Monday, July 31, 2017

BUNDI ATUA KWA AFISA MISITU HALMASHAURI MJI WA MBINGA DC AAPA KUCHUKUA HATUA KALI ZA KISHERIA

Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, Cosmas Nshenye wa pili kutoka kushoto akiwa ameshiriki katika kikao cha baraza hilo la Madiwani wa Halmashauri ya mji wa Mbinga ambapo wa kwanza kutoka kushoto ni Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo Robert Mageni na watatu kutoka upande huo wa kushoto ni Mwenyekiti wa halmashauri hiyo Ndunguru Kipwele. Upande wa kulia wa kwanza ni Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini, Sixtus Mapunda na wa pili yake ni diwani wa kata ya Luwaita Aureus Ndunguru ambaye alikuwa akikaimu kwa muda nafasi ya umakamu Mwenyekiti wa halmashauri hiyo.
Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

KUFUATIA kudaiwa kuwepo kwa ubadhirifu wa fedha za mapato yatokanayo na uvunaji wa msitu wa Mbambi uliopo katika kata ya Matarawe Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Mkuu wa wilaya ya Mbinga mkoani humo Cosmas Nshenye naye ameapa akisema kuwa Ofisi yake itachukua hatua kali za kisheria ikiwemo kulifanyia uchunguzi jambo hilo na kulifikisha kwenye vyombo husika vya kisheria.

Nshenye alisema yeye binafsi hakubaliani na hali hiyo kwani dhahiri inaonesha kuwa kumekuwa na vitendo viovu ambavyo vinatia shaka juu ya mwenendo wa uvunaji wa msitu huo kwani ukiukwaji mkubwa wa sheria na taratibu husika bila kufuata miongozo ya serikali umefanyika.

Mkuu huyo wa wilaya ya Mbinga alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza kwenye kikao cha baraza la Madiwani wa halmashauri ya mji huo kilichofanyika mjini hapa, baada ya kuibuka hoja ya kumtuhumu Afisa misitu wa mji huo David Hyera kuwa anadaiwa kwa namna moja au nyingine kushiriki katika ubadhirifu wa mapato hayo.

MFUKO WA TAIFA BIMA YA AFYA WAZINDUA TOTO KADI

Waziri wa afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto, Ummy Mwalimu akikata utepe ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa bima ya afya ya mtoto "Toto Kadi" leo katika viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dar es Salaam.
Na Mwandishi wetu,

UMMY Mwalimu ambaye ni Waziri wa afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto amesema kwamba kiu yake kubwa katika sekta ya afya anataka kuona kila Mtanzania katika maisha yake anamiliki bima ya afya.

Hayo yalisemwa leo na Waziri huyo wakati alipokuwa kwenye uzinduzi wa kadi ya bima ya afya katika viwanja vya Mnazi mmoja Jijini Dara es Salaam kwa mtoto yenye jina maarufu “Toto Kadi” ambapo alisema kuwa ili taifa liweze kuwa na maendeleo itatokana na kuwa na misingi bora ya afya.

Alifafanua kuwa katika kuhakikisha hilo linafanikiwa ni lazima pia kuwa na msingi mzuri wenye watoto wanaopata huduma bora za afya.

KAMATI MAALUM YA MAKINIKIA YAANZA MAZUNGUMZO RASMI NA BARRICK GOLD CORPORATION


Sunday, July 30, 2017

AFISA MISITU HALMASHAURI MJI WA MBINGA ASIMAMISHWA KAZI KUFUATIA SAKATA LA MGOGORO WA FEDHA ZA MAPATO YATOKANAYO NA UVUNAJI MSITU WA MBAMBI

Hii ni moja kati ya sehemu ya msitu wa Mbambi uliopo katika kata ya Matarawe halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma ambao miti yake imevunwa na kuleta mgogoro mkubwa kati ya Madiwani na baadhi ya Watendaji wa halmashauri hiyo kutokana na fedha za mapato yatokanayo na mavuno ya mbao za msitu huo yakidaiwa kufanyiwa ubadhirifu.   
Wapasuaji mbao walinaswa na kamera yetu wakiendelea juzi na kazi ya upasuaji mbao katika msitu huo kabla ya mgogoro kutokea kati ya Madiwani na baadhi ya Watendaji wa halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, juu ya mapato baada ya mauzo ya mbao hizo ambapo walipohojiwa na mwandishi wetu walithibitisha kufanya kazi hiyo kwa muda mrefu mpaka sasa bila kulipwa ujira wao.
Diwani wa Kata ya Mpepai Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Benedict Ngwenya (aliyesimama) juzi akichangia hoja katika kikao cha baraza la Madiwani hao, juu ya umuhimu wa kuchukua hatua dhidi ya ubadhirifu wa fedha za msitu wa Mbambi uliopo katika halmashauri hiyo. 
Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

SAKATA la Mgogoro wa fedha za mapato yatokanayo na uvunaji wa msitu wa Mbambi uliopo katika kata ya Matarawe Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, limechukua sura mpya kufuatia baraza la Madiwani wa halmashauri hiyo kumsimamisha kazi Afisa misitu wa mji huo, David Hyera ambaye anadaiwa kwa namna moja au nyingine kushiriki katika ubadhirifu wa mapato hayo.

Aidha kusimamishwa kazi kwa afisa huyo ni kwa ajili ya kupisha uchunguzi baada ya Madiwani hao kukubaliana kwamba iundwe Kamati maalumu ya kuchunguza suala hilo ili kuweza kupata ukweli zaidi wa jambo hilo na hatimaye hatua za kisheria zichukuliwe kwa wahusika watakaopatikana wameshiriki wizi huo.

Maamuzi hayo yalifikiwa juzi kwenye kikao cha robo ya nne cha baraza lao kilichoketi kwenye ukumbi wa Jumba la Maendeleo uliopo mjini hapa, kikiongozwa na Mwenyekiti wake Ndunguru Kipwele ambapo walieleza kuwa makisio ya awali baada ya kufanyika upembuzi yakinifu na mtaalamu huyo wa misitu na kuwasilishwa katika kikao cha baraza kilichoketi Oktoba 12 mwaka jana, yalikuwa zipatikane zaidi ya shilingi milioni 325 ambazo ni baada ya uvunaji huo kufanyika lakini wanashangaa kuelezwa kwamba zimepatikana shilingi milioni 196.

Akichangia hoja katika kikao hicho diwani wa kata ya Mpepai, Benedict Ngwenya alisema kuwa shughuli za uvunaji wa msitu wa Mbambi kabla hazijaanza kufanyika kupitia vikao husika walikubaliana kwamba Kamati husika ya mipango miji na mazingira ilibidi iende kwenye eneo la msitu huo na kujiridhisha lakini kamati hiyo ilizuiwa isiende huko kwa ajili ya kuukagua msitu huo na badala yake anadaiwa kwenda Mkurugenzi mtendaji, Robert Mageni na wataalamu wake.

TANZANIA NA MSUMBIJI WATAKIWA KUPAMBANA NA TATIZO LA UMASKINI

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Dokta Binilith Mahenge upande wa kushoto akiwa na Gavana wa Jimbo la Cabo Delgado nchini Msumbuji Celmira Da Silva upande wa kulia, juzi wakitiliana saini makubaliano yaliyofikiwa katika mkutano wa pamoja wa ujirani mwema na uhusiano kati ya mikoa ya Mtwara na Ruvuma kwa upande wa Tanzania pamoja na majimbo ya Cabo Delgado ya nchini Msumbiji.
Na Muhidin Amri,         
Songea.

MKUU wa Mkoa wa Ruvuma, Dokta Binilith Mahenge amewataka wananchi na viongozi wa Tanzania na Msumbuji kuhakikisha kwamba wanapambana na tatizo la umaskini ambao umekithiri katika nchi zao, ili kuweza kuendelea kuwa na hali ya amani na utulivu katika nchi hizo.

Dokta Mahenge alitoa kauli hiyo wakati alipokuwa akifunga mkutano wa ujirani mwema ambao ulishirikisha mikoa ya Ruvuma na Mtwara upande wa Tanzania na Jimbo la Niassa na Cabo Delgado nchini Msumbiji ambao ulifanyika juzi kwenye ukumbi wa Hunt Club uliopo mjini Songea mkoani Ruvuma.

“Kinachohitajika hivi sasa ni viongozi kushirikiana na wananchi kwa pande zote mbili na kuhakikisha mnasimama imara ili tuweze kufanya kazi kwa bidii na kuongeza uzalishaji wa mazao mashambani, hatua ambayo itasaidia vijana kujiepusha na vitendo vya uharibifu na ujangili”, alisema.

WAMILIKI WA VIWANDA WATAKIWA KUWATUMIA VIJANA WANAOMALIZA MAFUNZO VETA

Na Muhidin Amri,      
Songea.

WITO umetolewa na Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri mkuu, sera, bunge, ajira, vijana na watu wenye ulemavu Jenista Mhagama kwamba wamiliki wa viwanda pamoja na taasisi mbalimbali hapa nchini wajenge ushirikiano na vijana wanaomaliza mafunzo katika vyuo vya mafunzo na ufundi stadi (VETA) hapa nchini, kwa ajili ya kuzalisha bidhaa zitakazotosheleza mahitaji ya ndani na nje ya nchi ili kuweza kufikia uchumi wa kati.

Alisema kuwa kufanya hivyo ni hatua ambayo itasaidia kuwa na bidhaa zinazoweza kutosheleza mahitaji ya soko la ndani badala ya kukimbilia kutafuta nguvu kazi na bidhaa zinazotoka nje ya nchi.

Waziri Mhagama alisema hayo juzi alipokuwa akizungumza na  wanafunzi, walimu wa chuo cha VETA Songea pamoja na vijana 173 kutoka wilaya za mkoa wa Ruvuma, kwenye uzinduzi wa mpango  wa urasimishaji ujuzi uliopatikana nje ya mfumo rasmi wa mafunzo katika chuo hicho cha mafunzo ya ufundi stadi kilichopo mjini hapa.

Saturday, July 29, 2017

HOSPITALI MJI WA MBINGA YAKABILIWA NA CHANGAMOTO LUKUKI MBUNGE AKABIDHI MAGODORO, SHUKA NA VITANDA


Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini mkoa wa Ruvuma, Sixtus Mapunda aliyevaa shati la kijani jana akikabidhi sehemu ya vitanda 25 ambavyo ni kwa ajili ya kusaidia kulalia wagonjwa kwa uongozi wa hospitali hiyo. 
Sixtus Mapunda Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini mkoani Ruvuma akikabidhi sehemu ya magodoro kwa ajili ya kulalia wagonjwa wa hospitali ya mji wa Mbinga mkoani humo mbele ya uongozi husika wa hospitali, ambapo jumla ya magodoro 25 yalikabidhiwa ili yaweze kupunguza changamoto ya upungufu wa magodoro inayoikabili hospitali hiyo. 
Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini mkoani Ruvuma Sixtus Mapunda aliyesimama katikati akiwa amevaa shati lenye rangi ya kijani akikabidhi jana vitanda viwili vya kujifungulia akina mama wajawazito katika hospitali ya halmashauri mji wa Mbinga kwa uongozi wa hospitali hiyo. 
Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa hospitali ya Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, inakabiliwa na tatizo la ukosefu wa gari la kubebea wagonjwa wanaopata rufaa hasa kwa upande wa akina mama wajawazito, ili waweze kupelekwa hospitali ya ya mkoa Songea na misheni Litembo au Peramiho zilizopo mkoani humo kwa matibabu zaidi.

Kufuatia hali hiyo yamekuwa yakitumika magari ambayo hayapo katika mfumo rasmi wa kusafirisha wagonjwa hao ambayo pia ni chakavu, hali ambayo imekuwa ni kero kubwa katika jamii ikiwemo utekelezaji wa majukumu husika.

Hayo yalisemwa na Kaimu mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Aristachius Nkwenge wakati alipokuwa akitoa maelezo mafupi mbele ya Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini Sixtus Mapunda, ambaye alitembelea hospitalini hapo kwa ajili ya kukabidhi msaada wa vifaa mbalimbali na kujionea changamoto zilizopo.

KUHAMISHWA WATUMISHI KADA YA AFYA KUNAKWAMISHA UTOAJI HUDUMA KWA WAGONJWA MBINGA

Na Kassian Nyandindi,    
Mbinga.

KUFUATIA kuhamishwa kwa watumishi wa serikali kada ya afya waliokuwa wakitoa huduma kwenye hospitali, vituo vya afya na zahanati zilizokuwa chini ya mamlaka ya Jimbo Katoliki la Mbinga mkoani Ruvuma uongozi wa jimbo hilo unashindwa kuendelea kutoa huduma katika baadhi ya vituo vyake vya afya na hatimaye huenda vikafungwa wakati wowote kuanzia sasa na wananchi kukosa huduma husika.

Mwandishi wa habari hizi amebaini kuwa hata katika orodha ya watumishi hao ambao nakala yake tunayo, waliohamishwa wapo pia Watawa (Masista) kutoka mashirika mbalimbali katika jumuiya zao na kupelekwa kwenye vituo ambavyo havina Kanisa jambo ambalo imeelezwa kuwa ni kinyume na taratibu zao.

Vilevile kufuatia hali hiyo kumekuwa na mkanganyiko mkubwa kwa Wakuu wa mashirika ya jumuiya hizo na kuathiri kwa kiasi kikubwa huduma za afya zinazotolewa na Jimbo hilo kutokana na watumishi wengi kuhamishwa.

JENISTA MHAGAMA AWATAKA WAKURUGENZI KUTEKELEZA MAAGIZO YA SERIKALI

Na Muhidin Amri,
Songea.

SERIKALI imewaagiza Wakurugenzi watendaji katika Halmashauri za wilaya, miji manispaa na majiji hapa nchini kutenga maeneo katika halmashauri zao ili kuweza kutoa fursa mbalimbali za kiuchumi kwa vijana na makundi mengine yenye mahitaji maalumu ili yaweze kujiajiri na kufanya shughuli zao za maendeleo.
Jenista Mhagama.

Agizo hilo limetolewa jana mjini Songea mkoani Ruvuma na Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu sera, bunge, ajira, vijana na watu wenye ulemavu Jenista Mhagama wakati alipokuwa akizindua awamu ya pili mpango wa urasimishaji wa ujuzi (RPL) uliopatikana nje ya mfumo rasmi wa mafunzo kwa vijana 173 kutoka wilaya zote za mkoa huo.

Mhagama alisema kuwa serikali imekusudia kufikia nchi ya viwanda na uchumi wa kati, ifikapo mwaka 2020 hadi 2025 na kwamba mpango huo hauwezi kufanikiwa endapo halmashauri za wilaya hazitaunga mkono  juhudi hizo za serikali kuu kwa kuwaandaa na kuwapatia  vijana ujuzi, nyenzo na maeneo ya kufanyia shughuli zao.

Alisema kuwa kutokana na mafunzo hayo serikali inaamini kwamba watu wengi watapata ujuzi  na kuwawezesha kuwa na  sifa ya kufanya kazi zilizorasmi na zisizo rasmi, kwani watakuwa wamepata ujuzi na uzoefu utakaoweza kuharakisha kukua kwa uchumi wa Tanzania.

Thursday, July 27, 2017

WANANCHI MBINGA WASIKITISHWA KITENDO CHA SERIKALI KUHAMISHA WATUMISHI WAKE KADA YA AFYA

Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

WANANCHI wa wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, wamesikitishwa na kitendo cha serikali kuchukua hatua ya kuhamisha watumishi wake wa kada ya afya ambao walikuwa wakitoa huduma kwenye hospitali, vituo vya afya na zahanati zilizokuwa chini ya mamlaka ya Jimbo Katoliki la Mbinga mkoani humo.
Waziri wa afya maendeleo ya jamii jinsia wazee na watoto, Ummy Mwalimu.

Aidha wameiomba serikali kuwarejesha watumishi hao katika maeneo waliyokuwa wakifanyia kazi kwenye Jimbo hilo, ili kuweza kunusuru hali za wagonjwa waliokuwa wakipatiwa matibabu katika vituo hivyo vya kutolea huduma za afya.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na waandishi wa habari walisema kuwa hivi sasa uongozi wa Jimbo Katoliki la Mbinga unashindwa kuendelea kutoa huduma za afya katika vituo hivyo kutokana na kukosa wauguzi na wataalamu wenye uwezo wa kutibu wagonjwa.

Pia walidai kuwa kufuatia hali hiyo hospitali ya misheni Litembo na vituo vingine vinavyoendeshwa na Jimbo hilo muda wowote kuanzia sasa huenda vikafungwa visitoe huduma kwa wagonjwa kutokana na kukosa watumishi wenye uwezo wa kutibu magonjwa mbalimbali.

Wednesday, July 26, 2017

TANZANIA NA MSUMBIJI WASHAURIWA KUENDELEA KUDUMISHA UHUSIANO WAO

Gavana wa Jimbo la Cabo Delgado nchini Msumbuji, Celimira Da Silva upande wa kulia, akipokea jana zawadi mjini Songea ya kahawa inayokobolewa katika kiwanda cha Mbinga Coffee Curing Company Limited (MCCCO) kilichopo wilyani Mbinga kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dokta Binilith Mahenge wakati wa mkutano wa siku mbili wa ujirani mwema kati ya mikoa ya Ruvuma na Mtwara kwa upande wa Tanzania na majimbo ya Cabo Delgado na Niassa yaliyopo nchini Msumbuji.
Na Mwandishi wetu,      
Songea.

IMEELEZWA kuwa Watanzania na wananchi wa Msumbiji wametakiwa kuendelea kudumisha uhusiano wao ambao uliasisiwa kwa muda mrefu na viongozi wa nchi hizo mbili Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Samora Machel, ikiwa ndiyo hatua ya kuziwezesha nchi zao kupiga hatua kubwa ya kukuza uchumi na maendeleo yao kwa ujumla.

Katibu tawala wa mkoa wa Ruvuma, Hassan Bendeyeko alisema hayo jana mjini Songea wakati alipokuwa akifungua kikao cha kazi kwa wataalamu na viongozi wa mikoa ya Tanzania na Msumbuji kilichofanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya Hunt Club iliyopo mjini hapa.

Bendeyeko alisema kuwa nchi hizo zimekuwa na uhusiano mzuri kwa muda mrefu ambao wananchi wake wa pande hizo mbili wamekuwa wakishiriki kwa pamoja katika shughuli mbalimbali za maendeleo ya kijamii kama vile kilimo na uvuvi.

WANANCHI MKOA WA RUVUMA WATAKIWA KUWA NA MAZOEA YA KUTEMBELEA VIVUTIO VYA UTALII

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dokta Binilith Mahenge.
Na Kassian Nyandindi,     
Songea.

DOKTA Binilith Mahenge ambaye ni Mkuu wa mkoa wa Ruvuma amewahimiza Wananchi wa mkoa huo, kuwa na tabia yenye mazoea ya kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii vilivyopo mkoani humo badala ya kuwaacha wageni peke yao wakitumia fursa hiyo.

Mkuu huyo wa mkoa alitoa kauli hiyo jana wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake, huku akisisitiza kwamba ndani ya mkoa huo kumekuwa na vivutio vingi ambavyo vikitumika vyema vitasaidia kukuza pato la mkoa na maendeleo ya wananchi wake.

“Vivutio hivi vikitumika ipasavyo vitaufanya hata mkoa wetu kupata wageni ambao watachangia kukua kwa uchumi na pato la serikali na pia naviomba vyombo vya habari hakikisheni mnatangaza fursa hizi kama vile mbuga ya Selou, Ziwa Nyasa, Jiwe la Mbuji lililopo Mbinga ambalo linatajwa kuwa ndiyo refu kuliko yote hapa nchini na vivutio vingine tulivyonavyo”, alisisitiza Dokta Mahenge.

Monday, July 24, 2017

MADIWANI HALMASHAURI MJI WA MBINGA WAMCHAGUA DIWANI KELVIN MAPUNDA KUWA MAKAMU MWENYEKITI WA HALMASHAURI HIYO

Na Kassian Nyandindi,    
Mbinga.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, kupitia Madiwani wake wa Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani humo ambao wanatokana na chama hicho, wamemchagua Kelvin Mapunda ambaye ni diwani wa kata ya Bethlehemu mjini hapa kuwa Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya mji huo.

Kadhalika uchaguzi huo umefanyika leo majira ya asubuhi katika ukumbi wa CCM uliopo mjini hapa.

Aidha Katibu wa Chama hicho wilayani humo, Zainabu Chinowa ambaye alikuwa msimamizi mkuu wa uchaguzi huo, akitangaza matokeo hayo alimtaja Mapunda kuwa ndiye aliyeweza kushinda katika uchaguzi huo kwa kupata kura 13 dhidi ya mgombea mwenzake diwani wa kata ya Masumuni, Raphael Kambanga aliyepata kura 11.

DIWANI NDILIMALITEMBO SONGEA AWAKUMBUSHA WAANDISHI WA HABARI WAJIBU WAO

Na Muhidin Amri,
Songea.

WAANDISHI wa habari mkoani Ruvuma, wametakiwa kuondoa woga katika utendaji wa kazi zao za kila siku badala yake wameshauriwa kufanya shughuli zao kwa kujiamini na kufuata maadili yao ya kazi, kwa kuzingatia taratibu husika ikiwemo kuepuka kuandika habari za uongo au za kupika.

Cresencia Kapinga.
Mwito umetolewa jana na diwani wa kata ya Ndilimalitembo Manispaa ya Songea mkoani humo, Cresencia Kapinga wakati alipokuwa akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini hapa kuhusiana na mwelekeo na mchango wa vyombo vya habari katika kuleta maendeleo hapa nchini.

Kapinga alisema kuwa mwandishi mzuri wa habari ni yule ambaye anaandika habari zenye kuleta tija katika jamii na kuibua maovu yanayofanywa na baadhi ya watendaji wa taasisi, idara, mashirika ya umma na jamii kwa jumla dhidi ya vitendo vya rushwa, wizi na hata ukatili na unyanyasaji wa watoto na wanawake.

Mbali na diwani huyo kuwataka kufichua maovu yanayotokea katika jamii lakini pia amewaasa kuacha tabia ya kuandika habari zenye mrengo wa kushoto ambazo huchafua majina ya watu bila sababu yoyte ile ya msingi au kuwakwaza watu wengine katika jamii kwa misingi ya chuki zimepitwa na wakati kwa kile alichoeleza kuwa haziwezi kuleta tija na mafanikio katika taifa letu.

DED MADABA AWAASA WAZAZI KUZINGATIA UZAZI WA MPANGO

Na Muhidin Amri, 
Madaba.

WAZAZI na walezi  katika Halmashauri ya wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma, wameaswa kutambua wajibu wa malezi kwa watoto wao ikiwemo  kuzingatia uzazi wa mpango, ili kuweza kuepuka kuwa na idadi ya watoto wengi katika familia zao ambao ni mzigo mkubwa kutokana na hivi sasa kupanda kwa gharama ya maisha.

Hatua hiyo imeelezwa kuwa endapo watazingatia ipasavyo itawezesha watoto watakaozaliwa kupata haki yao ya msingi kama vile elimu, chakula, mavazi na kumudu gharama ya matibabu jambo ambalo litachangia kuwa na familia bora na yenye afya nzuri.

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Madaba mkoani humo, Shafi Mpenda alisema hayo wakati alipokuwa akizungumza na wazazi na walezi katika kituo cha afya Madaba ambao walikuwa kituoni hapo kwa ajili ya kupata huduma mbalimbali za matibabu.

Sunday, July 23, 2017

KOWELO ASHINDA NAFASI UMAKAMU MWENYEKITI KUONGOZA HALMASHAURI WILAYA YA MBINGA


Zoezi la kuhesabu kura zilizopigwa na Madiwani wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Halmashauri ya wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, kumchagua Makamu Mwenyekiti wa halmashauri hiyo likifanyika jana katika ukumbi wa chama hicho uliopo mjini hapa chini ya usimamizi mkuu wa Katibu wa CCM wa wilaya hiyo, Zainabu Chinowa ambaye amesimama akiwa ameshika karatasi iliyokuwa tayari kura imepigwa.
Na Mwandishi wetu,   
Mbinga.

MADIWANI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, wamemchagua Joackimu Kowelo ambaye ni diwani wa kata ya Maguu kuwa Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya hiyo.

Uchaguzi huo ulifanyika jana majira ya asubuhi katika ukumbi wa CCM uliopo mjini hapa.

Katibu wa Chama hicho wilayani humo, Zainabu Chinowa ambaye alikuwa msimamizi mkuu wa uchaguzi huo, akitangaza matokeo hayo alimtaja Kowelo kuwa ndiye aliyeweza kushinda katika uchaguzi huo kwa kupata kura 26 dhidi ya mgombea mwenzake diwani wa kata ya Matiri, Benuward Komba aliyepata kura 7.

SIXTUS MAPUNDA APONGEZA JITIHADA ZA UBORESHAJI MIUNDOMBINU YA MAJI KATIKA MJI WA MBINGA


Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini Sixtus Mapunda upande wa kulia wa kwanza, jana Julai 22 mwaka huu akiwa katika ziara yake ya kukagua ujenzi wa miundombinu ya mradi wa maji akipokea maelekezo juu ya maendeleo ya ujenzi huo unaoendelea kufanyika katika milima ya Lupembe kijiji cha Tukuzi kata ya Luwaita wilayani Mbinga, kutoka kwa wataalamu wa maji Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (MBIUWASA) iliyopo katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.
Meneja wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (MBIUWASA) Patrick Ndunguru wa kwanza kutoka kulia akiwa na Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini Sixtus Mapunda ambaye amesimama katikati, katika eneo ambalo tanki kubwa la kuhifadhia maji yatakayosambazwa katika mji wa Mbinga ambalo linajengwa katika milima ya Lupembe kijiji cha Tukuzi kata ya Luwaita wilayani Mbinga. Mbunge Mapunda jana Julai 22 mwaka huu alikuwa katika ziara yake ya kukagua ujenzi wa miundombinu hiyo ambayo inaendelea kufanyika.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MBUNGE wa Jimbo la Mbinga mjini Sixtus Mapunda amepongeza jitihada zinazoendelea kufanyika na Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira (MBIUWASA) katika mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, juu ya ujenzi wa tanki kubwa la kuhifadhia maji na miundombinu mingine ya kusambaza maji katika mji huo.

Aidha pamoja na ujenzi huo unaendelea kufanyika pia uchimbaji wa mitaro nayo inajengwa kwa ajili ya kuweza kufukia mabomba makubwa yatakayoleta maji kwa wingi zaidi katika mji wa Mbinga.

Mapunda alitoa pongezi hizo jana wakati alipokuwa kwenye ziara yake ya kutembelea mradi huo, ambao tanki hilo linajengwa katika chanzo cha maji kilichopo kwenye milima ya Lupembe iliyopo katika kijiji cha Tukuzi kata ya Luwaita.

Vilevile Mbunge huyo anaeleza kuwa katika kuendeleza na kuboresha mradi huo anaishukuru Serikali, kupitia Wizara ya maji na umwagiliaji kutenga shilingi Bilioni 1 katika bajeti yake ya mwaka 2017/2018 ambazo zitawezesha kupanua bomba kuu la uzalishaji maji hivyo kumudu ongezeko kubwa la mahitaji ya maji kufika katika eneo la mji huo.

“Katika kupambana na tatizo hili ndio maana Wizara ya maji na umwagiliaji kwa kushirikiana na Mamlaka hii, imeanza sasa kuboresha miundombinu ambayo ni chakavu ili kuweza kuondokana na changamoto hii ambayo imedumu kwa miaka mingi sasa”, alisema Mapunda.

Friday, July 21, 2017

DOKTA MASHINJI NA WENZAKE WAPATA DHAMANA BAADA YA KUKAMILISHA MASHARTI HUSIKA

Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MAHAKAMA ya Hakimu mkazi mkoa wa Ruvuma jana imempa dhamana Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Dokta Vicent Mashinji pamoja na baadhi ya viongozi wenzake wa chama hicho, ambao hapo awali walikuwa wakisota mahabusu katika gereza la mahabusu Songea baada ya kushindwa kukidhi vigezo na kamilisha masharti ya dhamana.

Aidha mbali na Dokta Mashinji, viongozi wengine katika shauri hilo ambao nao wapo nje kwa dhamana ni Mbunge wa Jimbo la Ndanda Fecil Daud ambaye pia ni Mwenyekiti wa CHADEMA Kanda ya kusini Masasi, Mwenyekiti wa CHADEMA mkoa wa Ruvuma Irineus Ngwatura, Katibu wa CHADEMA mkoa wa Ruvuma, Sang’uda Manawa na Mwenyekiti wa CHADEMA wilaya ya Nyasa Curthbeth Ngwata.

Washitakiwa wengine ni Katibu mwenezi wa chama hicho Leonard Makunguru, Katibu wa CHADEMA Kanda ya kusini Masasi Filbert Ngatunga, Mbunge wa viti maalum, Zubeda Sakuro na Katibu mwenezi wa chama hicho Kanda ya kusini Charles Leonard ambapo wote kwa pamoja wapo nje kwa dhamana ya wadhamini wawili waaminifu ambao wamesaini hati ya dhamana ya shilingi milioni 2 kila mmoja.

Thursday, July 20, 2017

KATIBU MKUU CHADEMA NA WENZAKE WAPANDISHWA KIZIMBANI SONGEA

Baadhi ya viongozi wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wakiwa katika Mahakama ya mkoa wa Ruvuma jana, ambapo wamesomewa mashtaka mawili na kupelekwa Mahabusu ya gereza Songea mjini.
Na Muhidin Amri,     
Songea.

VIONGOZI tisa wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) akiwemo Katibu Mkuu wa chama hicho  Dokta Vicent Mashinji wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu mkazi mfawidhi mkoa wa Ruvuma, kujibu mashtaka mawili yanayowakabili na baadaye wamepelekwa  katika gereza la Mahabusu Songea mjini huku kukiwa kumegubikwa na hali ya utata.

Aidha viongozi hao wamefikishwa Mahakamani hapo jana majira ya asubuhi na kusomewa mashtaka yao na Wakili wa serikali mwandamizi mkoani hapa, Renatus Mkude  ambaye alikuwa akisaidiwa na Wakili wa serikali Shaban Mwigole mbele ya Hakimu mkazi mfawidhi wa Mahakama ya mkoa huo, Simon Kobelo.

Wakili Mkude aliwataja Mahakamani hapo washitakiwa hao kuwa ni Dokta Vicent Mashinji ambaye ni Katibu Mkuu wa CHADEMA taifa, Cecil Mwambe Mwenyekiti wa CHADEMA Kanda ya kusini ambaye pia ni Mbunge wa jimbo la Ndanda Mtwara, Philberth Ngatunga Katibu wa CHADEMA Kanda ya kusini, Irineus Ngwatura Mwenyekiti CHADEMA mkoa wa Ruvuma pamoja na Delphin Gazia Katibu wa CHADEMA mkoa wa Ruvuma.

Wengine ni Zubeda Sakuru  Mbunge wa Viti maalum mkoa wa Ruvuma, Sanguru Manawa Katibu wa Oganaizesheni na mafunzo, Curthberth Ngwata Mwenyekiti CHADEMA wilaya ya Nyasa ambaye pia ni Diwani wa kata ya Kipingu wilayani humo pamoja na Charles Makunguru Katibu mwenezi wilaya ya Nyasa.

MADABA WAIOMBA SERIKALI KUWAJENGEA HOSPITALI

Na Muhidin Amri,       
Songea.

BAADHI ya Wananchi waishio katika Halmashauri ya wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma wameiomba serikali ya awamu ya tano kuwajengea hospitali ya wilaya ambayo wataweza kupata huduma za matibabu, ikiwemo kuhudumia wananchi wengi badala ya kuendelea kutegemea kituo cha afya Madaba ambacho kinaonekana kuelemewa na idadi kubwa ya wagonjwa wa aina mbalimbali.

Aidha walisema kuwa hivi sasa kumekuwa na ongezeko kubwa la watu hasa baada ya serikali kuanzisha halmashauri hiyo, hivyo kuna umuhimu wa kusogezewa karibu huduma hiyo ili wasiendelee kupata usumbufu kama wanaoupata sasa wa kufuata huduma ya matibabu umbali mrefu mjini Songea.

“Kituo hiki cha afya Madaba kwa sasa hakina uwezo wa kuhudumia wagonjwa wanaokuja hapa kwa ajili ya kupata matibabu, njia pekee tunaiomba serikali kujenga hospitali kubwa ambayo itakuwa na uwezo wa kuhudumia wananchi wengi kwa wakati mmoja sambamba na kuweka  vifaa tiba na wataalamu”, walisisitiza.

Tuesday, July 18, 2017

KATIBU MKUU CHADEMA TAIFA NA WENZAKE KUFIKISHWA MAHAKAMANI SONGEA KESHO

Na Kassian Nyandindi,
Songea.

VIONGOZI nane wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) akiwemo Katibu Mkuu taifa wa chama hicho, Dokta Vicent Mashinji wameripoti kwa Kamanda wa Polisi mkoa wa Ruvuma jana majira saa nne asubuhi na wapo nje kwa dhamana wakisubiri hatma yao.

Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Gemini Mushy alisema kuwa viongozi hao waliripoti Ofisini kwake majira hayo ambapo alikuwa akisubiri Jalada la kesi yao ambalo lipo kwa Wakili wa serikali mfawidhi mkoa wa Ruvuma.

Aliwataja viongozi hao wanaotuhumiwa kuandamana na kufanya mkutano bila kibali katika wilaya ya Nyasa kuwa ni Cecil Mwambe ambaye ni Mwenyekiti wa CHADEMA Kanda ya kusini na Mbunge wa jimbo la Ndada, Philbert Ngatunga Katibu wa Kanda ya kusini CHADEMA, Mwenyekiti wa chama hicho mkoa wa Ruvuma Ereneus Ngwatura na Delphin Gazia ambaye ni Katibu wa chama hicho mkoa wa Ruvuma.

MANISPAA YA SONGEA YAKAMATA VIPODOZI VYENYE SUMU

Baadhi ya aina ya vipodozi ambavyo vinadaiwa kuwa na sumu vilivyokamatwa Songea.
Na Mwandishi wetu,
Songea.

IDARA ya Afya katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, imefanikiwa kukamata vipodozi na vyakula vyenye sumu vikiwa na thamani ya zaidi ya shilingi milioni mbili.

Afisa habari wa Manispaa hiyo, Albano Midelo alisema kuwa vipodozi hivyo vimekamatwa katika kipindi cha kuanzia mwezi Aprili hadi Juni mwaka huu, katika ukaguzi endelevu ambao unafanywa na idara hiyo.

Vipodozi vyenye sumu ambavyo vimekamatwa baadhi yake ni Actif plus, Betasol, Broze, Cocoderm, Carolight, Carotone, Citrolight, Clairmen, Cocopulp, Corton, Diproson na Epiderm.

Monday, July 17, 2017

MKURUGENZI HALMASHAURI MJI WA MBINGA APEWA MWEZI MMOJA KUKARABATI JENGO LA UPASUAJI

Naibu Waziri wa wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala akizungumza na umati wa watu uliokusanyika kumsikiliza mara baada ya kukagua mazingira ya hospitali ya Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.
Naibu Waziri wa wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala akisisitiza jambo wakati akiwa katika ziara yake ya kikazi kukagua maeneo ya hospitali ya Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.
Na Kassian Nyandindi,    
Mbinga.

NAIBU Waziri wa Wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala amempa mwezi mmoja Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Robert Mageni ahakikishe kwamba jengo la upasuaji katika hospitali ya halmashauri ya mji huo linafanyiwa ukarabati haraka ili liweze kuwa katika hali nzuri.

Agizo hilo limetolewa juzi na Dokta Kigwangala alipokuwa katika ziara yake ya kikazi ambapo kufuatia jengo hilo kuwa chakavu katika maeneo mbalimbali ya ndani na nje hususan kwa yale yanayotumika kuoshea vifaa vya kutibu wagonjwa ameagiza pia yajengewe marumaru ili kuweza kuzuia uzalishaji wa wadudu ambao ni hatari kwa afya ya binadamu.

Vilevile ametaka pia chumba cha kunawia pamoja na miundombinu ya maji katika jengo hilo nayo vifanyiwe ukarabati mapema ikiwemo milango yake ili iweze kufunguka upande wa ndani na nje.

MADABA WANANCHI WAKE KUNUFAIKA NA MRADI WA NISHATI YA UMEME

Na Muhidin Amri,          
Madaba.

WANANCHI wanaoishi katika vijiji vilivyopo kwenye Halmashauri ya wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma, wanatarajia kuanza kunufaika na mradi wa nishati ya umeme ambao utasambazwa katika maeneo mbalimbali wilayani humo.

Mradi huo unatarajiwa kuanza mapema mwezi Agosti mwaka huu, ambapo serikali imepeleka Jenereta kubwa ambalo litajengwa kwa ajili ya kusambaza nishati hiyo muhimu.

Aidha mbali na kuusambaza kwenye vijiji hivyo, pia utapelekwa makao makuu ya Ofisi za halmashauri ya wilaya hiyo kwa ajili ya kusaidia kuimarisha mfumo wa ukusanyaji mapato kwa njia ya Kielektroniki.

DOKTA KIGWANGALA AMSHUKIA MKURUGENZI MTENDAJI HALMASHAURI YA MJI WA MBINGA

Naibu Waziri wa Wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala akiwa katika eneo la kituo cha afya cha Said Kalembo kilichopo katika kata ya Kihungu Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.
Naibu Waziri wa Wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala akimkaripia Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya mji wa Mbinga Robert Mageni upande wa kushoto ambaye amevaa koti lenye rangi nyeusi, kutokana na kushindwa kutekeleza majukumu aliyopewa na serikali. (Picha na Gwiji la Matukio Ruvuma) 
Na Kassian Nyandindi,         
Mbinga.

NAIBU Waziri wa Wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala amemjia juu Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Robert Mageni kutokana na kushindwa kutekeleza maagizo ya serikali ya kila kituo cha afya ni lazima ufanyike ujenzi wa jengo la upasuaji na utoaji wa huduma za maabara.

Dokta Kigwangala alifikia hatua hiyo juzi akiwa katika ziara yake ya kikazi baada ya kubaini kwamba haujafanyika ujenzi huo katika kituo cha afya cha Said Kalembo kilichopo kata ya Kihungu kwenye halmashauri hiyo, ili kuweza kuanzisha huduma ya upasuaji wa kumtoa mtoto tumboni kwa mama mjamzito pamoja na huduma za maabara kwa ajili ya uchunguzi wa magonjwa mbalimbali.

“Viongozi wazembe namna hii ndiyo mnaotuongezea vifo vya akina mama wajawazito kwa sababu hamtimizi wajibu wenu ipasavyo na msipotimiza wajibu maana yake inabidi mchukuliwe hatua hakuna chochote mnachokifanya mna vituo vya afya vimechoka hamfanyi ukarabati,

“Sera ya afya ipo wazi inasema vituo vyote vya afya hapa nchini vitapata usajili wa kuwa kituo cha afya endapo tu kama kutakuwa inatolewa huduma ya upasuaji na uchunguzi wa magonjwa ya maabara, hapa misingi ya uendeshaji wa kituo cha afya haifuatwi”, alisema Dokta Kigwangala.

Thursday, July 13, 2017

MANISPAA YA SONGEA YANUNUA MTAMBO WA KUZOLEA TAKA

Mtambo wa kisasa wa kuzolea taka ambao umenunuliwa na Manispaa ya Songea.
Na Mwandishi wetu,   
Songea

HATIMAYE Manispaa ya Songea iliyopo mkoani Ruvuma, imenunua mtambo wa kisasa wa kuzolea taka (kijiko) ambao kitaalamu unafahamika kwa jina la Back hoe Loader.

Afisa habari wa Manispaa ya Songea, Albano Midelo alisema kuwa mtambo huo umegharimu zaidi ya shilingi milioni 170 na kwamba umenunuliwa toka kampuni ya Hansom Tanzania Limited ya Jijini Dar es Salaam.

Midelo alieleza kuwa tayari mtambo huo umeanza kazi ya kukusanya taka katika viunga vya Songea mjini, hivyo kupunguza muda wa kuzoa taka kwa kutumia nguvu kazi.

Tuesday, July 11, 2017

MGODI WA NGAKA MBINGA WAKABILIWA NA CHANGAMOTO KUBWA KATIKA SOKO LA KUUZA MAKAA YA MAWE HAPA NCHINI

Aliyesimama ni Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dokta Binilith Mahenge akizungumza juzi wakati alipokuwa akitaka ufafanuzi juu ya masuala mbalimbali ya maendeleo ya soko la usafirishaji wa makaa ya mawe ambayo yanasafirishwa kwenda kwa watumiaji waliopo hapa nchini, ambayo yanachimbwa na kuzalishwa na Kampuni ya Tancoal Energy katika Mgodi wa Ngaka uliopo kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilaya ya Mbinga mkoani humo.
Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa uzalishaji wa makaa ya mawe yanayochimbwa katika mgodi wa Ngaka uliopo kijiji cha Ntunduaro kata ya Ruanda wilayani Mbinga mkoa wa Ruvuma, unakabiliwa na changamoto kubwa ya soko la kuuzia makaa hayo kutokana na viwanda vinavyotumia nishati hiyo hapa nchini kupunguza kasi ya ununuaji wa mkaa huo.

Aidha imefafanuliwa kuwa viwanda vya saruji ambavyo kwa kiasi kikubwa vilikuwa vikitumia mkaa huo, hivi sasa vimekuwa vikinunua kiasi kidogo cha mkaa jambo ambalo limekuwa likisababisha kuyumba kwa soko la ndani la bidhaa hiyo.

Hayo yalisemwa na Kaimu Meneja wa Kampuni ya Tancoal Energy, Edward Mwanga baada ya Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Dokta Binilith Mahenge kutembelea mgodi huo juzi kwa lengo la kutaka kujiridhisha juu ya hali ya uzalishaji wa mkaa huo.

RC RUVUMA AWAJIA JUU WATENDAJI WA SERIKALI AWATAKA WABADILIKE WAENDANE NA WAKATI


Msafara wa Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dokta Binilith Mahenge ukiwa katika kazi ya kukagua mradi wa ujenzi wa bweni la shule ya sekondari ya wasichana Mbinga iliyopo katika kata ya Kigonsera wilaya ya Mbinga mkoani humo. (Picha zote na Gwiji la Matukio Ruvuma)
Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

VIONGOZI ambao wamepewa dhamana na serikali ya kuongoza Halmashauri za wilaya mkoani Ruvuma, wameonywa kuacha mara moja tabia ya kukaa muda mwingi Ofisini badala yake watembelee na kukagua utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya wananchi vijijini ili iweze kujengwa kwa viwango vinavyotakiwa.

Onyo hilo limetolewa juzi na Mkuu wa mkoa huo, Dokta Binilith Mahenge wakati alipokuwa wilayani Mbinga katika ziara yake ya kukagua baadhi ya miradi ya ujenzi na ukarabati wa majengo ya shule za sekondari wilayani humo.

Mkuu huyo wa mkoa alisema kuwa umefika wakati sasa kwa kila kiongozi aliyekuwa katika nafasi yake mkoani humo anapaswa kutekeleza ipasavyo majukumu aliyopewa na serikali, ili kuweza kufikia malengo ya serikali ya awamu ya tano hususan katika kukuza sekta ya elimu kwa faida ya kizazi cha sasa na kile kijacho.

WAPOTEZA MAISHA BAADA YA PIKIPIKI WALIZOKUWA WAKIENDESHA KUGONGANA WAKIWA KATIKA MWENDO KASI

Na Muhidin Amri,       
Songea.        
    
WAENDESHA Pikipiki wawili wamefariki dunia baada ya Pikipiki zao walizokuwa wakiendesha kugongana wakiwa katika mwendo kasi katika kijiji cha Hanga kata ya Hanga wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma.

Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Gemini Mushy alisema kwamba tukio hilo lilitokea juzi katika kijiji hicho majira ya usiku.

“Vifo vya watu hawa vilitokea baada ya Pikipiki aina ya Yamaha yenye namba za usajili T 403 AGB iliyokuwa ikiendeshwa na Francis Mbawala (26) mkazi wa Mfaranyaki Hanga kugongana na Pikipiki nyingine ambayo haijafahamika namba zake za usajili”, alisema.

Kamanda huyo wa Polisi mkoani Ruvuma alifafanua kuwa Pikipiki nyingine ilikuwa ikiendeshwa na Sebastian Ngonyani (26) ambaye ni mkazi wa kijiji cha Hanga kata ya Hanga wilayani Namtumbo, ambapo ilitoroshwa na watu wasiofahamika mara baada ya tukio hilo kutokea hata hivyo Jeshi la Polisi linaendelea kuwatafuta watu waliotorosha Pikipiki hiyo.

Monday, July 10, 2017

RC RUVUMA KUWACHUKULIA HATUA VIONGOZI WATAKAOZEMBEA KUSIMAMIA UKARABATI WA MAJENGO YA MAABARA

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Dokta Binilith Mahenge upande wa kushoto akimsikiliza aliyekuwa Mkuu wa shule ya sekondari Ruanda, Stephano Ndomba wilayani Mbinga mkoani humo wakati alipokuwa juzi akitoa maelezo juu ya kuchelewa kwa ukarabati wa jengo la maabara la shule hiyo pamoja na jengo la kusomea wanafunzi wa kidato cha tano na sita.
Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

MKUU wa Mkoa wa Ruvuma, Dokta Binilith Mahenge amewataka Wakurugenzi na Maafisa elimu Sekondari wa Halmashauri za wilaya mkoani humo, wahakikishe kwamba fedha zilizotolewa na serikali shilingi bilioni 2.6 kwa ajili ya shughuli ya ukarabati wa majengo ya maabara kwa shule hizo zinafanya kazi husika na sio vinginevyo.

Dokta Mahenge alitoa agizo hilo kwa kile alichoeleza kuwa anazotaarifa kwamba baadhi ya shule ambazo zimepelekewa fedha tokea mwezi Machi mwaka huu, kwa ajili ya kukarabati majengo ya kusomea wanafunzi wa kidato cha tano na sita pamoja na majengo ya maabara hakuna kazi zilizofanyika mpaka sasa.

Hayo yalisemwa juzi na Mkuu huyo wa mkoa wakati alipofanya ziara yake ya kushitukiza katika wilaya ya Mbinga mkoani hapa, kwa lengo la kukagua ukarabati wa majengo ya shule ya sekondari Ruanda iliyopo katika kata ya Ruanda wilayani humo ambayo serikali imetoa shilingi milioni 259 kwa ajili ya kuweza kukamilisha kazi hiyo.

MWENYEKITI WA KIJIJI MATETELEKA MADABA LAWAMANI

Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma, Shafi Mpenda upande wa kulia, akiwaonesha waandishi wa habari (hawapo pichani) eneo ambalo limekatwa miti kwa ajili ya shughuli za kilimo ambalo ni chanzo kikubwa cha maji katika kijiji cha Mwande kata ya Mateteleka ambapo mkazi mmoja, Regan Mlelwa amekata miti hiyo katika eneo hilo na kuathiri chanzo hicho cha maji, upande wa kushoto ni Mwenyekiti wa kijiji hicho Sosmo Dominicus.
Na Muhidin Amri,     
Madaba.

MWENYEKITI wa Serikali ya kijiji cha Mateteleka kata ya Wino Halmashauri ya wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma, Remigius Njafula anatuhumiwa kugawa ardhi ya kijiji hicho kwa wageni, kinyume na taratibu husika jambo ambalo linasababisha kuzuka kwa mgogoro mkubwa kijijini hapo.

Wakitoa malalamiko yao mbele ya Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo Shafi Mpenda, katika kikao kilichowajumuisha Wazee pamoja na uongozi wa kijiji wazee hao walifafanua kuwa vitendo hivyo vya dhuluma ya ardhi amekuwa akiwafanyia hasa wanawake na vijana.

Aidha wazee hao wamelalamikia kitendo cha Mwenyekiti huyo kutumia nguvu na kupokonya msitu wa kijiji ambao uliuzwa kwa kikundi cha Jitegemee kilichopo kijijini humo, miaka 15 iliyopita na kuanza kugawa maeneo ya msitu huo bila kushirikisha wamiliki husika.