Thursday, April 7, 2016

WAKAGUZI ELIMU NAMTUMBO WATAKIWA KUONGEZA KASI UTEKELEZAJI MAJUKUMU YA KAZI ZA KILA SIKU



Na Muhidin Amri,
Namtumbo.

WAKAGUZI wa elimu katika Halmashauri ya wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, wametakiwa kuongeza kasi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kazi ikiwemo kutembelea shule za msingi na sekondari mara kwa mara na kuwachukulia hatua kali za kisheria, walimu wazembe ambao wanasababisha wanafunzi kufanya vibaya katika mitihani yao ikiwa ni mkakati wa kuongeza kiwango cha ufaulu katika shule hizo.

Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa wilaya hiyo, Chande Nalicho alipokuwa akizungumza na wakaguzi wa idara ya elimu ofisini kwake mjini hapa, ambapo alikemea tabia ya wakaguzi kutumia muda mwingi kukaa ofisini na kuwaacha walimu peke yao wakitumia muda mwingi wa kazi kufanya shughuli zao binafsi.

Mkuu huyo wa wilaya alisema kwamba, hata tatizo la kushuka kwa ufaulu katika wilaya ya Namtumbo linachangiwa na idara ya ukaguzi  kwa kushindwa kutembelea shule hizo kwa kuwafuatilia utendaji kazi wa walimu hao.


Alisema kuwa baadhi ya wakaguzi ni kikwazo katika mkakati wa wilaya hiyo, kuinua kiwango kiwango cha taaluma kwani wanatumia  muda wao kufanya shughuli zao binafsi na kushindwa kufuatilia maendeleo ya walimu, ambao wanapata mishahara mikubwa mwishoni mwa mwezi huku baadhi yao wakionekana wana randa randa mitaani kwa sababu zisizokuwa za lazima.

Mkuu huyo wa wilaya alikiri kwamba, idara hiyo inakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo suala la kutokuwa na magari ya kutosha ambayo yangewezesha kufanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa, kwani serikali inaendelea kutafuta majawabu ya kukabiliana na kero hizo zilizopo katika idara hiyo ya ukaguzi.

Nalicho ambaye pia kitaaluma ni mwalimu, alibainisha kuwa ni aibu kuona wilaya hiyo bado inaendelea kushika nafasi ya mwisho kila mwaka  katika mitihani ya kitaifa, wakati kuna mazingira mazuri ya walimu kufanya kazi zao hasa baada ya serikali kupitia halmashauri ya wilaya, kuzifanyia ukarabati mkubwa barabara ambazo zinaunganisha eneo moja kwenda jingine.

No comments: