Wednesday, April 27, 2016

MATUKIO KATIKA PICHA SIKU YA BONANZA LA VIJANA WA MBINGA KUELIMISHA RIKA NA USAFI WA MAZINGIRA MJI WA MBINGA MKOANI RUVUMA

Vijana wakishiriki katika zoezi la usafi, kwenye eneo la soko la wakulima lililopo katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma siku ya maadhimisho ya bonanza la vijana wa Mbinga kuelimisha rika na usafi wa mazingira.

Wanabonanza wakiwa katika picha ya pamoja, wakati wakijiandaa kukabidhi baadhi ya vifaa vya kufanyia usafi kwa wafanyabiashara wa soko la wakulima lililopo mjini hapa.

Upande wa kushoto, Baraka Mwabulesi ambaye ni Mwenyekiti wa bonanza la vijana Mbinga akikabidhi baadhi ya vifaa vya kufanyia usafi kwa mmoja kati ya wafanyabiashara waliopo katika soko la wakulima mjini hapa.

Kutoka kushoto ni Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya mji wa Mbinga, Oscar Yapesa naye alishiriki kikamilifu katika zoezi hilo la kuhamasisha wananchi wazingatie masuala ya kufanya usafi katika mji huo, ambapo hapo alikuwa akikabidhi sehemu ya vifaa vya kuhifadhia taka (dust bin) kwa wafanyabiashara wa soko la wakulima lililopo Mbinga mjini. (Picha zote na Gwiji la matukio Ruvuma)

VITENDO VYA USHIRIKINA SHULE YA SEKONDARI NGWILIZI VYADHIBITIWA BAADA YA WAZEE KUKETI PAMOJA DIWANI AELEZEA MIKAKATI YAKE YA KIMAENDELEO


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

VITENDO vya ushirikina ambavyo vilikuwa vikifanyika katika shule ya sekondari Ngwilizi iliyopo kata ya Kitanda Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, vimedhibitiwa baada ya wazee wa kata hiyo kuketi pamoja na kuzungumzia juu ya kumaliza kero hiyo.

Diwani wa kata hiyo, Zeno Mbunda alisema hayo alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu na kueleza kuwa muafaka huo ulifikiwa baada ya kukubaliana na wazee hao kwamba, visiendelee kufanyika kwani vimekuwa vikirudisha nyuma maendeleo ya walimu na wanafunzi wanaosoma katika shule hiyo na kata kwa ujumla.

Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Ngaga.
“Wazee wamekwisha kaa vikao na kumaliza tatizo hili, kwa makubaliano kwamba visiendelee kufanyika tena”, alisema Mbunda.

Awali hivi karibuni katika kikao kilichoketi Aprili 2 mwaka huu, ilielezwa kuwa walimu na wanafunzi hao hufanyiwa vitendo vya hovyo nyakati za usiku ambapo huteswa na wakati mwingine wakiwa wamelala, hujikuta wakiwa nje ya nyumba zao wamevuliwa nguo walizovaa mwilini.

Pamoja na mambo mengine, akizungumzia juu ya mikakati ya kimaendeleo aliyojiwekea katika kata hiyo Mbunda alisema kuwa wameunda kamati ya kuendeleza zao la kahawa katika kata hiyo yenye lengo la kuwafanya wananchi wake, waweze kushiriki kikamilifu katika kuendeleza kilimo cha zao hilo na kukuza uchumi wao.

Tuesday, April 26, 2016

DED LUSEWA APIGA MARUFUKU VIJANA KUFANYA MAANDAMANO YASIYOKUWA YA LAZIMA



Na Muhidin Amri,
Namtumbo.

MKURUGENZI mtendaji wa Mamlaka ya mji wa Lusewa, wilayani Namtumbo mkoa wa Ruvuma Astery Mwinuka, amepiga marufuku tabia ya vijana kufanya maandamano yasiyokuwa ya lazima pindi wanapodai haki zao, badala yake wafuate sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa ikiwemo kutumia Ofisi ya Mamlaka hiyo katika kutafuta majawabu ya kero zao mbalimbali zinazowakabili.

Mwinuka alitoa onyo hilo, mara baada ya kukabidhiwa rasmi  majengo  yatakayotumika kama Ofisi za Mamlaka ya mji wa Lusewa katika sherehe fupi iliyofanyika hivi karibuni na kuhudhuriwa na wananchi wa kata tatu za Lusewa, Msisima na Magazini ambazo kwa pamoja zimeunda mamlaka hiyo.

Alisema kuwa tayari serikali imesikiliza kilio chao  kwa kuanzisha mamlaka ya mji huo ambayo itakuwa na dhamana ya kusimamia shughuli zote za maendeleo, kutatua kero na kukabiliana na changamoto mbalimbali, hivyo ni vyema wananchi wakawa na utaratibu wa kupeleka kero zao katika ofisi hizo badala ya kuanzisha migogoro isiyokuwa na tija kwao.

“Tumepata mamlaka ya mji kamili hapa Lusewa, natoa onyo kali kuanzia sasa hakuna tena maandamano ambayo yatawapotezea muda wenu wa kufanya kazi kama kuna tatizo  tumieni ofisi za mamlaka na sio kukimbilia kwa mkuu wa wilaya, mtapoteza muda wenu wa kufanya kazi na wengine mtajikuta mkiishia mikononi mwa vyombo vya dola”, alisema Mwinuka.

BONANZA LA VIJANA MBINGA LASISITIZA MASUALA YA USAFI WA MAZINGIRA PIA LATOA MSAADA WA VIFAA MBALIMBALI KWA WATOTO YATIMA

Baadhi ya wanabonanza la vijana wa Mbinga mkoani Ruvuma, la kuelimisha rika na usafi wa mazingira wakishiriki kuzoa taka katika eneo la soko la wakulima Mbinga mjini.

Wanabonanza wakiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Ngaga mara baada ya kuwasili katika kituo cha Twiga kilichopo mjini hapa ambacho hulea watoto Yatima wanaoishi katika mazingira magumu.

Upande wa kulia Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga akikabidhi mafuta ya kupikia na vitu vingine mbalimbali kwa mlezi wa kituo cha kulea watoto Yatima ambao wanaishi katika mazingira magumu kinachofahamika kwa jina la Twiga, kilichopo Mbinga mjini. Msaada huo ulitolewa na Bonanza la vijana wa Mbinga la kuelimisha rika na usafi wa mazingira.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WANANCHI waishio katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, wametakiwa kuzingatia masuala ya usafi kuanzia kwenye mazingira yao wanayoishi majumbani kwao hadi katika maeneo wanayofanyia kazi au biashara, ili waweze kuuweka mji huo katika hali ya usafi na kuepukana na magonjwa mbalimbali ya mlipuko.

Rai hiyo ilitolewa na Mkuu wa wilaya ya Mbinga Senyi Ngaga alipokuwa kwenye maadhimisho ya bonanza la vijana wa Mbinga la kuelimisha rika na usafi wa mazingira, lililofanyika juzi katika uwanja wa taifa mjini hapa.

Bonaza hilo lilikuwa likienda sambamba na kauli mbiu isemayo; zuia ngono zembe, mimba za utotoni, madawa ya kulevya na elimu inalipa.

Maadhimisho hayo yalifanyika kwa kuanza kufanya usafi katika eneo la soko la wakulima lililopo mjini hapa kwa kuwashirikisha wananchi, watumishi wa serikali na wale wanaotoka kwenye sekta binafsi.

Watoto Yatima wakiwa na Wanabonanza kituo cha Twiga Mbinga.
Aidha waliweza kuwatembelea watoto yatima ambao wanalelewa katika kituo cha kulea watoto hao wanaoishi katika mazingira magumu kinachofahamika kwa jina la Twiga, kilichopo kata ya Matarawe Mbinga mjini kwa kuwapatia msaada wa vitu mbalimbali kama vile sabuni za kuogea na kufulia, daftari, kalamu, mafuta ya kupikia, sukari, pamoja na sare za shule.

Ngaga alisema kuwa kuna kila sababu katika jamii kuona umuhimu wa kusaidia watoto hao, ili wasiweze kujiona wakiwa katika hali ya kutengwa kwa kuwasomesha na hatimaye waweze kutimiza ndoto yao ya kuwa na maisha bora.

Monday, April 25, 2016

WALIMU WATAKIWA KUWA MABALOZI WAZURI KATIKA KUPINGA VITENDO VYA UKATILI WA KIJINSIA


Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MJUMBE wa Kamati ya utendaji Taifa, Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) mkoani Ruvuma, Jema Mapunda ameipongeza serikali ya awamu ya tano ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais Dkt. John Magufuli kwa kutoa elimu msingi bure, ambapo kupitia utekelezaji huo itaweza kuwapa fursa watoto wa kike kupata elimu hiyo hadi sekondari kwa ufanisi mzuri.

Mapunda alisema hayo juzi, alipokuwa akifungua mafunzo ya siku moja kwa walimu wanawake viongozi wa CWT mkoani hapa, yaliyofanyika mjini Songea.

Alisema kuwa familia nyingi awali zilikuwa zinasomesha watoto wao kwa kuwapa kipaumbele watoto wa kiume, huku wakike wakibaki nyumbani kwa kisingizio cha kukosa ada na michango mbalimbali jambo ambalo hivi sasa limekomeshwa na Rais Dkt. Magufuli.

NALICHO AWATAKA WATUMISHI KUWAHUDUMIA WANANCHI IPASAVYO MAMLAKA YA MJI WA LUSEWA



Na Muhidin Amri,
Namtumbo.

MKUU wa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Chande Nalicho amezindua rasmi Mamlaka ya mji wa Lusewa na kumuagiza Mkurugenzi wa mamlaka pamoja na watumishi waliopelekwa kufanya kazi katika mamlaka hiyo, kuhamia haraka huko ili waweze kwenda kuwahudumia na  kutatua kero zinazowakabili wananchi.

Mkuu huyo wa wilaya ametoa agizo hilo alipokuwa akizungumza na mamia ya wananchi wa kata ya Lusewa, Msisima na Magazini katika sherehe  za uzinduzi wa mamlaka ya mji huo zilizofanyika katika  kijiji cha Lusewa wilayani hapa.

Chande Nalicho.
Amewaagiza watumishi hao, kwenda kufanya kazi usiku na mchana kwa kushirikiana na wananchi ili waweze kupata vigezo vya kuwa  halmashuri ya mji badala ya kuendelea kuwa mamlaka ya mji, jambo ambalo linaweza kuwakosesha baadhi ya vitu muhimu vinavyotolewa na Wizara husika ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).

Alisema kuwa, mamlaka ya mji wa Lusewa ndiyo kwanza inaanzishwa kwa lengo la serikali kusogeza huduma karibu na wananchi wake hivyo ni jukumu sasa la watumishi hao kuhakikisha kwamba, wanajitolea muda wao kufanya kazi  na kutatua changamoto  zinazowakabili wananchi hao ambao wana mategemeo makubwa baada ya serikali kuanzisha mamlaka hiyo.

MUVI RUVUMA YAWAUNGANISHA WAJASIRIAMALI



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MRADI wa Muunganisho Ujasiriamali Vijijini (MUVI) mkoani Ruvuma umeendesha kongamano, lililokutanisha taasisi za kifedha na wajasiriamali wadogo wadogo kwa lengo la kuwafanya waweze kutambua na kuchagua ni taasisi gani ya fedha watakayoweza kutumia katika kuendesha shughuli zao za kilimo, usindikaji na upatikanaji wa masoko ya kuuzia bidhaa zao wanazozalisha.

Jumla ya Wajasiriamali 150 ambao waliwakilisha wenzao 545 waliopo katika mnyororo wa thamani wa zao la mhogo, kutoka wilaya nne za mradi za Mbinga, Namtumbo, Songea Vijijini, na Nyasa.

Kongamano hilo ambalo lilifanyika juzi katika ukumbi wa chuo kikuu Huria tawi la Songea, lililenga kuwasaidia wajasiriamali hao waweze kuchagua ni   taasisi gani za fedha  wanazoweza kuzitumia katika shughuli zao za ujasiriamali wanazofanya kila siku na masoko katika zao la mhogo ambalo sasa lina soko kubwa ndani ya nchi na  nje ya nchi.

Thursday, April 21, 2016

WAJUMBE KAMATI YA SIASA WAFUNGA MAKUFULI OFISI ZA CCM NYASA

Na Kassian Nyandindi,

Nyasa.

WAJUMBE wa Kamati ya siasa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, wamefunga kwa makufuli Ofisi za chama hicho wilayani humo wakishinikiza kuwakataa Katibu wa wilaya hiyo, Greyson Mwengu kutokana na kudaiwa kufanya ubadhirifu wa fedha zaidi ya shilingi milioni 50.

Aidha Katibu msaidizi wa CCM wa wilaya hiyo, Mussa Mwevi naye alikataliwa na kamati hiyo ya siasa kufuatia kutuhumiwa kushiriki kwa namna moja au nyingine kufanya ubadhirifu huo.

Tukio hilo lilitokea Machi 30 mwaka huu majira ya asubuhi, ambapo viongozi hao wa Chama cha mapinduzi wilayani humo wanadaiwa kutumia fedha hizo kinyume na taratibu ambazo zilitakiwa wakawalipe posho viongozi wa matawi, mabalozi na mawakala kipindi cha uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka jana.

TAKUKURU RUVUMA YASEMA HALMASHAURI ZIMESHAMIRI VITENDO VYA RUSHWA

Yustina Chagaka, Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Ruvuma.


Na Kassian Nyandindi,
Songea.

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoani Ruvuma imesema kwamba, katika mkoa huo watumishi wengi wa serikali wamekuwa wakijihusisha na vitendo vya kushawishi na kupokea rushwa kutokana na kuwa watovu wa maadili, katika utekelezaji wa majukumu yao ya kazi za kila siku.

Kufuatia hali hiyo, imeelezwa kuwa serikali imeazimia kupambana na vitendo hivyo na kuwaasa watumishi hao, kuzingatia maadili ya kazi zao na wananchi washiriki kikamilifu katika kutoa taarifa pale wanapoona au kusikia kuna harufu ya vitendo vya rushwa.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa TAKUKURU mkoa wa Ruvuma, Yustina Chagaka alipokuwa akitoa taarifa yake ya utendaji kazi kwa waandishi wa habari, kwa kipindi cha Januari hadi Machi mwaka huu.

SERIKALI KUBORESHA MITAMBO YA KURUSHIA MATANGAZO TBC




Na Kassian Nyandindi,
Songea.

IMEELEZWA kwamba serikali hapa nchini, itahakikisha inaboresha na kuimarisha mitambo yake ya kurusha matangazo katika mkoa wa Ruvuma, kupitia redio ya Taifa (TBC) kituo cha Songea ili kuifanya wilaya ya Nyasa na Namtumbo mkoani humo, ziweze kufikiwa na matangazo mbalimbali yanayorushwa na kituo hicho kwa ufanisi mzuri.

Kauli hiyo ya serikali inafuatia baada ya wananchi wa mkoa huo, kulalamika kwa muda mrefu kuwa redio hiyo ya taifa matangazo yake hayawafikii katika wilaya hizo na badala yake muda mwingi wanapofungua redio zao, husikia matangazo ya kutoka katika redio zilizopo nchi ya Malawi na Msumbiji.

Naibu Waziri wa habari, utamaduni, sanaa na michezo Anastazia Wambura alisema hayo hivi karibuni mjini hapa alipokuwa kwenye kikao maalum akizungumza na waandishi wa habari, pamoja na baadhi ya watumishi wa serikali mkoani humo.

TASAF SONGEA KUNUFAISHA KAYA MASKINI




Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MPANGO wa kunusuru kaya maskini unaotekelezwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) awamu ya tatu katika Halmashauri ya wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, unatarajia kunufaisha kaya 5,016 zilizopo katika wilaya hiyo ambazo zitapewa ajira za muda na kunufaika na mpango huo, utakaogharimu kiasi cha shilingi milioni 865,260,000.

Ofisa ushauri na ufuatiliaji wa TASAF katika halmashauri hiyo, Aniceth Kyaruzi, alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza na mwandishi wa gazeti hili ofisini kwake mjini hapa.

Kyaruzi alisema kuwa halmashauri ya wilaya ya Songea, imekwisha anza mchakato wake wa kuibua na kupanga miradi kwa ajili ya kutoa ajira za muda katika vijiji 37 wilayani humo, ambavyo ni miongoni mwa vijiji 48 vinavyotekeleza mpango huo wa kunusuru kaya maskini.

WAKULIMA WATAKIWA KUNUNUA PEMBEJEO ZINAZOUZWA NA TFA

Upande wa kulia Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Senyi Ngaga akihoji juu ya ubora wa pembejeo za kilimo zinazouzwa na TFA ambapo aliwataka wakulima wa wilaya hiyo kwenda katika duka la taasisi hiyo lililopo mjini hapa kununua pembejeo hizo ili waweze kuboresha mashamba yao.


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

WAKULIMA wa mazao ya chakula na biashara wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wametakiwa kujiunga uanachama na Umoja wa Chama Cha Wakulima Tanzania (TFA) ili waweze kunufaika na fursa zilizopo, ikiwemo uzalishaji wa mazao yao kwa ubora unaotakiwa.

Aidha imeelezwa kuwa ndani ya chama hicho, wakulima hao wataweza kupata elimu juu ya kilimo bora cha kisasa, matumizi sahihi ya pembejeo na kuingia mikataba na TFA ambayo baadaye itawawezesha kuwatafutia masoko ya kuuza mazao yao ya chakula na biashara.

Hayo yalisemwa na Mkuu wa wilaya hiyo, Senyi Ngaga alipokuwa akizungumza kwenye maadhimisho ya ufunguzi wa duka la pembejeo za kilimo tawi la TFA lililopo wilayani humo.

WANANCHI WAITAKA HALMASHAURI KUWAUNGA MKONO



Na Kassian Nyandindi,
Njombe.

WAKAZI wa kijiji cha Mwilamba kata ya Kipengele wilaya ya Wanging’ombe mkoani Njombe, wameitaka Ofisi ya Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya hiyo kuunga mkono jitihada zinazofanywa na wananchi hao, juu ya utunzaji wa vyanzo vya maji vilivyopo kijijini hapo ambavyo ni tegemeo kubwa kwa mkoa huo.

Aidha wamemuomba Mkuu wa wilaya hiyo, Asumpta Mshama kuacha kutumia muda mwingi kukaa ofisini badala yake atembelee vyanzo hivyo ambapo walieleza kuwa serikali ya wilaya, imevitelekeza kwa miaka mingi na kuwaachia wananchi pekee waendelee kuvitunza.

Kauli hiyo ilitolewa na wakazi hao ambao waliomba majina yao yasitajwe gazetini, walipokuwa wakizungumza na waandishi wa habari ambao walitembelea kijijini hapo, kwa ajili ya kujionea changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo.

Saturday, April 16, 2016

WANANCHI WAILALAMIKIA HALMASHAURI YAO


Haya ni madaraja yanayolalamikiwa na Wananchi wa kijiji cha Mwilamba wilaya ya Wanging'ombe mkoani Njombe, ambapo ujenzi wake umekuwa ni wa kusuasua. (Picha na Kassian Nyandindi)


Na Kassian Nyandindi,
Njombe.

WANANCHI wa kijiji cha Mwilamba kilichopo katika kata ya Kipengele wilaya ya Wanging’ombe mkoa wa Njombe, wameulalamikia uongozi wa Halmashauri ya wilaya hiyo kwa kutochukua hatua za haraka kukamilisha ujenzi wa madaraja mawili yaliyopo katika kijiji hicho, ambayo hivi sasa yanasababisha washindwe kuendesha shughuli zao za maendeleo. 

Aidha wananchi hao walisema kuwa kwa muda mrefu, madaraja hayo ambayo yalianza kujengwa tangu mwezi Aprili mwaka jana hadi sasa ujenzi wake unaonekana kusuasua, na hawajui ni lini yatakamilika ili huduma zao za maendeleo ziweze kutekelezeka bila kuwepo usumbufu wa aina yoyote.

Walifafanua kuwa madaraja hayo, ambayo yapo katika mto Nang’ano yanaunganisha kijiji cha Mwilamba hadi kwenye barabara kuu ya kutoka Njombe mjini kwenda wilaya ya Makete.

Baadhi ya wananchi ambao waliomba majina yao yahifadhiwe, waliwaambia waandishi wa habari kuwa kutokana na hali hiyo ya ujenzi wa madaraja hayo kutokamilika hasa kipindi hiki cha masika, mto huo hufurika maji na wanashindwa kuvuka kwenda ng’ambo ya pili hasa pale wanapokuwa na wagonjwa ambao wanapaswa kwenda nao kupata matibabu kwenye kituo cha afya cha Misheni Kipengele ambacho kipo makao makuu ya kata hiyo.

WAJASIRIAMALI MANISPAA SONGEA WAIANGUKIA SERIKALI

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Said Mwambungu.


Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WANAWAKE ambao ni wajasiriamali katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wameiomba serikali kuwaandalia maeneo maalum ya kufanyia shughuli zao za kila siku ili waweze kujiingizia kipato, badala ya kutumia maeneo yasiokuwa rasmi ambayo yamekuwa yakiwasababishia adha kubwa wakati wanapofanya biashara zao.

Baadhi ya wanawake hao walisema hayo hivi karibuni, walipokuwa wakizungumza na mwandishi wa habari hizi huku wakieleza kuwa licha ya kujikita na kutumia zaidi nguvu kubwa katika shughuli zao, changamoto kubwa wanayokabiliana nayo hivi sasa ni kukosekana kwa mazingira rafiki ya kufanyia shuguli zao badala yake hulazimika kutumia maeneo ambayo hayajatengwa kisheria jambo ambalo huwasababishia usumbufu mkubwa, wa kufukuzwa na askari mgambo wa Manispaa hiyo.

Walisema kuwa, jambo hilo linawafanya kushindwa kusonga mbele kimaendeleo katika maisha yao ya kila siku na hata  kushiriki wakati wa kuchangia  shughuli mbalimbali za kijamii.

SHIRIKA LA NSSF RUVUMA LAJIPANGA KUTOA ELIMU KWA WADAU WAKE



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

SHIRIKA la Taifa Hifadhi ya Jamii (NSSF) mkoani Ruvuma, limejipanga katika kuendelea kutoa elimu kwa wananchi na watumishi wa serikali kwa kuhamasisha wajiunge na mifuko iliyoanzishwa na shirika hilo, ili waweze kuepukana na ugumu wa maisha pale wanapofikia hatua ya kustaafu utumishi wao serikalini.

Kauli hiyo ilitolewa na Meneja wa shirika hilo mkoani humo, Dominic Mbwette alipokuwa akizungumza na gazeti hili ofisini kwake mjini Songea huku akielezea shughuli mbalimbali, zinazofanywa na shirika hilo.

Mbwette alisema kuwa kuna baadhi ya wastaafu wamekuwa wakiishi katika mazingira magumu na wengine hufariki dunia, kutokana na kukosa huduma za msingi katika maisha yao ya kila siku hivyo ni vyema wajiunge na mfuko huo ili waweze kuondokana na matatizo hayo yanayowakabili.

DIWANI AJIKUTA AKIINGIA KATIKA KASHFA NZITO NA FEDHA ZA TASAF



Na Steven Augustino,
Tunduru.

DIWANI wa kata ya Tuwemacho wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, Khadija Mohamed amejikuta akiingia katika kashfa nzito baada ya kubainika alikuwa amejiandikisha miongoni mwa kaya maskini, ambazo zimeingizwa kwenye mradi wa uhaulishaji fedha unaotekelezwa na Mfuko wa Mendeleo ya Jamii (TASAF) wilayani humo.

Khadija alibainika kuingizwa kwenye mpango huo, huku akitambua kwamba anao uwezo wa kujimudu kimaisha, ambapo alibainika kufanya hivyo baada ya TASAF wilayani hapa kufanya zoezi la kuhakiki majina ya walengwa wanaostahili kupewa msaada wa fedha hizo ambao ni maskini hawajiwezi.

Sambamba na diwani huyo pia zoezi hilo limemng'oa Kaimu mtendaji wa kijiji cha Nasya katika kata hiyo, Msamati Omary ambaye naye alijiandikisha kuwa ni kati ya watu ambao wanastahili kupewa fedha hizo.

Wednesday, April 13, 2016

AHUKUMIWA MIAKA 30 JELA KWA KOSA LA UNYANG'ANYI WA KUTUMIA SILAHA




Na Steven Augustino,
Tunduru.

Yassin Raibu (31) ambaye ni mkazi wa kijiji cha Kazamoyo wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, amehukumiwa kutumikia kifungo cha miaka 30 jela baada ya kupatikana na kosa la unyang’anyi wa kutumia silaha.

Adhabu hiyo ilitolewa na Hakimu mfawidhi wa Mahakama ya wilaya hiyo, Gladys Barthy baada ya Mahakama kujiridhisha na kutokuwa na mashaka dhidi ya ushahidi uliotolewa na upande wa Jamhuri, ambao ulipeleka mashahidi saba kwa ajili ya kuthibitisha kosa hilo lililokuwa likimkabili.

Wakati huo Mahakama hiyo iliwaachilia huru watuhumiwa wengine wawili waliokuwa wanadaiwa kushirikiana na Raibu katika tukio hilo na kupora vitu mbalimbali vyenye thamani ya shilingi milioni 7,175,000 mali ya Said Khatib Yunusi, mkazi wa kijiji cha Lukumbule wilayani humo.

Saturday, April 9, 2016

TUNDURU WASHUKURU KUPATIWA HUDUMA YA MATIBABU MACHO BURE

Wataalamu wa macho kutoka 'Bilal Muslim Mission Tanzania' wakitoa matibabu ya 'operation' kwa wagonjwa wa macho wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma.


Na Steven Augustino,
Tunduru.

WATU 4,292 wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wamepatiwa  huduma ya matibabu ya macho kwa lengo la kuboresha afya zao na kuondokana na matatizo ya macho ambayo yalikuwa yakiwasumbua kwa muda mrefu.

Kati yao, watu 217 sawa na asilimia 5.3 ya wagonjwa wote waliopatiwa huduma hiyo walifanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho, kansa ya macho, vikope na majipu yaliyokuwa yakiwasumbua katika macho yao huku wengine wakipewa miwani kwa wale wote waliobainika kuwa na mahitaji hayo.

Shirika la Bilal Musilm Mission Tanzania, ndilo lililotoa msaada wa matibabu hayo bure kwa watu hao, ambapo Mratibu wa matibabu hayo Dkt. Ain Sharif alisema hayo wakati alipokuwa akitoa taarifa ya majumuisho ya utekelezaji wa zoezi hilo lililofanyika katika kambi ya kutolea huduma hiyo, iliyowekwa shule ya sekondari Frank Weston mjini hapa.

WATOA DAWA MAGONJWA YALIYOSAHAULIKA TUNDURU WAPEWA ONYO



Na Steven Augustino, 
Tunduru.

WATOA dawa kwa ajili ya kinga na tiba ya magonjwa yaliyosahaulika, wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, ambao wanajiona kwamba hawaendani na kasi ya utendaji kazi juu ya ugawaji wa dawa hizo, wametakiwa kujitoa mapema kabla hawajachukuliwa hatua za kisheria.

Hayo yamejitokeza kufuatia uwepo wa taarifa kwa baadhi ya wagawa dawa katika vijiji vya Nakapanya, Nalasi na vitongoji vyake wilayani humo ambapo kati yao wametishia kutaka kugomea zoezi hilo wakishinikiza waongezewe malipo ya ujira wa kufanya kazi hiyo.

Kaimu Katibu tawala wa wilaya ya Tunduru, Augustino Maneno alisema hayo wakati alipokuwa akimwakilisha Mkuu wa wilaya hiyo Chande Nalicho, kwenye zoezi la kuwaongoza baadhi ya wananchi ambao walijitokeza katika uzinduzi wa umezaji dawa hizo, uliofanyika hospitali ya wilaya iliyopo mjini hapa.

Magonjwa yaliyosahaulika na yale ambayo hayapewi kipaumbele (NTD) ni pamoja na magonjwa ya matende, mabusha, ngiri maji na ndiyo ambayo watu hupewa dawa ili yasiweze kuathiri afya zao.

VITENDO VYA USHIRIKINA VYAWATESA WANAFUNZI SHULE YA SEKONDARI NGWILIZI

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa vitendo vya ushirikina ambavyo vinaendelea kufanyika katika shule ya sekondari Ngwilizi iliyopo kata ya Kitanda Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, vimekuwa vikirudisha nyuma maendeleo ya walimu na wanafunzi wanaosoma kwenye shule hiyo.

Diwani wa kata hiyo, Zeno Mbunda amekemea hali hiyo na kueleza kuwa walimu na wanafunzi hao hufanyiwa vitendo vya hovyo nyakati za usiku ambapo huteswa na wakati mwingine wakiwa wamelala, hujikuta wakiwa nje ya nyumba zao wamevuliwa nguo walizovaa mwilini.

Senyi Ngaga Mkuu wa wilaya ya Mbinga.
Mbunda alisema hayo alipokuwa kwenye kikao cha kujadili maendeleo ya kata ya Kitanda, kilichoshirikisha Wenyeviti wa vijiji na wazee ambacho kilifanyika juzi katika kata hiyo huku akiongeza kuwa hali hiyo inasababisha hata kwa watumishi wengine wa serikali waliopo huko, wanaishi kwa hofu wakiogopa mambo hayo ya ushirikina.

“Haya mambo wazee wenzangu hayafai inatupasa tuwe imara tubadilike, watoto nyakati za usiku pale shuleni hawalali wanateswa, masuala kama haya wanaoyafanya mnawafahamu, inabidi tuwaite tukae nao na kukemea hali hii kwa sababu wanaleta hofu kwa wengine na kushindwa kuishi kwa amani”, alisema Mbunda.

KITUO CHA AFYA MSINDO CHAKABILIWA NA TATIZO LA UKOSEFU WA MAJI



Na Julius Konala,
Namtumbo.

KITUO cha afya Msindo, kilichopo katika Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, kinakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ukosefu wa maji na umeme jambo ambalo linakwamisha utendaji kazi kwa watumishi waliopo katika kituo hicho.

Jimmy Runje ambaye ni Mganga mkuu wa kituo hicho alieleza kuwa wanapohitaji huduma ya maji, hulazimika kuyafuata umbali mrefu na kuwafanya kuwa katika wakati mgumu hasa pale wanapofikia hatua ya kufua mashuka ya kulalia wagonjwa.

Hayo yalisemwa mwishoni mwa wiki na mganga mkuu huyo alipokuwa akizungumza na mwandishi wetu, ambaye alitembelea kituo hicho kwa ajili ya kujionea changamoto mbalimbali.

Thursday, April 7, 2016

DOKTA MAGUFULI ASHIRIKI SHUGHULI ZA KUMBUKUMBU MAUAJI YA KIMBARI KIGALI NCHINI RWANDA

 Rais wa Rwanda Paul Kagame akimpokea Rais Magufuli katika viwanja vya Gishozi kabla ya kwenda kuweka mashada ya maua, kwenye makaburi ya watu waliouwawa katika mauaji ya Kimbari.
 Rais wa Rwanda Paul Kagame akiwa na Rais Magufuli pamoja na Mama Janeth Magufuli, Janeth Kagame wakielekea kwenye makaburi ya halaiki katika makumbusho ya mauaji ya Kimbari, Gishozi Kigali nchini Rwanda.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa pamoja na Mkewe Mama Janeth Magufuli wakisali mbele ya makaburi ya watu waliouwawa katika Mauaji ya Kimbari nchini Rwanda mwaka 1994. Kulia ni Rais wa Rwanda Paul Kagame pamoja na Mkewe Janeth Kagame na mtoto wake.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa pamoja na Mkewe Mama Janeth Magufuli wakisali mbele ya makaburi ya watu waliouwawa katika Mauaji ya Kimbari nchini Rwanda mwaka 1994. Kulia ni Rais wa Rwanda Paul Kagame pamoja na Mkewe Janeth Kagame na mtoto wake.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Rais wa Rwanda Paul Kagame wakiwasha mwenge wa matumaini kuashiria kutotokea tena kwa mauaji ya Kimbari nchini Rwanda.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na mkewe Mama Janeth Magufuli wakiangalia kwa uchungu mafuvu ya watu waliopoteza maisha katika mauaji hayo ya kimbari. 
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Rais wa Rwanda Paul Kagame, mama Janeth Magufuli, Mama Janeth Kagame wakisikiliza historia ya jinsi mauaji ya kimbari yalivyotokea katika eneo la kumbukumbu ya mauji hayo.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Rais wa Rwanda Paul Kagame, mama Janeth Magufuli, Mama Janeth Kagame waiwa wamesimama kutoa heshima kwa watu waliofariki katika mauaji hayo ya kimbari.
 Waziri wa Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashiriki, Kikanda na Kimataifa, Mhe. Dkt. Augustine Mahiga akiwa miongoni mwa wageni mbalimbali waliofika kwenye kumbukumbu hizo.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akiangalia picha za watoto waliouwawa kinyama katika eneo la Kumbukumbu ya Mauaji ya Kimbaria  Gishozi Kigali nchini Rwanda.
 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akisaini Kitabu katika Jengo la makumbusho ya mauaji ya Kimbari Gishozi Kigali nchini Rwanda. 
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli akipokea kitabu chenye maelezo mbalimbali kuhusu mauaji hayo ya kimbari. (Picha na IKULU)

WAKAGUZI ELIMU NAMTUMBO WATAKIWA KUONGEZA KASI UTEKELEZAJI MAJUKUMU YA KAZI ZA KILA SIKU



Na Muhidin Amri,
Namtumbo.

WAKAGUZI wa elimu katika Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, wametakiwa kuongeza kasi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kazi ikiwemo kutembelea shule za msingi na sekondari mara kwa mara na kuwachukulia hatua kali za kisheria, walimu wazembe ambao wanasababisha wanafunzi kufanya vibaya katika mitihani yao ikiwa ni mkakati wa kuongeza kiwango cha ufaulu katika shule hizo.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa wilaya hiyo, Chande Nalicho alipokuwa akizungumza na wakaguzi wa idara ya elimu ofisini kwake mjini hapa, ambapo alikemea tabia ya wakaguzi kutumia muda mwingi kukaa ofisini na kuwaacha walimu peke yao wakitumia muda mwingi wa kazi kufanya shughuli zao binafsi.

Mkuu huyo wa wilaya alisema kwamba, hata tatizo la kushuka kwa ufaulu katika wilaya ya Namtumbo linachangiwa na idara ya ukaguzi  kwa kushindwa kutembelea shule hizo kwa kuwafuatilia utendaji kazi wa walimu hao.

MILONJI LUSEWA WATAKIWA KUPELEKA WATOTO WAO SHULE



Na Kassian Nyandindi,
Namtumbo.

WANANCHI wanaoishi katika kijiji cha Milonji,  kata ya Lusewa wilayani Namtumbo mkoani Ruvuma wameaswa kupeleka kwa wingi watoto wao shule  ili waweze kupata elimu, ambayo itawasaidia kutoka katika hali  ya umaskini unaowakabili kwenye familia zao.

Mkuu wa wilaya hiyo, Chande Nalicho alitoa rai hiyo juzi alipokuwa akizungumza na wazazi na walezi  pamoja na wananchi  wa kijiji hicho, katika mkutano wa hadhara wenye lengo la kutafuta majawabu  ya kukabiliana na changamoto zilizopo za watu kutotaka kupeleka watoto wao shule, alipokuwa kwenye ziara ya siku mbili katika kata ya Lusewa wilayani humo.
Chande Nalicho.

Alisema kuwa, baadhi ya wazazi wamekuwa hawatendi haki kwa watoto wao kwa kuwapa mahitaji ya msingi ikiwemo suala la kuwapatia elimu, jambo ambalo ni sawa na ukatili mkubwa unaofanywa na wazazi  kwa watoto wao.

Alisisitiza kuwa kila mzazi anaowajibu wa kuhakikisha watoto alionao watakapofikisha umri wa  kwenda shule, ni lazima wawe wameripoti shule ili wapate elimu ambayo ni urithi  endelevu katika maisha yao ya kila siku.

Mkuu huyo wa wilaya ya Namtumbo alifafanua kuwa hadi kufikia mwishoni mwa mwezi uliopita,  tayari  shule ya msingi Milonji imekwisha andikisha watoto 107  na imekuwa shule ya 8 ambayo inaongoza kwa kuitikia wito wa Rais Dkt. John Magufuli ya elimu bure.

JAMII YATAKIWA KUJIUNGA NA MFUKO WA TAIFA WA BIMA YA AFYA



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

USHAURI umetolewa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) mkoani Ruvuma kwamba, Halmashauri za wilaya, mji na manispaa  mkoani humo kuanza utaratibu wa kutunga sheria maalum, itakayowabana watu wote wasiotaka kujiunga na mfuko wa  afya ya jamii na bima ya afya.

Abdiel Mkaro, ambaye ni Meneja wa NHIF Mkoani humo ametoa ushauri huo alipokuwa akizungumza na gazeti hili juu ya mwamko mdogo wa wananchi kujiunga na mfuko huo, kwa ajili ya kupata huduma bora za matibabu pindi wanapougua.

Halmashauri hizo amezitaka kuhakikisha kwamba zinaongeza dawa katika zahanati, vituo vya afya na hospitali zake ili wanachama waliojiunga na mfuko huo waweze kupata huduma  ipasavyo pale wanapokwenda kupata huduma kutokana na maradhi yanayowasumbua, ambapo baadhi ya maeneo wanachama wamekuwa wakikosa dawa jambo ambalo limechangia  kwa kiasi kikubwa wananchi wengine  kuogopa kujiunga na mpango huo.

Wednesday, April 6, 2016

MHANDISI ASHINDWA KUTOLEA MAELEZO JUU YA UJENZI WA MADARAJA



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MHANDISI mkaguzi wa barabara na majengo Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Jordan Kapinga amejikuta akiwa katika wakati mgumu kufuatia Diwani wa kata ya Kitanda katika halmashauri hiyo, Zeno Mbunda kumtaka atolee maelezo juu ya kwa nini ujenzi wa madaraja na barabara umejengwa kwa kiwango cha chini ndani ya kata hiyo.

Hali hiyo ilifuatia baada ya Diwani huyo kuibua hoja hiyo, katika kikao maalum cha Wenyeviti na wazee wa vijiji vya kata hiyo kilichoketi kwenye ofisi za makao makuu ya kata ya Kitanda Aprili 2 mwaka huu, kwa lengo la kujadili maendeleo ya kata hiyo na kero mbalimbali zinazowakabili wananchi wake.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa.
Akizungumza katika kikao hicho, Mbunda alisema kuwa ujenzi wa barabara na madaraja matatu ambao umefanywa katika kata hiyo haujashirikisha wananchi na mkandarasi husika aliyepewa kazi hiyo hakuripoti kwa uongozi wa kata hiyo jambo ambalo linawafanya wajenge shaka.

Kampuni ya Ndapa Interprises Corporation Company Limited kutoka Dar es Salaam, alisema kuwa ndiyo iliyopewa kazi hiyo ambapo ujenzi wa barabara na madaraja hayo umefanyika kwa kiwango cha chini.

Sunday, April 3, 2016

MKUU WA WILAYA SONGEA AWATAKA WANANCHI WAKE KUSHIRIKI KWENYE ZOEZI LA UMEZAJI DAWA



Na Julius Konala,
Songea.

MKUU wa wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, Benson Mpesya amewaongoza baadhi ya wananchi wa Manispaa ya Songea katika zoezi la umezaji dawa kwa  ajili ya kinga na tiba ya magonjwa yaliyosahaulika na yale ambayo hayapewi kipaumbele (NTD) mjini hapa, ikiwemo ugonjwa wa matende.

Mpesya aliwaongoza wananchi hao katika uzinduzi uliofanyika kwenye Zahanati ya gereza la Mahabusu mjini Songea, kwa kumeza dawa hizo za kinga na tiba ya magonjwa ya usubi, mabusha, ngilimaji, trakoma, kichocho na minyoo ya tumbo.

Akiwahutubia wananchi, wanafunzi wa shule ya msingi Majimaji, walimu, askari magereza na watumishi wengine wa serikali waliojitokeza katika uzinduzi huo, aliwataka kuondoa hofu  na dhana potofu ya kwamba dawa hizo kwamba zina madhara na kuwa na busha sio heshima katika jamii, bali ni matatizo makubwa.

Mkuu huyo wa wilaya aliwahimiza wananchi wengine, kujitokeza kwa wingi katika kushiriki zoezi hilo linaloendelea mjini hapa pindi wataalamu watakapokuwa wanazungukia maeneo mbalimbali, ikiwemo majumbani, shuleni na katika vyuo.

Friday, April 1, 2016

WANANCHI TUNDURU WAPATIWA HUDUMA YA MATIBABU MACHO BURE

Na Steven Augustino,
Tunduru.

ZAIDI ya watu 5,000 waishio wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wamenufaika na huduma ya matibabu ya macho iliyotolewa wilayani humo kwa lengo la kuboresha afya zao, kutokana na wengi wao kusumbuliwa na matatizo mbalimbali ya magonjwa ya macho.

Shirika la Bilal Musilm Mission, ndilo lililotoa huduma hiyo ambapo Dkt. Ain Sharif ambaye ni mratibu wa huduma hiyo alisema kuwa ilikuwa ikitolewa hivi karibuni katika shule ya  sekondari, Frank Weston iliyopo mjini hapa.

Sharif alisema kuwa jumla ya madaktari 12 wakiwemo madaktari bingwa watano wa huduma za macho walishiriki katika zoezi hilo, ambalo lilidumu kwa muda wa siku nne.

KAMPUNI YA USAFIRISHAJI ABIRIA KUPUNGUZA ADHA YA USAFIRI RUVUMA



Na Julius Konala,   
Songea.

KAMPUNI ya usafirishaji abiria mikoani inayofahamika kwa jina maarufu la, Ilyana Company Limited ya jijini Dar es salaam, imepanua huduma zake kwa kufungua ofisi zake katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma na kufanya idadi ya makampuni ya usafirishaji mjini hapa, kuwa matatu.

Akizungumza na gazeti hili ofisini kwake mjini Songea, Mkurugenzi mtendaji wa kampuni hiyo, Khalfan Kigwenembe alisema kuwa lengo la kufungua ofisi hiyo ni kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wa Manispaa ya Songea na mkoa kwa ujumla kusafiri kwa bei nafuu ambayo imepangwa na serikali.

Kigwenembe ambaye pia ni Diwani wa kata ya Namtumbo mjini, wilayani Namtumbo mkoani hapa, kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) alisema kuwa mabasi ya kampuni hiyo yatafanya safari zake kuanzia Songea, Mbinga, Namtumbo hadi  Dar es Salaam.

JESHI LA POLISI LAMSAKA ASKARI WAKE ALIYETOROKA BAADA YA KUGHUSHI VYETI VYA MASOMO



Na Kassian Nyandindi,
Songea.

JESHI  la Polisi mkoani Ruvuma,  linamsaka askari wake wa kikosi cha kutuliza na kuzuia ghasia (FFU) mkoani humo mwenye namba F 5425 PC Emmanuel Nyagoli (35) kwa kosa la kutoroka jeshini, baada ya kukabiliwa na tuhuma ya kugushi vyeti vya masomo wakati alipokuwa akijiunga na jeshi hilo mwaka 2003.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, Kamanda wa Polisi mkoani humo Zubery Mwombeji alisema kuwa askari huyo alitoroka tangu Machi 16 mwaka huu, ilipobainika kwamba ametenda kosa hilo.

Mwombeji alisema kuwa PC Emmanuel, alikuwa ni askari wa kikosi cha kutuliza na kuzuia ghasia na kwamba alipogundulika kuwa ana tatizo hilo, ndipo alitoroka na kutokomea kusikojulikana.

WAKULIMA NYASA KUNUFAIKA NA KILIMO CHA ZAO LA KOKOA



Na Mwandishi wetu,
Nyasa.

WAKULIMA wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, wamehimizwa kulipokea zao jipya la kibiashara la Kokoa, kwa lengo la kuongeza kipato chao na kuimarisha uchumi wa wilaya hiyo kwa ujumla.

Wito huo umetolewa hivi karibuni na Mkuu wa wilaya Nyasa, Margaret Malenga alipokuwa akizindua kilimo cha zao hilo wilayani humo, ambao ulifanyika katika kijiji cha Songambele kata ya Kihagara.

Malenga alisema kuwa endapo watazingatia kilimo cha zao hilo, wananchi hao wataweza kuongeza vipato vyao na kuwafanya kuachana na tabia ya kutegemea shughuli za uvuvi pekee.