Thursday, April 13, 2017

MBUNGE WA MADABA AWATAKA WALIMU KUFUNDISHA KWA BIDII

Na Mwandishi wetu,   
Songea.

MBUNGE wa Jimbo la Madaba wilaya ya Songea mkoani Ruvuma, Joseph Mhagama amewataka walimu wa shule za msingi na sekondari wilayani humo kuona umuhimu wakufanya kazi kwa bidii, katika kuwafundisha watoto darasani masomo ya sayansi na kuacha visingizio kwamba wilaya hiyo ina uhaba mkubwa wa walimu wa masomo hayo.

Kauli hiyo ya Mbunge huyo aliitoa juzi wakati alipokuwa akikagua utekelezaji wa miradi mbalimbali katika jimbo hilo, ikiwemo ujenzi wa madarasa manne ya shule ya sekondari Mahanje na shule ya msingi Nkwera zilizopo wilayani hapa.

Mbunge huyo ambaye alichangia pia shilingi milioni 2.1 kwa ajili ya kununulia vifaa vya ujenzi wa majengo hayo ili yaweze kukamilika ujenzi wake kwa wakati na yaweze kuanza kutumika.


Alisema kumekuwa na visingizio vya ajabu vikitoka kwa walimu kuwa katika wilaya hiyo wanafunzi wanaofeli masomo ya sayansi inatokana na uhaba wa walimu jambo ambalo sio la kweli kwani walimu waliopo wanaouwezo wa kufundisha kwa bidii na weledi na wanafunzi wakaweza kufaulu masomo hayo.

‘’Kuanzia sasa mimi Mbunge wenu wa jimbo hili sitakubali kuona uzembe wa mtindo huu ukiendelea kufanyika na watoto hawa wakiendelea kufeli mitihani ya masomo haya, nahitaji kuona mabadiliko”, alisisitiza Mhagama.


Vilevile aliongeza kuwa serikali imekuwa ikifanya jitihada ya kuboresha maslahi ya watumishi wake kazini hivyo nao wanapaswa kuonesha moyo wa kufanya kazi na sio vinginevyo.

No comments: