Sunday, July 23, 2017

SIXTUS MAPUNDA APONGEZA JITIHADA ZA UBORESHAJI MIUNDOMBINU YA MAJI KATIKA MJI WA MBINGA


Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini Sixtus Mapunda upande wa kulia wa kwanza, jana Julai 22 mwaka huu akiwa katika ziara yake ya kukagua ujenzi wa miundombinu ya mradi wa maji akipokea maelekezo juu ya maendeleo ya ujenzi huo unaoendelea kufanyika katika milima ya Lupembe kijiji cha Tukuzi kata ya Luwaita wilayani Mbinga, kutoka kwa wataalamu wa maji Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (MBIUWASA) iliyopo katika Halmashauri ya mji wa Mbinga mkoani Ruvuma.
Meneja wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (MBIUWASA) Patrick Ndunguru wa kwanza kutoka kulia akiwa na Mbunge wa Jimbo la Mbinga mjini Sixtus Mapunda ambaye amesimama katikati, katika eneo ambalo tanki kubwa la kuhifadhia maji yatakayosambazwa katika mji wa Mbinga ambalo linajengwa katika milima ya Lupembe kijiji cha Tukuzi kata ya Luwaita wilayani Mbinga. Mbunge Mapunda jana Julai 22 mwaka huu alikuwa katika ziara yake ya kukagua ujenzi wa miundombinu hiyo ambayo inaendelea kufanyika.
Na Kassian Nyandindi,
Mbinga.

MBUNGE wa Jimbo la Mbinga mjini Sixtus Mapunda amepongeza jitihada zinazoendelea kufanyika na Mamlaka ya Maji safi na Usafi wa Mazingira (MBIUWASA) katika mji wa Mbinga mkoani Ruvuma, juu ya ujenzi wa tanki kubwa la kuhifadhia maji na miundombinu mingine ya kusambaza maji katika mji huo.

Aidha pamoja na ujenzi huo unaendelea kufanyika pia uchimbaji wa mitaro nayo inajengwa kwa ajili ya kuweza kufukia mabomba makubwa yatakayoleta maji kwa wingi zaidi katika mji wa Mbinga.

Mapunda alitoa pongezi hizo jana wakati alipokuwa kwenye ziara yake ya kutembelea mradi huo, ambao tanki hilo linajengwa katika chanzo cha maji kilichopo kwenye milima ya Lupembe iliyopo katika kijiji cha Tukuzi kata ya Luwaita.

Vilevile Mbunge huyo anaeleza kuwa katika kuendeleza na kuboresha mradi huo anaishukuru Serikali, kupitia Wizara ya maji na umwagiliaji kutenga shilingi Bilioni 1 katika bajeti yake ya mwaka 2017/2018 ambazo zitawezesha kupanua bomba kuu la uzalishaji maji hivyo kumudu ongezeko kubwa la mahitaji ya maji kufika katika eneo la mji huo.

“Katika kupambana na tatizo hili ndio maana Wizara ya maji na umwagiliaji kwa kushirikiana na Mamlaka hii, imeanza sasa kuboresha miundombinu ambayo ni chakavu ili kuweza kuondokana na changamoto hii ambayo imedumu kwa miaka mingi sasa”, alisema Mapunda.


Kwa upande wake naye Meneja wa MBIUWASA, Patrick Ndunguru alipohojiwa na mwandishi wa habari hizi alifafanua kuwa changamoto kubwa waliyonayo sasa ni uchakavu wa miundombinu ya kuleta maji hayo kutoka kwenye chanzo cha Ndengu hadi Mbinga mjini, ambapo miundombinu yake ni ya zamani imejengwa mwaka 1970 hivyo imekuwa ikisababisha upotevu mkubwa wa maji ambayo yanapaswa kuwafikia walaji.

Ndunguru alisema kuwa hayo yote yanatokana na uwezo mdogo wa uzalishaji maji unaosababishwa na kupanuka kwa mji na kwamba mradi huo unahitaji kupanuliwa miundombinu hiyo haraka, kwani uzalishaji uliopo sasa ni mita za ujazo 2,100 kwa siku ikilinganishwa na mahitaji halisi yanayohitajika ni mita za ujazo 5,248.

“Wizara imekuwa ikitupatia fedha za ujenzi wa mradi huu kwa awamu kwa lengo la kuweza kukamilisha ujenzi ambao tumeanza kuujenga, hapa lengo kuu ni kuongeza uwingi wa maji, katika mwaka 2017 hadi 2018 malengo yetu pia ni kujenga machujio ambayo kazi yake kubwa yatakuwa ni kutibu maji kabla hayajasafirishwa kwenda kwa watumiaji”, alisema Ndunguru.

Kadhalika aliongeza kuwa mradi huo unalenga pia kupanua huduma kwa kuyafikisha maji katika maeneo mengine ya mji wa Mbinga ambayo hayajafikiwa na huduma, ambapo ujenzi wake utakuwa unatekelezwa kwa awamu kulingana na kiasi cha fedha watakachokuwa wanapata hivyo aliiomba serikali kupitia wizara husika iendelee kutoa fedha za ujenzi wa miundombinu hiyo ili mradi uweze kukamilika ujenzi wake kwa wakati.


No comments: