Thursday, April 21, 2016

SERIKALI KUBORESHA MITAMBO YA KURUSHIA MATANGAZO TBC




Na Kassian Nyandindi,
Songea.

IMEELEZWA kwamba serikali hapa nchini, itahakikisha inaboresha na kuimarisha mitambo yake ya kurusha matangazo katika mkoa wa Ruvuma, kupitia redio ya Taifa (TBC) kituo cha Songea ili kuifanya wilaya ya Nyasa na Namtumbo mkoani humo, ziweze kufikiwa na matangazo mbalimbali yanayorushwa na kituo hicho kwa ufanisi mzuri.

Kauli hiyo ya serikali inafuatia baada ya wananchi wa mkoa huo, kulalamika kwa muda mrefu kuwa redio hiyo ya taifa matangazo yake hayawafikii katika wilaya hizo na badala yake muda mwingi wanapofungua redio zao, husikia matangazo ya kutoka katika redio zilizopo nchi ya Malawi na Msumbiji.

Naibu Waziri wa habari, utamaduni, sanaa na michezo Anastazia Wambura alisema hayo hivi karibuni mjini hapa alipokuwa kwenye kikao maalum akizungumza na waandishi wa habari, pamoja na baadhi ya watumishi wa serikali mkoani humo.


Wambura alikuwa katika ziara yake ya kikazi ambapo alifafanua kuwa, wamejiwekea mikakati kwamba katika kipindi cha utawala wa serikali hii ya awamu ya tano lazima TBC iboreshe mitambo yake ili wananchi katika maeneo yote hapa nchini, hususan kwa yale yaliyopo pembezoni mwa nchi yanawafikia matangazo hayo ipasavyo.

Katika hatua nyingine, Waziri huyo alizitaka Halmashauri za wilaya kutenga bajeti ya kutosha katika sekta ya michezo, ambayo itaweza kuleta ufanisi mzuri kwa utekelezaji wa mambo mbali mbali.

“Licha ya kutenga bajeti naagiza pia katika michoro yenu ya mipango miji, hakikisheni mnatenga na viwanja vya michezo ambavyo wananchi watakuwa wanapata fursa ya kupumzika na kustarehe baada ya kufanya shughuli zao za kimaendeleo”, alisisitiza.

Awali akisoma taarifa fupi ya maendeleo ya michezo mkoani Ruvuma, Ofisa michezo wa mkoa huo Hassan Katuli alieleza kuwa kuna upungufu mkubwa wataalamu wa michezo na viwanja vyake.

Katuli aliongeza kwa kuiomba Wizara kuharakisha zoezi la kuajiri wataalamu hao kwenye halmashauri, ili waweze kutoa mafunzo kwa vijana mashuleni katika sekta hiyo ya michezo.

No comments: