majeshi ya ulinzi na usalama hapa nchini, Jenerali Venance Mabeyo amewataka Watanzania kujiepusha na vitendo vinavyoweza kutishia usalama wa nchi na kuharibu tunu ya amani tuliyonayo.

Aidha Jenerali Mabeyo, amewaomba Watanzania kuunga mkono juhudi mbalimbali zinazofanywa na Rais Dokta John Magufuli dhidi ya wizi, ufisadi na matumizi mabaya ya Ofisi za umma kwa kuwataja hadharani watu wanaojihusisha na vitendo hivyo.

Jenerali Mabeyo alitoa kauli hiyo juzi wakati akifunga maadhimisho ya tamasha la Mashujaa wa Vita ya Majimaji lililofanyika kwenye viwanja vya Makumbusho ya Mashujaa wa Vita hivyo mjini Songea.


Alisema kuwa mapambano ya vita dhidi ya wizi na ufisadi yaliyoanzishwa na Rais Dokta Magufuli siyo ya mtu mmoja, bali kila Mtanzania anapaswa kushiriki kikamilifu kwani mali zinazoibwa na baadhi ya Watanzania zinapaswa kuwanufaisha watu wote. 

Alifafanua kuwa kuna mambo yanayotishia usalama wa nchi yetu na kwamba Serikali imedhamiria kuwatumikia wananchi wake kikamilifu, kwa kuboresha huduma za kijamii na kutoa fursa ya kufanya kazi za kujiletea maendeleo.

“Baadhi ya mambo yanayotishia usalama wa nchi yetu ni pamoja na matumizi mabaya ya utandawazi ambayo mbali na kuharibu utamaduni wa nchi yetu, watu wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii vibaya kwa kuhamasisha wananchi kufanya na kushiriki katika matukio ambayo yanaashiria uvunjifu wa amani”, alisema.

Vilevile alishauri shule za msingi, sekondari na vyuo hapa nchini kufundisha wanafunzi wetu umuhimu wa kulinda, kutunza amani pamoja na Watanzania kuishi kwa kupendana badala ya kutumia muda wao kutafuta sababu za kutengana ambazo hazina tija kwa taifa letu.

Katika hatua nyingine, Jenerali Mabeyo ameitaka Wizara ya maliasili na utalii kuboresha makumbusho ya Mashujaa wa Vita ya majimaji ili yatumike kwa ajili ya utalii, ambapo yanaweza kuliingizia taifa letu fedha nyingi.

Alisema kuwa makumbusho hayo ni muhimu kwani yatasaidia kudumisha na kukumbusha historia ya nchi  yetu  na kuwataka Watanzania, kuwaenzi kwa vitendo Mashujaa waliopigana vita hivyo kwa ajili ya kulikomboa taifa letu kutoka  mikononi  mwa Wakoloni wa Kijerumani.

Kadhalika alisema Mashujaa wa majimaji walionesha uzalendo mkubwa kwa taifa letu, kwa hiyo Watanzania waliobaki hawana budi nao kuonesha kwa vitendo jinsi wanavyochukia vitendo vinavyoweza kudhoofisha kazi inayofanywa na Amiri Jeshi Mkuu, Rais Dokta John Magufuli.

Siku ya makumbusho ya Mashujaa hao inawakumbusha Watanzania namna Mashujaa walivyojitoa muhanga na kupoteza uhai wao kwa ajili ya wananchi wengine na kwa manufaa ya nchi yetu.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Chiristine Mndeme alisema Serikali ya Mkoa huo itahakikisha inaongeza nguvu katika kulinda mipaka yake ili wananchi wa Mkoa huo, waweze kuendelea na kazi ya uzalishaji mali.

Mndeme alisema Serikali itasimamia na kulinda mali za Mkoa na Taifa kwa ujumla kama walivyofanya Mashujaa hao ambao walikubali kupoteza maisha yao kwa ajili ya nchi yetu.

Pamoja na mambo mengine, Mndeme ambaye pia ni Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya Mkoa wa Ruvuma aliongeza kuwa kila mwaka ifikapo  Februari 27, Wananchi wa Mkoa wa Ruvuma na Watanzania wanakutana ili kuwakumbuka Mashujaa hao ambapo wataendelea kukumbukwa kwa faida ya vizazi vya sasa na vijavyo.

No comments: