Saturday, July 29, 2017

HOSPITALI MJI WA MBINGA YAKABILIWA NA CHANGAMOTO LUKUKI MBUNGE AKABIDHI MAGODORO, SHUKA NA VITANDA


Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini mkoa wa Ruvuma, Sixtus Mapunda aliyevaa shati la kijani jana akikabidhi sehemu ya vitanda 25 ambavyo ni kwa ajili ya kusaidia kulalia wagonjwa kwa uongozi wa hospitali hiyo. 
Sixtus Mapunda Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini mkoani Ruvuma akikabidhi sehemu ya magodoro kwa ajili ya kulalia wagonjwa wa hospitali ya mji wa Mbinga mkoani humo mbele ya uongozi husika wa hospitali, ambapo jumla ya magodoro 25 yalikabidhiwa ili yaweze kupunguza changamoto ya upungufu wa magodoro inayoikabili hospitali hiyo. 
Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini mkoani Ruvuma Sixtus Mapunda aliyesimama katikati akiwa amevaa shati lenye rangi ya kijani akikabidhi jana vitanda viwili vya kujifungulia akina mama wajawazito katika hospitali ya halmashauri mji wa Mbinga kwa uongozi wa hospitali hiyo. 
Na Kassian Nyandindi,      
Mbinga.

IMEELEZWA kuwa hospitali ya Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, inakabiliwa na tatizo la ukosefu wa gari la kubebea wagonjwa wanaopata rufaa hasa kwa upande wa akina mama wajawazito, ili waweze kupelekwa hospitali ya ya mkoa Songea na misheni Litembo au Peramiho zilizopo mkoani humo kwa matibabu zaidi.

Kufuatia hali hiyo yamekuwa yakitumika magari ambayo hayapo katika mfumo rasmi wa kusafirisha wagonjwa hao ambayo pia ni chakavu, hali ambayo imekuwa ni kero kubwa katika jamii ikiwemo utekelezaji wa majukumu husika.

Hayo yalisemwa na Kaimu mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Aristachius Nkwenge wakati alipokuwa akitoa maelezo mafupi mbele ya Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini Sixtus Mapunda, ambaye alitembelea hospitalini hapo kwa ajili ya kukabidhi msaada wa vifaa mbalimbali na kujionea changamoto zilizopo.


Nkwenge alimweleza Mbunge Mapunda kuwa changamoto nyingine wanayokabiliana nayo ni kutokamilika kwa ujenzi wa jengo la wodi ya wagonjwa mahututi (ICU) na uchakavu wa vichomea taka.

Alisema kuwa pia hospitali ya mji wa Mbinga haina jokofu la kuhifadhia maiti licha ya uwepo wa jengo maalumu ambalo limejengwa kwa muda mrefu kwa ajili ya kuhifadhia miili hiyo.

“Hospitali yetu inakabiliwa pia na changamoto ya kutokuwepo kwa jengo la wodi ya watoto na uchakavu wa miundombinu ya majengo ya hospitali pamoja na upungufu wa watumishi hususan wa kitengo cha mionzi na vifaa tiba”, alisema Nkwenge.

Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo hilo, Mapunda aliweza kupunguza changamoto zilizokuwa zinaikabili hospitali ya mji huo kwa kukabidhi msaada wa vifaa kama vile vitanda 25, magodoro ya kulalia wagonjwa 25, vitanda vya kujifungulia akina mama wajawazito 2 pamoja na mashuka ya kujifunika wagonjwa 105 vyote vikiwa na thamani ya shilingi milioni 5,050,000.


“Utoaji wa vifaa hivi utasaidia kupunguza baadhi ya changamoto zilizokuwa zinaikabili hospitali yetu, pia nitajitahidi kufanya ufuatiliaji serikalini juu ya changamoto nyingine ambazo zinahitaji kutatuliwa ili kuweza kuboresha mahitaji muhimu yanayotakiwa kuwepo na kutekelezwa katika hospitali hii”, alisisitiza Mapunda.

No comments: