Saturday, July 29, 2017

JENISTA MHAGAMA AWATAKA WAKURUGENZI KUTEKELEZA MAAGIZO YA SERIKALI

Na Muhidin Amri,
Songea.

SERIKALI imewaagiza Wakurugenzi watendaji katika Halmashauri za wilaya, miji manispaa na majiji hapa nchini kutenga maeneo katika halmashauri zao ili kuweza kutoa fursa mbalimbali za kiuchumi kwa vijana na makundi mengine yenye mahitaji maalumu ili yaweze kujiajiri na kufanya shughuli zao za maendeleo.
Jenista Mhagama.

Agizo hilo limetolewa jana mjini Songea mkoani Ruvuma na Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Mkuu sera, bunge, ajira, vijana na watu wenye ulemavu Jenista Mhagama wakati alipokuwa akizindua awamu ya pili mpango wa urasimishaji wa ujuzi (RPL) uliopatikana nje ya mfumo rasmi wa mafunzo kwa vijana 173 kutoka wilaya zote za mkoa huo.

Mhagama alisema kuwa serikali imekusudia kufikia nchi ya viwanda na uchumi wa kati, ifikapo mwaka 2020 hadi 2025 na kwamba mpango huo hauwezi kufanikiwa endapo halmashauri za wilaya hazitaunga mkono  juhudi hizo za serikali kuu kwa kuwaandaa na kuwapatia  vijana ujuzi, nyenzo na maeneo ya kufanyia shughuli zao.

Alisema kuwa kutokana na mafunzo hayo serikali inaamini kwamba watu wengi watapata ujuzi  na kuwawezesha kuwa na  sifa ya kufanya kazi zilizorasmi na zisizo rasmi, kwani watakuwa wamepata ujuzi na uzoefu utakaoweza kuharakisha kukua kwa uchumi wa Tanzania.


Katika hatua nyingine Waziri Mhagama amempongeza Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Dokta Binilith Mahenge kwa kile alichoeleza kuwa amekuwa na mipango mingi ya maendeleo ambayo inalenga kuharakisha kukua kwa maendeleo ya mkoa huo na kujali makundi mengine ya kijamii hususan kwa yale yenye mahitaji maalumu.

Alibainisha kuwa ni hatua nzuri sasa kuona serikali ya mkoa huo chini ya Dokta Mahenge imewatafutia mradi wa kuku wa nyama kikundi cha watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino) katika Manispaa ya Songea mkoani humo huku akiitaka mikoa mingine kuiga utendaji kazi wa Dokta Mahenge kwa kutafuta vyanzo vya mapato na kumaliza changamoto zinazowakabili wananchi wao na sio kuisubiri serikali peke yake itekeleze maendeleo ya wananchi.

Aidha katika hatua nyingine ametoa mwezi mmoja kwa Kaimu Mkurugenzi msaidizi Ofisi ya Waziri Mkuu kazi, vijana, ajira na wenye ulemavu Robert Masatu kuandaa andiko ambalo litawezesha kupata fedha kwa ajili ya kuunda kiwanda kidogo cha kutengeneza chakula cha kuku kwa ajili ya kikundi cha watu hao wenye ulemavu wa ngozi waliopo mjini hapa.

“Mkurugenzi nakuagiza juu ya jambo hili analofanya Mkuu wa mkoa huu sio kazi yake bali ni jukumu la sisi Wizara husika, nakupatia mwezi mmoja wewe shirikiana na watendaji wengine kuandaa andiko litakalosaidia kupata fedha za kuunda kiwanda cha kutengeneza chakula cha kuku hawa kwa ajili ya kuunga mkono juhudi hizi zinazofanywa hapa”, alisisitiza Mhagama.

Awali Mkuu wa mkoa wa Ruvuma, Dokta Binilith Mahenge amempongeza Rais Dokta John Magufuli kwa kuanza kutekeleza kwa vitendo ahadi zake ikiwemo ya kuzalisha ajira kwa wingi kwa vijana hapa nchini.

Dokta Mahenge alisema kuwa nchi kubwa duniani ikiwemo Ujerumani imepiga hatua kubwa ya kiuchumi baada ya kuwekeza nguvu kubwa katika ujenzi wa kazi za mikono na kuiomba serikali kupitia ofisi ya Waziri Mkuu sera, bunge, ajira, vijana na wenye ulemavu kusaidia mpango maalumu wa kilimo ujulikanao kwa jina la Green House, ambao uliibuliwa na serikali ya mkoa wenye lengo la kuinua shughuli za kilimo cha matunda na mboga mboga.


Pia Mkuu huyo wa mkoa huo alieleza kuwa tayari serikali imetoa fedha kwa kikundi cha watu hao wenye matatizo ya ngozi katika Manispaa ya Songea kwa ajili ya kuanzisha mradi wa ufugaji kuku wa nyama, katika eneo la nane nane lililopo mjini hapa ambapo mradi huo utawawezesha kuongeza kipato chao na kuboresha lishe.

No comments: