Wednesday, July 26, 2017

TANZANIA NA MSUMBIJI WASHAURIWA KUENDELEA KUDUMISHA UHUSIANO WAO

Gavana wa Jimbo la Cabo Delgado nchini Msumbuji, Celimira Da Silva upande wa kulia, akipokea jana zawadi mjini Songea ya kahawa inayokobolewa katika kiwanda cha Mbinga Coffee Curing Company Limited (MCCCO) kilichopo wilyani Mbinga kutoka kwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Dokta Binilith Mahenge wakati wa mkutano wa siku mbili wa ujirani mwema kati ya mikoa ya Ruvuma na Mtwara kwa upande wa Tanzania na majimbo ya Cabo Delgado na Niassa yaliyopo nchini Msumbuji.
Na Mwandishi wetu,      
Songea.

IMEELEZWA kuwa Watanzania na wananchi wa Msumbiji wametakiwa kuendelea kudumisha uhusiano wao ambao uliasisiwa kwa muda mrefu na viongozi wa nchi hizo mbili Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Samora Machel, ikiwa ndiyo hatua ya kuziwezesha nchi zao kupiga hatua kubwa ya kukuza uchumi na maendeleo yao kwa ujumla.

Katibu tawala wa mkoa wa Ruvuma, Hassan Bendeyeko alisema hayo jana mjini Songea wakati alipokuwa akifungua kikao cha kazi kwa wataalamu na viongozi wa mikoa ya Tanzania na Msumbuji kilichofanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya Hunt Club iliyopo mjini hapa.

Bendeyeko alisema kuwa nchi hizo zimekuwa na uhusiano mzuri kwa muda mrefu ambao wananchi wake wa pande hizo mbili wamekuwa wakishiriki kwa pamoja katika shughuli mbalimbali za maendeleo ya kijamii kama vile kilimo na uvuvi.


“Nchi hizi mbili zimekuwa na uhusiano huu kwa muda mrefu sasa tena wa damu ambao jamii wakati mwingine imekuwa ikiongea lugha moja inayofanana”, alisema Bendeyeko.

Katika kikao hicho kwa upande wa Tanzania wataalamu walitoka mkoa wa Ruvuma na Mtwara na upande wa Msumbuji mikoa iliyoshiriki ni Niassa na Cabo Delegado ambapo Ruvuma jopo la wataalamu liliwakilishwa na Katibu tawala wa mkoa huo Bendeyeko na upande wa Mtwara likiongozwa na Katibu tawala Alfred Luanda.

Vilevile kwa upande wa Serikali ya nchi ya Msumbiji, iliongozwa na Jenerali Yusuph Omary pamoja na wataalamu wengine wa masuala ya uchumi na  kisiasa ambao kwa pamoja walijadili namna ya kuendelea kuimarisha uhusino kwa nchi hizo.

Bendeyeko alifafanua kuwa mbali na wananchi kuongea lugha inayofanana wamekuwa pia wakishirikiana kufanya shughuli zao za kiuchumi kwa pamoja wakitumia mto Ruvuma.

Kwa upande wake Mkuu wa wilaya ya Mecula nchini Msumbiji, Almindo Alberto ametoa wito kwa Watanzania kudumisha uhusiano huo pamoja na kufanya kazi mbalimbali nchini humo kwa kufuata sheria na taratibu husika.

Pamoja na mambo mengine kikao hicho kinafuatia baada ya kufanyika kikao cha mwaka 2006 kwa viongozi wa nchi hizo mbili na kujenga makubaliano ya kuunda ushirikiano endelevu kwa manufaa ya wananchi wake.

No comments: