Sunday, July 30, 2017

AFISA MISITU HALMASHAURI MJI WA MBINGA ASIMAMISHWA KAZI KUFUATIA SAKATA LA MGOGORO WA FEDHA ZA MAPATO YATOKANAYO NA UVUNAJI MSITU WA MBAMBI

Hii ni moja kati ya sehemu ya msitu wa Mbambi uliopo katika kata ya Matarawe halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma ambao miti yake imevunwa na kuleta mgogoro mkubwa kati ya Madiwani na baadhi ya Watendaji wa halmashauri hiyo kutokana na fedha za mapato yatokanayo na mavuno ya mbao za msitu huo yakidaiwa kufanyiwa ubadhirifu.   
Wapasuaji mbao walinaswa na kamera yetu wakiendelea juzi na kazi ya upasuaji mbao katika msitu huo kabla ya mgogoro kutokea kati ya Madiwani na baadhi ya Watendaji wa halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, juu ya mapato baada ya mauzo ya mbao hizo ambapo walipohojiwa na mwandishi wetu walithibitisha kufanya kazi hiyo kwa muda mrefu mpaka sasa bila kulipwa ujira wao.
Diwani wa Kata ya Mpepai Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Benedict Ngwenya (aliyesimama) juzi akichangia hoja katika kikao cha baraza la Madiwani hao, juu ya umuhimu wa kuchukua hatua dhidi ya ubadhirifu wa fedha za msitu wa Mbambi uliopo katika halmashauri hiyo. 
Na Kassian Nyandindi,     
Mbinga.

SAKATA la Mgogoro wa fedha za mapato yatokanayo na uvunaji wa msitu wa Mbambi uliopo katika kata ya Matarawe Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, limechukua sura mpya kufuatia baraza la Madiwani wa halmashauri hiyo kumsimamisha kazi Afisa misitu wa mji huo, David Hyera ambaye anadaiwa kwa namna moja au nyingine kushiriki katika ubadhirifu wa mapato hayo.

Aidha kusimamishwa kazi kwa afisa huyo ni kwa ajili ya kupisha uchunguzi baada ya Madiwani hao kukubaliana kwamba iundwe Kamati maalumu ya kuchunguza suala hilo ili kuweza kupata ukweli zaidi wa jambo hilo na hatimaye hatua za kisheria zichukuliwe kwa wahusika watakaopatikana wameshiriki wizi huo.

Maamuzi hayo yalifikiwa juzi kwenye kikao cha robo ya nne cha baraza lao kilichoketi kwenye ukumbi wa Jumba la Maendeleo uliopo mjini hapa, kikiongozwa na Mwenyekiti wake Ndunguru Kipwele ambapo walieleza kuwa makisio ya awali baada ya kufanyika upembuzi yakinifu na mtaalamu huyo wa misitu na kuwasilishwa katika kikao cha baraza kilichoketi Oktoba 12 mwaka jana, yalikuwa zipatikane zaidi ya shilingi milioni 325 ambazo ni baada ya uvunaji huo kufanyika lakini wanashangaa kuelezwa kwamba zimepatikana shilingi milioni 196.

Akichangia hoja katika kikao hicho diwani wa kata ya Mpepai, Benedict Ngwenya alisema kuwa shughuli za uvunaji wa msitu wa Mbambi kabla hazijaanza kufanyika kupitia vikao husika walikubaliana kwamba Kamati husika ya mipango miji na mazingira ilibidi iende kwenye eneo la msitu huo na kujiridhisha lakini kamati hiyo ilizuiwa isiende huko kwa ajili ya kuukagua msitu huo na badala yake anadaiwa kwenda Mkurugenzi mtendaji, Robert Mageni na wataalamu wake.


“Mheshimiwa Mwenyekiti kamati yako haikupata nafasi ya kwenda kule mlimani kuona ule msitu kabla ya kuuvuna walizuiwa wasiende leo baraza hili sisi tuna mashaka na kitendo hiki kilichofanyika huu ni wizi uliokuwa wazi kimsingi mimi sijaridhika na shughuli zilizokuwa zinafanywa kule mlimani,

“Mbinga tunalaana kubwa leo hii ni mara ya pili kutokea tatizo kama hili kipindi cha nyuma wakati unavunwa msitu wa Ndengu kulikuwa na matatizo kama haya mheshimiwa Mwenyekiti jambo hili ni zito linaharufu ya ufisadi mkubwa, ambao haujawahi kutokea katika mji wa Mbinga binafsi nina haki ya kutoa hoja ya thamani ya fedha za msitu ule ni zaidi ya fedha zinazosemwa hapa leo”, alisema Ngwenya.

Naye diwani wa kata ya Kilimani Simon Ponera alisema kuwa msitu huo ulikuwa na hekta 135 ambazo ndani yake kuna ekari 75 huku kila ekari ikiwa na miti 640 endapo ikichanwa mbao ilibidi zipatikane mbao nyingi ambazo kama zingeuzwa ipasavyo kwa usimamizi mzuri mapato yake yangeweza kumaliza kero mbalimbali za miradi ya maendeleo ya wananchi ndani ya halmashauri ya mji wa Mbinga.

Raphael Kambanga diwani wa kata ya Masumuni na Kelvin Mapunda wa kata ya Betherehemu kwa nyakati tofauti walichangia hoja wakisema kuwa ni ajabu kuona kwamba pamoja na msitu huo kuvunwa, lakini hata wafanyakazi waliokuwa wakifanya shughuli za upasuaji mbao wanadai fedha zao zaidi ya shilingi milioni 20 kwa kazi ya upasuaji walioufanya huku wakifafanua kuwa hata fedha hizo zilizopatikana shilingi milioni 196 baada ya mavuno kufanyika mpaka sasa hazijulikani zipo wapi.

Pia afisa misitu huyo, David Hyera alipotakiwa kutolea ufafanuzi juu ya madai hayo alionekana kutoa taarifa ambazo zinapishana na maelezo yaliyonukuliwa kwenye makabrasha ya vikao vya madiwani hao ambapo baadaye aliamrishwa akae chini na kuzuiwa asiongee chochote kutokana na takwimu zake alizokuwa akizitoa mbele ya baraza hilo kutoendana sawa na makubaliano ya vikao husika.

Vilevile Mwenyekiti wa Kamati ya mipango miji na mazingira, Leonard Mshunju naye alithibitisha mbele ya baraza hilo la Madiwani huku akifafanua kuwa licha ya kutoa maazimio ambayo hata wafanyakazi waliofanya kazi ya uvunaji wa msitu ule wanapaswa kulipwa fedha zao lakini hakuna kilichotekelezwa mpaka sasa.

Mshunju alibainisha kuwa ni kweli kamati hiyo ilizuiwa kwenda kukagua msitu wa Mbambi kabla kazi ya uvunaji haijaanza kufanyika na kwamba licha ya kuomba wakaangalie nini kinachofanyika kule walizuiwa na hali hiyo alieleza kuwa ni ukiukwaji mkubwa wa kanuni na taratibu husika za baraza hilo.

Alipotakiwa kutolea ufafanuzi juu ya tuhuma hizo naye Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya mji wa Mbinga Robert Mageni alisema, “mapendekezo yote yaliyotolewa na kamati nayakubali ni kweli tuliwasilisha bajeti ya kupasua mbao zenye thamani ya shilingi milioni 325 lakini suala la kukaidi kamati kuizuia kuipeleka kule msituni sio la kweli ila kule msituni hata mimi binafsi nakumbuka nilishawahi kwenda baada ya kupata fununu kwamba kuna mabaya yanafanyika”.


Hata hivyo kwa upande wake Mwenyekiti wa baraza la Madiwani wa halmashauri ya mji huo, Ndunguru Kipwele aliunga mkono hoja zilizotolewa na Madiwani hao na kueleza kuwa kuna kila sababu ya suala hilo kuunda Kamati maalumu, ambayo itafanya kazi ya kuchunguza tatizo hilo kwa muda wa mwezi mmoja na baadaye litaitwa baraza la dharula kwa ajili ya kutolea ufafanuzi juu ya majibu ya uchunguzi walioufanya.

No comments: