Monday, April 25, 2016

NALICHO AWATAKA WATUMISHI KUWAHUDUMIA WANANCHI IPASAVYO MAMLAKA YA MJI WA LUSEWA



Na Muhidin Amri,
Namtumbo.

MKUU wa wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Chande Nalicho amezindua rasmi Mamlaka ya mji wa Lusewa na kumuagiza Mkurugenzi wa mamlaka pamoja na watumishi waliopelekwa kufanya kazi katika mamlaka hiyo, kuhamia haraka huko ili waweze kwenda kuwahudumia na  kutatua kero zinazowakabili wananchi.

Mkuu huyo wa wilaya ametoa agizo hilo alipokuwa akizungumza na mamia ya wananchi wa kata ya Lusewa, Msisima na Magazini katika sherehe  za uzinduzi wa mamlaka ya mji huo zilizofanyika katika  kijiji cha Lusewa wilayani hapa.

Chande Nalicho.
Amewaagiza watumishi hao, kwenda kufanya kazi usiku na mchana kwa kushirikiana na wananchi ili waweze kupata vigezo vya kuwa  halmashuri ya mji badala ya kuendelea kuwa mamlaka ya mji, jambo ambalo linaweza kuwakosesha baadhi ya vitu muhimu vinavyotolewa na Wizara husika ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).

Alisema kuwa, mamlaka ya mji wa Lusewa ndiyo kwanza inaanzishwa kwa lengo la serikali kusogeza huduma karibu na wananchi wake hivyo ni jukumu sasa la watumishi hao kuhakikisha kwamba, wanajitolea muda wao kufanya kazi  na kutatua changamoto  zinazowakabili wananchi hao ambao wana mategemeo makubwa baada ya serikali kuanzisha mamlaka hiyo.


Mamlaka ya mji wa Lusewa imeanzishwa kutoka halmashauri ya wilaya ya Namtumbo, kutokana na umbali uliopo  kutoka makao makuu ya wilaya mjini Namtumbo hadi kata ya Lusewa  ambapo ni umbali unaofikia zaidi ya kilometa 110 kwa lengo la kusogeza karibu huduma kwa wananchi ikiwa ni mkakati wa serikali ya awamu ya tano, kuhakikisha wananchi wanapata huduma za kijamii popote pale walipo ndani ya nchi.

Nalicho alimtaka Mkurugenzi wa Mamlaka hiyo, Astery Mwinuka pamoja na  timu yake kuhakikisha wanatekeleza majukumu husika ili waweze kutekeleza maagizo ya serikali ya kuwaletea maendeleo wananchi wake ikiwemo  agizo la Rais, Dkt. John Magufuli la kumaliza  tatizo la upungufu mkubwa wa madawati kwa shule za msingi  na sekondari.

Pia ameitaka halmashauri mama ya  wilaya ya Namtumbo, kuwa karibu na kuitazama mamlaka hiyo mpya kwa ukaribu zaidi na kuipatia kipaumbele ili watumishi  waliopelekwa huko, kwenda kuanzisha mamlaka hiyo waweze kutekeleza vyema majukumu yao ya kazi za kila siku.

Kuanzishwa kwa mamlaka ya mji huo kutachochea pia upatikanaji wa maendeleo ya wananchi kwa haraka, na kwamba serikali itaendelea kutoa ushirikiano kwa kuongeza wafanyakazi ambao ni wataalamu wa shughuli mbalimbali kama vile katika nyanja ya kilimo na ufugaji.

Pamoja na mambo mengine Nalicho, alisikitishwa na  kushuka kwa kiwango cha  elimu katika kata hiyo  kwa kushika nafasi ya mwisho kwenye matokeo ya kumaliza elimu ya msingi  mwaka uliopita 2015 ambapo kati ya shule 10 zilizofanya vibaya, katika mitihani hiyo shule tano zimetoka kata ya Lusewa.

No comments: