Friday, April 1, 2016

WAKULIMA NYASA KUNUFAIKA NA KILIMO CHA ZAO LA KOKOA



Na Mwandishi wetu,
Nyasa.

WAKULIMA wilayani Nyasa mkoa wa Ruvuma, wamehimizwa kulipokea zao jipya la kibiashara la Kokoa, kwa lengo la kuongeza kipato chao na kuimarisha uchumi wa wilaya hiyo kwa ujumla.

Wito huo umetolewa hivi karibuni na Mkuu wa wilaya Nyasa, Margaret Malenga alipokuwa akizindua kilimo cha zao hilo wilayani humo, ambao ulifanyika katika kijiji cha Songambele kata ya Kihagara.

Malenga alisema kuwa endapo watazingatia kilimo cha zao hilo, wananchi hao wataweza kuongeza vipato vyao na kuwafanya kuachana na tabia ya kutegemea shughuli za uvuvi pekee.


Licha ya kufanya uzinduzi  huo, Mkuu huyo wa wilaya ya Nyasa ameutaka uongozi wa vijiji kuhakikisha kwamba maeneo ya watu ambayo mpaka sasa hayajaendelezwa kwa shughuli za kibinadamu, yaendeshwe shughuli za kilimo cha zao la Kokoa.

Alisema kwamba, baadhi ya wananchi wa wilaya hiyo wamekumbatia maeneo makubwa yenye rutuba huku wengine wakihangaika maeneo ya kufanyia kazi, jambo ambalo linasababisha wakose  maeneo  ya kuendeshea shughuli za kiuchumi.

Maamuzi hayo yalifikia baada ya Mkuu huyo wa wilaya, kusomewa taarifa na wananchi hao kuwa wengi wao wanalipenda zao hilo lakini changamoto kubwa kwao, ni maeneo ya kufanyia shughuli za kilimo.

Naye kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Nyasa, Jabir Shekimweri alisema kuwa kwa upande wa wilaya hiyo wamejipanga kikamilifu kuhakikisha kwamba, wananchi wanakuwa na maeneo ya kufanyia kilimo cha zao hilo ambalo litakuwa mkombozi mkubwa kwa wananchi waishio mwambao mwa ziwa Nyasa.

Shekimweri alisema pia wanajipanga namna ya kuangalia uwezekano wa kuanzisha kilimo cha zao la Tangawizi, ambalo nalo halitumii mbolea wala madawa ambayo huwafanya wakulima wengi kukatishwa tamaa ya kuendesha shughuli za kilimo, kutokana na kukosa fedha za kununulia madawa au mbolea.

No comments: