Friday, July 21, 2017

DOKTA MASHINJI NA WENZAKE WAPATA DHAMANA BAADA YA KUKAMILISHA MASHARTI HUSIKA

Na Kassian Nyandindi,
Songea.

MAHAKAMA ya Hakimu mkazi mkoa wa Ruvuma jana imempa dhamana Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Dokta Vicent Mashinji pamoja na baadhi ya viongozi wenzake wa chama hicho, ambao hapo awali walikuwa wakisota mahabusu katika gereza la mahabusu Songea baada ya kushindwa kukidhi vigezo na kamilisha masharti ya dhamana.

Aidha mbali na Dokta Mashinji, viongozi wengine katika shauri hilo ambao nao wapo nje kwa dhamana ni Mbunge wa Jimbo la Ndanda Fecil Daud ambaye pia ni Mwenyekiti wa CHADEMA Kanda ya kusini Masasi, Mwenyekiti wa CHADEMA mkoa wa Ruvuma Irineus Ngwatura, Katibu wa CHADEMA mkoa wa Ruvuma, Sang’uda Manawa na Mwenyekiti wa CHADEMA wilaya ya Nyasa Curthbeth Ngwata.

Washitakiwa wengine ni Katibu mwenezi wa chama hicho Leonard Makunguru, Katibu wa CHADEMA Kanda ya kusini Masasi Filbert Ngatunga, Mbunge wa viti maalum, Zubeda Sakuro na Katibu mwenezi wa chama hicho Kanda ya kusini Charles Leonard ambapo wote kwa pamoja wapo nje kwa dhamana ya wadhamini wawili waaminifu ambao wamesaini hati ya dhamana ya shilingi milioni 2 kila mmoja.


Mara ya kwanza washitakiwa hao wote walipelekwa katika Mahakama ya Hakimu mkazi mbele ya Hakimu mkazi mfawidhi wa mahakama ya mkoa wa Ruvuma, Simon Kobelo kwa makosa mawili ya kufanya mkusanyiko usio halali na kufanya maandamano bila kuwa na kibali jambo ambalo ni kinyume cha sheria.

Wakili mfawidhi wa serikali kutoka Ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali Kanda ya Songea, Renatus Mkude alisema kuwa hana pingamizi juu ya dhamana kwa washtakiwa wote na kwamba Hakimu wa mahakama hiyo, Kobelo ndipo naye aliungana na maelezo hayo ya mwanasheria mkuu wa serikali na hatimaye kuwapatia dhamana hiyo kwa sharti la kwanza kuwa na wadhamini wawili waaminifu kila mmoja.

Kwa mujibu wa Hakimu huyo alifafanua kuwa sharti la pili, wadhamini hao aliwataka wasaini hati ya dhamana ya shilingi milioni mbili kila mmoja jambo ambalo waliweza kutekeleza na kukidhi vigezo husika kwa washtakiwa wote na kwamba kesi hiyo itatajwa tena Agosti 21 mwaka huu.

Akizungumza nje ya Mahakamna baada ya kupata dhamana Dokta Mashinji aliwaeleza waandishi wa habari kuwa kukamatwa na kufikishwa Mahakamani ni kama mchezo mchafu wa serikali ya awamu ya tano ambao unataka kuviua vyama vya upinzani hapa nchini.

Pia Dokta Mashinji alilitaka Jeshi la Polisi kuacha kutumika vibaya badala yake lifanye kazi kwa weledi na kuacha kutumika upande mmoja jambo ambalo linaweza kuleta taswira mbaya kwa Watanzania.

Alisema kuwa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo kipo katika jukumu la kuwa andaa wanachama wake kwa ajili ya maandalizi ya uchaguzi mkuu wa chama hicho ambao unatarajiwa kufanyika mwaka huu, hivyo wapo katika ziara mikoa ya Kanda ya kusini kuzungumza na wanachama wake ili wajiandae kushiriki vyema katika chaguzi hizo.

Alibainisha kuwa katika kufanikisha zoezi hilo chama kilimtuma Mbunge wake Zubeda Sakuro kwenda wilayani Nyasa kwa ajili ya kufanya kazi hiyo, ndipo akiwa katika mkutano na wanachama wengine alikamatwa na Jeshi la Polisi kwa kosa la kufanya mkutano huo.

Dokta Mashinji alieleza kuwa walianza ziara yao tangu Julai 14 mwaka huu wakiwa Mbamba bay Nyasa mkoani Ruvuma, ikiwa ni maandalizi ya uchaguzi wa Chama hicho ambapo wakiwa wanajiandaa kufanya mkutano wa ndani walipata taarifa kwa Zebeda Sakuru ambaye ni Mbunge wa viti maalum mkoa wa Ruvuma amekamatwa na Polisi na walipo mtuma mtu mwingine naye aliwekwa ndani na kila waliyemtuma alikamatwa na kufanyiwa hivyo.


Pamoja na mambo mengine amewataka wanachama na viongozi wa chama hicho kote nchini kuwa imara hasa wakati huu ambao chama kimeamua kuendelea kujiimarisha kwa ajili ya kushiriki vyema chaguzi za ndani ya chama ili kuweza kupata viongozi ambao wataweza kushiriki katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.

No comments: