Monday, December 23, 2013

UJENZI WA BARABARA KIWANGO CHA LAMI SONGEA HADI MBINGA UTATA MTUPU

Na Kassian Nyandindi,
Songea.
 
UJENZI wa barabara kiwango cha lami kuanzia eneo la Likuyufusi pacha ya Peramiho wilaya ya Songea hadi Mbinga, umeanza kuzua malalamiko kutokana na barabara hiyo kuanza kuwekwa viraka kabla ya kukabidhiwa rasmi mikononi mwa serikali.
 
Barabara hiyo ambayo ni ya kilometa 78 inagharimu kiasi cha shilingi bilioni 79.8 na kutekelezwa chini ya mradi mkuu wa changamoto za milenia Tanzania (MCAT).
 
Fedha za ujenzi wa barabara hiyo ni miongoni mwa dola 698 za Kimarekani zilizotolewa nyakati za mwisho katika utawala wa Rais mstaafu George Bush, ikiwa ni sehemu ya msaada kwa ajili ya kujenga miradi mbalimbali ya kimaendeleo hapa nchini.
 
Malalamiko hayo yalitolewa kwa nyakati tofauti wakati mwandishi wa habari hizi alipokuwa akizungumza na wananchi wa Songea na Mbinga, ambapo walisema kuwa ni jambo la kushangaza kuona ujenzi wa barabara hiyo kabla haijakabidhiwa rasmi imeanza kuwekwa viraka baadhi ya maeneo.

Sunday, December 22, 2013

TAMCU TUNDURU WALIA NA TAKWIMU ZA KOROSHO



Na Steven Augustino,

Tunduru.

CHAMA kikuu cha ushirika Wakulima wa korosho wilaya ya Tunduru (TAMCU) mkoani Ruvuma, kimefanikiwa kukusanya tani  554 ambazo ni kidogo, kati ya tani 9115 zilizokadiriwa kuzalishwa katika msimu wa mwaka huu.

Hayo yalisemwa na Katibu mkuu wa chama hicho wilayani humo, Imani Kalembo akiwemo na Mwenyekiti wake Mahamudu Katomondo mbele ya waandishi wa habari, waliokuwa wakifanya mahojiano nao mjini hapa juu ya maendeleo ya uzalishaji wa zao hilo.

Viongozi hao walifafanua kwamba wamepata wakati mgumu kukusanya takwimu hizo za uzalishaji, kwa kile walichoeleza kuwa kutokana na wilaya hiyo kuwa na utaratibu mbovu uliotumika kununulia zao hilo katika msimu wa mwaka huu.

"Takwimu tulizowapeni ni zile ambazo tu zimetokana na manunuzi yaliyofanywa na TAMCU kupitia vyama 18 vya ushirika vya wakulima ambavyo vipo katika tarafa za Lukumbule, Namasakata, Nalasi, Matemanga, Mlingoti Nakapanya na Namtumbo ambako chama kilipeleka fedha kwa ajili ya ununuzi wa Korosho", alisema Kalembo.

MAHAKAMA KUTOA MAAMUZI JUU YA MAUZO MBAO ZILIZOKAMATWA KATIKA OPARESHENI TOKOMEZA UJANGILI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

MAHAKAMA ya wilaya Tunduru mkoani Ruvuma, imepanga kutoa maamuzi ya kuuza au kutouzwa kwa mbao 8,328 zenye thamani ya shilingi milioni 291.4 ambazo zilikamatwa kupitia “Oparesheni tokomeza ujangili”, iliyofanyika hivi karibuni kuanzia Oktoba hadi Desemba mwaka huu.

Hakimu mfawidhi wa Mahakama hiyo Ernest Mgongolo alisema hayo wakati alipokuwa akijibu, maombi yaliyotolewa na Mawakili waliokuwa wakiwakilisha upande wa serikali katika kesi tano zinazowakabili watuhumiwa saba ambao walinaswa wakati wa oparesheni hiyo wakiwa na na mbao hizo kinyume cha sheria.

Watuhumiwa hao ni wakazi wa Jijini Dar es Salaam na Mtwara  ambapo awali wakitoa maombi, Wanasheri  wa serikali  Mwahija Sembeni na Francis Aloyce waliiomba Mahakama kwa mamlaka iliyonayo kutumia kifungu cha sheria namba 352 kifungu kidogo (2) kinacho ambacho huruhusu kutoa kibali cha kuuzwa kwa kidhibiti chochote au mali ambayo ipo mbele ya mahakama na yenye kuweza kuharibika.

Wednesday, December 18, 2013

MKUU WA MKOA WA RUVUMA ALIA NA WAKUGURUGENZI WA HALMASHAURI KUWAPA KAZI WAKANDARASI WAZEMBE

Na Muhidin Amri,

Ruvuma.

SERIKALI mkoani Ruvuma imewaagiza Wakurugenzi wa Halmashauri  za wilaya katika mkoa huo, kutowapa tena zabuni Wakandarasi ambao ni wababaishaji, wazembe na wenye rekodi mbaya katika utendaji wa kazi zao, ili wasiweze kuisababishia serikali hasara ya kuingia gharama nyingine upya ya ujenzi wa miradi ya Wananchi.

Mkuu wa mkoa huo Said Mwambungu aliyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati akifungua kikao cha siku moja cha Wajumbe wa jumuiya ya serikali za mitaa(ALAT) kilichofanyika mjini Namtumbo mkoani humo, ambapo alitumia nafasi hiyo kupiga marufuku wakandarasi wasiokuwa na sifa kuomba na kufanya kazi katika mkoa wa Ruvuma kwani wamekuwa wakiurudisha nyuma maendeleo ya taifa letu kwa ujumla.

Mwambungu amesikitishwa na usimamizi mbovu wa fedha zinazotolewa na serikali wakati wa utekelezaji wa miradi mbalimbali, ambapo imebainika kuwa wakandarasi wengi wamekuwa na tabia ya wizi kwa kuingia mikataba hewa na halmashauri husika na wakishapata fedha hukimbia bila kukamilisha kazi walizoomba kufanya, tatizo ambalo alidai kuwa linachangiwa kwa kiasi fulani na baadhi ya watumishi hasa wakuu wa idara wasiokuwa waaminifu.

Alisema ni kosa kumpa kazi Mkandarasi mwenye rekodi mbaya huku akiwaonya Wakurugenzi na Wenyeviti wa Halmashauri  juu ya tabia ya kuwa na urafiki wa jirani na wakandarasi hao kwa kile alichoeleza kuwa kinatokana na tamaa ya fedha huku akisisitiza ni vema  kutoa kipaumbele kwa wakandarasi waaminifu  na wenye sifa ambao wanatimiza majukumu yao ya kazi kwa viwango vinavyotakiwa.

AURIC AIR YAJIVUNIA MAFANIKIO YAKE MKOANI RUVUMA

















Na Mwandishi wetu,
Songea.

WAKAZI wa mkoa wa Ruvuma wameombwa  kuunga mkono juhudi mbalimbali za wawekezaji wanaokwenda kuwekeza katika mkoa huo, badala ya kubeza kwani hali hiyo inaweza kuwakatisha tamaa wawekezaji hao na hatari ya kubaki watazamaji  na  mabingwa  wa kusifia maendeleo yaliyopo kwenye mikoa mingine.

Wito huo umetolewa mjini Songea na mfanyabiashara   Abbas Hemani wakati akizungumza na Mwandishi wetu, kuhusu fursa nyingi za uwekezaji zilizopo katika mkoa wa Ruvuma na kuongeza kuwa iwapo wakazi wa mkoa huo hawataunga mkono juhudi hizo basi mkoa huo,   utabaki na umasikini licha ya kuwepo kwa fursa na rasilimali nyingi.

Abbas ambaye  ni wakala wa shirika la ndege la AURIC AIR ambalo ndege zake hufanya safari kati ya Dar es slaam na Songea mkoani humo, amewaomba wakazi wa mkoa huo hususani wafanyabiahara kutumia usafiri wa ndege za kampu8ni hiyo, ili kumuunga mkono katika jitihada zake  za kutaka mkoa wa Ruvuma unakuwa miongoni mwa mikoa  yenye usafiri wa uhakika  na kusaidia kuleta maendeleo.

Alisema lengo la kuanzisha usafiri huo wa ndege ni  kuisaidia serikali katika kuboresha baadhi ya huduma ambazo yenyewe ilishajitoa, hivyo kutoa nafasi kwa wananchi wenye uwezo  waweze kuwekeza katika maeneo mbalimbali kwa lengo la kuwahudumia  wananchi.

Tuesday, December 17, 2013

KADA WA CHAMA CHA MAPINDUZI AFARIKI DUNIA KWA KUJINYONGA


















Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

KADA mmoja wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambaye ni mkazi wa kitongoji cha Lulambo wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, amekutwa akiwa amefariki dunia baada ya kujinyonga katika msitu uliopo jirani na kitongoji hicho.

Tukio hilo ambalo limetokea hivi karibuni, imethibitishwa kuwa Kada huyo ambaye ni Gisberth Haulle (45) alikuwa Mwenyekiti wa tawi la Ngamanga kupitia tiketi ya CCM ambalo lipo katika kitongoji hicho.  

Kwa mujibu wa maelezo ya Mwenyekiti wa kitongoji cha Lulambo, Gisberth Ndimbo alisema chanzo cha tukio hilo inadaiwa kuwa marehemu huyo alifikia uamuzi wa kujinyonga kutokana na ugomvi ambao ulidumu kwa muda mrefu katika familia yao.

TUNDURU WAWEKA MIKAKATI YA KUKABILIANA NA NJAA, SHERIA KUUNDWA KUWABANA WAZEMBE



Steven Augustino,
Tunduru.

SERIKALI wilayani Tunduru mkoani Ruvuma, imeweka mkakati wa kuhakikisha kuwa kila kaya inakuwa na chakula cha kutosha wilayani humo ili kuweza kuepukana na baa la njaa ambalo linaweza kutokea hapo baadaye.

Mikakati hiyo inaenda sambamba kwa kuanza kuwapeleka Mahakamani  watu wote, ambao hawatakuwa na mashamba ya kuzalisha mazao ya chakula katika msimu wa mvua wa mwaka huu na kuendelea.

Chande Nalicho ambaye ni Mkuu wa wilaya hiyo, ndiye aliyetangaza msimamo huo wa serikali na kuitaka jamii ya wanatunduru kuhakikisha suala hilo linatekelezwa mara moja.

Kadhalika serikali itafanya mzunguko kwa kupita kutoa elimu kwa wananchi wote wilayani Tunduru, na kwamba kesi za wavivu zichukuliwe hatua kwa walengwa wanaoshinda vijiweni ikiwemo kufungwa.

Msimamo huo ulitangazwa na mkuu huyo wa wilaya, wakati alipokuwa akizungumza katika mdahalo wa uzinduzi wa kampeni ya kutokomeza njaa duniani uliofanyika katika ukumbi wa Sky way, uliopo mjini hapa.

ABIRIA TUNDURU WALALAMIKIA KUNYANYASWA, SUMTRA YAOMBWA KUINGILIA KATI



Na Steven Augustino,
Tunduru.

WADAU na Abiria ambao hufanya safari zao kutoka wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, kwenda jijini Dar es Salaam wamelalamikia kutozwa nauli za mabegi jambo ambalo linasababisha usumbufu mkubwa kwao.

Sambamba na tukio hilo pia wasafiri hao walidai kuwa wamekuwa wakitukanwa na kutolewa lugha chafu na wafanyakazi wa mabasi ambayo hufanya safari katika ukanda huo wa kusini.

Kilio cha wasafiri hao kiliwasilishwa na Leonsi Kimario wakati akizungumza na maafisa wa Mamlaka ya udhibiti wa usafiri wa nchi kavu na majini (SUMATRA) katika kikao kilichofanyika ukumbi wa New Generation bar uliopo mjini hapa.
   
Kimario ambaye alionekana kuungwa mkono na wajumbe wengi waliohudhuria mkutano huo, alisema abiria hao wamekuwa wakitozwa fedha  kati ya shilingi 10,000 na 5,000 kama malipo ya nauli ya mabegi yao hali ambayo imekuwa ikiwakwaza abiria wengi ambao hufanya safari zao kutoka katika maeneo hayo.

Wednesday, December 11, 2013

VYAMA VYA KUWEKA NA KUKOPA VYATAKIWA KUTOA TAARIFA SAHIHI KWA WANACHAMA WAKE



Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

VIONGOZI wa Chama cha kuweka na kukopa (SACCOS) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wametakiwa kujenga ukweli na uwazi katika utendaji wa kazi zao za chama, na sio kutoa taarifa zisizo sahihi kwa wanachama ambazo baadaye zinaweza kusababisha migogoro isiyokuwa ya lazima.

Aidha wametakiwa kutuoa ushirikiano wa kutosha kwa Mamlaka husika ambayo inasimamia vyama vya ushirika, kufanya ukaguzi na kutoa hali halisi ya mwenendo wa chama kwa wanachama, ili waweze kuwa na uhakika wa usalama wa mali zao.

Rai hiyo ilitolewa na Ofisa elimu Msingi wilaya ya Mbinga, Mathias Mkali alipokuwa mgeni rasmi kwenye mkutano mkuu wa chama cha kuweka na kukopa cha Mbinga Kurugenzi SACCOS, uliofanyika kwenye ukumbi wa Jimbo la Mbinga uliopo mjini hapa.

Vilevile aliwashauri wanachama wa umoja huo, wahakikishe kuwa wanarejesha mikopo waliyokopa kwa wakati ili chama kiweze kusonga mbele.

“Napenda niwashauri, tujenge tabia ya kurejesha mikopo tunayokopa kwa wakati uliopangwa na tukifanya hivyo chama hiki kitakuwa na mzunguko mzuri kifedha, pia ili tuweze kufanikiwa jambo hili elimu ya ushirika itolewe kwa wanachama”, alisema Mkali.

Tuesday, December 10, 2013

NGAGA ALIA NA KATIBU WA CWT, AMSHUKIA ASEMA NI KIKWAZO CHA MAENDELEO YA ELIMU WILAYANI MBINGA

Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga akitoa msisitizo wake mbele ya Wadau wa elimu wa wilaya hiyo(Hawapo pichani) katika ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa, juu ya Katibu wa CWT wilaya humo kuwa ni kikwazo cha maendeleo ya elimu. 


Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MKUU wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga amemshukia Katibu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT) tawi la Mbinga Samwel Mhaiki, akidai kwamba ni kikwazo cha maendeleo ya elimu wilayani humo, kutokana na katibu huyo kupenda kuendesha migogoro na kuchonganisha walimu mashuleni.

Ngaga alisema hayo alipokuwa akizungumza na Wadau wa elimu, Kata ya Mbinga mjini juu ya kukuza maendeleo ya sekta ya elimu wilayani humo, katika hafla fupi iliyofanyika ukumbi wa Umati uliopo mjini hapa.

Alisema kuwa katibu huyo amekuwa kinara namba moja wa kupita mashuleni na kushinikiza walimu waache kufundisha (Wagome) hadi watakapolipwa madai yao, jambo ambalo alilieleza kuwa limekuwa likileta mgogoro usio na tija katika jamii.

Alieleza kwamba licha ya Mhaiki kuitwa mara nyingi ofisini kwake na kumtaka aache kuendeleza migogoro hiyo, anashangaa kumuona bado akiifanya.

Thursday, December 5, 2013

KUKOSEKANA KWA SHULE MAALUM YA WALEMAVU WILAYANI MBINGA KUNASABABISHA WALEMAVU KUKOSA HAKI ZAO ZA MSINGI

Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Senyi Ngaga (upande wa kulia) akizungumza na wananchi na watu wenye ulemavu katika kijiji cha Luhagara kata ya Litumbandyosi wilayani humo, katika maadhimisho ya sherehe za siku ya walemavu.

Kutoka kushoto Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Mbinga, Allanus Ngahy, katikati ni Diwani wa kata ya Litumbandyosi James Yaparama na upande wa kulia ni Mkuu wa wilaya hiyo Ngaga, akiweka sahihi katika kitabu cha wageni mara baada ya kuwasili katika uwanja wa maadhimisho ya sherehe hizo kijiji cha Luhagara. (Picha zote na Kassian Nyandindi)

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa kukosekana kwa shule maalum kwa watu wenye ulemavu wa aina mbalimbali wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, kunasababisha watu hao kukosa haki zao za msingi za kupata elimu, ambayo ingelifanya kundi hilo, kuweza kuondokana na maadui wawili ujinga na umasikini.

Kutokana na ukosefu huo baadhi yao kutoka katika familia zenye uwezo mkubwa hulazimika kwenda kusoma mikoa mingine ambayo ipo mbali kwa kutumia gharama kubwa, hivyo serikali imeombwa kunusuru hali hiyo kwa kujenga shule ya watu wenye ulemavu wilayani humo.

Hayo yalisemwa na Katibu mkuu wa Chama Cha Walemavu (CHAWATA) wilayani Mbinga Kassian Nyandindi, wakati alipokuwa akisoma risala ya watu wenye ulemavu hivi karibuni mbele ya mgeni rasmi Mkuu wa wilaya hiyo Senyi Ngaga, katika siku ya maadhimisho ya sherehe za watu hao zilizofanyika kijiji cha Luhagara kata ya Litumbandyosi wilayani humo.

Wakati akisoma taarifa hiyo alisema bado kundi hilo linakabiliwa na tatizo la miundo mbinu ya majengo mbalimbali kutokuwa rafiki kwao na gharama kubwa ya viungo bandia kuwa bei ghali na kufikia hatua wengi wao hushindwa kuvinunua.

Vilevile watu wenye ulemavu wilayani humo wamelalamikia kukosa uwakilishi kuanzia ngazi ya mtaa, vitongoji mpaka kwenye vikao vya Madiwani (Full Council) ili uwakilishi huo uweze kutetea haki zao za msingi.

Sunday, December 1, 2013

MBINGA WATAKIWA KUKABILIANA NA ATHARI ZA MABADILIKO YA TABIA NCHI

Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.
 
VIONGOZI kwa kushirikiana na Wananchi wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wametakiwa kuhakikisha kwamba wanakabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi, na sio kusubiri nguvu au misaada kutoka nje jambo ambalo ni hatari kwa kizazi cha sasa na kijacho.
 
Rai hiyo ilitolewa na Wananchi wa wilaya hiyo walipokuwa wakitoa maoni yao kwenye mdahalo uliohusu athari za mabadiliko ya tabia nchi, ambao ulikuwa ukiendeshwa na shirika lisilo la kiserikali (MBINGONET) lililopo wilayani humo, uliofanyika kwenye ukumbi wa Jumba la maendeleo uliopo mjini hapa.
 
Walisema kuwa katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi, viongozi kwa kushirikiana na jamii lazima wabuni ufumbuzi wao wenyewe na sio kungojea misaada kutoka nje, wakati wilaya hiyo na taifa kwa ujumla linazidi kuangamia siku hadi siku.
 
Mkazi mmoja wa Mbinga mjini Godfrey Ngonyani alieleza kuwa imefika wakati sasa, elimu itolewe katika jamii juu ya kunusuru hali hiyo isiweze kuendelea na Viongozi hapa nchini wanapaswa kushikilia msimamo wa kuhakikisha kuwa athari hizo tunakabiliana nalo, na kama haitafanyika hivyo ni wazi kuwa tunatengeneza mazingira mabaya ambayo ni hatari hapo baadaye.

Sunday, November 24, 2013

WAJASIRIAMALI WAMPA PONGEZI DIWANI WAO



Na Steven Augustino,
Tunduru.

KIKUNDI cha akina mama wajasiriamali wa tawi la Majengo B wilayani  Tunduru mkoa wa Ruvuma, kimempongeza Diwani wa kata ya Majengo  Athuman Nkinde kwa moyo wake wa kujitoa na kufanikisha utekelezaji wa miradi mbalimbali wilayani humo, ambayo aliahidi wakati wa kuwania nafasi hiyo mwaka
2010.

Mwenyekiti wa tawi la Majengo B la Chama cha Mapinduzi (CCM) Fatuma Mtesa alisema hayo wakati akisoma taarifa ya utekelezaji wa Mafunzo ya uzalishaji mali, kwa wanakikundi hao katika hafla fupi iliyofanyika viwanja vya ofisi za CCM katani humo.

Mtesa alisema kuwa katika mafunzo hayo ya siku 10 jumla ya akina mama wajasiriamali 46 walishiriki, ambapo yalitolewa chini ya ufadhili wa diwani Nkinde.

Tuesday, November 19, 2013

TUNDURU YAPONGEZWA KWA KUANZA UJENZI WA MAABARA


Na Steven Augustino,
Tunduru.

KATIBU wa Siasa na ushirikiano wa kimataifa wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Dkt. Asha Rozi Migiro ameipongeza Halmashauri ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, kwa kuanza kwa kasi utekelezaji wa ujenzi wa vyumba vya maabara katika shule mbalimbali za sekondari wilayani humo, ikiwa ni juhudi ya serikali ya awamu ya nne kuinua taaluma kwa wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi.

Dkt. Migiro ambaye amefuatana na Katibu mkuu wa CCM taifa   Abrahaman Kinana alisema hayo wakati alipokuwa katika shule ya sekondari ya kutwa, Mgomba sekondari iliyopo kata ya Majengo wilayani humo.

Alisema huo ni mpango ambao umewekwa na serikali katika kuhakikisha wilaya husika vyumba vya maabara vinajengwa katika shule ili kuinua kiwango cha taaluma katika masomo ya sayansi kwa wanafunzi.

Ujenzi huo unaenda sambamba na nyumba za walimu, nayo imekuwa ni kero kubwa hususani kwa shule zilizopo vijijini.

Awali akisoma taarifa ya ujenzi wa maabara ya shule hiyo kwa niaba ya Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Tunduru Bw. Robart Nehatta, ambapo mkuu wa shule hiyo Elis Banda alimweleza Dkt. Migiro na msafara wake kuwa mradi wa ujenzi huo unatekelezwa kupitia  mpango wa Maendeleo ya Elimu ya Sekondari(MMES II) katika mwaka wa fedha 2012/2013.   

Monday, November 18, 2013

WAANDISHI WA HABARI WANOLEWA MJINI DODOMA, WASISITIZWA KUZINGATIA MAADILI YA KAZI ZAO

Mratibu wa mafunzo ya kuandika habari na kuziweka kwenye mtandao Japhet Sanga (kushoto) kutoka TMF, akisisitiza jambo wakati alipokuwa akizungumza na Waandishi wa habari ambao wanashiriki mafunzo hayo ya siku tano mjini Dodoma.

Mwandishi wa habari Franci's Godwin (aliyesimama) kutoka mkoani Iringa, akichangia hoja katika mafunzo ya siku tano ya uandishi bora wa habari na kuziweka kwenye mitandao, yanayoendelea kufanyika mjini Dodoma. (Picha zote na Kassian Nyandindi)

Na Kassian Nyandindi,
Aliyekuwa Dodoma.

WAANDISHI wa habari nchini wamesisitizwa kuendelea kuzingatia misingi ya taaluma yao, ili kuweza kulinda heshima katika tasnia ya habari na taifa kwa ujumla.


Wito huo ulitolewa leo na Mratibu wa mafunzo ya habari za mitandao(Online Journalism) Japhet Sanga, kutoka shirika la Tanzania Media Fund (TMF) Jijini Dar es Salaam, alipokuwa akizungumza na baadhi ya Waandishi wa habari mjini Dodoma.


Sanga alikuwa akizungumza na Waandishi hao, ambao wanashiriki mafunzo ya siku tano ya uandishi bora wa habari za uchunguzi na kuziweka mitandaoni, yanayofanyika kwenye ukumbi wa New Dodoma hotel uliopo mjini hapa.


Waandishi hao ni wale ambao wanashughulika katika majukumu ya kazi zao za kila siku, katika kuandika habari na kuziweka kwenye mitandao yao.


“We want to have Quality blogger's…………… tunahitaji mtu ambaye anazingatia maadili ya vyombo vya habari, hatuhitaji mtu anayeandika vitu vyenye kulenga uchochezi”, alisema.



Naye Mkufunzi mkuu wa mafunzo hayo Beda Msimbe alisema, katika zama hizi Waandishi wengi wamekuwa wakizembea kuzingatia maadili ya kazi zao, na hivyo kujikuta jamii kukosa imani nao.  

KATIBU MKUU WA CCM TAIFA AKUMBANA NA KERO YA KOROSHO TUNDURU, WATENDAJI WIZARA YA KILIMO WATILIWA SHAKA

Na Steven Augustino,
Tunduru.

KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Taifa Abrahaman Kinana ambaye anaendelea na ziara yake wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, amekutana na kero inayoendelea kulitesa Soko la korosho huku wananchi wa wilaya hiyo wakilalamikia kwamba tatizo hilo kutokana na kudumu kwa muda mrefu, linawafanya wakose imani na Wizara ya kilimo chakula na ushirika ambayo ilipaswa kusimamia.


Kufuatia hali hiyo Kinana naye ilimlazimu kutilia shaka utendaji wa Wizara hiyo na kuahidi kuwa litafanyiwa utekelezaji wa haraka ili kuondoa kero hiyo iliyopo sasa. 


Kilio hicho cha Wakulima wa korosho wilayani Tunduru kilijitokeza katika vijiji vya Lukumbo, Munjaku, Mchoteka, Nalasi na Mtina vilivyopo katika Jimbo la Tunduru Kusini wilayani humo.  

Wednesday, November 13, 2013

UHARIBIFU WA MAZINGIRA NA UCHOMAJI MOTO MISITU WATISHIA KUTOWEKA KWA VYANZO VYA MAJI RUVUMA

Mazingira yanavyoharibiwa kama hivi, ni hatari kwa maisha ya binadamu na viumbe hai. 

Na Kassian Nyandindi,
Songea.

WANANCHI waishio mkoani Ruvuma, wameshauriwa kuwa na tabia ya kutunza mazingira pamoja na vyanzo vya maji na kuvifanya kuwa endelevu, kwa  faida ya vizazi vijavyo na hata kwa matumizi yao wenyewe ili waweze kuwa na maisha endelevu.

Hivi sasa kumekuwa na kasi kubwa ya uharibifu wa vyanzo hivyo kunakosababishwa na shughuli za kibinadamu kama vile kilimo na ufugaji hali ambayo inatishia kutoweka kwa uoto wa asili.

Wito huo ulitolewa na mshindi wa tuzo ya mazingira ambaye pia ni mwanaharakati  wa msuala ya mazingira na uhifadhi wa vyanzo vya maji mkoani Ruvuma, Menas Andoya alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini Songea, kuhusiana na kasi  kubwa ya uchomaji  moto misitu na uchafuzi wa vyanzo vya maji ambao umeshamiri mkoani humo.

Alisema viongozi kuanzia ngazi ya vitongoji, vijiji   na hata kata wanapaswa kusimamia kikamilifu suala la utunzaji wa mazingira pamoja na vyanzo vya maji kutokana na wao ndiyo wanaoishi na wananchi.

WAZAZI WILAYANI TUNDURU WATAKIWA KUWAJENGEA WATOTO WAO MALEZI BORA

Na Mwandishi wetu,
Tunduru.

WAZAZI na Walezi wilayani Tunduru mkoa wa Ruvuma, wameaswa kushirikiana na serikali kusimamia na kufuatilia   kwa karibu mienendo na maendeleo ya watoto wao hasa wa kike, ikiwa ni juhudi ya kuhakikisha  kuwa  watoto hao wanafanya  vizuri katika masomo yao na kujiletea maendeleo yao.

Ofisa mtendaji wa kata ya Mhuwesi  Shijabu Ngoronje alisema hayo wakati alipokuwa akizungumza kwenye mkutano wa Wadau wa elimu uliofanyika katika Kijiji cha Mhuwesi, ukiwa ni mwendelezo wa juhudi za mradi  wa usimamizi na utetezi wa haki ya mtoto wa kike kupata elimu .

Akifafanua taarifa hiyo Ngoronje alisema, ili kufanikisha adhima hiyo serikali imejipanga kutoa elimu kwa kuwaomba wazazi na walezi kujitoa kuchangia chakula  cha mchana kama kivutio kwa watoto wao na kuwafanya wapende masomo.

Saturday, November 9, 2013

WALEMAVU WA MKOA WA RUVUMA WALIA NA SERIKALI, WASEMA UNYANYAPAA UMEKITHIRI KATIKA NYANJA MBALIMBALI

Mgeni rasmi Anton Nginga ambaye ni Afisa maendeleo ya jamii mkoani Ruvuma, akihutubia katika mkutano wa uchaguzi wa viongozi CHAWATA wa mkoa huo, kwenye ukumbi wa halmashauri ya wilaya ya Songea uliopo mjini hapa.


Baadhi ya Wajumbe ambao ni Watu wenye ulemavu, wakimsikiliza kwa makini mgeni rasmi(hayupo pichani) wakati alipokuwa akihutubia katika  mkutano wao.

Mwenyekiti wa CHAWATA Songea mjini, ambaye amesimama Kassim Mgwali akisisitiza jambo kwa kuitaka serikali, izingatie uwepo wa mahitaji muhimu kwa watu wenye ulemavu.           (Picha zote na Kassian Nyandindi)





Na Kassian Nyandindi,

Songea.

IMEBAINISHWA kuwa changamoto kubwa inayoathiri maendeleo ya watu wenye Ulemavu mkoani Ruvuma, ni unyanyapaa uliokithiri katika nyanja mbalimbali, ikiwemo mazingira magumu ya kupata elimu na kuwezeshwa kiuchumi kuweza kupata nafasi ya kuingia katika vyombo vya maamuzi.

Aidha uongozi wa halmashauri za mkoa huo umetupiwa lawama kwamba umekuwa ukiwatenga kundi la watu hao, pale wanapohitaji msaada au ufafanuzi wa mambo mbalimbali.

Kufuatia hali hiyo, serikali imeombwa kuingilia kati na kuhakikisha tatizo hilo linafanyiwa kazi ikiwemo ushirikishwaji kwa watu wenye ulemavu katika kupanga bajeti ya maendeleo kwa ngazi mbalimbali, uwe unatekelezwa ipasavyo.

Hayo yalibainishwa na Wajumbe wa mkutano Mkuu wa uchaguzi wa viongozi wa ngazi ya mkoa wa Ruvuma, uliofanyika leo kwenye ukumbi wa Halmashauri ya wilaya ya Songea uliopo mjini hapa na kuhudhuriwa na mgeni rasmi afisa maendeleo ya jamii wa mkoa huo, Anton Nginga.

Thursday, November 7, 2013

MADIWANI TUNDURU WALIA NA SEHEMU YA KUJIFUNGULIA AKINA MAMA WAJAWAZITO, WENGINE WAJIFUNGULIA SAKAFUNI

Na Steven Augustino,
Tunduru.

MADIWANI wa viti maalumu katika halmashauri ya wilaya ya Tunduru mkoani Ruvuma, wameomba kuridhia na kuruhusu kufunguliwa kwa wodi mpya iliyojengwa katika hospitali ya Wilaya hiyo kwa ajili ya kujifungulia akina Mama wajawazito, wanaoenda kupata huduma hiyo muhimu hospitalini hapo kwa kuanza. 


Kilio hicho kilianza kuwasilishwa na Diwani wa Viti maalumu wa Tarafa ya Matemanga Stawa Omari huku akiungwa mkono na Swema Kalipungu wa Tarafa ya Mlingoti na Alus Yunus wa Nalasi walisema hivi sasa hali ya akina mama hao ni tete kutokana na wengine hujifungua wakiwa wamelala chini sakafuni.
  

Madiwani hao walisema kuna wakati akina mama wajawazito wamekuwa wakijifungulia katika chumba cha kupokelewa wagonjwa. 


Walidai kuwa imefikia hatua wakati mwingine hata wagonjwa wanaoenda kupata matibabu hospitalini hapo hupata shida pale wanapohitaji huduma za vipimo choo ndogo na kubwa ambapo hulazimika kwenda vyoo vya nyumba za jirani kutokana na miundo mbinu ya hospitali hiyo kutotosheleza.


Walisema kila wanapohitaji maelezo kwa wataalamu husika wamekuwa wakiambiwa kuwa tatizo linalo wa kwaza ni kutokana na wodi hizo mpya kutokamilika miundo mbinu husika.

  
Aidha madiwani hao waliendelea kuiomba halmashauri kutenga eneo jingine la kujifungulia akina mama, ambao wanaenda kujifungua katika hospitali hiyo kujisitiri mahali pa zuri. 

Sunday, November 3, 2013

BARAZA LA MADIWANI WILAYANI MBINGA LAMSHUSHIA RUNGU AFISA ELIMU TAALUMA, WAMKATAA WATAKA AREJESHWE KWA KATIBU MKUU WIZARA YA ELIMU NA MAFUNZO YA UFUNDI

Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Shukuru Kawambwa.














Na Kassian Nyandindi,
Ruvuma.


HATIMAYE Baraza la Madiwani katika Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, limefanya maamuzi mazito ya kumkataa Afisa Elimu Taaluma wa wilaya hiyo Rashid Pilly, na kumwagiza Mkurugenzi na Mwenyekiti wake wa halmashauri hiyo kumwondoa haraka afisa huyo na kumrejesha kwa Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya ufundi.


Pilly analalamikiwa kwa muda mrefu kutokana na kile kinachoelezwa kuwa ni kikwazo katika utendaji kazi wa idara hiyo, amekuwa akitumia muda mwingi badala ya kufanya kazi husika, yeye amekuwa akiandika barua zenye kuzua migogoro, kuchafuana na kugombanisha wafanyakazi wenzake na afisa elimu wa wilaya hiyo Mathias Mkali.


Hatua ya Madiwani hao kumkataa Afisa elimu taaluma wa wilaya hiyo, imejitokeza hivi karibuni katika kikao cha Baraza hilo kilichoketi kwenye ukumbi wa Jumba la Maendeleo, uliopo mjini hapa.


Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Madiwani wilayani Mbinga ambaye alikuwa akiendesha kikao hicho, Winfrid Kapinga alisema wamekasirishwa na tuhuma hizo na kubaini kwa muda mrefu kuwa vitendo hivyo vinavyofanywa na Pilly, vinaweza kudumaza mikakati iliyowekwa ya kimaendeleo katika kukuza elimu wilayani humo.


Kapinga alifafanua kuwa Afisa elimu msingi wa wilaya hiyo Bw. Mkali alipohamia wilayani Mbinga mwaka 2011 aliweza kuinua kiwango cha taaluma kutoka asilimia 40 hadi kufikia asilimia 53.6 na kuifanya halmashauri hiyo kushika nafasi ya pili mkoani Ruvuma, kati ya wilaya tano zilizopo mkoani humo.


“Tumeamua kumkataa huyu mtu kutokana na matendo yake, ni vyema arejeshwe kwenye mamlaka yake ya uteuzi ili kuondoa migogoro hii ambayo imekuwa kero kubwa katika idara hii ya elimu”, alisema Kapinga.


Mwenyekiti huyo aliongeza kuwa Mkali alipohamia wilayani Mbinga, aliweza kukabiliana na tatizo la watoto 1,744 wasiojua kusoma, kuandika na kuhesabu (KKK) kwa kuweka mikakati madhubuti ambayo ilishirikisha walimu wote mashuleni na kuifanya wilaya hiyo iweze kusonga mbele.


Pamoja na mambo mengine, Diwani wa kata ya Litembo Altho Hyera alipozungumza na Waandishi wa habari nje ya ukumbi wa mikutano, alisema hatua iliyochukuliwa na baraza hilo inapaswa kuungwa mkono huku akieleza kuwa Pilly amekuwa akiendeleza migogoro ya kuandika barua hizo, kwa kushirikiana na Katibu wa Chama Cha Walimu Tanzania (CWT) tawi la Mbinga Samwel Mhaiki na kuufanya uongozi wa wilaya hiyo kushindwa kufanya kazi zake za kimaendeleo, kutokana na muda mwingi kuutumia kujibu tuhuma wanazoziandika katika barua hizo na kuzipeleka ngazi ya juu.


“Huyu Pilly muda mwingi yeye badala ya kufanya kazi anafikiria kuandika mabarua ya kuchafuana yasiyo na faida kwetu, kamati husika iliundwa kufuatilia jambo hili na imebaini kuwa hakuna ukweli wa mambo anayo andika na sisi tumeona hatufai………..aondoke”, alisema Hyera.


Naye Mwenyekiti wa Kamati ya elimu, afya na maji wilayani Mbinga ambaye ni Diwani wa kata ya Litumbandyosi, James Yaparama alieleza kuwa wamechoshwa na mambo yaliyofanywa na  afisa elimu taaluma wa wilaya hiyo hivyo hawaoni sababu ya kuendelea kukaa na mtu ambaye muda mwingi amekuwa akileta matatizo katika wilaya yao ambayo yakiendelea kufumbiwa macho huenda maendeleo katika sekta ya elimu yakarudi nyuma.


Hata hivyo alipoulizwa Pilly alieleza kuwa yeye tuhuma hizo anazisikia tu watu wakizungumza mitaani na bado hajapata barua rasmi ya kumuhamisha katika kituo chake cha kazi kutoka kwa mwajiri wake, huku akiongeza uamuzi uliochukuliwa na baraza hilo hautambui na ataendelea na kazi kama kawaida ambapo vilevile alipotafutwa kwa njia ya simu Katibu wa CWT tawi la Mbinga, Samwel Mhaiki ili aweze kujibia suala la kuhusishwa na tuhuma hizo, hakuweza kupatikana na simu yake ilikuwa imefungwa kwa muda mrefu.

Tuesday, October 29, 2013

KERO YA UPATIKANAJI WA MAJI MJI WA SONGEA YAZIDI KUKERA WANANCHI

Mji wa Songea.























Na Muhidin Amri,
Songea.


WAKAZI wa Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, wametakiwa kutumia maji kwa uangalifu kutokana na huduma hiyo kutolewa kwa mgao ambao unasababishwa na  ukosefu wa umeme wa uhakika katika Manispaa  hiyo, kutokana na mashine za kusukuma maji kwenda kwenye makazi ya watu kushindwa kufanya  kazi yake ipasavyo.


Kauli hiyo imetolewa hivi karibuni, na afisa uhusiano wa Mamlaka ya maji safi na mazingira (SOUWASA) Neema  Chacha, alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Songea.


Chacha alisema kufuatia tatizo  la umeme unaotolewa kwa mgao mjini Songea, mamlaka hiyo  hulazimika kutoa maji  kwa mgao pele umeme unapowaka na wao ndipo waweze kuwasha mashine zao.

UKOMBOZI SACCOS JIMBO LA SONGEA YAJIVUNIA MAFANIKIO YAKE

Rais Jakaya Kikwete.























Na Dustan Ndunguru,
Songea.

CHAMA cha akiba na mikopo cha Ukombozi Jimbo la Songea (SACCOS) kilichopo katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, kimekopesha wanachama wake shilingi bilioni 2.2 katika kipindi cha miaka saba tangu kuanzishwa kwake.


Meneja wa SACCOS hiyo Rainer Ngatunga alisema kuwa fedha hizo zilizokopeshwa ni kutokana na akiba za wanachama, na sasa chama kina wanachama 1104.


Ngatunga alisema kuwa kati ya fedha hizo shilingi bilioni 1.6 zimekwisha rejeshwa huku akiwataka wanachama wake, watumie fedha wanazokopeshwa kwa malengo yaliyokusudiwa sambamba na kujenga tabia ya kurejesha mikopo wanayokopa kwa wakati.