Thursday, July 20, 2017

MADABA WAIOMBA SERIKALI KUWAJENGEA HOSPITALI

Na Muhidin Amri,       
Songea.

BAADHI ya Wananchi waishio katika Halmashauri ya wilaya ya Madaba mkoani Ruvuma wameiomba serikali ya awamu ya tano kuwajengea hospitali ya wilaya ambayo wataweza kupata huduma za matibabu, ikiwemo kuhudumia wananchi wengi badala ya kuendelea kutegemea kituo cha afya Madaba ambacho kinaonekana kuelemewa na idadi kubwa ya wagonjwa wa aina mbalimbali.

Aidha walisema kuwa hivi sasa kumekuwa na ongezeko kubwa la watu hasa baada ya serikali kuanzisha halmashauri hiyo, hivyo kuna umuhimu wa kusogezewa karibu huduma hiyo ili wasiendelee kupata usumbufu kama wanaoupata sasa wa kufuata huduma ya matibabu umbali mrefu mjini Songea.

“Kituo hiki cha afya Madaba kwa sasa hakina uwezo wa kuhudumia wagonjwa wanaokuja hapa kwa ajili ya kupata matibabu, njia pekee tunaiomba serikali kujenga hospitali kubwa ambayo itakuwa na uwezo wa kuhudumia wananchi wengi kwa wakati mmoja sambamba na kuweka  vifaa tiba na wataalamu”, walisisitiza.


Alphonce Danda alifafanua kuwa wakati umefika kwa serikali kuanza kutekeleza ahadi zake kwa wananchi wa wilaya hiyo, kujenga miundombinu ya kutosha ya afya kama vile huduma ya maji, afya na barabara jambo ambalo litasaidia kuboresha maisha na maendeleo ya wananchi wake.

Danda alibainisha kuwa serikali imeamua kuanzisha halmashauri ya wilaya miaka miwili iliyopita kwa lengo la kusogeza karibu huduma za kijamii ikiwemo matibabu kwa wananchi wake, lakini halmashauri hiyo bado pia inakabiliwa na matatizo kama vile ukosefu wa watumishi wa kutosha katika kada mbalimbali, makazi ya watumishi hao ikiwemo nyumba ya kuishi Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya.

Naye John Mlelwa alisema mbali na tatizo la makazi ya kuishi watumishi pia kuna upungufu mkubwa wa watumishi hasa wakuu wa idara mbalimbali kwani waliopo ni wale wanaokaimu tu na kusababisha shughuli nyingi kukwama kutokamilika kwa wakati.


Mlelwa aliwapongeza watumishi wachache waliopo kwa utendaji kazi mzuri kwani licha ya uchache wao hata hivyo wamesaidia kuboresha huduma husika na kuleta tija sehemu ya kazi.

No comments: