Monday, July 17, 2017

DOKTA KIGWANGALA AMSHUKIA MKURUGENZI MTENDAJI HALMASHAURI YA MJI WA MBINGA

Naibu Waziri wa Wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala akiwa katika eneo la kituo cha afya cha Said Kalembo kilichopo katika kata ya Kihungu Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.
Naibu Waziri wa Wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala akimkaripia Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya mji wa Mbinga Robert Mageni upande wa kushoto ambaye amevaa koti lenye rangi nyeusi, kutokana na kushindwa kutekeleza majukumu aliyopewa na serikali. (Picha na Gwiji la Matukio Ruvuma) 
Na Kassian Nyandindi,         
Mbinga.

NAIBU Waziri wa Wizara ya afya, maendeleo ya jamii, jinsia, wazee na watoto Dokta Khamis Kigwangala amemjia juu Mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, Robert Mageni kutokana na kushindwa kutekeleza maagizo ya serikali ya kila kituo cha afya ni lazima ufanyike ujenzi wa jengo la upasuaji na utoaji wa huduma za maabara.

Dokta Kigwangala alifikia hatua hiyo juzi akiwa katika ziara yake ya kikazi baada ya kubaini kwamba haujafanyika ujenzi huo katika kituo cha afya cha Said Kalembo kilichopo kata ya Kihungu kwenye halmashauri hiyo, ili kuweza kuanzisha huduma ya upasuaji wa kumtoa mtoto tumboni kwa mama mjamzito pamoja na huduma za maabara kwa ajili ya uchunguzi wa magonjwa mbalimbali.

“Viongozi wazembe namna hii ndiyo mnaotuongezea vifo vya akina mama wajawazito kwa sababu hamtimizi wajibu wenu ipasavyo na msipotimiza wajibu maana yake inabidi mchukuliwe hatua hakuna chochote mnachokifanya mna vituo vya afya vimechoka hamfanyi ukarabati,

“Sera ya afya ipo wazi inasema vituo vyote vya afya hapa nchini vitapata usajili wa kuwa kituo cha afya endapo tu kama kutakuwa inatolewa huduma ya upasuaji na uchunguzi wa magonjwa ya maabara, hapa misingi ya uendeshaji wa kituo cha afya haifuatwi”, alisema Dokta Kigwangala.


Naibu Waziri huyo alifikia hatua pia ya kutaka kukishusha hadhi kituo hicho cha afya kutokana na tokea kijengwe miaka mingi iliyopita hakijakidhi vigezo husika na kwamba aliongeza kuwa kuna timu yake ya wataalamu ambayo inazunguka nchi nzima kufanya tathimini vituo vyote vya afya ambapo kama watakuta kuna kituo hakijatimiza matakwa yaliyotolewa na serikali viongozi wote wazembe watawajibishwa.

Alisema kuwa ameshangazwa na uongozi wa halmashauri ya mji wa Mbinga licha ya kuwa na kituo kimoja cha afya lakini umeshindwa kutekeleza maagizo hayo ya serikali tokea yalipotolewa miezi sita iliyopita, ikiwemo hata kukifanyia ukarabati kituo hicho hivyo serikali itahakikisha wale wote ambao walipaswa kutekeleza agizo hilo na hakuna kilichofanyika watendaji husika watawajibika.

“Wakati Rais Dokta John Magufuli anawapatia majukumu mlipaswa kuyatekeleza lakini hamna mlichotekeleza mmebaki kukaa tu na kupuuza mimi kabla sijatumbuliwa nitawatumbua ninyi kwanza, nitahakikisha nimewatoa wa chini yangu kwa sababu inaonesha hamtilii maanani maagizo ya serikali ikiwemo hata hiki kituo kimoja cha afya mlichokuwa nacho kinawashinda”, alihoji Dokta Kigwangala.

Alifafanua kuwa viongozi waliopewa dhamana na serikali wanapaswa kumsaidia Rais Dokta Magufuli kwa kufanya kazi zao kwa bidii katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo ya wananchi.

Vilevile aliongeza kuwa sera ya afya inawataka viongozi waliopo katika ngazi ya halmashauri kusimamia majukumu yote ikiwemo kufanya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za maendeleo ya sekta hiyo ili serikali inapofanya ufuatiliaji wake ikute utekelezaji husika umekwisha fanyika na sio kuiachia Wizara afya pekee.

Hata hivyo wakati wa kuhitimisha ziara hiyo ya Dokta Kigwangala kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Mbinga, Cosmas Nshenye naye alisema kuwa atahakikisha anaendelea kusimamia maagizo hayo yaliyotolewa na serikali ikiwemo kuwabana watumishi wake wa ngazi ya chini ili waweze kuwajibika ipasavyo.

No comments: