Thursday, April 13, 2017

MBINGA YAONGOZA KWA KASI YA MAAMBUKIZI UGONJWA WA UKIMWI MKOANI RUVUMA

Dkt. Joachim Henjewele.
Na Kassian Nyandindi,   
Mbinga.

IMEELEZWA kwamba, hali ya maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi katika Halmashauri ya mji wa Mbinga na wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma, inaendelea kukua kwa kasi ambapo hivi sasa kwa pamoja halmashauri hizo zimekuwa zikiongoza kwa asilimia 9.6 ya maambukizi ya ugonjwa huo, ukilinganisha na kiwango cha mkoa huo ambacho ni asilimia 7.2.

Takwimu hizo zimetolewa katika kipindi cha miezi sita kuanzia mwezi Oktoba mwaka jana hadi Machi mwaka huu, ambapo jumla ya watu 2,890 waliweza kupimwa na kwamba waliogundulika kuwa na maambukizi ya ugonjwa huo kati ya hao walikuwa ni watu 278.

Hayo yalisemwa na Dkt. Joachim Henjewele ambaye ni Meneja Mkuu wa shirika lisilokuwa la kiserikali la Health Promotion Tanzania (HDT) lililopo mjini hapa, ambalo linajishughulisha na udhibiti wa maambukizi mapya ya Virusi Vya Ukimwi (VVU) ndani ya halmashauri hizo wakati alipokuwa akizungumza juzi na waandishi wa habari ofisini kwake.


“Kwa picha hii hali ya maambukizi Mbinga bado ipo juu ukilinganisha na kiwango cha mkoa huu ambacho ni 7.2 na kitaifa ni 5.1 hivyo jitihada za kuendelea kuelimisha jamii ili iweze kuepukana na maambukizi mapya ya Virusi vya ukimwi inahitajika kwa kiasi kikubwa”, alisema Henjewele.

Katika maambukizi hayo Dkt. Henjewele alifafanua kuwa makundi yanayoongoza kuwa na maambukizi ni makundi ya wanawake wanaofanya biashara ya ngono ambayo maambukizi yake yamefikia asilimia 18, kundi la mme na mwenza wake asilimia 15.8 na mwisho ni kundi maalumu la wasichana wanaofikia umri wa kubalehe lenye asilimia 11.7.

Henjewele alisema kuwa maeneo yanayotisha kwa maambukizi katika eneo la halmashauri ya mji wa Mbinga ni kata ya Mbinga mjini A na B, Masumuni, Betlehemu, Mpepai na Mbambi.

Kwa upande wa halmashauri ya wilaya ya Mbinga maeneo yanayoongoza kuwa ni kata ya Mapera, Ruanda, Amani makolo, Langiro, Kihangi mahuka, Mkako na Amani makolo.

Alieleza kuwa zoezi hilo la upimaji linatekelezwa kwa kuwatumia watoa huduma za magonjwa majumbani, waelimishaji rika, upimaji wa nyumba kwa nyumba na upimaji wa mme na mwenza wake.

Hata hivyo shirika la HDT aliongeza kuwa limekuwa likifanya kazi kwa kata 25 ambapo halmashauri ya mji wa Mbinga limekuwa likifanya kazi zake kwa kata 10 na wilaya ya Mbinga kwa kata 15 ambazo zina maambukizi makubwa ya VVU.


No comments: